Thursday, November 16

Kikao chaitwa kuwajadili waliowalaza walimu nje

Buchosa. Siku moja baada ya walimu saba wa Shule ya Msingi Soswa kujikuta wamelala nje na kati yao wawili kunyolewa nywele kichwani na sehemu za siri, uongozi wa kisiwa cha Soswa umeitisha mkutano  wa hadhara kujadili suala hilo.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Soswa, Rafael Majura amesema mkutano huo utafanyika leo Alhamisi katika kisiwa hicho ambapo utahudhuriwa na wazee maarufu na viongozi wa Kata ya Bulyaheke.
Amesema mkutano huo utajadili  namna ya kukabiliana na tukio hilo ambalo limeleta taswira mbaya kwenye jamii na Taifa kwa ujumla.
“Tunategemea kuanza mkutano wa hadhara ili kujadilia suala hili ambalo limechafua taswira ya kisiwa hiki na kuleta hofu miongoni mwa walimu,” amesema Majura
Majura amesema tayari viongozi wa kata hiyo wakiongozwa na Mtendaji wa Kata ya Bulyaheke, Musa Mwilomba wamekwisha fika kwa ajili ya kikao hicho.
Mkazi wa kisiwa hicho, Mjura Magafu amesema  kitendo hicho kimeleta aibu kubwa na kwamba ni lazima waliofanya wapatikane na waadhibiwe.
“Na ikiwezekana tutapiga kura kuwabaini watu hao waliochafua taswira ya kisiwa chetu,” amesema Magafu.

Waziri Mkuu azuiwa kujibu maswali


Dodoma. Spika wa Bunge, Job Ndugai amemzuia  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kujibu maswali mawili ya papo kwa hapo kutoka kwa wabunge kwa sababu hayakuwa maswali ya kisera.
Spika amezuia  maswali ya wabunge Susan Lyimo wa Viti Maalum (Chadema) na Mbunge wa Karagwe (CCM), Innocent Bashungwa huku akimwambia Bashungwa kuwa hata swali lake lilikuwa halieleweki.
Hayo yamejitokeza leo Alhamisi wakati Majaliwa akijibu maswali ya papo kwa hapo kutoka kwa wabunge ikiwa ni utaratibu uliowekwa na Bunge kila siku ya Alhamisi asubuhi kabla ya kipindi cha maswali na majibu.
Katika swali lake kwa Waziri Mkuu, Lyimo alihoji kumekuwa na malalamiko  kutoka kwa watumishi wa umma ambao walistahili kupandishwa madaraja Novemba mwaka jana.
“Hapa nina barua iliyotoka kwa katibu mkuu utumishi juzi tu akisema watumishi 60,000 waliokuwa wapandishwe vyeo Juni, 2016 hawatapandishwa na badala yake watapandishwa Novemba mwaka huu,”
“Kwa maoni yangu naona watumishi hawa wameonewa sababu itakuwa na athari mwaka mzima hawa watu hawataingiziwa michango inayolingana na mishahara yao,” amesisitiza Lyimo..
Hata hivyo, kabla ya hajafikia hatua ya kuulizwa swali, Spika aliingilia kati na kusema “hayo ndio maswali ninayoyakataa. Mimi nataka uulize swali la kisera moja kwa moja. Swali linasemaje?
Huku akiendelea, Lyimo alihoji ni  kwa nini Serikali inawahujumu wafanyakazi wake na mbali na kuwahujumu akitaka kujua kwa nini inawapunguzia morali na kuhoji kama itawalipa fedha hizo.
Kabla ya kujibu Spika akasema, “Napata taabu kuliruhusu hilo swali. Kwa sababu linahusu barua ambayo siyo lazima waziri mkuu ameshaiona. Tunaendelea na swali linalofuata.”
Bashungwa katika swali lake ambalo nalo lilikataliwa amesema wakulima wa kahawa wanakabiliwa na changamoto ya kukopa fedha kutoka kwa madalali, katika kipindi cha kuandaa mashamba.
Amesema wakulima hutakiwa kulipa fedha hizo kipindi cha mavuno na wakati mwingine wakati kahawa ziko shambani na kutolea mfano wa Mkoa wa Kagera kwamba tatizo hilo ni changamoto kubwa.
“Je waziri mkuu, Serikali ipo tayari kuingilia kati kwa kuweka utaratibu kupitia benki ya wakulima ili kupata mikopo ya riba nafuu? Aliuliza Bashungwa na ndipo Spika akasema maneno yafuatayo;
“Mheshimiwa Bashungwa mpaka sasa hivi nakusikiliza sijajua swali lako ni nini. Mheshimiwa Bashungwa kaa chini. Tunaendelea.”

