Thursday, November 30

Uongozi wa kijiji watishiwa kwa kuzuia uuzaji sekondari


Mwanga. Kuuzwa kwa Sekondari ya Mangio wilayani Mwanga mkoani Kilimanjaro, kumeibua mtafaruku kwa wakazi wa kijiji hicho baada ya kununuliwa na tajiri mmoja kutokana na kukosa wanafunzi.
Inadaiwa kuwa shule hiyo imeuzwa na Jumuiya ya Wazazi ya CCM baada ya uongozi wake mkoani Kilimanjaro kushindwa kuiendesha na kuifunga mwaka jana.
Akizungumzia kuuzwa kwa shule hiyo, mwenyekiti wa kijiji cha Mangio, Malaki Mmbaga alisema amekuwa akipata vitisho kwa watu wasiojulikana baada ya kukuta barua chini ya ofisi yake iliyodai kwamba hana mamlaka ya kuzuia kuuzwa kwa shule  ya hiyo.
 Mmbaga alionyesha barua hiyo ya vitisho iliyoandikwa Oktoba 19 inasomeka: “Kwako mwenyekiti wa Kijiji cha Mangio, pole kwa kutetea shule isiuzwe kwa anayehitaji, kwa taarifa yako tunakujulisha shule itauzwa kama tunavyotaka wewe ni mtu mdogo sana kwetu, tunakupa onyo la mwisho funga mdomo wako kabla haujafungwa na watu wengine, tunakujua vizuri wewe hutujui, hizi ni salamu kwako ‘Funga Mdomo’.”
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo juzi, Mmbaga alisema haiwezekani shule ya wananchi iuzwe kinyemela bila kuwashirikisha wakazi na uongozi wa kijiji.
“Waliouziwa shule hii hatuwatambui, ni wezi na wavamizi haiwezekani kitu kama hicho tunaiomba Serikali iingilie kati,” alisema.
Naye mwenyekiti mwanzilishi wa kijiji hicho, Mlangeni Kimaso alisema hawatawaonea haya viongozi wa jumuiya ya CCM kwa kuuza maeneo ya wananchi kiholela.
“Wilaya hii tumeona makengeza maana hakuna hata kiongozi wa juu anayezungumzia suala hili, haiwezekani mbunge asijue shule hii imeuzwaje,” alisema Kimaso.
Mfanyabiashara Yusuf Mfinanga maarufu Njuweni alikiri kuinunua shule hiyo, lakini alikataa kutaja kiwango cha fedha na kwamba hakumbuki kwa sababu alikuwa akitoa fedha kidogo kidogo kwa  jumuiya ya wazazi makao makuu.
“Ndio nimenunua shule hiyo lakini nilianza kulipa kidogo kidogo jumuiya ya wazazi makao makuu, baada ya kumaliza kulipa walinikabidhi shule hiyo,” alisema.
Naye katibu wa wazazi mkoa wa Kilimanjaro, Hatibu Mnuwa alisema hawezi kulizungumzia suala hilo kwa sasa mpaka apate taarifa za kutosha kwa kuwa linaweza kuibua hisia za watu wengi na akipata muda ataliweka wazi.

No comments:

Post a Comment