Wednesday, November 22

Upande wa mashtaka kuita mashahidi sita kesi ya Nyerere


Dar es Salaam. Upande wa mashtaka unatarajia kuwaita mashahidi sita na kutoa vielelezo vitatu katika kesi ya kuchapisha maneno yenye nia ya uchochezi kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook inayomkabili mfanyabiashara Yericko Nyerere.
Hayo yalielezwa leo Jumanne na Wakili wa Serikali, Clara Charwe wakati akimsomea maelezo ya awali (PH) mshtakiwa huyo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Respicius Mwijage.
Akisomewa maelezo ya awali, Yericko alikubali maelezo yake binafsi ikiwa ni jina lake, yeye ni mfanyabiashara na kuwa alipelekwa mahakamani na kusomewa mashtaka.
Hata hivyo, aliyakana mashtaka yote yanayomkabili na anatetewa na Wakili Peter Kibatala.
Yericko anadaiwa kuwa Mei 28, 2017 kwa nia ya kuwachochea Watanzania alichapisha maneno kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook.

Mbowe asema Chadema haitatetereka



Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema chama hicho hakiwezi kutetereka au kufa kwa kiongozi au mwanachama wake kuondoka.
Amesema kuna mkakati mkubwa unaotumia fedha unaofanywa kuwalaghai viongozi na wanachama wake kukihama chama hicho.
Kauli hiyo ameitoa leo Jumatano baada ya aliyekuwa mwenyekiti wa vijana wa chama hicho, Patrobas Katambi kutangaza kujiunga na CCM.
Akizungumza leo Jumatano na Mwananchi, Mbowe ambaye pia ni amesema, "Tuko ‘strong enough’ sio mara ya kwanza watu kuondoka hivyo wanachama wetu wasiogope waendelee kujenga chama na kuendelea na kampeni za udiwani,"
"Huiwezi kututeteresha, kuondoka kwa Katambi si hivi hivi, ushawishi wa fedha umetumika...ingawa ni haki yao ila hao hawaondoki kwa mapenzi yao na hilo halina ubishi,"
"Badala ya nguvu na fedha kuzielekeza kujenga viwanda wao nguvu wamezielekeza kushawishi viongozi wetu, wamewashawishi wengi na Katambi ni miongoni ingawa wengine wamekataa."
Mbowe amesema, "Katambi alikuwa katika majukumu ya chama na aliwaaga wenzake anakwenda kumuguza mama yake mgonjwa hivyo akakatiwa tiketi ya ndege, kumbe alikuwa anakwenda kukamilisha dili ambalo naambiwa limetumia saa 48 kukamilika."
Amesema Chadema ilipofika haiwezi kufa kwani imejijenga na hapo walioondoka lakini mpaka sasa kimeendelea kuwapo.
Mbowe amesema mwitikio wa wananchi katika kampeni za udiwani kwenye kata 43 umeishtua CCM ikiwamo kuhama kwa aliyekuwa mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu.

Wadau wataka mamlaka ya elimu, Mkapa azungumzia mfumo




       Rais mstaafu, Benjamin  Mkapa     
       Rais mstaafu, Benjamin  Mkapa      
Dodoma. Wakati wadau wa elimu wakipendekeza kuundwa kwa mamlaka ya kusimamia sekta ya elimu ili iendane na mkakati wa uchumi wa viwanda, Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa amesema nchi haijaweka msukumo katika kutafakari mfumo wa elimu.
Akizungumza katika kongamano la wanataaluma Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) jana, Mkapa alisema jamii ni lazima ikiri kazi kubwa inayofanywa na wakufunzi ambao wanaifanya katika mazingira magumu na changamoto nyingi.
“Hatuwezi kuridhika mno na kufikiri kuwa ni sawa, sote tunatambua jinsi mataifa yaliyoendelea yalivyofanya kuweza kufika walipo hivi sasa,” alisema.
Alitoa mfano wa mataifa kama Singapore, Korea Kusini na Vietnam ambayo yalitumia nguvu ya ziada katika kutoa elimu bora na kufanya mageuzi.
“Walifanya mapinduzi ya elimu. Walitumia rasilimali, wakafanikiwa. Bila shaka na sisi tunaweza tukafanya hivyo pia,” alisema.
Mkapa aliishauri Serikali kuviongezea fedha vyuo vikuu nchini ili vijikite katika utafiti wa kina kwenye ajenda ya maendeleo.
Alisema kufundisha na kujifunza pekee hakutoshi, bali vinatakiwa kutoa huduma ya utafiti ambayo itasaidia kulielekeza Taifa katika ajenda za maendeleo.
“Elimu itaendelea kuwa msingi na kiini katika Taifa kwenye ajenda ya maendeleo ya Taifa masikini. Ni kamba ambayo inawafunga watu pamoja,” alisema.
Wadau wa elimu UDSM
Katika kongamano jingine lililofanyika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Shirika la HakiElimu, John Kalage alisema mamlaka itakayosimamia elimu itawezesha kusaidia mabadiliko yanayofanywa na watunga sera.
Kongamano hilo lililoanza juzi na kumalizika jana ambalo lilikuwa linajadili umuhimu wa sera ya elimu ya ujamaa na kujitegemea katika kuelekea uchumi wa viwanda liliandaliwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na shirika la HakiElimu.
Katika kongamano hilo, wadau wa elimu walipendekeza kuundwa kwa mamlaka ya kusimamia sekta ya elimu ili kuwezesha elimu inayotolewa iendane na uchumi wa viwanda.
Kalage alisema mamlaka itakayoundwa itasimamia elimu, itawezesha kusaidia mabadiliko yanayofanywa na watungasera kufanyiwa upembuzi kabla ya kuingizwa katika mfumo rasmi wa utekelezaji.
“Kuna baadhi ya mambo tunajadili leo, lakini si mapya. Kuna wakati waziri anakuja na kubadili mfumo bila kufanya tafakuri na uchambuzi wa kina kwani unaathiri mamilioni ya Watanzania kwa hiyo tukiwa na mamlaka ya kusimamia elimu, itatuwezesha kutoa elimu iliyo bora,” alisema Kalage.
“Tutakapokuwa na chombo hicho, kitaweza kusaidia kufanya upembuzi kwa kina na kitaweza kubaini tumefikaje hapa tulipo na tunatokaje,” alisema.
Mwenyekiti wa kongamano hilo, Jaji Joseph Warioba alisema mapendekezo yaliyotolewa, ikiwamo kuupitia mfumo wa elimu yatakuwa na tija kwa kuwa yatawezesha kubaini changamoto zilizopo na jinsi ya kuzitatua.
“Tunapaswa kutoa elimu iliyo bora na tunatakiwa kuwa na mwelekeo wa aina ya elimu tunayoitoa. Ni imani yangu, Serikali ambayo tumekuwa nayo toka jana (juzi) hadi leo itatusaidia kuyatumia mapendekezo na kuyaingiza katika sera na kanuni na kuona itaboreshaje elimu,” alisema Jaji Warioba ambaye pia aliwahi kuwa waziri mkuu.
Jaji Warioba aliungwa mkono na mchangiaji wa mada, Dk Joviter Katabaro aliyesema kama nchi inataka kutoa elimu, basi ianzishe vyuo vya ufundi katika kila wilaya ambavyo vitawafundisha vijana kwa vitendo na shule ya mfano ya sayansi kwa kila wilaya kufanikisha sera ya uchumi wa viwanda.
“Tanzania ya viwanda inahitaji watu wenye ujuzi na mbinu mbalimbali kuanzia ngazi ya chini, na vyuo hivi vya ufundi ni muhimu sana. Wazazi au walezi wakuze vipaji vya watoto wao,” alisema Dk Katabaro.
Mwanafunzi wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari ya Jangwani, Ashura Mohamed alisema: “Vipaji vya wanafunzi vinapaswa kuendelezwa. Wapo wanaotaka kuwa waimbaji, wapo wanataka kuwa wachezaji. Si wote wanaokwenda shule ambao wanataka kuwa kama wanavyotaka wazazi au walezi wao. Kwa hiyo mzazi aendeleze kipaji cha mtoto wake.”
Kwa upande wake, naibu waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhandisi Stella Manyanya alikubaliana na ushauri wa wadau.
“Michango mingi iliyotolewa ina lengo la kujenga, kwa hiyo Serikali inayapokea na imani yangu tutafikia Tanzania ya viwanda,” alisema naibu waziri huyo.   

