Thursday, October 12

Dar mpya kuanza kusukwa pembezoni

Dar es Salaam. Utekelezaji wa mradi wa pili wa mabasi yaendayo kasi (BRT) na mradi wa awamu ya kwanza wa uendelezaji Jiji la Dar es Salaam (DMDP) utafungua fursa za kiuchumi kwa maeneo ya pembezoni mwa jiji.
Akiwasilisha matokeo ya utafiti wa mpango wa DMDP, James Rayner ambaye aliongoza timu ya wataalamu kutoka Benki ya Dunia kufanya utafiti huo alisema umebaini uwapo wa fursa za kiuchumi maeneo ya pembezoni, lakini kikwazo ni changamoto ya upangaji wa maeneo usiofuata utaratibu.
“Utekelezaji wa awamu ya pili ya BRT utakapokamilika na matumizi ya ardhi yatakapopitiwa upya wakati wa kutekeleza miradi hii miwili maeneo ya pembezoni yatanufaika,” alisema Rayner.
Aliongeza kuwa maeneo hayo yatanufaika kwa kugeuka kuwa ya uwekezaji na shughuli za kibiashara.
Rayner alitolea mfano mabadiliko yaliyopo kwa wakazi wa maeneo ya Ubungo ambapo kuwapo kwa huduma ya usafiri wa magari yaendayo kasi na maduka makubwa ya bidhaa eneo la Mlimani City kumewapunguzia kutumia muda mwingi kutafuta bidhaa na huduma mahala pengine..
Kwa upande wake Emmanuel Ndyamukama ambaye ni mratibu msaidizi wa mradi wa kuendeleza jiji la Dar es Salaam (DMDP), alisema awamu ya pili ya utafiti huo itaendana na matumizi ya miundombinu ya BRT katika kuboresha hali ya kiuchumi ambayo itakamilika Juni mwaka ujao.

No comments:

Post a Comment