Monday, May 18

FIHIR MVUNGI: DIWANI ALIYEONGOZA KATA YA MSANGENI KWA MIAKA 55, BADO ANATAKA KUENDELEA AKIWA NA UMRI WA MIAKA 80

*Hajawahi kung'atuka wala kuondolewa, afikiria kugombea tena mwaka huu, azungumzia thamani ya Mzee Msuya wilayani Mwanga

Charles James, Michuzi TV

JINA lake ni Fihir Mvungi, umri wake ni miaka 80. Ameongoza kwa miaka 55 kama Diwani wa Kata ya Msangeni iliyopo wilayani Mwanga, Kilimanjaro.

Ndio. Unaweza kusema Mvungi ndiye kiongozi wa kuchaguliwa ambaye amehudumu kwenye nafasi yake kwa muda mrefu bila kung'atuka wala kuondolewa na wananchi.

Katika mahojiano maalum ambayo amefanya na Michuzi Blogu, Mvungi anaeleza kuwa moyo wa utumishi alionao, upendo kwa wananchi wake ni sababu zinazomfanya aendee kuwa Diwani wa kata hiyo ya Msangeni kwa muda mrefu.

Diwani huyu aliingia kwa mara ya kwanza kwenye nafasi yake mwaka 1965 akiwa kijana mdogo wa miaka 25 baada ya kugombea nafasi hiyo kwa mara ya pili baada ya kugombea 1962 na kuikosa.

" Kwanza niligombea mwaka 1962 lakini nilikosa nafasi hiyo, lakini nilipogombea tena 1965 nilipita bila kupingwa. Toka hapo nimekua diwani wa kata hii toka kipindi hicho.

Lakini wakati nachaguliwa Wilaya ilikua ni moja tu, bado wilaya ilikua ni Same. Haikua imegawanywa kama sasa ambavyo ni Same na Mwanga. Hivyo nimeongoza kwa kipindi chote hicho hadi leo," Anaeleza Mvungi.

Diwani huyu pia ameweka rekodi yake ya kufanya kazi na marais wa awamu zote tano kuanzia Mwalimu Nyerere hadi sasa chini ya Rais Dk John Magufuli ambaye yeye Mvungi anamuona kama kiongozi mwenye maono mengi ya kiuongozi.

SIRI YA KUDUMU MUDA MREFU

Mvungi anasema uwezo wake wa kushirikiana na watu wake katika Matatizo na raha, kuwasaidia kupata maendeleo na kuwaletea pindi inapobidi ni sababu zingine zinazomfanya aendelee kuongoza kwa kipindi kirefu tofauti na madiwani wengine.

Anasema kazi ya uongozi haijawahi kumletea fedha lakini yeye anaifanya kwa moyo mmoja bila kunung'unika kwani anaamini nafasi aliyopewa na wananchi wa kata yake imetokana na moyo wa uaminifu walionao kwake.

" Ningeweza kuitumia nafasi yangu kujinufaisha lakini inamaana gani kama wewe unaishi maisha mazuri ilihali watu waliokuchagua wanalalamika? Mimi ni mtu ambaye naitazama kesho yangu zaidi kuliko leo.

Unadhani ningekua mtu wa kujinufaisha mwenyewe ningekaa kwenye uongozi tena wa kupigiwa kura kwa muda wote huu bila kuondolewa?

Kuna watu wana kipato kikubwa kuliko mimi, ingekua ishu ni fedha wangeshanitoa. Lakini wananchi wangu wamewekeza uaminifu kwangu. Wananiamini na mimi nawafanyia kazi yao ipasavyo," Anasema Mvungi.

Anasema ndani ya miaka 55 aliyodumu amesaidia upatikanaji wa Shule Nne za Sekondari zenye mahitaji karibu yote kwa asilimia 90 pamoja na Zahanati ambazo zinawahudumia wananchi wake bila matatizo.

Anaeleza Zahanati Moja ya Sungo ndio inayomuumiza kichwa maana haina nyumba ya Daktari lakini anaamini mwaka huu hautoisha atakua imeshajengwa.

Kuhusu Miundombinu Mvungi anasema hakuna barabara ambayo haijajengwa kwenye Kata yake. Tena anaeleza suala la barabara sio ajenda kabisa kwenye Wilaya ya Mwanga.

Anasema Wilaya ya Mwanga licha ya kuwa milimani lakini ina Lami kutokea Barabara kuu ya Moshi-Dar es Salaam hadi vijijini huko na wala hapajawahi kuwa na changamoto hiyo.

Kata yake pia kila kaya inawasha umeme. Hakuna nyumba ambayo ina changamoto ya umeme wala haipo ambayo inawasha kibatari kwa kukosa umeme.

Hii inaonesha jinsi gani miaka 55 aliyodumu amemaliza changamoto zinazogusa maisha ya binadamu Moja kwa Moja.

Kutokua na changamoto ya Maji, Afya, Elimu, Miundombinu na Umeme ni uthibitisho tosha kwamba miaka 55 aliyoongoza kata hiyo amelet maendeleo ya kuridhisha kwa wananchi wake.

ANAMUONGELEAJE MSUYA.