Kindamba azungumzia kubadilika kwa TTCL


Dar es Salaam. Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), Waziri Kindamba amesema mabadiliko ya sheria iliyounda kampuni hiyo na kuifanya kuwa shirika la umma kutaliimarisha shirika hilo na Serikali haitakuwa na woga wa kuweka mtaji.
Amesema sasa Serikali inamiliki kwa asilimia 100 kampuni hiyo baada ya kumlipa mbia mwenza ambaye alikuwa na hisa 35, Bharti Airtel ya India kiasi cha Sh14.7 bilioni na kujitoa katika umiliki wa kampuni hiyo ambayo ilibinafsishwa.
Akizungumzia muswada wa sheria uliopitishwa na bungeni juzi, Kindamba amesema sheria hiyo ya Shirika la Mawasiliano Tanzania italiwezesha shirika hilo kutengeneza faida ya kati ya Sh7 – 8 bilioni na kutekeleza majukumu yake mengine kwa mujibu wa sheria.
Mtendaji huyo amesema kabla ya kubinafsisha, shirika hilo lilikuwa likipeleka serikalini gawio la Sh1 bilioni lakini kwa zaidi ya miaka 15 baada ya kubinafsishwa halijawahi kupeleka gawio.  Amesisitiza kwamba mwaka huu wa 2017/18, TTCL itapeleka serikalini gawio la Sh1 bilioni.
“Miongoni  mwa mapungufu yaliyojitokeza kwenye sheria ya awali ni kuwa sheria hiyo ilililenga kuwezesha mazingira ya ubia ndani ya TTCL, hitaji ambalo sasa halipo kutokana na TTCL kurejea mikononi mwa Serikali kwa asilimia 100,”
“Kuna baadhi ya mambo ambayo tulikuwa tunayafanya lakini hayapo kwenye sheria, tulikuwa tunasaini makubaliano tu. Sasa Serikali ikaona ni bora kufanya mabadiliko ya sheria ili iendane na mahitaji,” amesema Kindamba.
Kindamba amebainisha kwamba kumekuwa na upotoshaji kwamba shirika hilo sasa linakwenda kuuawa na sheria hiyo, hata hivyo amewahakikishia wananchi kwamba sheria hiyo italiimarisha shirika hilo na kuwa litakaloongoza kwa mawasiliano nchini.
Amewahakikishia watumishi kwamba ajira zao ziko salama, madeni yote ambayo kampuni hiyo inadai na kudaiwa yatalipwa kwa kadri ya makubaliano waliyoingia na huduma zinazotolewa zitaendelea kama kawaida.
“Nimepokea simu nyingi sana za watu wakitaka kujua hatma ya kampuni hii, niwaambie tu kwamba kilichobadilika ni sheria kutoka kuwa Sheria ya Kampuni ya Simu Tanzania na kuwa Sheria ya Shirika la Mawasiliano Tanzania,” amefafanua Kindamba.

