Sunday, September 17

MAJAJI NCHINI WAAGIZWA KUMALIZA MLUNDIKANO WA MASHAURI IFIKAPO DESEMBA 15, 2017

Majaji nchini wameagizwa kumaliza kesi zote za muda mrefu Mahakamani ifikapo Disemba 15, mwaka huu ili kuendana na azma ya Mahakama ya kutoa haki  kwa wote na kwa wakati.
Akizungumza katika Mkutano wa Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Jaji Kiongozi Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Ferdinand Wambali alisema kuwa Kanda zote za Mahakama Kuu nchini tayari zimeshaainisha idadi ya kesi zote za kuanzia miaka miwili kuendelea (kesi za mlundikano) ambazo zitafanyiwa kazi.
“Nawaagiza Majaji wote nchini kuendelea na zoezi la kusikiliza kesi hususani kesi za muda mrefu Mahakamani, na zoezi hili lianze kufanyika Oktoba 16,mwaka huu na kazi hii nataka ikamilike kufikia Desemba 15,mwaka huu,” alisisitiza.
Mhe.Jaji Kiongozi amezitaja Kanda za Mahakama Kuu ambazo zinaonekana kuelemewa na mzigo wa mashauri kuandaa orodha ya mashauri ‘causelist’wanayohitaji kusaidiwa.
Mahakama hizo ni Mahakama Kuu-Kanda ya Dar es Salaam, Mahakama Kuu-Kanda ya Mwanza, Mahakama Kuu-Kanda ya Bukoba, Mahakama Kuu-Kanda ya Mbeya, Mahakama Kuu-Kanda ya Shinyanga, Mahakama Kuu-Divisheni ya Ardhi na Mahakama Kuu-Divisheni ya Kazi.
Aidha Mhe. Wambali ameagiza zoezi hilo lifanyike ndani ya wiki moja kuanzia Jumatatu, Septemba 18 ili kuwezesha kujua uhitaji wa msaada wa Majaji wengine kutoka Kanda nyingine watakaoenda kusaidia kusikiliza na kumaliza mashauri hayo katika maeneo tajwa.
Aidha Mhe. Jaji Kiongozi amewataka Majaji Wafawidhi kuitisha vikao na Wadau wa Mahakama ili waweze kujua juu ya kuwepo kwa Programu maalum ya kusikiliza na kumaliza kesi zote za muda mrefu Mahakamani.
Kwa upande wake Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahimu Hamis Juma amewataka Majaji na Watumishi wa Mahakama kwa ujumla kufanya kazi kwa kuzingatia nguzo tatu za Mpango Mkakati wa Mahakama ili kutekeleza majukumu kimkakati na hatimaye kupata matokeo chanya.
“Majaji Wafawidhi ni nguzo muhimu katika utekelezaji wa Mpango Mkakati hususani katika nguzo namba mbili ambayo ni Upatikanaji na utoaji wa Haki kwa wakati, kupitia Majaji na Mahakimu waliopo chini yao” alisema Mhe. Jaji Mkuu.
Akiongelea juu ya jukumu kuu la utoaji haki nchini, Mhe. Jaji Mkuu amesisitiza juu ya kuwa na kumbukumbu sahihi ya takwimu za mashauri zilizopo katika Mahakama husika hali ambayo itawezesha kujua ni msaada utakaohitaji, bajeti na kadhalika.
Kwa upande mwingine Mhe. Jaji Mkuu amesisitiza juu ya matumizi ya TEHAMA katika uendeshaji wa kesi ili kuendeana na kasi ya Teknolojia hali ambayo itawezesha huduma ya haki kuwafikia wananchi kwa wakati.
Mambo mengine aliyoyasisitiza Mhe. Jaji Mkuu alipokuwa akifunga Mkutano wa Majaji Wafawidhi ni pamoja na ufanyaji kazi kwa ushirikiano kwa Watumishi wote wa Mahakama na kubadili mtazamo hasi ‘change of attitude’ na kuzingatia maadili katika utendaji kazi.
Mkutano wa Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, uliofanyika kwa siku mbili (2), Septemba 15&16 ni mwendelezo wa Vikao mbalimbali ambavyo vimekuwa vikifanyika mara kwa mara vyote vikiwa na lengo la kuhakikisha kuwa azma ya Mahakama ya Tanzania ya kutoa haki kwa wakati inaonekana kutekelezeka.
 Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akitoa neno alipokuwa akifunga Mkutano wa Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa-AICC jijini Arusha, Septemba, 15 na 16, 2017. 
 Sehemu ya Waheshimiwa Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu nchini wakimsikiliza kwa makini Mhe. Jaji Mkuu (hayupo pichani) 
Waheshimiwa Majaji Wafawidhi pamoja na Wasajili wakiwa katika Mkutano huo uliokamilika Septemba 16, 2017
 Waheshimiwa Majaji Wafawidhi pamoja na Wasajili wakiwa katika Mkutano huo uliokamilika Septemba 16, 2017
 Mtendaji Mkuu-Mahakama ya Tanzania,Mhe. Hussein Kattanga akitoa neno, akisisitiza juu ya ufanyaji kazi kwa malengo.
 Jaji Kiongozi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Ferdinand Wambali akiongea katika Mkutano wa Majaji Wafawidhi
 Mkuu wa Kitengo cha Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama,Mhe.Zahra Maruma akitoa mara ya utekelezaji wa kazi mbalimbali za Mradi mbele ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania mara baada ya kuhitimisha kikao cha siku mbili cha kujadili juu ya mikakati ya kuondosha mashauri ya muda mrefu Mahakamani. aliyeketi katikati ni Jaji Mkuu wa Tanzania,Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Ferdinand Wambali, wa kwanza kushotoni Jaji Mfawidhi, Mahakama Kuu-Kanda ya Iringa pia ni Jaji namba moja wa Mahakama Kuu ya Tanzania, wa pili kulia ni Kaimu Jaji Mfawidhi,Mahakama Kuu, Kanda ya Arusha, Mhe. Sekela Moshi na wa kwanza kulia ni Mtendaji Mkuu-Mahakama ya Tanzania, Mhe. Hussein Kattanga.Picha na Habari na Mary Gwera wa Mahakama

No comments:

Post a Comment