Saturday, September 30

Tamko la Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wazee Duniani, Oktoba 1, 2017


Mhe. Iddi Ramadhani Mapuri
Makamu Mwenyekiti 
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) inaungana na wadau wote duniani katika kuadhimisha siku ya wazee duniani. Wakati dunia inaadhimisha siku hii, Tume inatoa wito kwa jamii ya Watanzania kuondoa vitendo vyote vya unyanyasaji dhidi ya wazee ili kuhakikisha kuwa wanaishi katika kutekeleza kauli mbiu ya taifa inayosema “Kuelekea uchumi wa viwanda: Tuthamini mchango, uzoefu na ushiriki wa wazee kwa maendeleo ya taifa.

Uzee na kuzeeka havikwepeki; hivyo ustaarabu wa jamii au nchi yoyote duniani si wingi wa raslimali na mazingira mazuri bali katika uwekaji wa mifumo madhubuti ya kulinda na kutetea haki za makundi maalum yanayohitaji ulinzi wa jamii husika. Kwa kulitambua hilo Desemba 14, 1990, Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Azimio lake Na. 45/106 ulipitisha tarehe 01 Oktoba, ya kila mwaka kuwa siku ya wazee Duniani. Vipaumbele katika Azimio hilo ni pamoja na suala la uhuru wa wazee, wazee kushiriki na kushirikishwa katika shughuli za maendeleo, kutunzwa na kuheshimiwa.

Hivyo siku hii ya tarehe 01 Oktoba, dunia inawapa nafasi wazee kukutana pamoja na kubadilishana mawazo juu ya nini cha kufanya kuhusiana na mustakabali wa haki zao kwa ujumla, katika kuleta maendeleo ya Taifa tunapoelekea Tanzania ya viwanda.

Katika kutambua, kulinda kukuza na kutetea haki za wazee serikali imeridhia Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu, yaani “The African Charter on Human and People’ Rights (ACHPR)” pamoja na Itifaki ya kusimamia haki za wazee ’’Protocol to the African Charter on Human and People’ Rights on the Rights of elder persons in Africa”.  Kadhalika kuna Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa, yaani TheInternational Convenant on Civil and Political Rights (ICCPR), na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kiutamaduni, yaani The International Convenant on Economic, Social and Cultural Rights (ICESCR).

Kitaifa, kuna Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 pamoja na marekebisho yake ibara ya 12 (2) na ibara ya 14 ambazo zimeeleza juu ya wazee kupewa heshima na kupata hifadhi kutoka kwa jamii wanamoishi.

Aidha, kuna Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ambayo ni Idara huru ya Serikali iliyoanzishwa kwa mujibu wa Ibara ya 129 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, na Sheria Na. 7 ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ya mwaka 2001 ambayo ni kitovu cha kulinda, kutetea na kukuza haki za binadamu nchini.

Takwimu za wazee kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2002, Tanzania ilikuwa na wazee 1,952,041 (sawa na wanaume 940,229 na wanawake 1,011,812) na katika sensa ya mwaka 2012 idadi ya wazee iliongezeka hadi kufikia 2,507,568 (wanaume 1,200,210 na wanawake 1,307,358) sawa na 5.6% ya wananchi wote. Hivyo, kwa kadiri idadi ya wazee inavyoongezeka ndivyo changamoto zinazowakabili zinavyoongezeka. Hivyo jitihada mahsusi lazima zifanyike kukabiliana nazo.

Tume kama taasisi ya kitaifa yenye jukumu la kulinda, kukuza na kutetea haki za binadamu imefanya jitihada mbalimbali kuhakikisha kuwa wazee wanapata haki zao. Jitihada hizo ni pamoja na:
i)      Kushughulikia malalamiko yanayohusu uvunjifu wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora kwa wastaafu hasa katika suala linalohusu mapunjo na wastaafu kutolipwa stahiki zao kwa wakati.

ii)     Tume imekuwa ikitoa elimu ya haki za binadamu ikiwemo haki za wazee kwa viongozi wa ngazi mbalimbali ikiwemo taasisi za serikali, asasi za kiraia na wadau mbalimbali wa haki za binadamu na umma kwa ujumla.

iii)   Tume imeshiriki kikamilifu katika mchakato wa kutunga sheria ya wazee kwa kutoa maoni yanayohakikisha kuwa haki za wazee zinalindwa na kuhifadhiwa. Pia inashiriki katika mchakato wa mpango wa pensheni jamii.

iv)   Tume imetoa matamko mbalimbali kulaani mauaji ya wananchi wakiwemo wazee yanayotokea katika maeneo mbalimbali nchini.

