Monday, June 5

Sipati picha Chadema bila Ndesamburo



Mengi yamekwishasemwa kuhusu kifo cha Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Kilimanjaro, Philemon Ndesamburo. Sifa zake nyingi zimetajwa, zikihusisha ni mcgangio kiasi gani alikuwa nao kwa chama hicho na kwa taifa kwa ujumla.
Pamoja na hayo yote, jambo ambalo wengi wanajiuliza ni baada ya kifo hicho cha ghafla cha mfadhili mkuu wa chama na mwana mikakati ya ushindi, Chadema mkoa wa Kilimanjaro itakuwaje bila yeye?
Mipango mingi ya kimkakati na kifedha ilimtegemea Ndesamburo kwa kiwango kikubwa. Alikuwa akirusha helkopta yake katika majimbo mbalimbali ya mkoa Kilimanjaro ili kutafuta ushindi kwa chama.
Ndesamburo aliyekuwa na kadi namba 10 ya uanachama wa Chadema, akiwa Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini kwa vipindi vitatu (2000-2015), alifadhili sehemu kubwa ya kampeni ya madiwani waliounda halmashauri ya Manispaa ya Moshi kwa kipidi chote hicho.
Kwa maneno mengine, mtu anaweza kusema kwa Kilimanjaro, Ndesamburo ndio alikuwa Chadema na Chadema ilikuwa Ndesamburo, bila yeye chama kisingeweza kufurukuta dhidi ya CCM.
Aliyekuwa katibu wake wa nafasi ya ubunge kwa vipindi vyote vitatu ambaye pia ni Katibu wa Chadema mkoa Kilimanjaro, Basil Lema anasema itachukua muda kumpata mtu wa aina ya Ndesamburo.
Sifa ndani ya chama
Lema anasema kuna sifa kuu tano za Ndesamburo, ambazo inawezekana ikachukua muda mrefu kupata mtu wa kuzifikia na hivyo pengo lake kuiathiri sana Chadema. “Kikubwa sana ambacho kitaonekana ni kwamba Ndesamburo alikuwa ni mtu mwenye ushawishi mkubwa. Alipewa hata jina la Koffi Annan alipofanikiwa kusuluhisha mgogoro wa uongozi huko Rombo,” anasema.
“Kweli tumempoteza mtu aliyekuwa na uwezo wa kuzileta pande zinazokinzana mezani zikasikilizana. Lakini tumempoteza mtu mwenye nguvu ambaye akikuita unakwenda ukiwa na hofu.”
“Hofu kwa maana ya busara zake nyingi, hofu kwa maana ya umri wake mkubwa na hofu kwa maana ya sifa aliyonayo kwa jinsi alivyoijenga ngome imara ya Chadema,” anasema Lema na kuongeza:
“Unaenda ukiwa na hofu kuwa aliyekuita ndiye mwenye chama na amekifikisha hapo kilipo yeye mwenyewe. Hiyo hofu lazima ikupate unavyomfuata pale ofisini kwake Keys au nyumbani.”
“Pia hofu kutokana na nguvu yake ya kifedha kwamba yeye ni mfadhili mkuu wa chama. Ni mfadhili wetu binafsi.”
“Sasa anapokuita, umeitwa na mamlaka ya fedha pia.”
“Lazima uangalie amekuita mwenye pesa na hiyo ni nature (asili). Tunawaheshimu watu wenye pesa. Anapendwa sana na anaheshimiwa sana kwa hiyo akikuita unajua umeitwa na kipenzi cha watu.”
“Kwa hiyo watu watakushangaa sana kama unapambana na mtu anayeheshimika sana na mtu unique (wa kipekee) na mtu mwema. Wewe ndio unaonekana wa ajabu.”
“Pia alikuwa ni mwana mikakati ya ushindi, mimi nimekuwa katibu wake. Ningekuwa na sababu nyingi za kufikia juu kabisa kwenye hatima yangu ya kisiasa lakini nilibaki naye.”
“Nilikuwa navutwa mno kufanya kazi na mtu mwenye mipango na mikakati yenye akili sana. Ndesamburo ni mjanja ni mtu wa mikakati mno. Anapanga mikakati ya miaka 10 mbele na inakua.”
“Anapanga kuanzia mbinu, gharama na wahusika. Sasa hayupo tuna kazi ngumu. Tunahitaji mwana mikakati, tunahitaji msuluhishi sasa hayupo ni hatari kwetu. Na inawezekana chama kikateketea kwa kukosa msuluhishi,” anasema Lema ambaye mwaka 2015 alijitosa kumrithi Ndesamburo lakini akalazimika kuondoa jina lake baada ya kuombwa na Ndesamburo.
Nini kitainusuru Chadema
Katibu huyo anasema hakuna mtu binafsi ambaye ni mbadala wa Ndesamburo, kinachotakiwa ni chama kuheshimu katiba, kanuni na maadili.
“Kwa kuwa chama kilidekezwa kuanzia makao makuu kikijua kuna mbeleko ya kubeba mizigo, uchafu, uvunjaji wa katiba kikijua yupo mbebaji,” anasema Lema na kuongeza:
“Basi itabidi chama kianze kuwa mtiifu sana kwa katiba, kanuni na maadili kushughulikia wakosaji mara moja. Kisiendelee kuamini yuko Ndesamburo kwamba atamaliza tatizo la Kilimanjaro.”
“Hayupo tena. Mbadala wa Ndesamburo ni katiba, maadili na kanuni za chama. Ugonjwa ulioingia kwenye chama unaopambana na mikakati ni tamaa ya madaraka.”
“Ndesamburo ameondoka, kama chama hakitarithi mila za kuenzi na kuheshimu wana mikakati lazima watu wenye tamaa ya madaraka wajenge ufalme wao kwa kuwa hakuna mtu wa kuwatisha tena.”
“Matokeo yake chama kitapasuka vipande vipande, migogoro itakuwa mikubwa na itaanzishwa na wenye fursa ya uongozi wakitengeneza ufalme wao.”
CCM waitabiria Chadema shida
Sio wana Chadema pekee wanaoona kivuli cha Ndesamburio, washindani wao CCM pia wanaona kuondoka kwa Ndesamburo kunaweza kukiteteresha chama hicho katika Mkoa Kilimanjaro kutokana na kumpoteza mtu mwenye ushawishi wa usuluhishi.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Moshi Mjini, Priscus Tarimo anasema inahitajika kazi ya ziada kuwarudisha wanachama na viongozi katika kundi moja, kama kweli wanataka Chadema ibaki imara.
“Kwa kweli itakuwa ni ngumu maana ushawishi wake haukuwa ndani ya chama tu, bali zaidi nje ya chama. Watu walikuwa wanamkubali, mzee mtu mzima (Ndesamburo) akisema kitu anamaanisha,” anasema Tarimo
Anaongeza, “Kwa hiyo heshima ya Chadema Moshi ilikuwa inamtegemea sana Ndesamburo kama mtu, si chama. Hapa ndipo utagundua umuhimu wa yule mzee licha ya hapa mwishoni kuanza kubeza kazi yake.”
“Ukiangalia katika vipindi vya nyuma Rais anashinda wa CCM na Baraza la Madiwani linakuwa la CCM lakini alipoingia kuwa mbunge ndio akabadili, baraza likawa la Chadema.”
“Heshima yake ilikuwa yeye kwanza kabla ya chama na hiyo ndiyo ilisababisha Chadema ikawa na nguvu hapa Moshi. Kwa kweli bila yeye Chadema itakuwa na kazi ya kufanya,” anasisitiza Tarimo.
Tangu kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu mwaka 2015, Chadema Moshi mjini hawakurudi wamoja, kulikuwapo kundi linalomtii Ndesamburo na jingine linalomuunga mkono mbunge, Jaffar Michael.
Lakini kitendo cha baadhi ya wabunge akiwamo Anthony Komu wa Moshi Vijijini, kumpinga waziwazi Ndesamburo asigombea uenyekiti wa Chadema Kanda ya Kaskazini kwa sababu ya umri, nacho kilichochea zaidi mgogoro.
Nguvu ya Ndesamburo
Kada huyo maarufu kwa jina la ‘Ndesa Pesa’ kutokana na kumiliki vitega uchumi kadhaa ndani na nje ya nchi, ndiye anayetajwa kukijenga chama hicho mkoani Kilimanjaro na kuwa na nguvu kubwa.
Katika Uchaguzi Mkuu 2015 ambapo Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa alipeperusha bendera ya Ukawa katika nafasi ya urais, Mkoa wa Kilimanjaro ni miongoni mwa mikoa iliyofanya vizuri.
Akiwa ni mwenyekiti wa mkoa, Ndesamburo pamoja na viongozi wenzake, walimwezesha Lowassa kupata kura 266,636 dhidi ya 167,691 alizopata Rais John Magufuli na kuzoa majimbo saba kati ya tisa.
Si hivyo tu, ni chini ya utawala wake, Ndesamburo aliiwezesha Chadema kupata wabunge tisa, madiwani 145, vitongoji 910, vijiji 472 na mitaa 38 katika uchaguzi wa mitaa 2014 na Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Lakini kubwa zaidi, katika uchaguzi huo, Chadema iliibuka mshindi katika majimbo ya Hai linaloongozwa na Freeman Mbowe na Rombo linaloongozwa na Joseph Selasini.
Mbali na majimbo hayo, Chadema ilishinda katika majimbo ya Same Mashariki kwa Naghenjwa Kaboyoka; Dk Godwin Mollel wa Siha na Anthony Komu (Moshi Vijijini).
Kubwa zaidi ambalo bado litabaki katika vichwa vya wengi, ni kitendo chake cha kumtangaza Jaffar Michael kama mrithi wake na akampigania hadi akashinda katika uchaguzi huo wa 2015.
CCM wakati huo ikimtegemea mfanyabiashara tajiri nchini, Davis Mosha iliamini kwa kutumia mwanya huo wa Ndesamburo kustaafu ubunge ingeweza kushinda lakini haikuwa hivyo.
Kwa hiyo, kuondoka kwa Ndesamburo hakika kutaifanya Chadema ifanye kazi ya ziada na kuja na mikakati mipya ya kuwaaaminisha wananchi kuwa bila Ndesamburo mambo yataenda kama uilivyokuwa.
Meya wa Manispaa ya Moshi (Chadema), Ray Mboya alisema Ndesamburo alikuwa ni baba wa Jimbo la Moshi mjini na kifo chake kimewashtua wengi kwa kuwa aliamka asubuhi akiwa mzima wa afya.
Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa alisema chama kimepoteza mtu aliyekuwa na mchango mkubwa.
“Alikuwa na mchango mkubwa ndani ya chama chetu. Kwa muda mrefu amekuwa akikisaidia chama. Wakati mwingine tumekuwa tukitumia chopa yake,” alisema.
“Pengo kubwa sana kwa sisi, busara zake, mawazo yake kwa kweli tuta-miss sana. Lakini kwa sababu wote tutapita njia hiyo hiyo, hatuna la kufanya.”
Mbunge wa viti maalumu (CCM), Martha Mlata alisema Ndesamburo alikuwa mzalendo wa kweli na kama kuna jambo ambalo wapinzani wanatakiwa kujifunza ni yale mazuri ambayo amefanya wakati wa uhai wake.
“Nakumbuka wakati wote alipokuwa mbunge hajawahi kusikika akikashifu wala kusema maneno makali bungeni. Kama alikuwa anataka kushauri jambo, alitumia maneno ya hekima na busara. Wapinzani wakitaka kuheshimika wafuate mazuri aliyoyafanya mzee Ndesamburo. ‘Tulimmisi’ bungeni lakini tutaendelea kumkumbuka sana kwa hekima na busara zake,” alisema.
Mbali na wanasiasa, Ndesamburo alijenga jina hata nje ya chama kama anavyoeleza Askofu wa Kanisa la Victorious, Dk Sixbert Mkelemi kuwa kanisa limepokea kwa masikitiko kifo chake kwa kuwa alikuwa mmoja wa wadhamini wa Umoja wa Kongamano la Makanisa Afrika.