Mgombea asema mahabusu imemuongezea ari ya ushindi


Mwanza. Mgombea udiwani Kata ya Mhandu (Chadema), Godfrey Misana amesema siku tano alizokaa gerezani Butimba jijini Mwanza zimemuongezea ari, nia na ujasiri wa kushinda katika uchaguzi mdogo Novemba 26,2017.
Kwa siku tano kuanzia Novemba 17,2017 hadi jana Jumanne Novemba 21,2017 alikuwa mahabusu kutokana na kesi inayomkabili akidaiwa kujeruhi.
Akihutubia mkutano wa kampeni eneo la Machinjioni jijini Mwanza jana muda mfupi baada ya kuachiwa kwa dhamana katika shauri la jinai namba 540/2017 la kumjeruhi meneja wa kampeni za CCM katika kata hiyo, Thomas Warioba, mgombea huyo amesema kunyimwa dhamana na kupelekwa mahabusu hakujamdhoofisha, bali kumemuimarisha.
"Muda wote niliokaa mahabusu nimepata ushirikiano na kutiwa moyo na kila mmoja; nadhani ni mipango ya Mungu mimi kwenda mahabusu ili Chadema inyakue kiti hiki,” amesema.
Amesema kwa kipindi alichokaa gerezani, amepata wafuasi zaidi ya 2,800 miongoni mwao wakiwa mahabusu na wafungwa.
“Chadema inapendwa hadi gerezani na wafungwa na mahabusu ambao kwa siku zote wamenitia moyo wa kutokata tamaa,” amesema Misana.
Meneja kampeni wa mgombea huyo, Charles Chinchibela ambaye pia alikuwa mahabusu amewasihi wakazi wa kata hiyo kuwapa pole kwa madhila yaliyowafika kwa kumpigia kura Misana kuwa diwani wao.
“Tumefunguliwa kesi na kupelekwa mahabusu kwa kutetea haki ya wakazi wa Mhandu ya kupata maji safi na salama, huduma bora ya afya na miundombinu ya barabara; tulipeni kwa kumchangua mgombea wa Chadema,” amesema Chinchibela.
Misana, Chinchibela na watu wengine wawili wameachiwa kwa dhamana baada ya Hakimu Mkazi Ainawe Moshi kutupilia mbali pingamizi la dhamana lililowasilishwa na Wakili wa Serikali, Elizebeth Barabara.
Moshi, ambaye ni hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza alikubali hoja za mawakili wa utetezi Gasper Mwanaliela na Paul Kipeja kuwa shauri linalowakabili wateja wao lina dhamana na hakuna hoja za msingi za kuizuia.