Sadc waamua kumjadili Mugabe


Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Augustine Mahiga ni miongoni mwa mawaziri wanaokutana kwa dharura mchana huu kujadili hali ya kisiasa nchini Zimbabwe ikiwa siku mbili baada ya jeshi kumweka kizuizini Rais Robert Mugabe.
Tanzania inashiriki kwenye mkutano huo kama mmoja ya wajumbe wa chombo kinachojulikana kama Troika.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc), Rais Jacob Zuma ndiye aliyeitisha mkutano huo.
Baadaye amepanga kuzungumza na marais wenzake wa Sadc kwa ajili ya kuwapa taarifa juu ya kile kinachoendelea nchini Zimbabwe.
Mkutano huo umepangwa kufanyika Zimbabwe na utaongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Afrika Kusini, Maite Nkoana-Mashabane, pia utahudhuriwa na mawaziri wengine kutoka Angola na Zambia.
Jana Jumatano, Rais Zuma alizungumza kwa njia ya simu na Rais Mugabe na kueleza kwamba kiongozi huyo alikuwa amezingirwa nyumbani kwake lakini alikuwa salama. Mugabe (93) ameitawala Zimbabwe tangu taifa hilo lilipopata uhuru 1980.
Wakati huohuo ,Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres amehimiza kuwepo utulivu nchini Zimbabwe na kuzitaka pande zote kujiepusha na matendo yanayoweza kulivuruga taifa hilo.
Amesema njia bora ya kupatikana kwa suluhu ya kisiasa ni ile inayozingatia majadiliano na mazungumzo ya amani na wala siyo vinginevyo.
Kupitia msemaji wake, Farhan Haq, Guterres amesema anafuatilia kwa karibu yale yote yanayoendelea nchini humo. Pia ameelezea matumaini yake kuhusu juhudi zilizoanza kuchuliwa na jumuiya ya Sadc kuhusu mzozo huo.
Kauli ya Guterres inatolewa huku hatma ya Rais Mugabe ikibakia kuwa kitendawili baada ya kuzuiliwa katika makazi yake.
Wakati huohuo, Umoja wa Afrika (AU) umesema kuwa hatua ya jeshi la Zimbabwe ya kuchukua madaraka na kumzuilia Rais Mugabe inaonekana kama mapinduzi wa kijeshi.
Mkuu wa kamisheni ya umoja huo, Alpha Conde amesema AU inataka kurejea mara moja hali ya kawaida.

OPEC YAIPATIA TASAF DOLA ZA KIMAREKANI MILIONI 12 KUTEKELEZA MRADI WA KUPUNGUZA UMASKINI AWAMU YA TATU

Umoja wa nchi zinazozalisha Mafuta kwa wingi OPEC- umeupatia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF kiasi cha Dola za kimarekani milioni 12 kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa Kupunguza Umasikini Awamu ya Tatu katika mikoa ya Njombe na Arusha. 

Akifungua kikao kazi cha mradi wa kupunguza Umasikini awamu ya tatu (TPRP III ) kwa wasimamizi wa halmashauri za wilaya za mikoa ya Njombe na Arusha kwenye ukumbi wa mikutano wa TASAF jijini Dar es salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF ,Bwana Ladislaus Mwamanga, amesema kiasi hicho cha fedha kimetolewa ili kuendeleza miradi ya wananchi kwa jamii zenye upungufu wa huduma za jamii ,uhaba wa kipato na kujiongezea kipato. 

Katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na mkurugenzi wa miradi wa TASAF,Bwana Amadeus Kamagenge, bwana Mwamanga amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha kuwa fedha hizo zinazowanufaisha walengwa na kusaidia kufanikisha mkakati wa serikali wa kupambana na umasikini nchini.

Aidha Bwana Mwamanga amesema takribani miradi 407 iko katika hatua mbalimbali za utekelezaji baada ya kupatiwa fedha na kuwaagiza watendaji hao wa halmashauri kuongeza kasi ya kuibua miradi mingine kwenye maeneo yao ili kusaidia jitihada za serikali za kusogeza huduma za kijamii hususani elimu na afya karibu zaidi na walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini. 

