Wednesday, August 23

Nyumba ya Lissu kupekuliwa tena


Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje wa Chadema, John Mrema amesema polisi wamemchukua mwanasheria mkuu wa chama hicho, Tundu Lissu na kwenda naye nyumbani kwake kwa ajili ya kumpekua.
Msafara wa magari ya maofisa wa Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam umeongozana na Lissu ambaye ni mbunge wa Singida Mashariki na mawakili wake.
"Wamemchukua hapo kituoni na kuelekea naye hadi nyumbani, lengo ni kumkagua.Mawakili wanaomsaidia Lissu wameshaondoka muda huu ili kujua ni kitu gani atapekuliwa," amesema Mrema.
Kaimu Kamanda wa Polisi, Kanda Maalum Lucas Mkondya alipotakiwa kuzungumzia taarifa hizo alikata simu baada ya kuulizwa kuhusu upekuzi huo.
Jana  Agosti 22,Lissu alinyimwa dhamana baada ya kukamatwa kwa tuhuma za kumkashifu Rais John  Magufuli na uchochezi.
Hii ni mara ya pili maofisa wa Jeshi la Polisi kwenda kumpekua Lissu nyumbani kwake ikiwa ni ndani ya wiki kadhaa.
Julai 21, mwaka huu Chadema inasema Polisi ilimpekua Lissu nyumbani kwake na kuchukua CD 6 zinazohusiana na utafiti alioufanya mwaka 1999 katika sakata la mgodi wa Bulyanhulu.

No comments:

Post a Comment