Saturday, May 25

Kiama hiki cha gesi Mtwara kisiigawe Tanzania - GAZETI MWANANCHI



Licha ya utajiri huo mkubwa unaweza kujiuliza, je, ni kwanini bara hili limeendelea kuwa maskini kwa miaka mingi huku likikabiliwa na mizozo mingi na migogoro kuhusu mgawanyiko wa rasilimali hizi.

Jiulize, leo ikiwa ni miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU), sasa Umoja wa Afrika (AU), kwanini bara hili tajiri kiasi hiki bado linatajwa kuwa maskini pengine kuliko mabara mengine duniani?

Tunaambiwa, Afrika ina asilimia kubwa ya madini, lakini, jiulize, kwa nini asilimia kubwa ya madini hayo haitumiwi vizuri au kikamilifu katika kuliinua bara hili. Kwanini hayalisaidii bara hili?

Kwa kutaja machache, Afrika ni tajiri kwa madini kama vile, almasi, dhahabu, shaba urani na mengine mengi.

Bara hilo linajivunia asilimia 40 ya umeme wa nguvu za maji unaopatikana duniani, linazalisha madini mengine kama chromium, asilimia 30 ya uranium na asilimia 50 ya dhahabu inayopatikana kote duniani.

Pia, asilimia 90 ya cobalt, asilimia 50 ya phosphates, asilimia 40 platinum, asilimia 7.5 au zaidi ya makaa ya mawe, asilimia 8 ya petroli na bidhaa zake, asilimia 12 ya gesi asilia, asilimia 3 ya madini ya chuma na mamilioni ya ekari za ardhi nzuri na inayofaa kwa kilimo cha mazao mbalimbali yakiwamo ya chakula, biashara ambayo ni mengi mno kuyataja.

Pia, bara hili linayo mito, maziwa, bahari ambako kwa kiasi kikubwa wanapatikana samaki wengi na wa aina mbalimbali wakiwamo hata wale wenye bei kubwa katika soko la dunia.

Pia, Afrika inavyo vitu vingine vingi kama mbuga za wanyama ambazo zimejaa tele, zinavutia watalii wengi, ambao huongeza fedha za kigeni, lakini mbona havijaweza kulisaidia bara hili kuondokana na lindi hili la umaskini?

Huenda ni bahati mbaya kwamba mgawanyo usiyo sahihi au sawa kwa rasilimali hizi, ulafi wa baadhi ya viongozi, hasa wale waliokabidhiwa jukumu la kusimamia idara au taasisi zinazoshughulikia uchimbaji, usambazaji wake na usiri mkubwa katika mikataba.

Kutokana na usimamizi duni wa rasilimali hizi zinaweza kuwa baadhi ya sababu za kuzuka kwa mizozo hii mikubwa ambayo inalikumba bara hili, kama ambavyo inaanza kuzuka Tanzania.

Rais Yoweri Museveni wa Uganda katika moja ya hotuba zake mwaka jana wakati akizindua mradi wa kuchimba mafuta katika Ziwa Natron nchini mwake alieleza mengi kuhusu rasilimali hizi na jinsi zinavyoweza kuigawa nchi na Afrika kwa jumla.
Dar es Salaam. Bara la Afrika kwa hakika limebarikiwa kuwa na rasilimali lukuki ambazo ni lulu katika kukuza uchumi.

“Tunafurahi kuwa tunayo mafuta hapa, hii ni rasilimali ambayo haina budi kutuunganisha zaidi sisi (Waganda) badala ya kutugawa,” alieleza Museveni mbele ya wageni, wenyeji na wawekezaji kutoka China ambao wanashiriki katika mradi huo.

Rasilimali hizi nyingi zinapatikana katika Afrika ikiwamo Tanzania ambako imegunduliwa gesi asilia kiasi cha trilioni 41 futi za ujazo kule Mtwara na Lindi.

Kwa bahati mbaya, rasilimali hii imeanza kuimega tunu ya amani, utulivu ambayo nchi yetu ilijaliwa kuwa nayo kwa muda mrefu na sasa ni dhahiri inaweza kuigawa nchi.

Upo ushahidi wa jinsi ambavyo Muungano wa Tanzania, uliotokana na kuungana kwa Tanganyika na Zanzibar kwa siku za karibuni umekuwa ukitiwa majaribuni, kisa ni hisia za kugundulika au kupatikana kwa mafuta kule Pemba au kwingineko katika bahari kuu.

Huu ni mtihani mkubwa ambao matukio haya ya Mtwara yanasababisha wananchi kuamini kuwa gesi inaweza kuwakomboa kutoka katika lindi la umaskini tena kwa haraka bila kuwashirikisha wenzao wa maeneo mengine ya nchi. Huu ni mtihani ambao nchi inatakiwa kuushinda, lakini kwanza inatakiwa kuwa makini.