Katambi, mwenyekiti Bavicha aliyetoka kama alivyoingia


Dar es Salaam. Aliingia bila kutegemewa na ameondoka bila kudhaniwa.
Ndivyo unavyoweza kuelezea uamuzi wa aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi kujiunga na CCM jana.
Katambi, aliyechanguliwa kuwa mwenyekiti Bavicha Septemba 11, 2014 akichukua nafasi iliyoachwa na John Heche, hakuwa anategemewa kama angeweza kuaminiwa na vijana kushika wadhifa huo.
Na hakutegemewa kama angeiacha jumuiya hiyo siku chache baada ya kusimama jukwaani kusisitiza msimamo wake mbele ya mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.
Na hakutegemewa kuwa angepewa nafasi adimu ya kuzungumza mbele ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), tena katika kikao kilichofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam, kutangaza tu uamuzi wa kujiunga na chama hicho.
Lakini yote yamewezekana.
Katika uchaguzi wa Bavicha 2014, Katambi alipambana na Daniel Naftali na Upendo Peneza waliokuwa wakipewa nafasi kubwa, lakini sarakasi za hapa na pale ziliwatupa nje.
Nguvu ya Katambi haikuwa kubwa kutokana na ugeni wake ndani ya Chadema, ikilinganishwa na Naftali pamoja na Peneza.
Lakini aliibuka kidedea akikusanya kura 173 wakati aliyekuwa mshindani wake mkubwa, Peneza akipata kura 70 katika uchaguzi wa ng’we ya pili baada ya awali uliohusisha wagombea 13 kushindwa kupata asilimia 50 ya kura zote 243.
Mara baada ya kutangazwa mshindi na msimamizi wa uchaguzi huo, Roderick Lutembeka ambaye ni katibu mkuu wa Baraza la Wazee Chadema, Katambi aliwashukuru wote.
“Makundi yameisha hapa leo. Nawashukuru walionipa kura lakini hata walioninyima, twendeni tukaijenge Bavicha yetu iwe imara,” alisema.
Kabla ya ngwe ya pili, maneno dhidi ya Katambi yalipamba moto mitandaoni na kusababisha kuwe na makundi mawili makubwa yaliyowalazimu viongozi wawili wa juu, Mbowe na katibu mkuu wa wakati huo, Dk Wilbroad Slaa kufika ukumbini usiku wa manane kutuliza hali.
Katambi, aliyekuwa mwanasheria wa kampuni za Sahara Media Group inayomilikiwa na mwenyekiti wa CCM wa Mwanza, Anthony Diallo alionekana kama amepandikizwa na chama hicho tawala, huku Peneza akihusishwa na mfanyabiashara mmoja maarufu nchini.
Saa 8.47 usiku baada ya wagombea 13 kumaliza kujinadi, Mbowe alilazimika kutoa neno la kuweka mambo sawa ili kuhakikisha vijana hao wanamchagua kiongozi wao pasipo vishawishi.
Mbowe aliwataka vijana hao kuacha siasa za kuchafuana katika mitandao ya kijamii.
“Nimefanya juhudi sana kukijenga chama hiki. Ninaumia kuona watu wanaotaka uongozi, wanachafuana kupitia mitandao ya kijamii,” alisema Mbowe.
“Kila mtu anataka kuwa kiongozi lakini si kwa kuchafuana. Mnachafuana katika mitandao, mnakidhalilisha chama na mnakivua nguo chama chenu. Huo ni uhuni.
“Mtakapomaliza uchaguzi tokeni na umoja, wekeni makundi kando, nendeni mkaijenge Bavicha na Chadema yenu. Sitaki makundi. Yaliyoifikisha CCM hapo ni makundi sasa hatutaki kuona yanajitokeza kwetu.”
Hata hivyo akizungumza na Mwananchi kuhusu kuhama kwa Katambi na kile kilichojitokeza katika uchaguzi wa Bavicha jana, Peneza alisema amefanya uamuzi katika kipindi kinachohitaji wenye roho ngumu.
“Katambi ni kijana mwenzetu ambaye tumeshirikiana na tulishindana katika uchaguzi, lakini alichokifanya ni uamuzi wake,” alisema.
“Ameufanya katika kipindi ambacho (wanahitajika) wenye roho ngumu bila kuogopa vitisho na kukamatwa. Katika harakati hizi unahitaji wenye moyo.”
Pendeza alisema wakati wa uchaguzi wa Bavicha, Suala la jinsia lilimnyima uenyekiti.
“Lakini chama kilitambua umuhimu wangu mwingine na kunipa nafasi hii ya kuwatumikia Watanzania,” alisema.
“Hata kama kuna watu wanasema Katambi alibebwa, basi angeonyesha utofauti lakini alishindwa. Bavicha aliirudisha nyuma.”
Katambi alivyobadilika ghafla
Katika mkutano wa kampeni za udiwani uliofanyika Novemba 14 mjini Masasi, Katambi alipanda juwaani akiwa pamoja na Mbowe na alichokisema ni tofauti na alichofanya siku saba baadaye mbele ya mwenyekiti wa CCM, John Magufuli.
“Mambo mengi yalikuwa mrama na watu tunapenda mabadiliko ila hatutaki kubadilika. Kama nitaitwa msaliti basi nitakuwa msaliti kundi la wasaliti wa nchi hii, ukombozi ulishapatikana, siyo tunachokisema majukwaani ndiyo tunachokiamini,” alisema baada ya kupewa nafasi na mqwenyekiti huyo wa CCM jana.
Lakini Novemba 14, Katambi alisema huu ni wakati ambao vyama vinapita kujinadi kila kimoja na ahadi zake.
“Ahadi zetu tulizoziahidi zote tunazitekeleza hasa za kusimamia Serikali na kwamba mngetupa Serikali tungehakikisha tunaboresha maisha ya Watanzania bila uongo,” alisema.
“Lakini baadhi yenu pengine walichagua CCM, sasa ni wakati kwa wale waliochagua CCM kujisahihisha. Mtu unapojisahihisha maana yake unaonyesha hasira kwenye mambo makubwa matano ambayo nataka niyazungumze.
“Jambo la kwanza, kunja kidole cha kwanza tusema tulidanganywa, tuliambiwa Sh50 milioni zinakuja, hazijaja. Tuna hasira, tunaanza kukunja ngumi taratibu.
Pia alizungumzia upatikanaji dawa kwa kila mtu, hasa watoto na wazee.
“Hao wamedanganywa. Kunja kidole cha pili tunaelekea kwenye ngumi kumpandisha CCM kuonyesha hasira,” alisema.
“Tatu, tunasema kwamba sasa nchi hii hali ni mbaya. Njaa balaa, mtu anadaiwa benki, kwenye kilimo, amekopa Voda, amekopa Tigo, kila sehemu ana madeni. Njaa ni kali. Kunja ngumi.
“Nne, kuonyesha kwamba haya waliyotuahidi wameonyesha sifa kuu za mnafiki kwanza akiahidi hatekelezi, pili akisema jambo anasema uongo na mwisho ukimwamini haaminiki anafanya hiana.
Pia aliwataka wakumbuke kutoipigia kura CCM.
“Tunakunja kidole cha tano kwa sababu tunataka kuonyesha CCM kwamba Serikali hii sio ya CCM wala sio ya mtu mwingine yeyote,” alisema.

