Saturday, September 30

DC WA KAKONKO KANALI NDAGALA APIGA MARUFUKU UNYANYASAJI KWA WAZEE,KUWATUHUMU WANAZUIA MVUA



MKUU wa Wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala amewaagiza Wananchi wa Wilaya ya Kakonko kuacha tabia ya kuwatuhumu baadhi ya wazee kuwa Wanazuia Mvua na kutaka kuwaondoa ikiwa ni pamoja na kuwauwa kwa kwa imani za kishirikina , na vikundi vitakavyo gundulika vinawatuhumu watachukuliwa hatua ili kukomesha vitendo hivyo.

Akizungumza na Wananchi jana katika maadhimisho ya siku yaWazee Wilayani humo katika kijiji cha Kasanda ,Ndagala alisema kumekuwa na tabia ya Wananchi wengi kuwatuhumu baadhi ya wazee kuwa wanazuia mvua, jambo ambalo ni imani za kizamani na zilizopitwa na wakati.
 
 "Kwa hiyo mimi nawaomba tuendelee kushirikiana na wazee wetu hawa kwa kuwa pia wana mchango wao mkubwa katika jamii,ni vyema tukawafanya wazee wetu waishi kwa amani na kuachana na imani hizo zinazoweza kuleta chuki na uhasama mkubwa baina yetu",alisema Ndagala.

Alisema vitendo kama hivyo vilijitokeza mwaka jana, baadhi ya wazee walitaka kuuwawa kwa tuhuma hizo,aliema na kuongeza kuwa imani hizo zinapaswa kupuuzwa kwani zinaweza kuchochea uvunjifu wa amani Kwa Wazee hao ambao ni hadhina kubwa kwa jamii. 
 
"Niwaombe wananchi mshirikiane na Wazee waliopo katika maeneo yenu, tumeona mchango wao ni mkubwa sana katika jamii na Taifa kwa ujumla Kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ni thamini mchango wa wazee kwa maendeleo ya Nchi yetu, na serikali inalitambua hilo ndio maana inatoa kipaumbele kwa Wazee kwa kuhakikisha wanakuwa na Afya njema kwa kupatiwa matibabu bure kutokana na mchango wao", alisema Ndagala.
 
Aidha Ndagala alimuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kuandaa watumishi watakao kuwa wakishughulikia masuala ya Wazee na kuhakikisha jamii ina tambua na kuthamini mchango wa wazee na kuihamasisha jamii kutambua umuhimu wa wazee na kuihamasisha jamii kuwathamini wazee na kuwapenda kwa kuweka mipango shirikishi kwa wazee na jamii ilikuweka usawa kati yao.

Alieleza kuwa Serikali inaendelea kuwajali wazee kwa kutoa huduma ya afya bure,Wilaya imeamua kuwatambua wazee na kutoa huduma za Afya bure kwa wazee 1700 wamepatiwa vitambulisho vya msamaa vya matibabu vya muda na kumuagiza Mkurugenzi kuandaa utaratibu mzuri wa wazee kupatiwa vitambulisho vy a kudumu.

Nao Wazee hao katika risala yao iliyo wasilishwa na Mwenyekiti wa chama cha wazee Wilaya ya Kakonko Mbonipa Kisama, waliishukuru Serikali ya awamu ta tano kwa kutambua umuhimu wa wazee na kuwapa kipaumbele kwakuwapatia matibabu bure na kuiomba serikali kuanza kutoa petion jamii waliyo ahidiwa kwa muda mrefu kwa Wazee iliwaweze kufanya shughuli ndogo ndogo za kujikimu katika kipindi hicho na kuondolewa tozo za kijamii kwa wazee.

Alisema Wazee wanamahitaji yao ya ziada iliwaweze kuishi bila wasiwasi wilaya ina wazee 7103 ambapo wazee wanawake ni 3135 na wanaume ni 3975 ambao ni Wanachama wa chama cha Wazee ambapo kupitia chama hicho serikali imeweza kitumia Wadau kufanya sensa ya kuwatambua wazee na mahitaji yao na kuweza kutoa msaada kwa Wazee wasio jiweza.

Aidha Wazee hao waliyashukuru mashirika ya Help age international na shirika la TCRS kwa kutoa misaada kwa wazee wasio jiweza na kuomba kuendelezwa kwa misaada ya kisheria na haki za wazee kuishi na kutoa mchango wa huduma za kijamii kwa Wazee na wanaamini maombi waliyatoa serikali itatue changamoto hizo ilikuondokana na changamoto hizo.

Hata hivyo katika maadhimisho hayo yaliadhimishwa kwa Wazee kucheza michezo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mpira wa miguu, uvutaji wa kamba na ukimbizwaji wa kuku ambapo mshindi alikabidhiwa mbuzi na kiasi cha shilingi 20,000/= na Mkuu huyo kuomba michezo hiyo kwa wazee kuendelezwa katika kila kata ili kuimarisha Afya za wazee hao .
 Baadhi ya Wazee wakifuatilia yaliyokuwa yakijiri kwenye maadhimisho hayo
 Mkuu Wawilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala akikabidhi zawadi ya Mbuzi kwa timu ya wazee wa kijiji cha Kasanda iliyofanya vizuri katika michezo wakati wa maadhimisho hayo ya Wazee.
  MKUU wa Wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala akikabizi vitambulisho vya matibabu kwa baadhi ya wazee wilayani Kakonko.
  MKUU wa Wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala akikabizi vitambulisho vya matibabu kwa baadhi ya wazee wilayani Kakonko.
 Baadhi ya wazee wakicheza ngoma katika maadhimisho ya siku ya wazee.

No comments:

Post a Comment