KWAHERI MZEE NDESAMBURO





Wafanyakazi wa Manji walipa faini kuikwepa jela



Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana iliwahukumu wafanyakazi 16 wa Kampuni ya Quality Group Ltd, inayomilikiwa na mfanyabiashara maarufu, Yusuph Manji kulipa faini ya Shilingi laki tano katika kila kosa linalowakabili ama kutumikia kifungo cha miaka mitatu jela.
Akitoa hukumu hiyo Hakimu Mfawidhi, Cyprian Mkeha alisema mshtakiwa wa kwanza hadi wa 14 wanakabiliwa na mashtaka matatu hivyo katika kila kosa, kila mmoja atatoa jumla ya faini ya Sh1.5 milioni.
Iwapo wangeshindwa, kila mshtakiwa angetumikia kifungo cha miaka mitatu jela katika kila kosa hivyo kufanya watumikie kifungo cha miaka tisa jela.
Kwa upande wa washtakiwa 15 na 16 ambao ni Meneja mradi Jose Kiran na Katibu wake, Prakash Bhatt walihukumiwa kulipa faini ya Shilingi laki tano au kwenda jela miaka mitatu.
Kiran na Bhatt, wao walikuwa wanakabiliwa na tuhuma za kukiuka amri ya Ofisa Uhamiaji na kujaribu kutoroka. Hata hivyo, washtakiwa hao wamekwepa kifungo kwa kulipa faini hiyo.
Kiran na Bhatt wanadaiwa kuwa Februari 20, 2017, wakiwa ni waajiriwa wa Quality Group Ltd, walimzuia Ofisa wa Uhamiaji kufanya kazi zake na kwamba, walikataa kuripoti katika ofisi za Uhamiaji zilizopo jijini Dar es Salaam kwa kujaribu kutoroka nchini kwa kupitia mpaka wa Horohoro.
Washtakiwa 14 ambao ni washauri, Jagadish Mamidu (29), Niladri Maiti (41), Divakar Rajasekaran (37), Mhasibu, Mohammad Taher Shaikh (44), mshauri Bijenda Kumar (43) na mshauri Prasoon Kumar Mallik(46).
Wengine ni mshauri Nipun Dinbadhu Bhatt (32), Meneja Msaidizi, Pintu Kumar (28), mshauri Anuj Agarwal (46), mshauri Varun Boloor (34), mshauri Arun Kumar Kateel (46), mshauri Avinash Chandratiwari (33) na mshauri Vikram Sankhala (50), wamefanikiwa kulipa faini na kukwepa vifungo hivyo na waliambiwa ili waweze kuendelea kuishi Tanzania lazima wafuate sheria za nchi.
Wakili wa Serikali wa washtakiwa hao, Hudson Ndusyepo kabla ya hukumu kutolewa, aliiambia Mahakama kuwa mshtakiwa wa kwanza hadi wa 14 hawakuwa na nia mbaya ya kutenda makosa hayo.
Alidai kuwa walikutana na Ofisa wa Uhamiaji wakamwambia wanahitaji kuongeza muda wa viza za kufanya kazi na wakamkabidhi hati zao za kusafiria na baadae aliwarejeshea zikiwa na viza ndani.
Aliendelea kudai kuwa, wao waliamini viza hizo zilipatikana kwa halali na malipo yalifanyika na fedha kuingia serikalini kupitia mpaka wa Tunduma na risiti walipata.
Alidai baada ya kukamatwa iligundulika zilipatikana kinyume cha sheria.
Alikiri hilo ni kosa lao la kwanza na akaomba Mahakama iwasamehe, wapewe adhabu ndogo na nafasi nyingine ya kuwapo nchini.
Mwendesha Mashtaka wa Idara ya Uhamiaji, Method Kagoma alidai washtakiwa waliingia nchini mwishoni mwa 2016 na wakapewa viza za miezi mitatu za kufanya kazi. 


