Monday, September 11

UFUNGUZI WA UCHUNGUZI WA KINYWA NA MENO WAFANYIKA ZANZIBAR

Jamii inatakiwa kuweka utaratibu wa kupima afya ikiwemo afya ya kinywa na meno ili kupatiwa uchunguzi wa awali pamoja na elimu sahihi ya afya angalau mara mbili kwa mwaka .

Hayo aliyaeleza na Mkurugenzi wa Kinga na Elimu ya Afya Dr Fadhil Mo’hd Abdalla huko katika Kituo cha Afya Rahaleo, wakati akifungua zoezi la uchunguzi wa afya ya kinywa na meno linaloendeshwa na Chama cha Madaktari wa Kinywa na Meno kutoka Tanzania .

Alisema afya hiyo ni muhimu kufanyika awali kabla ya madhara, kwa kupatiwa ushauri wa mapema kabla ya athari kujitokeza na kusababishwa kupoteza meno .Alifahamisha kuwa katika miaka ya nyuma elimu ya afya ya kinywa na meno zilikuwa zikitolewa katika maskuli ,wataalamu hutoa elimu kwa wanafunzi pamoja na kung’oa meno kwa wale ambao meno yao yameadhirika .

Aidha alisema mpango huo wa uimarishaji afya ya jamii iko haja kurejea utaratibu wa kizamani , wataalamu wa afya ya kinywa na meno kutoa huduma za matibabu katika maeneo mbali mbali ikiwemo maeneo ya maskuli na vijijini .

“Huu usiwe mwanzo wa kuonyesha njia kwa jamii na wala msisubiri kuumwa kila muda mujiwekee utaratibu wa kujichunguza afya zenu ikiwemo afya ya kinywa na meno pamoja na maradhi yasioambukiza ili muweze kupata ushauri mapema kwa Madaktari ,”alisema Mkurugenzi Kinga.

Alieleza kutoa elimu na uchunguzi wa afya kwa jamii itasaidia kupunguza gharama za matibabu na kuimarisha kinga ya awali na kujiepusha na matumizi ya vyakula ambavyo vinachangia kuleta madhara ikiwemo vyakula vya sukari kuchangia uozeshaji wa meno hasa kwa watoto .

Nae Mwenyekiti wa Chama cha Madaktari wa Afya ya Kinywa na Meno ( TBA) Dr Lorna Carneiro alisema mara hii wamepata fursa ya kuja Zanzibar kwa kufanya uchunguzi wa afya ya kinywa na meno ili kujua wale wagonjwa  ambao wanamatatizo na kuwapatia tiba pamoja na kuwapa elimu ya afya .

Alisema Chama hicho kinahimiza umuhimu wa afya bora kwa jamii na kutoa ushauri wa maradhi mbalimbali ikiwemo ukimwi ,saratani ,Kifua kikuu,afya ya kinywa na meno pamoja na maradhi yasioambukiza kwa kuifanya jamii ipate uelewa na kujikinga na maradhi ambayo yanauwezo wa kuepukika .

“Hali ya idadi ya Wagonjwa ni kubwa wakati ya kuwa magonjwa haya yanakingika kwa haraka na kupona lakini kikwazo ni kuwa na uchache wa madaktari ,“alisema Dr Lorna .

Alifahamisha kila ifikapo tarehe 20 machi ya kila mwaka huadhimisha siku ya afya ya kinywa na meno kwa mwaka ujao wanatarajia uzinduzi wa zoezi hilo litafanyika Zanzibar .

Nae Mgonjwa BI Nargisi Uzia ambae alifika kupatiwa huduma ya matibabu katika kituo hicho alisema anaishukuru Serikali kwa kuwaletea wataalamu wa kuchunguza afya zao lakini pia iko haja ya zoezi hilo liwe endelevu kwani matatizo yako mengi yanahitaji uchunguzi.
Rais wa Chama cha Madaktari wa Kinywa na Meno Tanzania Dokt,Lorna Carneiro kulia akitoa hotuba ya makaribisho katikaUfunguzi wa Zoezi la Uchunguzi wa Maradhi ya kinywa na Meno katika Kituo cha Afya Rahaleo Mjini Unguja.

Mkurugenzi wa Kinga na Elimu ya Afya katika Hospitali ya Mnazi mmoja Dkt,Fadhil Abdalla akitoa hotuba ya Ufunguzi wa Zoezi la Uchunguzi wa Maradhi ya Kinywa na Meno katika Kituo cha Afya Rahaleo Mjini Unguja.Zoezi linalofanywa na Chama cha madaktari wa Kinywa na Meno Tanzania(TDA).wakishirikiana na madaktari wa Zanzibar.
Mkurugenzi wa Kinga na Elimu ya Afya katika Hospitali ya Mnazi mmoja Dkt,Fadhil Abdalla katikati akiwa katika picha ya pamoja na Madaktari kutoka Chama cha madaktari wa Kinywa na Meno Tanzania(TDA).pamoja na madaktari wa Zanzibar katika Zoezi la Uchunguzi wa Maradhi ya Kinywa na Meno katika Kituo cha Afya Rahaleo Mjini Unguja.
Daktari wa Kinywa na Meno kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili Dkt,Ismail Amour akitoa Elimu ya kujikinga na maradhi hayo katika Ufunguzi wa Zoezi la Uchunguzi wa Maradhi ya Kinywa na Meno katika Kituo cha Afya Rahaleo Mjini Unguja.Zoezi linalofanywa na Chama cha madaktari wa Kinywa na Meno Tanzania(TDA).wakishirikiana na madaktari wa Zanzibar.


Rais wa Chama cha Madaktari wa Kinywa na Meno Tanzania Dokt,Lorna Carneiro kushoto akifanya mahojiano na Muandishi wa Habari kutoka ITV Farouk Kariym pamoja na muandishi wa Habari Maelezo Zanzibar Khadija Khamis katika Ufunguzi wa Zoezi la Uchunguzi wa Maradhi ya Kinywa na Meno katika Kituo cha Afya Rahaleo Mjini Unguja.Zoezi linalofanywa na Chama cha madaktari wa Kinywa na Meno Tanzania(TDA).wakishirikiana na madaktari wa Zanzibar.

Daktari wa Kinywa na Meno kutoka Haspitali ya Arrahma Zanzibar akimfanyia Uchunguzi wa mardhi ya Kinywa na Meno Kauthar Vuai mkaazi wa meli nne, katika Zoezi la Uchunguzi wa Maradhi ya Kinywa na Meno katika Kituo cha Afya Rahaleo Mjini Unguja.Zoezi linalofanywa na Chama cha madaktari wa Kinywa na Meno Tanzania(TDA).wakishirikiana na madaktari wa Zanzibar.PICHA NA YUSSUF SIMAI/MAELEZO ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment