Sunday, January 29

Madaktari wawagomea mawaziri mkutanoni


SAKATA la madaktari nchini linazidi kuchukua sura mpya baada ya wataalamu hao kukataa hoja za ujumbe wa Serikali ulioongozwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi, Hawa Ghasia huku wakigoma kusikiliza kauli yoyote kutoka kwa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk Hadji Mponda

Wakati mawaziri hao wakikumbwa ana tafrani hiyo tayari wauguzi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na ile ya Mkoa wa Dodoma wametishia kusitisha utoaji huduma ifikapo Jumatatu kama masuala yao hayajapatiwa ufumbuzi.

Vigogo wa Serikali waliofika kukutana na madaktari hao jana ni Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hadji Mponda na naibu wake, Dk Lucy Nkya, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Blandina Nyoni, Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Deo Mtasiwa.
Tukio hilo lilitokea jana kwenye Ukumbi wa Hoteli ya Star Light, Jijini Dar es Salaam ambako madaktari hao walikusanyika na baadaye kupewa taarifa kuwa kuna ujumbe wa Serikali utafika kwa majadiliano. Madaktari hao waliwatimua ujumbe huo baada ya kuusikiliza juu ya wito wao wa kuwataka wasitishe mgomo ili wafungue ukurasa wa majadiliano, wakajibiwa kuwa kwa sasa ni wakati wa kutekeleza kwa vitendo na siyo ahadi.

Ujumbe huo wa Serikali uliwasili ukumbini hapo majira ya mchana na kukaribishwa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Stephen Ulimboka ambaye baada ya kuwawekea viti pembeni mwa jukwaa kuu, aliwatambulisha kwa washiriki. “Ugeni tuliokuwa tunasubiri umefika, si rahisi sisi wote kuwafahamu ni vema wangejitambulisha wao kwa majina kisha tuendelee na utaratibu tuliojiwekea,” alisema Dk Ulimboka.

Mara baada ya kauli hiyo, wageni hao walianza kujitambulisha. Wa kwanza alikuwa Waziri Ghasia aliyewasalimia madaktari hao na kujitambulisha kisha kueleza kuwa aliongoza ujumbe huo kuwasilisha taarifa ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Dalili mbaya kwa ujumbe huo, zilianza kujitokeza walipoitika kwa nguvu salamu ya Waziri Ghasia huku wakiwanyamazia Waziri wa Afya na maofisa waandamizi wa wizara hiyo.

Baada ya tukio hilo kumalizika, Dk Ulimboka alitoa taratibu za mkutano kuwa ni kusoma taarifa maalumu iliyoandaliwa kwa ajili ya kupelekwa kwa Waziri Mkuu. “Sisi hapa tutawakabidhi taarifa iliyoandaliwa na madaktari ambayo ni maalumu kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda na baada ya kuwasomea, tutawakabidhi kisha tusubiri majibu ya taarifa yetu tukiwa hapahapa,” alisema Dk Ulimboka.

Dk Ulimboka alisoma taarifa hiyo mbele ya wageni hao ambayo ilitaja madai yao kadhaa ikiwemo kumtaka Waziri Ghasia kumshauri Rais Jakaya Kikwete kuwaondoa katika wizara hiyo, Waziri Mponda na naibu wake Dk Nkya, Katibu Nyoni na Mganga Mkuu, Dk Mtasiwa.

Mara baada ya kusoma taarifa hiyo alikabidhi barua hiyo kwa Waziri Ghasia huku akisisitiza kuwa wataendelea na mgomo hadi watakapopatiwa majibu ya hoja zao.

“Tunaomba taarifa hiyo imfikie haraka Waziri Mkuu, ijadiliwe kwa haraka na kutoa majibu yatakayotupatia ufumbuzi ili nasi turudi kazini tukaokoe maisha ya Watanzania,” alisema Dk Ulimboka ambaye kwa kauli yake iliashiria kufunga mjadala.