Ahadi ya Sh50 milioni kila kijiji isisubiri 2020



        Mwaka 2015 CCM iliahidi kuwa iwapo ingeshinda Uchaguzi Mkuu, ingetekeleza programu maalumu ya kutoa Sh50 milioni kwa kila kijiji ili fedha hizo zitumike kuchochea maendeleo ya watu wa vijiji hivyo. Jambo hili halikuwa wazo baya, lakini tulitahadharisha kuwa CCM isingeweza kulitekeleza kwa ufanisi.
Machi 2016 Baraza la Taifa la Uwezeshaji (NEEC), lilitangaza kuwa Serikali imetenga Sh800 bilioni kwenye bajeti yake ili kuanza utekelezaji huo. NEEC ilirudia tena tangazo lake hilo Septemba 2016 kuwa fedha hizo zitaanza kutolewa mapema mwaka 2017.
Mpaka sasa hakuna kijiji ambacho kimepata hata senti tano ya mkoloni.
Katika kugonga msumari wa mwisho kwenye jeneza, majuzi Rais Magufuli akiwa Mwanza ametamka rasmi kuwa yeye hana hizo fedha na kwamba anasafisha kwanza ili aweze kuzipata. Kwa hiyo CCM imetoa ahadi isiyotekelezeka. Ni dhahiri kuwa wamewahadaa wananchi. Lakini duru nyingine zinaonyesha kuwa CCM inataka kulifanya jambo hili mwaka 2019/2020, si kwa lengo la kuchochea maendeleo ya watu, bali kwa lengo la kutapanya fedha ili kupata kura.
Rai yetu ni kuwa, kama lengo ni kuinua maisha ya watu, programu hii ilipaswa kutekelezwa sasa, ili itumike kuchochea uchumi wa wananchi wa vijijini nchini.
Sisi ACT Wazalendo tunakubaliana na wazo hili, japo uzoefu wa miaka iliyopita unatuonyesha kuwa CCM haina uwezo, maarifa na njia nzuri za kutekeleza mipango na programu za namna hii. Pia ni lengo letu kupitia makala hii kutoa njia nzuri mbadala ya utekelezaji wa programu hii.
ACT Wazalendo ingefanya nini?
Sisi tuliwaahidi kwenye ilani yetu mwaka 2015 kuwa iwapo tungechaguliwa na kushika madaraka tungetekeleza sera ya hifadhi ya jamii kwa wananchi wote nchi nzima. Hifadhi ya jamii ni mfumo wa kuweka akiba kwa muda mrefu na kupata mafao kama vile fao la matibabu, fao la uzazi, fao la mikopo ya ujasiriamali, fao la bei na fao la ukame.
Mafao ya muda mrefu ni pensheni ambapo mwanachama wa hifadhi ya jamii hulipwa baada ya kupoteza nguvu za kufanya kazi. Tungetekeleza wazo hili zuri la Sh50 milioni kila kijiji kwa kutumia ahadi yetu hii ya hifadhi ya jamii kwa wote.
Tanzania ina jumla ya vijiji 15,000. Jumla ya Sh750 bilioni zingehitajika kutekeleza ahadi ya Sh50 milioni kila kijiji. Kwenye ilani yetu ya Uchaguzi ya mwaka 2015 tulipendekeza mfumo wa akiba wa Serikali kuchangia sehemu na mwananchi kuchangia sehemu iliyosalia.
Katika Manispaa ya Kigoma Ujiji ambayo sisi ACT Wazalendo tunaiongoza, tunatekeleza wazo hili kwa kutumia fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo (CDCF), ambapo mwananchi anachangia asimilia 50 kwenye hifadhi ya jamii na Manispaa inachangia asilimia 50 iliyobakia.
Iwapo Serikali ingetumia mfumo huu ingeweza kuwa na Skimu ya Hifadhi ya Jamii yenye jumla ya Sh1.5 trilioni kwa yenyewe kumchangia kila mwananchi anayeingia Sh10,000 na mwananchi kuchangia Sh10,000 iliyobaki kila mwezi.
Kwa Sh750 bilioni za Serikali, watu 6,250,000 wangeweza kulipiwa na kuingizwa kwenye hifadhi ya jamii kwa wao kuchangia nusu tu ya michango ya kila mwezi.
Idadi hii ni wastani wa watu 400 kila kijiji na Mitaa kwa maeneo ya mijini. Watu hawa wanakuwa kwenye chama cha msingi cha ushirika kwa madhumuni haya. Na wote, pamoja na wategemezi wao watano kila mmoja angekuwa anapata bima ya afya na mikopo ya ujasiriamali ilhali akiba yao ipo palepale.
Katika vijiji na mitaa mingi nchini tatizo la huduma za afya lingekwisha kabisa, wananchi mngeweza kutibiwa kwa bima na wajibu wa Serikali ungebaki kwenye kushirikiana nanyi kujenga vituo vya afya na zahanati tu. Kwa wafugaji, skimu hii ingekuwa ni mkombozi mkubwa, vikundi vya ushirika vya wafugaji vingeweza kupata mikopo pamoja na kujengewa uwezo wa kuanzisha ranchi ndogondogo za ufugaji na kuondoa kabisa tatizo la kuhamahama na mifugo, huku ukame ukitokea wanalipwa fidia kutokana na fao la ukame kwa mifugo.
Skimu hii ingewakomboa wakulima pia, ambao ni asilimia 75 ya Watanzania wote vijijini, karibu robo tatu ya wananchi wote. Kwanza ingetoa urahisi kwa mikopo kupitia vyama vya ushirika, ingechangia uanzishwaji wa viwanda vidogo vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo na uwepo wa fao la bei ungewahakikishia uhakika wa soko na fidia iwapo bei ya mazao yao ingeporomoka.
Jambo muhimu zaidi, kwa mfumo huu, Serikali itaweza kuwa na Watanzania milioni 36 wenye bima ya afya, ndoto ya bima ya afya kwa wote ingetimia.
Programu hii ingefanyika kwa miaka mitano tu mfululizo basi wananchi wangeweza kufikia uwezo wa kujilipia wenyewe akiba kwa asilimia 100 na kuukuza Mfuko wa Skimu hii mpaka kufikia jumla ya Sh7.5 trilioni.
Jambo hilo pia lingeweza kukuza uchumi kutokana na uwekezaji wake kwenye maeneo yanayohusu wananchi wa chini na kwenye miradi yenye masilahi kwa Taifa, ukijengwa utaratibu utakaofanya maamuzi ya kiuwekezaji kuamuliwa na bodi huru ya wadhamini yenye uwakilishi wa wananchi waliomo kwenye Skimu hiyo.
Hivyo kuifanya skimu hii shirikishi na iliyo wazi kwenye uendeshaji wake, ili kuziba mianya ya maamuzi mabaya pamoja na rushwa na ufisadi.
Faida ya yote haya isingekuwa kwa wananchi, Serikali nayo ingefaidika, kwani fedha za mifuko ya hifadhi ya jamii huwekezwa kwenye miradi ya Serikali kupitia hati fungani na hata uwekezaji wa moja kwa moja kwenye miradi mikubwa kama ya kilimo, mifugo na viwanda vya kuongeza thamani za mazao ya kilimo na mifugo.
Skimu hii pia ingesaidia kuongeza uwezo wa uwekaji wa akiba katika nchi yetu, kwa sasa uwiano wa uwekaji wa akiba nchini ni asilimia 16 tu ya Pato la Taifa, wakati kwa muundo wa uchumi wetu tulipaswa kufikia hata asilimia 30 tu, nchi kama China wamefikia asilimia 50. Kuwa na akiba ndani ya nchi kutaongeza uwezo wa uwekezaji utokanao na fedha za ndani nchini.
Lakini pia Serikali ingetumia fedha kidogo kwenye bajeti ya afya kwani zaidi ya nusu ya wananchi wangekuwa na Bima ya Afya kupitia skimu hii, na uchumi wa nchi yetu usingesinyaa kama ilivyo sasa kwa sababu mikopo ya ujasiriamali na kwa vikundi vya ushirika wa wakulima na wafugaji kupitia mifuko hii ya hifadhi ya jamii ingeongeza mzunguko wa fedha kwenye uchumi na kuchochea uzalishaji wa mali.
Ni jambo la kushangaza kuwa Serikali inasema haina fedha za kutekeleza ahadi yake yenyewe. Utekelezaji wa Sh50 milioni kila Kijiji kupitia Skimu ya Hifadhi ya Jamii ingeifanya Serikali iwe na fedha zaidi za kutekeleza miradi yake.
Hivi majuzi Serikali imekwenda kukopa Sh1 trilioni kwenye benki moja kwa riba kubwa ili kutekeleza miradi yake, ingekuwa imetekeleza hifadhi ya jamii isingehitaji kwenda huko nje kukopa kwani ingekopa fedha hizo ndani na malipo ya riba yangebaki ndani na kurudi kwa wananchi kupitia bima ya Afya, uwekezaji kwenye kilimo, mifugo na viwanda, pamoja na mikopo kwa Wajasiriamali.
Tungeweza kuupanua uchumi wa nchi yetu kupitia hifadhi ya jamii, ni bahati mbaya kuwa CCM hawayafanyi haya.
Kila wakati nasema Serikali ya CCM inasumbuliwa na ukosefu wa maarifa, si dhamira. Sina mashaka na dhamira yake bali maarifa ya kuchambua matatizo ya nchi yetu na kuyatatua.
Katika nchi yeyote ya Kidemokrasia, nakisi ya maarifa hutatuliwa kwa mijadala. Serikali ya Awamu ya Tano haitaki mijadala, haitaki mawazo mapya ambayo yangewasaidia kuongeza maarifa.
Ndio maana uchumi unaporomoka, na wananchi wanalia na hali mbaya lakini mawazo mazuri ya kutatua hali hiyo kama haya, hayasikiki, kwa sababu haki na uhuru wa kujieleza vinaminywa.
ACT Wazalendo pamoja na mazingira haya ya kuminywa kwa nafasi ya kutoa mawazo mbadala, bado tunaendelea kutimiza wajibu wetu kwa Taifa kwa kuhakikisha tunakosoa na kushauri juu ya sera mbadala. Suala la kusikia na kutekeleza litabaki kwa Serikali.
Zitto Kabwe, ambaye ameandika haya, ni Kiongozi wa ACT Wazalendo.     