Bwana Mwamanga pia ametoa wito maalumu kwa viongozi wa halmashauri za wilaya katika mikoa ya Njombe na Arusha kuendelea kuwahamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa miradi inayotekelezwa kwenye maeneo yao hususani ile inayohitaji mchango wa jamii husika ili miradi hiyo iweze kuwa endelevu na yenye manufaa kwa wananchi. 

Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii-TASAF inatekeleza Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini ambao pamoja na mambo mengine unajenga miundombinu hususani ile inayolenga moja kwa moja kaya za walengwa wa Mpango kwa kuongeza kasi ya kupunguza umasikini miongoni mwa wananchi. 
 Mkurugenzi wa miradi wa TASAF ,Bw. Amadeus Kamagenge (aliyesimama) akifungua kikao kazi cha Mradi wa kupunguza Umasikini awamu ya Tatu,katika ukumbi wa mikutano wa TASAF jijini Dar es salaam.,Kulia kwake ni Mkurugenzi wa fedha, Bi. Chiku Thabiti,kushoto kwake ni meneja wa miradi ya miundombinu wa TASAF Mhandisi Elisifa Kinasha. 
 Meneja wa miradi ya miundombinu wa TASAF,Mhandisi  Elisifa Kinasha (aliyesimama) akitoa maelezo ya kikao kazi cha Mradi wa kupunguza umasikini awamu ya tatu kwa wasimamizi wa halmashauri za wilaya za mikoa ya Arusha na Njombe yaliyoanza leo kwenye ukumbi wa mikutano wa TASAF jijini Dar es salaam.

 Baadhi ya washiriki wa kikao kazi cha mradi wa kupunguza  umasikini awamu ya tatu (TPRP) kwa wasimamizi wa halmashauri za wilaya za mikoa ya Arusha na Njombe.Kikao kazi hicho kinafanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa TASAF jijini Dar es salaam.

 Washiriki wa kikao kazi cha mradi wa kupunguza  umasikini awamu ya tatu (TPRP) kwa wasimamizi wa halmashauri za wilaya za mikoa ya Arusha na Njombe wakisikiliza hotuba ya ufunguzi wa kikao kazi hicho  kinachofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi za makao makuu ya TASAF jijini Dar es salaam.

TAARIFA YA AJALI YA NDEGE YA COASTAL AVIATION ILIYOTOKEA JANA


Baadhi ya Wananchi wakishuhudia ajali katika eneo la Empakai ilipotokea ajali ya ndege ya Coastal Aviation jana mkoani Arusha,ambapo katika ajali hiyo imethibitishwa kuwa watu 11 walipoteza maisha

TAMKO LA MHE. UMMY MWALIMU KUHUSU WIKI YA KUZUIA USUGU WA VIMELEA DHIDI YA DAWA ZA ANTIBIOTIKI TAREHE 13- 19 NOVEMBA, 2017



TAKUKURU KILIMANJARO YAMSHIKILIA DAKTARI WA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA,MAWENZI KWA TUHUMA ZA RUSHWA

Anaandika Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii Kanda ya Kaskazini. 

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU)mkoani Kilimanjaro,imemtia mbaroni Daktari wa Hospital ya rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro ya Mawenzi akituhumiwa kudai na kupokea rushwa ya shilingi 150,000.

Daktari huyo,Deogratias Godfrey Urio,alikamatwa jana katika mji mdogo wa Himo kwenye baa maarufu ya Mombasa High Way baada ya kuwekewa mtego na makachero wa takukuru mkoani Kilimanjaro.

Taarifa iliyotolewa leo Alhamisi kwa vyombo vya habari na Mkuu wa Takukuru mkoa wa Kilimanjaro(RBC),Holle Makungu imesema kuwa kukamatwa kwa daktari huyo kunatokana na malalamiko ya ndugu wa mgonjwa aliyekuwa akipigwa dana dana kupatiwa huduma ya upasuaji katika hospital hiyo.