Mdee, Bulaya ‘out’ mpaka bunge lijalo la bajeti


Halima Mdee na Esther Bulaya wamehukumiwa kutohudhuria vikao vyote vya bunge linaloendelea mpaka mkutano ujao wa Bunge la Bajeti ya 2018/19.
Hukumu hiyo imeungwa mkono na wabunge wengi waliopitisha azimio hilo.
Mapema leo, Jumatatu Kamati ya Maadili  ilisema Bulaya na Mdee wamemaliza adhabu za kawaida zilizopo kwenye kanuni za bunge.
Hata hivyo, Bunge liliendelea  kujadili makosa ya wabunge hao wa Bunda na Kawe.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, George Mkuchika aliliomba Bunge kujadili adhabu inayostahili kulingana na makosa yao.
Kanuni inasema, mbunge anayefanya kosa la kwanza anaweza akazuiwa kuhudhuria vikao visivyozidi 10 na atayakosea kwa mara ya pili anaweza kuzuiwa kuhudhuria vikao visivyozidi 20.

Saturday, December 24

Serikali yapiga marufuku shule binafsi kufanya mitihani ya kuchuja wanafunzi

Serikali imepiga marufuku utaratibu wa shule binafsi kuendesha mitihani ya mchujo kwa wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya kitaifa ili shule zao ziweze kuongoza kwa kubaki ma wanafunzi wazuri(walio na uwezo mzuri darasani)

Agizo hilo pia linapiga marufuku kuwafukuza shule wanafunzi wanaoshindwa mitihani ya mchujo,kuwasajili kama private candidate wale wanafunzi wanaofeli mitihani hiyo,kuwahamisha shule au kuwakaririsha madarasa.

========

Kibano kipya chaja kwa shule binafsi
Hiyo ni baada ya kutangaza kupiga marufuku utaratibu wa kuwachuja wanafunzi wanaotakiwa kufanya mitihani ya taifa uliokuwa unaofanywa na baadhi yao kwa lengo la kuonekana shule zao zinafaulisha vizuri.

Hivi karibuni, Nipashe iliripoti kuhusu hofu ya baadhi ya shule hizo; za msingi na sekondari ziko hatarini kubadilishwa matumizi kutokana na kukosa wanafunzi wa kutosha baada ya Serikali kuboresha shule zake na kutoa elimu bure, huku hali ya kiuchumi ikiwaumiza wananchi.

Huku udahili kwenye shule za serikali ukiongezeka na kuonekana kuwa tishio kwa ustawi wa shule za watu na taasisi binafsi, imewabana tena wamiliki wa shule binafsi kwa kuwazuia kufanya mchujo wa wanafunzi wanaoingia kwenye madarasa au vidato vyenye mitihani ya taifa.

Mmoja wa wazazi aliliambia Nipashe kuwa mwanawe anayesoma kidato cha tatu katika shule moja ya binafsi jijini Dar es Salaam, amepangiwa kuhamishiwa shule nyingine ya mmiliki huyo huyo kutokana na kufaulu kwa daraja la tatu.

Kwa mujibu wa mzazi huyo, kuna wanafunzi takribani 70 wa kidato cha tatu, wanatarajiwa kuhamishwa katika shule hiyo waliyosajiliwa tangu kidato cha kwanza, watahamishwa shule hiyo na kubaki wale waliofaulu kwa viwango vya madaraja ya kwanza na pili tu.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Leonard Akwilapo, akizungumza na Nipashe jijini Dar es Salaam juzi, alisema ni marufuku shule kumkaririsha darasa, kumfukuza, kumhamishia shule nyingine au kumsajili kama mtahiniwa binafsi (PC) mwanafunzi kwa kigezo cha kutofanya vizuri katika mitihani ya shule husika.

"Ni marufuku kabisa kufanya hivyo. Mitihani tulionayo sisi (Wizara ya Elimu) ndiyo mchujo sahihi. Na mtihani ambao unamkaririsha mwanafunzi ni mtihani wa taifa wa kidato cha pili na mtihani wa darasa la nne tu," alisema.

"Wala siyo mtihani wa shule na madarasa mengine hayana mtihani wa kumkaririsha mtoto au kumfanya aondolewe shuleni au ahamishiwe shule nyingine, hatuna utaratibu huo na serikali haiwezi kukubaliana nao," aliongeza Dk. Akwilapo.

Katibu Mkuu wa Chama cha Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi (Tamongosco), Benjamin Nkonye, aliiambia Nipashe jana kuwa utaratibu wanaoutumia ni kushauriana na wazazi wa wanafunzi wanaoshindwa kufanya vizuri shuleni ikiwamo kuwapeleka katika vyuo vya ufundi (Veta).