Vyama vya siasa viachwe vipambane majukwaani




Musa Juma.
Musa Juma. 
Kampeni za uchaguzi mdogo wa madiwani zinazoendelea katika kata 43 nchini zimeibua mambo mengi, kubwa ni kuwa wananchi wanaonyesha kuwa kiu ya kuona mikutano ya kisiasa.
Hayo yamedhihirika katika ziara ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na viongozi wengine wa chama hicho ambayo imeingia wiki ya pili katika mikoa mbalimbali ambako uchaguzi wa marudio unafanyika.
Katika ziara hizo, viongozi hao na wengine wa vyama vingine vya siasa huzungumza na wananchi wa kata hizo pamoja na kuwanadi wagombea udiwani huku wananchi wakionekana kutamani kusikia kinachoendelea kwenye ulingo wa siasa za mageuzi nchini.
Hilo halina ubishi katika msafara wa kampeni za Chadema kutokana na wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye mikutano na kusababisha misafara mirefu ya pikipiki, baiskeli na wengine kujipanga kando ya njia wakipungia mkono kuonyesha ishara ya vidole viwili.
Hayo yameonekana katika maeneo mengi hata vijijini ndani, katika maeneo ya Mtwara Mjini, Masasi, Rungwe, Mbeya, Tunduma, Sumbawanga, Mwanza, Arusha na Kilimanjaro.
Katika baadhi ya maeneo, polisi wameamua kutumia mabomu ya machozi katika baadhi ya maeneo kama Mwanza na Moshi kuwatawanya mashabiki waliojitokeza kuwalaki viongozi, Edward Lowassa na Mbowe.
Kutokana na hali iliyojitokeza mkoani Mtwara, Mkazi wa Kata ya Reli, Emmanuel Kagenzi anasema, “Ni kama ndoto, tuliambiwa mkutano utakuwa saa tisa alasiri, lakini nimefika hapa tangu saa sita mchana, lengo ni kuhakikisha napata majibu ya maswali niliyokuwa nayo.
Anasema haamini kama nchi imefikia ilipo kiasi cha wananchi kushindwa kuzungumza na viongozi wao na kusikia misimamo na mwelekeo wa vyama vyao kutokana na zuio la mikutano ya kisiasa alilosema linawakosesha haki yao ya msingi.
Katika uwanja wa mkutano uliofanyika Kata ya Chanikanguo, wilayani Masasi ambako Mbowe alimnadi mgombea udiwani wa kata hiyo, James Kaombe umati wa watu ulionekana kuzidi ule wa Mtwara.
“Nimewahi na familia yangu, nilitaka kusikia mambo mengi na undani na ukweli kuhusu tukio la (kupigwa risasi) Tundu Lissu.
“Nimesikia kwenye vyombo vya habari, lakini mwenyekiti wetu ambaye tunamshukuru kwa kutuokolea jembe letu ana maelezo mazuri, ametueleza kuwa Lissu hayupo kwenye hatari ya kifo na anaendelea vema,” alisema Azidu Juma.
Juma anasisitiza kuwa wapo pamoja na viongozi wao licha ya kuwakosa katika majukwaa ya siasa kwa zaidi ya miaka miwili.
Kadri ziara ilivyoendelea ndivyo mapokezi ya Mbowe yalivyokuwa yakiongezeka. Katika Kata ya Ibhigi wilayani Rungwe mkoani Mbeya watu waliongezeka zaidi na katika baadhi ya maeneo walitanda barabarabi wakitaka mwenyekiti huyo azungumze nao.
“Haya ni madhara ya kutaka kuwaweka watu ndani ya chupa wasizungumze, hata mtoto ukimfungia muda mrefu anaweza kupoteza uelewa na kujifunza anavyoviona tu hata kama ni tabia za wanyama,” anasema Mbowe.
Hali hiyo iliendelea katika wilaya ya Momba Kata ya Ndalambo, mkoani Songwe ambapo wananchi walimpokea Mbowe kilomita 20 kabla ya kufika eneo la tukio.
Muda mwingi wakati anahutubia, Mbowe alilazimika kuzuia mihemko ya furaha ya wananchi ili waweze kusikilizana.
Kwa upande wa Kusini na Nyanda za juu Kusini, funga kazi ilikuwa Rukwa katika Kata ya Sumbawanga Asilia ambako Jeshi la Polisi lililazimika kuharakisha kumuondoa kiongozi huyo wa Chadema.
Katika uwanja wa Momoka ambako alihutubia kumnadi mgombea udiwani, kulijaa watu hadi ungeweza kudhani ni kampeni za kuwania urais.
Gari la Polisi lenye askari wenye silaha lilitangulia mbele, katikati la Mbowe na lingine nyuma na kwa umbali na kumsindikiza kwa kilomita tano ambako walishuka na kumtaka Mbowe na msafara wake kuondoka eneo hilo haraka kuelekea Iringa.
Lissu aibua simanzi
Mapema katika mkoa huo, kila wakati Mbowe alipokuwa akimtaja Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu aliyepigwa risasi na watu wasiojulikana shangwe iligeuka simanzi.
Kila anapopita ilionekana watu walikuwa wanataka kufahamu nini kilitokea kwa Lissu, kila Mbowe alipotaka kuzungumzia hakutumia nguvu kuwatuliza wananchi, walinyamaza wenyewe huku baadhi yao wakisikika wakieleza masikitiko yao.
“Mbowe ameokoa kiumbe tulicholetewa na Mungu kama zawadi, Lissu ni wa kipekee ni zawadi kutoka mbinguni,” alisema Zephania Kalinga mkazi wa kata ya Sumbawanga Asilia mkoani Rukwa.
Mbowe alitumia mikutano hiyo kuelezea kilichotokea na hali ya Lissu ambaye bado anaendelea kupatiwa matibabu nchini Kenya.
Utekelezaji ahadi
Wananchi katika maeneo mengi walionekana kutaka kufahamu hatma ya ahadi walizoahidiwa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa 2015, huku Mbowe akiwataka kuacha ushabiki wa kisiasa kwenye mikutano, badala yake waitumie kuwabana watawala wanapokwenda kuwaomba kura.
“Kuna suala la milioni 50 kila kijiji, kuna suala la wazee, watoto kutibiwa bure, dawa kupatikana kila kona, hayo ni miongoni mwa mambo mnayopaswa kuhoji badala ya kushangilia na kupuliza mavuzezela kwenye mikutano ya watawala,” anasema Mbowe
Akizungumzia suala la ahadi Mkazi wa Mtwara, Johari Kidugo (46), anasema chama tawala kinapaswa kujitafakari kabla ya kurudi na kuomba kura hata ya uchaguzi mdogo wa madiwani.
Anasema hafahamu watakuja na sera na ahadi gani ilihali zile walizotoa hazijatimia. “Sikatai yapo mazuri wanafanya, lakini yanamezwa na hali ngumu ya wananchi, kama hakuna unafuu katika maisha ya mwananchi wa kawaida” alisema Kidugo.
Akizungumzia mwamko wa wananchi kwenye kampeni hizo, Mbowe anasema unatokana na kilichotokea baada ya uchaguzi mkuu 2015 baada ya taifa kukumbwa na ganzi na wananchi wakibaki na maswali mengi juu ya matokeo ya uchaguzi huo.
Alisema kabla hawajakaa vizuri majukwaa mawili muhimu ya kuwapa taarifa wananchi, matangazo ya moja kwa moja ya Bunge na mikutano ya hadhara, yalizuiwa.
Aliongeza, wapinzani walichoambulia ni kamatakamata, kufungwa, kubezwa na kutumika nguvu nyingi isiyohitajika dhidi yao.
Alisema hamu kubwa ya wananchi katika mikutano ya kampeni za uchaguzi mdogo imechangiwa na kukaa miaka miwili bila mikutano ya hadhara.
“Hili unaweza kuliona katika mikutano hii, si mashabiki tu wa Chadema wanaojaa kwenye mikutano, bali wa vyama vyote, huku wote wakiwa wahanga wa kunyimwa haki yao muhimu kikatiba,” anasema Mbowe.     