Makungu ameeleza katika taarifa yake kuwa,mgonjwa huyo alikuwa akihitaji kufanyiwa upasuaji wa uvimbe katika kizazi chake tangu oktoba mwaka huu baada ya kufanyiwa vipimo kwenye hospital hiyo na kubainika kuwepo kwa uvimbe.

Lakini licha ya kubainika kuwepo na uvimbe huo,mgonjwa huyo hakuweza kupata tiba haraka baada ya kuelezwa na daktari huyo kuwa hawezi kufanyiwa upasuaji huo hadi hapo atakapotoa fedha hizo.

Makungu ameeleza kuwa,baada ya taarifa hizo kuwafikia,mtego uliandaliwa na daktari huyo aliweza kutiwa mbaroni jana Novemba 15 akiwa kwenye baa hiyo ya Mombasa High Way.

“Tunaendelea na uchunguzi wa tuhuma hizo na atafikishwa mahakamani mara tu uchunguzi utakapokamilika,takukuru inatoa rai kwa madaktari na wauguzi katika hospital ya Mawezi kuzingatia viapo vyao ili Mawenzi iwe hospital ya kuigwa kwa huduma bora”,amesema makungu.

Mkuu huyo wa Takukuru mkoa wa Kilimanjaro akahitimisha taarifa yake kwa kuonya kuwa kwa wale wachache watakaoendelea kutozingatia viapo vyao,watakamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria na pia kuwataka waajiri wao wachukue hatua kali za kinidhamu dhidi ya watumishi hao .

UFANYE NINI UKIGUNDUA UMENUNUA ARDHI ILIYOWEKWA REHANI BILA KUJUA ?

Image result for NYUMBA NA KIWANJA

NA BASHIR   YAKUB - 

Umenunua  kiwanja  au  nyumba.  Aliyekuuzia  amekuhahakikishia  kuwa kiwanja/nyumba  hiyo iko  salama  na  haina  mgogoro  wowote. Mbali  na  mgogoro  pia  amekuhakikishia  kuwa  kiwanja/nyumba  hiyo  hajaiweka  rehani  popote  ili  kuchukua  mkopo.

Amekuhakikishia  kuwa  mpaka  wakati unanunua  kiwanja/nyumba hiyo, ni kuwa  iko  salama  na  haijashikiliwa  na  benki  au taasisi  yoyote  ya  fedha  kwa  ajili  ya  mkopo.

Au pengine  hukuuliza  kabisa  kama  kuna  deni lolote,  umejikuta tu  umenunua  bila  kuuliza  swali  kama hilo. Baadae  sasa  ndio  unagundua  kuwa  kiwanja/nyumba  uliyonunua kuna taasisi  moja  ya  fedha  ambapo  aliyekuuuzia  alichukua  mkopo  na  kuiweka   dhamana/rehani  na  bado  hajamalizia  mkopo huo.

Taasisi  hiyo inakuonesha  nyaraka  halali  za  kushikilia  kiwanja/nyumba  hiyo kama  dhamana  muda  mrefu  hata  kabla wewe  hujanunua. Na  kwa  bahati  mbaya  aliyekuuzia hujui  tena  alipo  au  bahati  nzuri  unajua  alipo.

 Lakini hata ukijua alipo, tayari  umeishanunua  na  hela  ulishampa  na  kila  kitu  kilikwishakamilika. Nini  kinakusaidia  kukutoa  katika  hali  hii  ambayo  sasa unaelekea  kuingia  katika mgogoro  mkubwa wenye  sura ya hasara.
Sheria  namba 4 ya 199, Sheria  ya  ardhi  itatupatia majibu   ya  jambo  hili.

1.UNUNUZI WA AINA HIYO UNAVYOTAMBULIKA KISHERIA.