Baada ya kauli hiyo, Waziri Ghasia alisimama na kueleza kuwa wao walifika wakiwa na ujumbe toka kwa Waziri Mkuu hivyo ni vema wangekubaliwa wauwasilishe ambapo alimtaja Waziri wa Afya Dk Mponda kuwa angeusoma.
Dk Ulimboka alijibu hoja hiyo akisema “Madaktari hatuna tatizo na ujumbe toka kwa waziri Mkuu Mizengo Pinda ila ujumbe kutolewa na Waziri wa Afya Dk Hadji Mponda hatukubali kwasababu hatuna imani naye labda kama kweli ni taarifa, ungesoma wewe,” alisema Dk Ulimboka na kukaa chini.

Waziri Ghasia alikubaliana na hoja hiyo na katika kuwasilisha taarifa hiyo, alisema alisononeshwa kusoma majibu yanayohusu madai ya madaktari hao kwa niaba ya waziri mwenye dhamana ya Wizara ya Afya wakati yeye (Dk Mponda) akiwepo.

Ghasia alisema wizara imetafakari kwa kina suala la madaktari waliokuwa kwenye mafunzo katika Hosptali ya Taifa ya Muhimbili na kuwarudisha kwenye kituo hicho cha kazi huku ikiahadi kuwalipa stahili zao.
“Wazira imetafakari kwa kina na imeamua kuwarejesha madaktari wote waliokuwa kwenye mafunzo ya vitendo katika Hosptali ya Taifa ya Muhimbili na wanatakiwa kuripoti katika vituo hivyo vya kazi kuanzia Jumatatu,” alisema Ghasia.

Kuhusu madai mengine, alisema Serikali itaendelea na majadiliano ya pamoja huku akiwaomba warejee kazini.
“Sisi tuwaombe tu kwamba madai yenu yote Serikali inayafanyia kazi. Suala la nyumba tayari tumeshapata fedha kutoka Global Fund kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za madaktari ili waweze kukaa karibu na vituo vyao vya kazi,” alisema Ghasia. Akijibu ombi la kuwataka warejee kazini, Dk Ulimboka alisema hilo litategemea majibu ya taarifa walioiwasilisha kwa Waziri Mkuu, ambapo alisisitiza kuwa wao wataendelea na mikutano katika ukumbi huo.

“Sisi tutaendelea na mikutano kujadili taarifa yenu na pia tungeshauri taarifa hii mtuletee kwa maandishi, lakini pia tunasubiri majibu ya taarifa yetu tuliyoiwasilisha kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda ambayo tumeitoa kwa maandishi,” alisema Dk Ulimboka. Dk Uliomboa aliwataka wawakilishi hao wa Serikali kutambua kuwa ujumbe haukuwa wa kushawishiana kurudi kazini bali ni wa kupeana taarifa.

Kauli hiyo iliashiria kwamba hoja ya ujumbe huo haina uzito wa kuwashawishi kuacha mgomo huku wakikataa hoja zao sasa kujadiliwa na wizara badala yake walisisitiza Waziri Mkuu kushughulikia suala hilo. Walimtaka Waziri Mkuu, kutoa majibu ya madai yao kwa wakati ili asiwafanye kufikia hatua ya kusitisha huduma katika vitengo vya dhararu.

“Mgomo huu unaendelea nchi nzima hadi majibu ya madai yetu tuliyowasilisha kwa Waziri Mkuu yamepatiwa majibu.
Tunashauri kazi hiyo ifanywe haraka vinginevyo tusije tukashawishika kusitisha huduma kwenye vitengo vya dharura,” alisema Ulimboka.

Tishio la mgomo zaidi
Wakati huo huo, Chama cha Wauguzi wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kimesema kuwa wauguzi wataendelea kutoa huduma kwa kusuasua hadi Jumatatu na kama suala hilo litakuwa halijapatiwa ufumbuzi, watasitisha huduma na kufunga hospitali.

“Sisi tutaendelea kutoa huduma katika mazingira ya shida hivi mpaka Jumatatu tu,” alisema Mwenyekiti wa chama hicho, Paul Magesa.

Habari kutoka katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma zilieleza pia kuwa, kwa sasa hakuna wagonjwa wapya wanaopokelewa na kuwa waliopo wodini wakitoka, hospitali hiyo nayo itasitisha kutoa huduma.

No comments:

Post a Comment