Sunday, December 3

Waziri aagiza mkandarasi akamatwe


Naibu Waziri Maji na Umwagiliaji Jumaa Aweso ameviagiza vyombo vya dola mkoani Ruvuma kumsaka mkandarasi (jina tunalo) kwa tuhuma za kulipwa Sh500 milioni na kuondoka.
Agizo hilo alilitoa wilayani Tunduru jana baada ya kupokea taarifa ya mradi mkubwa wa maji unaogharimu Sh1 bilioni uliopo Mironde, Kijiji cha Matemanga.
Naibu Waziri Aweso alisema kwamba Serikali haitamvumilia mkandarasi yeyote atakayekula pesa ya mradi wa maji na kuwataka waliokula pesa hizo kujiandaa ‘kuzitapika.’
Naibu Waziri aliwaagiza wakuu wa idara na wakurugenzi wa halmashauri kuacha kutoa tenda kwa ushemeji au mtoto wa mjomba.
Awali, mhandisi wa maji wa halmashauri ya Tunduru, Emmanuel Mfoi alisema mradi huo ulianza kujengwa mwaka 2013 na ulitakiwa kukamilika mwaka 2014 lakini umekuwa ukisuasua.
Alisema kwamba mkandarasi alikuwa akiongezewa muda mara kwa mara na kutakiwa akabidhi mradi huo kwa halmashauri kabla ya Novemba 27 mwaka huu lakini kashindwa.
Mkazi wa kijiji cha Matemanga, Said Hamis alimweleza Naibu Waziri kuwa wananchi wanateseka kutokana na kutopata huduma ya maji.
“Tunashukuru umefika kiongozi wetu, huduma ya maji hapa hakuna kabisa hali ni mbaya na hatuna matumaini ya kupata majisafi na salama, tunaomba Serikali itutatulie kero hii ya muda mrefu,” alisema Hamis.

No comments:

Post a Comment