Wednesday, November 1

Watumishi 71 wafutwa kazi kutokana na rushwa


Watumishi 71 wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wanaofanya kazi katika kitengo cha mizani wamefukuzwa kazi kwa tuhuma za rushwa.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Mhandisi Patrick Mfugale amesema watumishi hao wanadaiwa kupokea rushwa ili kuruhusu magari yanayozidisha uzito kupita kwenye mizani bila kutozwa faini. Amesema watumishi wengine saba wanachunguzwa kwa tuhuma hizo.
Mfugale amesema hayo leo Jumatano Novemba Mosi, 2017 katika mkutano wa tisa wa baraza la wafanyakazi wa Tanroads unaofanyika mjini Kigoma.
“Hatua hizi zimechukuliwa kati ya Januari na Oktoba,2017, tutaendelea kuchukua hatua kwa wote wanaojihusisha na vitendo hivyo,” amesema Mfugale.
Akizungumza katika mkutano huo, Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Samson Anga amewataka watumishi wa umma kujiepusha na vitendo vya rushwa. Ameonya watakaobainika watachukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria.
“Bila kudhibiti magari yanayozidisha uzito, barabara zetu zinazojengwa kwa gharama ya mabilioni ya fedha za umma hazitadumu,” amesema Anga.
Mkuu wa wilaya ametoa mfano wa miradi ya ujenzi wa barabara zinazogharimu mamilioni ya fedha za umma kuwa za Nyakanazi-Kakonko na Kasulu -Kidahwe zinazounganisha Kigoma na mikoa mingine.
Mwenyekiti wa Bodi ya Tanroads, Hawa Manga amewaasa watumishi kuzingatia sheria, kanuni na maadili.

No comments:

Post a Comment