Wednesday, November 1

MAVUNDE ASISITIZA KUWA NA NGUVU KAZI YA VIJANA WENYE UJUZI KATIKA UJENZI WA UCHUMI WA TAIFA


Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu(Kazi,Vijana na Ajira) Mh. Anthony Mavunde leo ametembelea Chuo cha Ufundi Don Bosco kilichopo mkoani Kilimanjaro na kukagua maendeleo ya Vijana ambao wanasomeshwa hapo na Serikali kupitia mpango wa Ukuzaji Ujuzi Nchini.

Akizungumza na Vijana hao ambao wanasomea masomo ya Komputa,Mavunde amewataka Vijana hao kuutumia ujuzi watakaoupata hapo chuoni kujiajiri kwa  kuunda vikundi na Makampuni ili wapate nafasi ya kuwezeshwa kupitia mifuko ya uwezeshwaji wananchi kiuchumi nchini na hivyo kusaidia kutatua changamoto ya ukosefu wa Ajira kwa Vijana.

Mavunde pia amewaeleza Vijana hao kwamba watambue siku zote wao ndio moyo wa Taifa  na hivyo ndio nguvu kazi inayotegemewa kwa kiasi kikubwa ndio maana Serikali inaona umuhimu wa kuwekeza katika Mpango huu wa ukuzaji Ujuzi ili kuhakikisha Taifa linakuwa na nguvu kazi yenye ujuzi stahiki katika kuelekea nchi Uchumi wa Viwanda na ya kipato cha kati.

Kwa upande wao Vijana hao wanufaika na Mpango huu wameishukuru serikali kwa kutekeleza mpango huu wa ukuzaji ujuzi ambao utawasaidia kupata ujuzi na baadaye kuweza kujiajiri na Kuajiri Vijana wengine.

Mpango huu wa ukuzaji ujuzi unatarajia kuwanufaisha Vijana 3445 ambao serikali itagharamia mafunzo yao katika kozi za Tehama,Umeme,Ushonaji,Useremala,Uchomeleaji,Kuweka vigae,Ufundi bomba,Upigaji chapa na Ufundi Magari.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu(Kazi,Vijana na Ajira) Mh. Anthony Mavunde akikagua maendeleo ya Vijana ambao wanasomeshwa na Serikali kupitia mpango wa Ukuzaji Ujuzi Nchini katika Chuo cha Ufundi Don Bosco kilichopo mkoani Kilimanjaro.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu(Kazi,Vijana na Ajira) Mh. Anthony Mavunde akizungumza na vijana katika Chuo cha Ufundi Don Bosco kilichopo mkoani Kilimanjaro.

No comments:

Post a Comment