Friday, September 1

MKEMIA MKUU WA SERIKALI: HUDUMA ZETU ZINAPATIKANA KOTE NCHINI

Na. Georgina Misama – MAELEZO

Serikali kupitia Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali inafanya maboresho katika maabara zake za kanda zilizopo kote nchini ili kusogeza huduma hiyo kwa wananchi.

Akiongea na waandishi wa habari leo Jijini Dar es salaam, Kaimu Meneja Masoko, Mawasiliano na Huduma kwa Wateja kutoka Mamlaka hiyo Cletus Mnzava alisema kwamba Mamlaka inafanya maboresho katika Ofisi zake za kanda kwa kuboresha miundombinu na kuzipatia vifaa vya maabara vya kisasa.“Lengo kuu la kuimarisha Maabara zetu za kanda ni kusogeza huduma karibu na wananchi kote nchini ili kuwaondolea ulazima wa kuja kufuata baadhi ya huduma kwenye ofisi zetu za Dar es salaam”. Alisema Mnzava

Mnzava amesema sehemu ya maboresho hayo ni pamoja na kujenga majengo ya kudumu ya Ofisi za Mamlaka katika kanda ili kuwekeza katika mitambo ya kisasa na ya kudumu. Aidha, ujenzi wa jengo la Ofisi za Kanda za Nyanda za Juu Kusini unatarajiwa kukamilika mwaka huu wa fedha.

Akizitaja Ofisi hizo za kanda Mnzava anasema kuna kanda ya Ziwa ambayo inahudumia mikoa ya Mwanza, Bukoba, Simiyu, Mara, Shinyanga, Geita na Kigoma, na kanda ya Kaskazini kwa ajili ya mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Tanga na Manyara. Kwa mikoa ya Dodoma, Singida, Morogoro, Tabora na Iringa inahudumiwa na ofisi za Kanda ya Kati, wakati Kanda ya Mashariki ni kwa ajili ya Mikoa ya Dar es salaam na Pwani.

Vilevile kuna Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kwa ajili ya Mikoa ya Mbeya, Katavi, Songwe, na Rukwa na Kanda ya Kusini kwa ajili ya kuhudumia mikoa ya Lindi, Mtwara na Songea.Mamlaka pia imejipanga kuanzisha Maabara yenye vifaa vya kisasa kwa kanda ambazo bado hazina maabara hizo ili kutoa huduma kwa weledi na ufanisi kulingana na mahitaji ya eneo husika.

Mzava anasema ili kuendana na kasi ya Serikali ya awamu ya tano, Mamlaka imeimarisha shughuli zake za ukaguzi kwa mipaka yote nchini, ambapo kwa mipaka mikubwa kama vile Namanga na Tunduma huduma hizo za ukaguzi hutolewa kwa masaa 24.

Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali inawaasa watanzania kujenga utamaduni wa kuzitumia Ofisi zake za Kanda kwa lengo la kufanya kazi zinazoweza kufanyika kwa haraka kwenye Kanda husika badala ya kutegemea zaidi Maabara zilizoko Ofisi za Dar es salaam.

Kaimu Meneja Masoko, Mawasiliano na Huduma kwa Wateja wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemi Mkuu wa Serikali Bw.Cletus Mnzava akiwasomea Waandishi wa Habari (hawapo pichani) baadhi ya mikakati ya mamlaka ya hiyo kuhusu uimarishwaji wa ofisi zao hapa nchini, kulia ni Afisa Mawasiliano wa Mamlaka hiyo Bw. Silvester Omary katika mkutano uliofanyika katika ukumbI wa Idara ya Habari (MAELEZO) Jijini Dar es Salaam leo.
Kaimu Meneja Masoko, Mawasiliano na Huduma kwa Wateja wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemi Mkuu wa Serikali Bw.Cletus Mnzava akisisitiza jambo kwa Waandishi wa Habari( hawapo pichani) katika mkutano wa mamlaka hiyo katika ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) leo Jijini Dar es Salaam .
Baadhi ya Waandishi wa Habari wakifuatilia mkutano wa Kaimu Meneja Masoko, Mawasiliano na Huduma kwa Wateja wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemi Mkuu wa Serikali Bw.Cletus Mnzava katika mkutano wa Mamlaka hiyo ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) leo Jijini Dar es Salaam.
Picha na: Paschal Dotto(31.08.2017

No comments:

Post a Comment