Kauli za ubabe au vitisho dhidi ya wananchi hao, ziwe kutoka kwa viongozi wetu kama wa Wizara ya Nishati na Madini, chini ya Profesa Sospeter Muhongo na wasaidizi wake, George Simbachawene na Stephen Masele, hazifai.

Pia, kwa kuwa Rais Jakaya Kikwete ndiye amepewa mamlaka na katiba yetu kusimamia mgawanyo huu wa rasilimali, hana budi naye kuchukua hatua sasa, wala si kusubiri wananchi waanze kukumbatia kile kinachozalishwa kwao, kwa maslahi yao.

Ni wazi kwamba kama kuna wanasiasa, kundi la wanaharakati wanaodhani kuwa watafanikiwa kuwatumia wananchi wa Mtwara kudai gesi ibaki ili wapate maendeleo, wanapaswa kujitazama upya.

Ni wazi kwamba gesi inataka uwekezaji mkubwa, inataka masoko ya uhakika, ambayo yanaweza kuwa mbali ya eneo lao, ilimradi wao wahakikishiwe huduma zote muhimu za jamii kama shule, zahanati, barabara nzuri na kadhalika.

Hakuna shaka kwamba huu ni mradi mkubwa ambao Tanzania kama nchi haikuwahi kuwekeza, lakini pia ni mtihani ambao Serikali ya awamu ya nne, chini ya uongozi wa Rais Kikwete na wenzake wote hawana budi kujifunza kutoka yaliyotokea kwingineko.

Afrika, imeshuhudia nchi iliyokuwa kubwa kieneo, Sudan imegawanyika na mojawapo ya sababu ni mgawanyo wa rasilimali, mafuta na sasa imeparaganyika na kubakia mataifa mawili, Sudan na Sudan Kusini, ambazo zote hazijiwezi kiuchumi.

Kumbukumbu za Nigeria na mizozo kule Niger Delta ni ushahidi mwingine wa jinsi ambavyo bila umakini, nchi inaweza kuingia katika vita.

Miundombinu iliyogharimu kiasi kikubwa cha fedha imekuwa ikichezewa, kuharibiwa karibu kila mwaka kule Nigeria ambako nchi imepata hasara, wananchi wamepoteza maisha, jambo ambalo linapaswa kuepukwa kwa gharama zozote zile, kwani nafasi bado ipo ya kuweza kufanya hivyo.

Kwa mfano, mzozo baina ya Nigeria na Cameroon ambazo awali ziliingia kwenye mzozo mkubwa zikigombea rasi ya Bakassi yenye mafuta, hadi jumuiya ya kimaifa imelazimika kuingilia kati, sote tumeona. Je, tumepata fundisho gani kuhusu rasilimali na jinsi zinavyoweza kuwa sababu na chanzo cha mizozo na migogoro?

Kumbukumbu zetu kule Bungeni mjini Dodoma zinatuonyesha kuwa hivi karibuni kuwa wabunge walijadili rasimu ya sera ya gesi na wengi walionekana kuwa na wasiwasi kuhusu ugawaji wa rasilimali hiyo ndani na kwa wageni.

Wabunge wengi walitaka mikataba iwekwe wazi kwa viongozi na wananchi wote ambao kimantiki gesi hiyo ni mali yao.

Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe(Chadema ) alitaka vitalu vya gesi visiuzwe mapema kwa wawekezaji hadi pale sheria rasmi ya gesi itakapokamilika.

Hata hivyo, Profesa Muhongo alisema serikali iliamua kuanza uuzaji wa vitalu hivyo ili isiwe nyuma katika soko la dunia la nishati.

“Hatuna haja ya kubaki nyuma, tukichelewa katika hili tunaweza kukosa fursa kwani nchi nyingine zinazonunua gesi zipo katika mchakato wa kutafuta mbinu mbadala za nishati hiyo” alisema Profesa Muhongo.

Ni dhahiri kwamba hili la Mtwara linaweza kuichelewesha Tanzania, hasa wakati huu ambao jirani zetu, Msumbiji wamewekeza katika gesi kwa kiasi kikubwa.

Ushauri hapa ni kuwa busara zaidi itumike, pande zote ili zichume na kuvuna kutoka kwenye gesi asilia ya Mtwara hadi bomba litakapojengwa, viwanda kama kile cha saruji, wananchi wanufaike, serikali ikusanye kodi, ambazo hatimaye zitasaidia kukuza uchumi.

Inawezekana kuwa hiki kinachotokea kule Mtwara, bila umakini kinaweza pia kuibuka Ruvuma au hata Manyoni (Singida) ambako pia imegundulika urani, madini mengine ambayo pia yameanza kuzua mijadala na mizozo mingi ikiwamo ile ya kimazingira.

Kuna madini aina ya nickel kule Kabanga, Ngara Mkoani Kagera, ambayo pia yana thamani kubwa na ambayo pia yanaweza kuzua mzozo mwingine. Kama nchi, tujihadhari, tujaribu kuwa makini!

No comments:

Post a Comment