Kampeni zinavyoamsha hamu ya mikutano ya siasa


Kampeni za uchaguzi wa mdogo madiwani katika Kata 43 unaotarajiwa kufanyika Jumapili, zinaendelea kwa kasi.
Uchaguzi huu wa madiwani, ni moja ya vipimo vya kujua uhai wa vyama vya siasa katika ngazi za chini.
Vyama vyote vikubwa vya siasa, CCM, Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi, ACT-Wazalendo na vingine zimesimamisha wagombea na vinaendelea kuwanadi kwa wananchi.
Tofauti na chaguzi ndogo zilizopita, hadi sasa hakuna mgombea yoyote wa udiwani ambaye amepitia bila kupingwa, japo jaribio la kuwaengua baadhi yao lilifanyika na kukataliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.
Hii ni ishara nzuri ya kukua kwa demokrasia nchini, ingawa kuna kata ambazo uchaguzi unafanyika kutokana na madiwani kujiuzulu kwa sababu mbalimbali yakiwamo madai ya kurubuniwa au kuhongwa.
Tofauti na chaguzi zilizopita za udiwani, hivi sasa tunashuhudia vyama vya siasa vikiwatumia viongozi wake wa kitaifa katika kampeni.
Vilevile tunashuhudia baadhi ya mawaziri, wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya wakipanda katika majukwaa ya kampeni kuwaombea kura wagombea wa vyama vyao.
Hatua hii inaonesha ni jinsi gani, uchaguzi huu ulivyopewa uzito na vyama vyote vya siasa.
Jambo zuri zaidi hadi sasa kampeni katika maeneo mengi ni shwari japo kuna maeneo ya kuanza kuumizana miongoni mwa wafuasi wa vyama, jambo ambalo halina tija kwa nchi wala vyama vyao.
Vilevile katika siku za karibuni, tumeanza kuona kukamata ya wanasiasa kutokana na kauli zao majukwaani au mizozo baada ya kampeni.
Ingawa sheria zinaruhusu kukamata watuhumiwa wanapovunja sheria wakati wowote, lakini naamini ni busara sasa vyama vya siasa vikaachwa kupambana vyenyewe kwa hoja.
Kamatakamata ikiendelea inaweza kuathiri uchaguzi huu mdogo jambo ambalo sio zuri katika kushamirisha demokrasia.
Naamini kutokana na kuzuiwa mikutano ya hadhara kwa vyama vya siasa, sasa wamepata fursa ya kuwasiliana na wananchi, hivyo wangeachwa kufanya kazi hiyo ambayo ni kwa mujibu wa Katiba kwa kuwa katika mazingira ya sasa, uvumilivu wa kisiasa ni jambo jema sana kwani taifa linapita katika kipindi kigumu ambacho wanasiasa wengi hawakukizoea.
Vyama vya siasa vilizoea mikutano na maandamano, kila kukicha lakini sasa utaratibu umewekwa kuzuia maandamano na mikutano isiyo na tija kwa Serikali.
Ingawa suala hili linakinzana na sheria ya vyama vya siasa, lakini limeanza kuzoeleka taratibu, hivyo uchaguzi mdogo wa madiwani umekuwa ni fursa kwa vyama vya siasa kurejesha siasa za majukwaani walau kwa mwezi mmoja.
Wanasiasa wakipata nafasi ya “kupumua” ni afya katika ujenzi wa demokrasia kuliko kukaa wakiwa wananung’unika na mwisho wanaweza kuibuka na mambo ambayo yanaweza kuyumbisha utulivu na amani.
Lakini ni vizuri vyombo vyetu vya dola sasa vikawavumilia wanasiasa wetu kidogo, kwa kuzingatia kuwa wamepata fursa kupumua yaliyo moyoni mwao, la sivyo vinaweza kuwa na utaratibu wa kuwaita viongozi wa kisiasa na kuwapa onyo na wakirudia makosa wawachukulie hatua.
Kufanya hivi wataacha uwanja ulio sawa wa kisiasa katika kampeni hizi za madiwani ambazo kimsingi hazina madhara makubwa.

Mijadala ya Bungeni tuna jambo la kujifunza?