Tume inapongeza sana jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya awamu ya tano katika kushughulikia masuala ya wazee. Jitihada hizo ni pamoja na:
i)        Kuimarisha Wizara inayoshughulikia masuala ya wazee kwa kutaja neno “wazee” katika jina la Wizara.

ii)       Kuimarisha huduma za afya kwa kuongeza bajeti ya Afya inayoiwezesha Serikali kununua dawa na vifaa tiba kwa wakati.

iii)      Kuweka madirisha ya wazee katika hospitali na vituo vya afya.

iv)     Kuanzisha mchakato wa mfuko wa Afya ya jamii.

v)       Kuanzisha mchakato wa malipo ya pensheni kwa wazee wote.

vi)     Kuanzisha mchakato wa kupambana na mauaji ya wazee.

vii)    Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) imeanzisha mpango wa malipo ya pensheni jamii kwa wazee wenye umri  wa miaka 70+.

viii)   SMZ pia imo katika mchakato wa kutoa vitambulisho maalum kwa wazee vitakavyowawezesha kupata huduma mbalimbali.

ix)     SMZ imeimarisha huduma za wazee kwa kuanzisha idara ya wazee.

Pamoja na jitihada ambazo zimefanywa na Serikali, Tume, Asasi za Kiraia, Mikataba, Maazimio na Itifaki za kikanda na kimataifa, bado wazee wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo kimsingi huvunja haki. Changamoto hizo ni pamoja na:
i)     Ukosefu wa Sheria maalum inayoweka ulinzi na kuzitambua haki za wazee.

ii)    Wazee walio wengi kutofaidika na mafao mbalimbali ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (Pensheni jamii) licha ya kwamba maendeleo yaliyofikiwa na nchi hii ni matokeo ya mchango wa wazee kwa kazi zao walizofanya.

iii)  Umaskini wa kipato miongoni mwa wazee.

iv)  Usalama mdogo kwa wazee kutokana na ukatili na manyanyaso wanayofanyiwa, hususani vitendo vya unyanyasaji kwa wanawake, walemavu na mauaji ya wazee kutokana na imani potofu. Kwa mfano, takwimu za Wizara ya Mambo ya Ndani (2016) zinaonyesha kuwa wazee wameendelea kuuawa katika sehemu mbalimbali nchini. Kwa mfano, mwaka 2014 waliuawa wazee 557, mwaka  2015 wazee 190 na katika kipindi cha mwezi  Januari hadi Oktoba 2016 wazee 119 waliuawa. Mikoa  inayoongoza kwa mauaji  ya wazee kwa kipindi cha Julai 2015 hadi Machi 2016 ni: Tabora (49), Shinyanga (17), Mbeya (15), Geita (11), Rukwa (9), Njombe (9) na Simiyu (7).

Kutokana na changamoto hizo, na ili kuhakikisha kuwa haki za wazee zinalindwa, zinadumishwa, zinakuzwa na kuendelezwa, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inatoa mapendekezo yafuatayo kwa Serikali, wadau na jamii kwa ujumla:
i)        Elimu ya haki za binadamu na misingi ya utawala bora itolewe kwa wananchi wote. Hii itasaidia katika kujenga jamii inayoheshimu haki za binadamu nchini.

ii)       Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikamilishe kutunga Sheria ya Wazee ili kurahisisha utekelezaji wa Sera ya Wazee ya mwaka 2003.

iii)      Serikali iendelee kuboresha huduma za afya na zitolewe bure kwa wazee wote, ikiwa ni pamoja na kukamilisha mpango wa afya ya jamii.

iv)     Serikali ikamilishe mpango wa malipo ya pensheni jamii (Social Pension) kwa wazee wote.

v)       Serikali kupitia vyombo vya ulinzi na usalama ihakikishe panakuwepo ulinzi madhubuti kwa wazee ikiwa ni pamoja na kuwakamata wahusika wa mauaji ya wazee na kuwafikisha katika vyombo vya dola kwa wakati na jamii ijitokeze kutoa ushahidi.

vi)     Kamati za ulinzi za Kata na Vijiji ziimarishwe ili kulinda maisha ya wazee.

vii)    Kupitia mkakati wa kunusuru kaya maskini unaosimamiwa na TASAF, kipaumbele kitolewe kwa wazee kote nchini.

viii)   Mabaraza ya wazee yaanzishwe na kuimarishwa ili kutoa nafasi ya ushirikishwaji wa wazee katika maendeleo ya nchi.

Mwisho, Tume inatoa rai kwa Serikali na wananchi wote kwa ujumla kulinda na kutetea haki za wazee. Aidha, tuthamini mchango, uzoefu na ushiriki wa wazee kwa maendeleo ya taifa.

“Uzee na kuzeeka havikwepeki”

Imetolewa na: 
Iddi Ramadhani Mapuri
Makamu Mwenyekiti 
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA 

Oktoba 1, 2017

No comments:

Post a Comment