Wilaya ya Mwanga ni mojawapo ya Wilaya ambazo zimebarikiwa kutoa viongozi wakubwa nchini ambao wamewahi kushika nafasi za juu za kiuongozi nchini.

Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa David Msuya ambaye ana rekodi ya kuongoza katika Serikali mbili ya awamu ya kwanza chini ya Mwalimu Nyerere na ya pili chini ya Alhaji Hassan Mwinyi kwao ni Mwanga.

Mwanamke wa kwanza kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ni Asha-Rose Migiro ambaye kwa sasa ni Balozi wa Tanzania nchini Uingereza. Huyu nae kwao ni Mwanga.

Profesa Uruma wa Makinikia, Waziri wa zamani wa Habari, Phenela Mkangala, Waziri wa zamani wa Utalii na Elimu, Prof Jumanne Maghembe. Ni baadhi ya viongozi wanaotoka Mwanga.

Turudi kwa Msuya: Napenda kujua namna ambavyo Jamii ya Wapare ambao ndio hasa wazawa wa Mwanga wanavyomtazama lakini pia Mkoa wa Kilimanjaro kwa ujumla.

Mvungi anasema mafanikio yote ya Mwanga na Kilimanjaro yalichangiwa na Msuya akiwa Mbunge na Waziri Mkuu.

Namna ambavyo Mwanga usiku inapendeza kwa mwanga wa Umeme na siyo kibatari, namna ambavyo licha ya Milima ya Usangi na Ugweno ilivyo mikubwa na barabara inapitika tena ya lami ni wazi heshima na sifa vinapaswa kurudi kwa Msuya.

Anasema simu za mikononi kwao zilikuepo toka zamani, changamoto ya Shule, Afya na miundombinu mingine ilimalizwa na Msuya katika utumishi wake.

" Kama Nyerere ni Baba wa Tanzania, kwa hakika Mzee Msuya ni Baba wa Mwanga. Wanasema Nabii hakubaliki kwao lakini Msuya anakubalika kwenye kila moyo wa mwana-Mwanga.

Ukitaka upigwe n uchakae zungumza maneno mabaya ya kumhusu Msuya hapa Mwanga. Tunafahamu yeye ni binadamu na ana makosa yake lakini hapa Mwanga Msuya ni Baba hasemwi hadharani," Anasema Mzee Mvungi.

Anasema Msuya ni vile aliamua kung'atuka mwenyewe lakini tofauti na hapo angeiongoza Mwanga pengine hadi leo. Maana kwa mambo aliyoyafanya hakuna ambaye angethubutu kugombea nae.

" Ukitaka kujua Msuya alikua kichwa tazama ameweka rekodi ya kuwa Waziri Mkuu kwa awamu mbili. Kwa Mwalimu Nyerere na Mzee Mwinyi. Hii ni sifa kubwa na ya kipekee sana. Kuaminiwa na marais wawili haiji hivi hivi," Anasema Mvungi.

JE ANA MPANGO WA KUGOMBEA MWAKA HUU?

2020 huu ni mwaka wa uchaguzi na tayari wanasiasa mbalimbali nchini washaanza kupigana vikumbo kwenye nafasi mbalimbali. Udiwani, Ubunge na Urais.

Mvungi ambaye yeye hajawahi kutamani hata kuwa Mwenyekiti wa Halmashauri anatueleza kama bado anahitaji kuendelea kuongoz kwa kipindi kingine.

" Ujue mimi sikujichagua mwenyewe kuwa Kiongozi, mimi nilifuatwa na watu kuombwa kugombea. Nikagombea na wakanipa kura. Na hata kila uchaguzi huwa siamui mwenyewe kwa utashi wangu nafuatwa kuambiwa nigombee.

Hivyo mwaka huu pia wananchi wangu wakisema endelea nitaendelea, wakisema Mvungi imetosha kaa pembeni nakaa pembeni. Binafsi naamini katika Demokrasia ya kuwaacha wananchi kuamua nani wanataka awaongoze," Anasema Mvungi.

Pamoja na umri wake wa miaka 80 bado Diwani huyu ana kumbukumbu nyingi za mambo ya zamani, ana uwezo wa kusoma bila kutumia miwani lakini hata gari anayoendesha ni 'Manual' jambo ambalo ni tofauti na wazee wengine wa umri wake.

ANAMZUNGUMZIAJE RAIS MAGUFULI?

Ni Kiongozi mzuri, jasiri ambaye akiamua jambo lake basi litatimia bila kujali watu wanasema nini. Ameonesha kwamba anaweza kuleta mabadiliko zaidi ya kimaendeleo ndani ya muda mfupi aliokaa.

Kafufua shirika letu la Ndege, miundombinu ya barabara inajengwa kila kona nchini, elimu bure ambayo inampa fursa kila mtoto sasa kusoma imerejea. Huu ni uzalendo ambao ameuonesha.



Diwani wa Kata ya Msangeni, Fihir Mvungi ambaye amedumu kwenye nafasi hiyo kwa miaka 55 ambapo alianza kuhudumu nafasi hiyo mwaka 1965 akiwa kijana wa miaka 25 na sasa ana miaka 80.

No comments:

Post a Comment