Asilimia kubwa ya Watanzania bado wanatamani Bunge kuonyeshwa moja kwa moja kwenye televisheni. Tafiti nyingi zilizofanywa na hasa ule wa Twaweza zilionyesha kwa takwimu ukweli huu. Ukizingatia ukweli kwamba Serikali imefanikiwa kusambaza umeme vijijini na hivyo maeneo mengi hapa Tanzania yana umeme, watu wanaweza kuona televisheni majumbani kwao au vijiweni.
Kiu hii ya Watanzania ya kutaka kuona na kusikia yale ambayo wabunge wao wanayajadili bungeni ni vigumu kuipima faida yake. Ingawa ni wazi, ni haki yetu sisi wapiga kura kusikiliza na kuyaona yale tuliyowatuma, kama kweli tunawatuma wabunge wetu.
Swali la msingi hapa ni je, mijadala hiyo ina maana yoyote? Serikali inafuatilia mijadala hiyo? Inawasikiliza wabunge wetu? Inayafanyia kazi yale yanayotolewa na wabunge wetu? Tunajifunza kutokana na mijadala ya Bunge au tunaendeleza mipasho na ushabiki?
Majuma mawili yaliyopita, kulikuwa na mjadala mkali bungeni juu ya mpango wa maendeleo uliotolewa bungeni na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Phillip Mpango.
Mmoja wa wabunge walioshiriki katika mjadala huo ni aliyekuwa waziri wa habari, vijana na michezo,Nape Nnauye, ambaye alielezea juu ya hatari ya Tanzania kupoteza sifa ya kukopa ikiwa itatekeleza miradi yake mitatu mikubwa ya maendeleo.
Nape iliitaja miradi hiyo kama ujenzi wa umeme wa kutumia nguvu za maji katika Stiegler’s Gorge katika pori la akiba la Selous, ununuzi wa ndege sita ili kufufua shirika la ndege na ujenzi wa reli ya standard gauge.
Kufuatana na maelezo ya Nape, ufufuaji wa shirika la ndege utaigharimu serikali dola za kimarekani billion moja, mradi wa umeme utagharimu Serikali dola bilioni tano na ujenzi wa reli ya kati katika kiwango cha kisasa utaigharimu Serikali dola 15bilioni.
Nape alidai kuwa mpaka sasa deni la taifa ni dola za Marekani 26 bilioni. Na kwamba ili Tanzania ipoteze sifa ya kukopa, deni lake la taifa linatakiwa lisifikie dola za Marekani 45 billion.
Ukijumlisha dola bilioni moja za ufufuaji wa shirika la ndege, dola bilioni tano za ujenzi wa bwawa la umeme na dola 15bilioni za ujenzi wa reli ya kati katika kiwango cha kisasa, utapata jumla ya dola 21 bilioni ambazo ukijumlisha na deni la taifa la dola bilioni 26, unapata dola 47 bilioni ambazo ni zaidi ya ukomo, kwa dola bilioni mbili.
Akijibu hoja ya Nape, Waziri Mpango alisema hakuna kitu kama ukomo wa kukopa na akatoa mifano ya nchi kama Uingereza na Marekani ambazo zimepita ukomo huo, lakini bado zinakopesheka.
Hata hivyo, pamoja na majibu ya Dk Mpango, tuna mifano ya nchi kama Ugiriki ambazo si tu zimefikia mwisho ya ukomo wa kukopa, bali zimeshindwa kulipa madeni kiasi ya uhuru wa nchi hiyo kama kuingiliwa na wakopeshaji kama vile Serikali ya Ujerumani.
Kwa hiyo, si ukweli kwamba hakuna ukomo wa kukopa kwa nchi, ukomo upo na si busara kwa nchi kuendelea tu kukopa, kwa ajili ya ujenzi wa miradi ambayo uwezo wa miradi hiyo kurudisha madeni ni mdogo.
Hapa, ni kujitahidi kuzitoa hoja hizi kwa uangalifu mkubwa. Wakati watu wana mpango wa kwenda kwa kasi, hoja kama hizi hazifurahishi.
Kwa vile Tanzania ni yetu sote, madeni haya yatatugusa wote, sisi na vizazi vyetu, ni muhimu kujadiliana hadi kufikia maelewano. Hakuna asiyependa maendeleo, lakini tusitake maendeleo kwa kuangamiza vitu vingine muhimu kwetu na kwa taifa letu.
Tukiangalia miradi hii mitatu, ni muhimu tujiulize maswali muhimu na ya msingi, je ni miradi ipi ina uwezo wa kurudisha madeni hayo. Kwa harakaharaka tunaweza kusema ni mradi wa ufufuaji tu wa shirika la ndege la Tanzania ambao si tu una faida kwa taifa, bali pia una uwezo wa kurudisha deni lake la dola bilioni moja za marekani. Hoja hii inatolewa kwa kuzingatia upepo wa biashara hii ambayo kwa upande mwingine ni ngumu maana tunashuhudia makampuni makubwa ya ndege na ya miaka mingi yakishindwa biashara hii na kuifunga.
Mungu, atubariki tuiendeshe biashara hii kwa ufanisi na kwa faida.
Uwezo wa mradi huu wa ndege kurudisha deni hili unatokana na ukweli kwamba mradi huu una nia ya kuboresha biashara ya utalii nchini ambayo kwa sasa inaliingizia taifa dola bilioni mbili za kimarekani kwa mwaka.
Ili ufufuaji wa shirika la ndege la Tanzania uwe na tija kwa taifa na kuweza kulipa deni hilo kwa muda mfupi, Tanzania inatakiwa kuboresha biashara ya utalii hasa katika pori la akiba la Selous, na hifadhi za Ruaha na Katavi.
Umuhimu wa kuboresha maeneo hayo matatu unatokana na ukweli kwamba mpaka sasa zaidi ya dola bilioni moja na nusu kati ya dola bilioni mbili zinazoingizwa na utalii hapa nchini zinatokana na utalii unaoletwa na vivutio vilivyoko kaskazini ya nchi kama vile Mlima Kilimanjaro, hifadhi za Serengeti, Tarangire na Ngongoro.
Hivyo, ili kuboresha utalii, Serikali inapaswa sasa kusimamia utalii kusini mwa nchi ambako kuna vivutio vizuri zaidi kuliko vile vilivyoko kaskazini mwa nchini.
Kwa mfano, Ruaha ni mbuga ya wanyama pori kubwa kuliko nyingine zote hapa nchini. kadhalika pori la akiba la Selous ni kubwa kuliko mapori yote ya akiba barani Africa na pori hilo lina wanyama wengi zaidi kuliko mapori mengine. kwa mfano tembo tu hivi sasa ni zaidi ya 15,000. Kabla ya ujangili wa miaka 40, Selous lilikuwa na tembo 110,000.
Kadhalika hifadhi ya Katavi ina twiga weupe, jambo ambalo ni kivutio kikubwa kwa utalii. Kuboreshwa kwa shirika la ndege la Tanzania na vivutio vya utalii kusini mwa Tanzania kunaweza kabisa kuongeza pato la utalii kutoka dola bilioni mbili hadi dola bilioni 12 na hivyo kushindana na Morocco.
Kwa hiyo badala ya kujenga bwawa la umeme Stiegler’s gorge na hivyo kuharibu mapitio ya wanyama pori, tunapaswa kuboresha pori la akiba la Selous na kuboresha pori hilo hatupaswi kujenga miundo mbinu itakayokaribisha watu wengi ambao wataendeleza ujangiri katika pori hilo la akiba la Selous.
Inapaswa kukumbukwa kuwa wakati Serikali inajenga hoja kwa Unesco kulifanya pori la akiba la Selous liwe urithi wa dunia mwaka 1976, pori hilo lilikuwa na tembo 110,000, vifaru zaidi ya 2,000 na mbwa mwitu wengi kuliko pori lolote barani Afrika.
Lakini, pia ikumbukwe kwamba ni wakati huohuo mwaka 1976, ambapo Reli ya Tazara yenye umbali wa kilomita 1,800 kutoka Dar es Salaam mpaka Kapiri Mposhi inayokatisha katika pori hilo ilikuwa inafunguliwa rasmi baada ya ujenzi wa reli hiyo kwa msaada wa Serikali ya China, na hivyo kufungua pori hilo kwa dunia. Na katika miaka 40 iliyopita mpaka mwaka 2014, pori hilo lilipoteza asilimia 90 ya tembo kutoka tembo 110,000 mpaka tembo 15,000. Idadi ya vifaru hivi sasa inasemekana kuwa chini ya 30.
Hayo ndiyo madhara ya kuweka miradi ya miundombinu katika maeneo yanayopaswa kuwa ya kulinda mazingira kwa faida ya utalii.
Kitu kimoja tunachopaswa kujiuliza ni kwamba mpaka sasa tuna mabwawa ya kufulia umeme makubwa matatu ya Kidatu, Mtera na Kihansi. tunapaswa sasa kujiuliza tumekidhi mahitaji yetu ya umeme?
Ili mabwawa haya ya kufulia umeme yawe na faida, tunapaswa kulinda vyanzo vya mito yetu. Je, tumefanikiwa katika hilo. Ijapokuwa ujenzi wa reli ya kati katika kiwango cha kisasa pia hauwezi kulipa haraka, lakini kwa nchi inayohudumia nchi zaidi ya sita zisizo na bandari kama vile Malawi, Zambia, Congo ya DRC, Burundi, Rwanda and Uganda, tunahitaji si reli tu, bali reli ambayo iko katika kiwango cha kisasa, ambayo ina uwezo wa kubeba mizigo mingi zaidi na inayokwenda nchi hizo kwa chini ya saa 12.
Kwa hiyo, hapa nieleweke kwamba, sipingi kwa sababu ya kupinga tu; natoa maoni hayo ili Serikali ifikirie mara mbili kabla ya kujiingiza katika mradi ambao unaweza kuigharimu na kutugharimu sote pia.
Kwa hiyo, kwa maoni yangu, ningeacha mradi wa stiegler’s hasa wakati huu ambapo tuna gesi zaidi ya mahitaji yetu.
Kwani kama mradi wa Kinyerezi II unaweza kuingiza megawati 600, hii ina maana miradi minne ya aina ya Kinyerezi inaweza kutupa megawati 2,400 ambazo ni zaidi ya umeme wa stiegler’s gorge ambao unataraajiwa kupata megawati 2,100.
Wito wangu ni kwa viongozi serikalini ambao wengi wao walikuwa waalimu vyuo vikuu kutumia elimu zao za juu, kufikiri namna ya kuipeleka nchi yetu juu. Hakuna faida ya kuwa na shahada ya uzamivu ambayo haiwezi kumsaidia rais katika kupanga maendeleo ya nchi.

