Tuesday, September 26

Mwigulu ‘awagomea’ Chadema



Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba

Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba 
Singida. Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba amesema hakuna haja ya kuanza kuhangaika kutafuta wachunguzi kutoka nje kwa ajili ya kufuatilia wahusika wa shambulizi la Mbunge wa Singida Mashariki(Chadema), Tundu Lissu kwa vile vyombo vya ulinzi na usalama nchini vinajitosheleza na vina weledi na kazi hiyo.
Waziri huyo amesema haoni kwa nini baadhi ya watu wanasisitiza kuletwa kwa wataalamu wa nje kwani hata kama wataletwa bado watalazimika kufanya kazi kwa mazingira ya Kitanzania wakitumia wataalamu waliopo na hata ikiwekezana watahukumiwa kwa kutumia sheria za nchini.
“Nchi yetu inajitegemea hakuna haja ya kuleta vyombo vya nje kufanya uchunguzi...upelelezi utafanywa na vyombo vyetu, watafikishwa katika vyombo vya muhumu na watahukumiwa na watoto wetu,” alisema.
Hivi karibuni Chadema ilitaka wachunguzi nje kuendesha upelelezi kuhusiana na tukio la kushambuliwa kwa Lissu ikidai kuwa hatua yake hiyo haimaanishi kuwa vyombo vya ulinzi na usalama havina uwezo bali vimetuhumiwa katika tukio hilo.
Hata hivyo, Waziri Nchemba alisisitiza kuwa vyombo vya ulinzi na usalama daima viko macho na vinaendelea na kazi ya kuwasaka wale wote wanaojihusisha na matukio ya kushambulia watu.
Amesema suala la uchunguzi haliwezi kukamilika kwa siku moja akitolea mfano jinsi Marekani ilivyotumia muda mwingi kumsaka mtuhumiwa wa ugaidi, Osama bin Laden aliyekuwa kiongozi wa kundi la Al Qaida.
“Uchunguzi hauna ukomo...unaisha pale tu wanapokamatwa wahusika wote lakini vinginevyo uchunguzi hauishi maana hata Marekani walimtafuta Osama kwa muda mrefu sana hawakusema sasa tumesitisha kumsaka,” amesema.
Kiongozi huyo wa Al Qaida aliuawa Mei 2, 2011 na vikosi vya Marekani vilivyoendesha operesheni maalumu iliyoratibiwa kutoka Pentagon na kufuatiliwa kwa karibu na Rais Barack Obama ambaye hivi sasa amestaafu.
Osama alikuwa amejichimbia katika maficho yake nchini Pakistan katika eneo lililojulikana Abbottabad.
Waziri Nchemba aliwatumia salamu wale wanaojulikana kama ‘watu wasiojulikana’ akisema kasumba ya wahalifu wachache kufanya mauaji na kisha kujinadi kwa jina la watu wasiojulikana inaelekea ukingoni.
Ameeleza kuwa dakika za wale wanaojihusisha na uhalifu huo kufikishwa kwenye mkono wa sheria zinahesabika.

No comments:

Post a Comment