Thursday, September 28

Jaji Manento: Nimeamua kukaa kimya kwa sababu ni mstaafu

Mwenyekiti mstaafu wa Tume ya Haki za Binadamu

Mwenyekiti mstaafu wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Jaji Amiri Manento 
Dar es Salaam. Mwenyekiti mstaafu wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Jaji Amiri Manento amesema asingependa kuwa mzungumzaji katika vyombo vya habari.
Jaji Manento amesema ameamua kukaa kimya kwa sababu yeye ni mstaafu katika nafasi yake.
Kauli hiyo ameitoa siku chache baada ya Rais John Magufuli kuwapiga kijembe wastaafu, akisema kuna baadhi yao wanaowashwa washwa kuzungumza kwenye vyombo vya habari.
"Ujumbe uliotumwa kwangu (kuwa mgeni rasmi) sijui niliuonea aibu... nikakubali lakini nilikuwa nimeamua nisiongee siku hizi sababu mimi ni mstaafu," amesema Jaji Manento leo Alhamisi jijini hapa wakati wa mkutano wa siku ya kimataifa ya kupata taarifa.
Hata hivyo, amewataka watendaji wa Serikali kuhakikisha kanuni za Sheria ya Haki ya Kupata Taarifa ya 2016 zinapatikana mapema ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa kwa wananchi.
"Haki ya kupata taarifa ni haki inayotakiwa kulindwa kwa nguvu zote, ni kiashiria kimojawapo cha Serikali yenye uwazi, kwa hiyo watendaji wa serikali wahakikishe wanashiriki kufanikisha uandaaji wa kanuni za sheria hiyo ili isaidie kuongeza uwazi na uwajibikaji," amesema.

No comments:

Post a Comment