Chama cha ‘Mtikila’ champeleka mahakamani msajili wa Vyama vya Siasa

     Msajili wa Vyama vya Siasa nchini,Jaji
     Msajili wa Vyama vya Siasa nchini,Jaji Francis Mutungi.  
Dar es Salaam. Chama cha Democratic (DP), kimeomba kibali cha kumfungulia mashtaka msajili wa Vyama vya Siasa nchini.
Chama hicho ambacho kiliasisiwa na Mchungaji Christopher Mtikila ambaye sasa ni marehemu kimewasilisha maombi Mahakama Kuu, kikiomba kibali cha kumfungulia kesi msajili wa Vyama vya Siasa kikimtuhumu pamoja na mambo mengine kuingilia mambo yake ya ndani.
Maombi hayo yaliyofunguliwa na Bodi ya Wadhamini wa chama hicho katika Mahakama Kuu, Masjala Kuu Dar es Salaam dhidi ya Msajili na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) yamepangwa kusikilizwa na Jaji Kiongozi, Ferdinand Wambali, Jumatatu ijayo.
Kwa mujibu wa hati ya maombi ya faragha yaliyowasilishwa mahakamani hapo chama hicho kimefikia uamuzi huo baada ya msajili kukiandikia barua mbalimbali ikiwemo ya kubatilisha mkutano mkuu wa chama uliofanyika Mei 26.
Pia, chama hicho kinapinga hatua ya msajili kutowatambua viongozi wa chama hicho waliochaguliwa katika mkutano huo na badala yake kuwatambua wasio viongozi na wasio wanachama.
Chama hicho kinawakilishwa na mawakili Daimu Halfan na Juma Nassoro.
Kwa kujibu wa hati ya kiapo cha mwenyekiti wa chama hicho, Georgia Mkitila, Aprili 6, msajili alikiandikia barua chama hicho kukikumbusha kuwa uongozi wake ulikuwa unafikia mwisho wake Mei 26, mwaka huu.
Katika barua hiyo, msajili pia alikumbushia chama hicho kufanya mkutano mkuu tarehe hiyo na si vinginevyo.
Georgia, ambaye ni mke wa marehemu Mtikila anaeleza kuwa kutokana na maelekezo hayo ya msajili, chama hicho kiliandaa mkutano mkuu na kikamwandikia msajili barua ya mwaliko.
Anaeleza kuwa msajili alijibu kuwa mkutano huo utakuwa ni batili isipokuwa tu malalamiko yaliyowasilishwa kwake kuhusu uchaguzi wa Mkoa wa Dar es Salaam yatakuwa yamepatiwa ufumbuzi.
Georgia anaeleza kuwa Mei 25, chama hicho kilimwandikia barua msajili kutoa maelezo na kusisitiza kuwa mkutano huo utakuwa halali.
Alisema kuwa walifanya mkutano mkuu Mei 26 kwa mujibu wa katiba yao ya mwaka 2002 na kwamba licha ya kumwalika, msajili hakuhudhuria yeye wala ofisa yeyote kutoka ofisi yake.
Alibainisha kuwa baada ya mkutano huo waliwasilisha kwa msajili taarifa zote na mwenendo wa mkutano, ikiwemo orodha ya wajumbe waliohudhuria.
Alifafanua kuwa msajili katika barua yake ya Juni 16, alikiri kupokea taarifa za mkutano mkuu wa chama hicho na kwamba angezitafakari pamoja na malalamiko kutoka kwa baadhi ya viongozi wa chama hicho ili kujiridhisha.
Georgia alidai kuwa Julai 3, msajili alitangaza kuwa mkutano huo ulikuwa batili na akaamuru chama hicho kiandae mkutano mwingine.
Alisema chama hicho kupitia mamlaka yake ya ndani ya nidhamu kilishamvua wadhifa wa ukatibu mkuu,  Feruzi Msimbachaka na kumjulisha msajili,ambaye alikataa kutambua mamlaka hayo ya kinidhamu ya chama.
Alisema msajili amekataa kuwatambua viongozi waliochaguliwa ama kuteuliwa na chama, badala yake anawatambua na kukubali kila kitu kutoka kwa watu walioondolewa madarakani.