Monday, January 9

Filamu Bongo 2011

WASANII wa filamu Bongo mwaka 2011 walifanya mambo makubwa na kupiga hatua katika tasnia ya filamu, huku wasanii wengine wakiibuka na kuwa gumzo.

RAY
Ray yeye kama ilivyo kawaida ndiye kioo cha tasnia ya filamu kwa mwaka huo. Aliweza kufanya mambo makubwa ikiwa ni pamoja na kusafiri kwenda kununua vifaa vyake vya kazi Ulaya.
Pia kwa kutumia kampuni yake aliibua wasanii wapya kama Otilia Joseph.

MONALISA
Yvonne Cherryl �Monalisa� alishiriki tuzo za Pan African zilizofanyika nchini Marekani kupitia filamu yake ya Binti Nusa iliyotengenezwa na kampuni yake.

Mwaka jana pia alipata nafasi ya kwenda kushiriki filamu nchini Ghana ikiwa ni sehemu mojawapo ya kutafuta soko la kimataifa. Jambo jingine kubwa kwa mwanadada huyo ni kuwa alisambaza filamu ya Binti Nusa yeye mwenyewe.

KANUMBA
Kanumba naye hakuwa nyuma kwani alitoa filamu nyingi zilizofanya vizuri, si hayo tu bali pia alitumia uwezo wake katika kumleta msanii nyota wa kimataifa kutoka nchini Nigeria, Ramsey Nouah, kushiriki katika filamu yake ya Devil Kingdom.

Filamu ilitikisa katika tasnia ya filamu Bongo. Pia ndiye msanii ambaye amekuwa balozi wa makampuni mbalimbali kwa mwaka jana. Alisafiri kwenda nchini Marekani katika shughuli za sanaa, pia alikwenda Ghana kwa ajili ya kurekodi filamu akishirikiana na nyota wa filamu Afrika kutoka nchi kama Nigeria, Ghana na Afrika Kusini.

WOLPER
Jacqueline Wolper ni moja kati ya wasanii ambao kwa mwaka uliopita alifanya vizuri katika mauzo hata kuweza kuwafunika baadhi ya wasanii wa kike katika tasnia ya filamu.
Wolper pia alitengeneza filamu zake akiwa kama mtayarishaji, amefanya vema katika tasnia hii ya filamu Bongo anastahili Pongezi.

JB
Jacob Stephen �JB� ndiye msanii anayeshikilia nafasi ya kwanza kwa mauzo Bongo kupitia filamu anazoshiriki na kutengeneza mwenyewe.
Filamu yake ya Senior Bachelor ilionyesha uwezo wake wa hali ya juu na kumfanya ashikilie nambari moja.
Filamu zake nyingine ni pamoja na Nipende Monalisa, DJ Ben na Regina.

PATCHO
Patcho Mwamba ni mwanamuziki, lakini tangu alipoingia katika tasnia ya filamu akiwa sambamba na swahiba yake Kanumba. Moja ya sifa ya Patcho pamoja na kuigiza vizuri ni bingwa wa viwalo Bongo, kwa hiyo kama unampatia nafasi ya kuigiza suala la pamba unasahau.

DOTNATA
Dotnata alifungua kampuni ya Tanganyika Entertainment kwa ajili ya kusambaza kazi zake. Alitengeneza filamu iliyojulikana kwa jina la Chupa Nyeusi akiwashirikisha wasanii kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na Burundi.

MR. MTUNIS
Amefanya vizuri sokoni baada ya filamu yake ya Mrembo Kikojozi kuwa gumzo. Hata filamu zake nyingine za Clinic Love na Kisasi zilitamba.

NDAUKA
Rose Ndauka ni moja kati ya akina dada waliofanya vizuri katika tasnia ya filamu Bongo, ikiwa ni pamoja na kufungua kampuni yake ya Rose Ndauka Entertainment kwa ajili ya kazi zake na kufanikiwa kutengeneza filamu kama Bad Girl, The Diary, Reuben na Angel.
Alienda Rwanda kwa ajili ya kurekodi filamu ya Maisha Baada ya Vita Rwanda.
Alitangaza ndoa na meneja wake Mariki iikiwa sambamba na kubadili dini, sasa anaitwa Aisha.


RICHIE
Single Mtambalike �Richie� ni moja kati ya wasanii waliofanya vizuri katika mauzo ya filamu Bongo na aliwaingiza wanaye katika uigizaji kwenye filamu ya Uswahilini Kwetu.

TINO
Hisani Muya �Tino� msanii huyu anarudi kwa nguvu zote, baada ya filamu yake ya Cut Off kufanya vizuri na kufuatiwa na Zowa, sasa ameingiza sokoni filamu ya Loreen inayofanya vizuri sokoni.

Kumbuka kuwa filamu yake ya Shoga ilikuwa gumzo baada ya Bodi ya filamu kuizuia na hatimaye kuibadili jina na kuwa ni Shoga Yangu badala ya Shoga.


DR CHENI
Naye alifanya vema kupitia filamu yake ya One By One na kuwa gumzo akiendelea kuuza sokoni.

Funga mwaka kubwa kuliko zote ni lile wazo la magwiji wa tasnia hiyo, Vincent Kigosi �Ray The Greatest� na Steven Kanumba �Kanumba The Great� walipoamua kutengeneza filamu kwa pamoja na kuipa jina la Off Side,

Walipoenda kuizindua nchini Kongo, ilisababisha baadhi ya watu kupoteza maisha wakipigania kuwaona nyota hao ambao waliandamana na Irene Uwoya, Jenifer na Johari.

Ukija katika fani ya uchekeshaji kwa vichekesho vya filamu, waliofanya vizuri ni King Majuto, Kingwendu, Sharo Milinea, Pembe bin Kichwa na Erick.
Katika upande wa wachekeshaji wa televisheni, kijana Lucas Mhuvile �Joti�' hakuwa na mpinzani. Kila siku amekuwa akibuni na kuibuka na kitu kipya ambacho ni burudani kwa mtazamaji.

Joti ameufunga mwaka kwa kuwa na pointi nyingi pengine kuliko msanii mwingine yeyote.

1 comment:

  1. Useful article, thank you for sharing the article!!!

    Website bloggiaidap247.com và website blogcothebanchuabiet.com giúp bạn giải đáp mọi thắc mắc.

    ReplyDelete