Alisema shule binafsi zinapaswa kupongezwa kwa kudahili hata wanafunzi hasa wa sekondari ambao shule za serikali huwa haziwachukui kutokana na kushindwa kufanya vizuri katika mitihani ya shule za msingi.

“Hakuna shule ambazo zinapaswa kupongezwa kama za binafsi, serikali yenyewe imekuwa ikichagua wanafunzi wote. Inatuachia ‘vilaza’, lakini sisi kwa kujitoa kuwasaidia watoto wa Kitanzania, tunakubali kuwachukua hao hao wanaoonekana wabaya, tunawafundisha na mwisho wa siku wanakuwa wazuri kuliko hata hao wanaokuwa wamethaminiwa na serikali,” alisema Nkonya.

“Na sisi hatuchuji wala kumfukuza mwanafunzi, isipokuwa kinachofanyika kwa kuwa tunapokea wakati mwingine wanafunzi ambao ni ‘vilaza’ kabisa, huwa tunawagawanya katika makundi kulingana na uelewa wao, wenye uelewa wa kwanza, wa kati na wa mwisho. Na mwisho na tunawafundisha kulingana na ‘speed’ (kasi) ya uelewa wao na wanajikuta wanafanya vizuri.

“Lakini kwa sababu sisi tunakuwa na wanafunzi ambao ni wagumu sana, inapoonekana wakatokea wachache hawawezi kabisa huwa tunashauriana na wazazi wao, kuwapeleka Veta ili kule wanapokuwa wanaendelea kujifunza, wengine wanafanya vizuri hadi wanafika vyuo vikuu, hatuwaachi kama ilivyo katika shule za serikali na vyuo vya serikali, haya maneno mengine yanayozungumzwa ni ya kisiasa tu."

HALI ILIVYO

Uchunguzi wa Nipashe uliofanyika hivi karibuni katika baadhi ya mikoa, ulibaini baadhi ya wamiliki wa shule binafsi wamekuwa na utaratibu wa kuchuja wanafunzi kila mwaka kwa lengo la kupata wenye uwezo mkubwa darasani.

Ilibainika kuwa utaratibu huo umekuwa ukifanywa kwa nia ya kuwa na wanafunzi wenye uwezo mkubwa ili shule hizo zifanye vizuri katika mitihani ya taifa, hivyo kuvutia wazazi wengi zaidi kupeleka watoto wao.

Gazeti hili lilibaini kuwa, baadhi ya shule binafsi zimekuwa zikiendesha utaratibu huo kipindi cha mitihani ya mwishoni mwa mwaka kwa kuwafukuza, kuwakaririsha darasa au kuwahamishia shule nyingine wanafunzi wanaoshindwa kufikia kiwango kinachowekwa na shule husika kwenye mitihani ya kufunga mwaka.

Nipashe pia ilibaini baadhi ya shule hizo zimekuwa na utaratibu wa kuwachuja kwa kuwasajili kama watahiniwa binafsi (Private Candidates) kwenye mitihani ya taifa wanafunzi wake wanaoshindwa kiwango kilichowekwa wanapofanya mitihani ya shule husika.

MTOTO WA PROFESA AKACHA KULA

Akizungumzia suala hilo katika mahojiano maalumu na gazeti hili jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Masomo ya Shahada ya Kwanza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Prof. Allen Mushi, alisema haungi mkono utaratibu wa baadhi ya shule binafsi kuwafukuza wanafunzi wanaoshindwa kufikia kiwango cha alama zilizojiwekea.

Alisema: "Ni makosa kumfukuza shule mwanafunzi aliyekuwa amedahiliwa, anasoma halafu unamsitishia, unamwambia nenda katafute shule nyingine.

"Na ni kweli wana tabia hiyo. “Nina kijana wangu yuko ‘Form One’ (Kidato cha Kwanza) anasoma shule ... (anataja eneo ilipo shule hiyo), yaani anasoma kupindukia. Nilikuwa na wasiwasi hata akija likizo hawezi kula vizuri, anasoma tu."

