Wednesday, June 28

TAKUKURU YAENDELEA KUWASHIKILIA RAIS WA TFF MALINZI NA KATIBU WAKE MWESIGWA


Na Zainab Nyamka-Globu ya Jamii.
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imethibitisha kuwashikilia Rais wa TFF Jamal Malinzi na Katibu Mkuu wake Selestine Mwesigwa kwa mahojiano.
Afisa uhusiano wa TAKUKURU Musa Misalaba amesema, ni kweli wanawashikilia viongozi wa TFF kwa ajili ya mahojiano ambapo wamekuwa wakifanya uchunguzi kwa muda mrefu kabla ya kuamua kuwashikilia kwa ajili ya mahojiano.
“Ni kweli kwamba tunaendelea na uchunguzi dhidi ya viongozi mbalimbali wa TFF na uchunguzi huo tumekuwa nao kwa muda mrefu lakini kuhusu kuwashikilia kwa nini, bado ni siri yetu upande wa uchunguzi, katika uchunguzi tunaongozwa na misingi ya sheria, kanuni na taratibu hatuwezi tukaweka wazi kila jambo.”

Misalaba amesema kuwa Jambo la msingi ambalo wananchi wanatakiwa kuelewa ni kwamba, kuna uchunguzi ambao wanaendelea nao ambao umekuwa ukifanywa kwa muda mrefu na kuhusiana kuwashikilia Malinzi na Mwesigwa wamesema muda wa uchunguzi ukikamilika watawapeleka mahakamani.
“Tunawashikilia na bado tuko nao chini ya ulinzi wetu , tunaongozwa na sheria tutakapomaliza uchunguzi wetu tutaweka wazi kama ni kuwaachia ila ushahidi ndio utakaoamua lakini ni lini ni swala kiuchiunguzi, lakini ni siri ya uchunguzi.”
Hivi karibuni gazeti la Nipashe liliandika mfululizo wa makala zilizokuwa zikielezea tuhuma za ufisadi zilielekezwa kwa Malinzi na viongozi wenzake wa TFF.

Rais wa TFF Jamal Malinzi na Katibu Mkuu wake Selestine Mwesigwa.

No comments:

Post a Comment