Ununuzi  wa  aina hiyo  unatambulika  kama  aina  ya ununuzi ambao  unaingilia  haki  ya  mtoa  mkopo. Kifungu  cha  69(1) cha  sheria  hiyo  kinauita  ununuzi  huo  kama  ununuzi  unaolenga  kupora/kuharibu(defeat)  haki  ya  mtoa  mkopo.

Mtoa  mkopo  hapa  ni  benki  au  taasisi  nyingine  ya  fedha iliyotoa  mkopo.
Kwahiyo  kujikuta  umenunua  eneo  lenye  mazingira  ya namna hiyo hadhi  yake ni kama ilivyoelezwa hapa juu.

2. HAKI  ALIZONAZO MTOA  MKOPO DHIDI YAKO MNUNUZI.    

Kifungu  cha  7(1)( cha  sheria  tajwa   kinasema  kuwa  ikiwa mtoa  mkopo  atagundua  kuwa  rehani  aliyoshikilia  imeuzwa bila taarifa/kuhusishwa, basi  atakuwa  na  haki  ya  kwenda  mahakamani  na  kudai  kutenguliwa(set aside)  kwa  ununuzi  huo.  Ununuzi  wako  wa  eneo  husika  utatenguliwa  na  mahakama.

 Kwenda  mahakamani  ni  baada  ya  kukutaka  mnunuzi  uondoke  au  uachie hiyo  ardhi  kwakuwa  ilikuwa  rehani  na  pengine  ukakataa.  Ikiwa  utakubali kuachia  kirahisi na kukubali  hasara  basi  haitakuwepo  haja  ya  mtoa  mkopo  kwenda  mahakamani.

Lakini ikiwa  utakaidi  basi  ataiomba  mahakama  itengue  ununuzi  wako kwakuwa  umeuziwa  wakati  akiwa  ameshikilia eneo  hilo  kama  dhamana/rehani.

3.  JE  WEWE MNUNUZI  UNA  HAKI  GANI.      

Kifungu  cha  71 ( 1) kinaeleza jambo  moja  ambalo  linaweza  kukusaidia  kama mnunuzi  katika  mazingira  kama  haya.  Ni  kuwa  utatakiwa  kuthibitisha  kuwa  wakati  unanunua  haukujua  kabisa  kama  nyumba/kiwanja hicho  kiliwekwa  rehani  sehemu.  Ni  kazi  yako  kuhakikisha  unathibitisha  kutokufahamu kabisa  lolote  kuhusu  kuwekwa  kwake  rehani  wakati  ukinunua.

Ikiwa  utaweza  kulithibitisha  hilo  basi  kifungu hicho  kinaeleza  kuwa  mahakama  haitatoa  amri  ya  kutengua  ununuzi  wako. Hilo  ndilo  linaloweza  kukuokoa  na kadhia  hii.

Hata  hivyo  kuthibitisha  jambo hili kuwa  hukujua  kuna  misingi  yake. Kifungu  cha 71(2) kimetaja  msingi  mkuu  wa  kuthibitisha  kuwa   hukujua ni  kuonesha kwa ushahidi   kuwa  kabla  ya  kununua  ulifanya  utafiti  wa kutosha(due diligence/actual  and constructive notice),  na  unaokidhi  viwango  vya  kisheria ili  kujiridhisha  kuwa eneo  unalonunua halina  tatizo/mgogoro.

Moja ya  hatua  unayotakiwa  kuthibitisha  ni kuonesha  kuwa  ulifanya  “official  search”  na taratibu nyingine ambazo  zinakidhi  viwango vya kisheria katika  kujiridhisha  kabla  ya  kununua.

Basi  ukiweza  kuthibitisha  hayo  ununuzi  wako hautatenguliwa. Na hapo ndipo tunaposisitiza  sana kuhusu  kufuata taratibu za kisheria za manunuzi ya ardhi lengo likiwa  kukuweka  salama na hatari  kama hizi  mbeleni. Tujihadhari.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

PITIA VICHWA VYA HABARI KATIKA MAGAZETI YA LEO NOVEMBA 16,2017