Monday, August 7

Mbunge kuwajengea wajane nyumba za kudumu Kibiti


 Mbunge wa Kibiti Ally Seif Ungando anatarajia kuanza ujenzi wa nyumba za kudumu kwa wajane wote waishio wilayani Kibiti ambao waume zao wameuwa kwa kupigwa risasi na watu waliokuwa wakifanya mauaji kwa viongozi wa Serikali za vitongoji na vijiji, na wana Chama Cha Mapinduzi.
Hayo ameyazungumza jana kwenye ofsi ya Mkuu wa Wilaya Kibiti,alipokuwa akizungumza na viongozi wa Dini na Wazee juu ya kufanya Kongamano la kuzidi kuiombea Wilaya ya Kibiti iwe na amani.
Ungando amesema mbali na kujenga nyumba hizo,pia atawasomesha watoto wote wa marehemu ambao wameuawa kwa kupigwa risasi kuanzia Mwezi May 2016 hadi sasa.
Amesema tayari ameanza kuwasiliana na wadau mbalimbali ili kumsaidia ujenzi huo kwa kuwa watu waliouawa hawakuwa na makosa yoyote.
Ungando,ambaye ameonekana kuguswa na mauaji yaliyotokea mara kwa mara wilayani hapo kwa nyakati kadhaa alijikuta akitokwa na machozi katika mkutano huo hali iliyoelezwa na baadhi ya Wazee kuwa mauaji hayo yamemuumiza sana.
Amesema kila alipokuwa akifika kwenye maziko ya viongozi wa Serikali za Mitaa au ya mwanachama wa chama cha Mapinduzi aliyeuawa kwa kupigwa risasi alikuwa akiumia sana moyoni mwake hali iliyomfanya kushindwa kuzungumza chochote kutokana na kuwa na machungu mengi moyoni mwake.
"Kila nilipokuwa nakwenda kwenye Msiba wa kiongozi wa Serikali za Mitaa au msiba wa mwanachama wa chama cha Mapinduzi na kwenye maeneo yalipotokea mauaji ya Polisi moyo wangu ulikuwa ukiumia hali iliyokuwa ikisababisha kushindwa kuzungumza" amesema.
Akizungumza katika Kikao hicho Sheikh Mkuu wa Wilaya ya Kibiti Juma Mlindo alisema kwa sasa ni wakati muafaka kwa wananchi wote kushikamana pamoja na kuiombea dua wilaya hii irejee kwenye hali yake ya usalama na Utulivu pamoja na wilaya za Rufiji na Mkuranga.
Mlindo amesema wao kama viongozi wa Dini mara kadhaa wamekuwa wakiiombea wilaya hii Dua,ili Mwenyezi Mungu aweze kurejesha hali ya utulivu kama hapo awali.
Mmoja wa wajane ambaye alifiwa na mumewe mwaka jana,bi Mwajuma Mustafa alisema hatua hiyo ya kujengewa nyumba na watoto wao kusomeshwa na Mbunge itakuwa faraja kwao.
Amesema msaada huo utawawezesha waishi katika nyumba zilizo salama wakiwa na watoto wao kwa kuwa wengi wa wajane ambao waume zao waliuawa kwa kupigwa risasi wamelazimika kurudi kwao wakiwa na watoto,huku wakiwa hawapati msaada toka kwa ndugu wa waume zao.
Mwajuma ambaye mumewe alikuwa ni Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nyang'undu kilichopo katika kijiji cha Nyambunda aliuawa Desemba 6,2016 kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana akiwa njiani akirejea kwake.

No comments:

Post a Comment