Saturday, October 7

CUF kushiriki uchaguzi wa madiwani kivyake


Dar es Salaam. Chama cha Wananchi(CUF), upande wa Profesa  Ibrahim Lipumba kimesema kitashiriki kikamilifu katika uchaguzi wa madiwani uliopangwa kufanyika Novemba 26 lakini kimesisitiza kutoshirikiana na Ukawa.
Hii ni mara ya kwanza kwa chama hicho kuweka msimamo wake katika uchaguzi tangu kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ambapo CUF ilikuwa miongoni mwa vyama viliunda umoja huo kwa kuweka wagombea waliokubaliana.
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CUF, Abdul Kambaya amesema leo Jumamosi jijini kuwa chama hicho hakioni sababu yoyote ya kushirikiana na vyama vingine kwenye uchaguzi huo ambao unahusisha halmashauri 34.
“CUF tunashiriki kwenye uchaguzi huu lakini hatututegemei kushirikiana na umoja wowote ule, sisi hatuitambui Ukawa lakini tunajua kuna chama kama Chadema, CUF na vyama vingine,” amesema Kambaya wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za chama hicho zilizopo Buguruni.
Amesema chama hicho kimejipanga vilivyo kuelekea kwenye uchaguzi huo na kwamba ili kuwaletea maendeleo wananchi wa maeneo hayo kunahitajika kuwa na viongozi wenye utulivu wa akili.
“Sisi tuko tayari kuelekea kwenye uchaguzi huo bila kuhusishwa na chama kingine chochote tunaamini tutafanya vizuri,” amesema.
Awali, mkurugenzi wa uchaguzi wa chama hicho, Jafari Mneko aliwataka wana CUF kujitokeza kwa wingi katika kinyang’anyiro hicho. Amesema chama chake kimepokea taarifa kutoka ofisi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi ikiwaarifu kuhusu uchaguzi huo.
“Tumepata barua kutoka tume ambayo imetueleza kuhusu tarehe ya kufanyika kwa uchaguzi huo na sisi tumeanza kujiandaa na ndiyo maana tunawaomba wanachama wetu wanaohisi wana uwezo wajitokeze kuomba nafasi na baadaye viongozi wa chama watachuja majina yao,” amesema.
Katika hatua nyingine mkurugenzi huyo alionya kile alichokiita mali ya chama kutumika kinyume na sheria na akawataka wanachama kutetea maslahi ya chama chao.
“Kuanzia sasa hatutapenda kuona mali ya chama kama mihuri, bendera ikiendelea kuchezewa ovyo, tunawataka wanachama kuzingatia katiba ya chama ibara ya 12 ambayo inamtaka kila mwanachama kulinda katiba na imani ya chama,” amesema.

No comments:

Post a Comment