Alisema kuwa katika shule hiyo ya jijini Dar es Salaam anayosoma mtoto wake, wameambiwa ni lazima awe na wastani wa kuanzia alama 50 katika mitihani ya shule ili aruhusiwe kuingia kidato kinachofuata, vinginevyo wakatafute shule nyingine.

"Katika utaratibu wa elimu, siyo sahihi kufanya hivyo, wewe kama wanafunzi wameshindwa, wewe siyo ndiyo mwalimu, ndiyo kazi yako ya kufanya wanafunzi waelewe," alisema na kufafanua zaidi:

“Sasa ukiwa unafanya hivyo, mwisho wa siku utakuwa unafelisha darasa zima na kujitamba kwamba unafaulisha kwa sababu umefukuza wengi na kubaki na wazuri wachache. Sasa hiyo ni biashara, siyo elimu tena. Wewe kama ni mwalimu, unatakiwa kufundisha wanafunzi wote.

“Kwa hiyo, wanasema shule za ‘private’ (binafsi) zinafaulisha wanafunzi wote, kumbe wengine mliowachuja. Mimi binafsi sikubaliani na hali hiyo kabisa."

Alisema ni muhimu wizara yenye dhamana ya elimu nchini iweke masharti kwamba ukishadahili wanafunzi, wasiondolewe shuleni kwa utaratibu wa viwango vya ufaulu katika mitihani ya shule husika isipokuwa kwa sababu za tabia mbaya na zisizofaa kwa mwanafunzi kwa mujibu wa sheria za nchi.

MAKUNDI YA UELEWA

Msomi huyo alisema wanafunzi wamegawanyika katika madaraja mawili kiuelewa darasani, la kwanza likiwa la wenye uelewa wa haraka (fast learners) na jingine likiwa la wenye uelewa hafifu (‘slow learners).

"Wote hao wanapaswa wazingatiwe katika elimu. Sasa hawa (shule binafsi) wenyewe wanaangalia 'fast learners' tu. Ni vema wote wakachukuliwa katika vigezo sawa, siyo unawachuja wengine halafu unasema unafaulisha wote," alisema Prof. Mushi.

BIASHARA

Aliyekuwa Rais wa Chama cha Walimu (CWT), Gratian Mukoba, akizungumza na Nipashe jana kuhusu changamoto hiyo, alisema si vyema kumfukuza, kumkaririsha darasa au kumhamisha mwanafunzi aliyefanya vibaya katika mitihani ya shule.

"Mtihani wa Kidato cha Pili ni mchujo sahihi tu. Shule binafsi wanakosea. Ufundishaji wa kawaida huwezi kuwa na wanafunzi wanaopata daraja la kwanza na la pili tu," alisema.

"Hao shule binafsi kuna muda wanateleza kidogo, kwa sababu hakuna mwanafunzi asiyefundishika labda kwa sababu wao wanataka suala la biashara. Ni kuonea wanafunzi, bahati mbaya akishaanza shule ya 'private' (binafsi) kidato cha kwanza, hawezi kurudi kwenye mfumo wa serikali, kwa hiyo wanafunzi wanahangaika," alisema zaidi Mukoba.

Tuesday, December 20

Trump aadhinishwa rasmi Rais wa Marekani


Washington, Marekani. Wajumbe wa Jopo la Kuamua Mshindi wa Urais nchini Marekani wamemuidhinisha Donald Trump kuwa mshindi wa uchaguzi wa urais uliofanyika Novemba. Wajumbe hao walikutana katika majimbo yao kupiga kura.
Awali, kulikuwa na juhudi za kutaka kumzuia bilionea huyo kuingia ikulu kwa madai amekuwa akiendesha siasa za kibaguzi.
Hata hivyo, Trump amesema atakuwa rais wa Marekani wote na atafanya kila liwezekanalo kuwaunganisha wananchi.
Wajumbe walikuwa wametumiwa ujumbe kupitia baruapepe na pia kupigiwa simu wakihimizwa kutomuunga mkono bilionea huyo kabla yao kukutana kupiga kura.
Shughuli yao ya kupiga kura kwa kawaida huwa kama shughuli ya kutimiza wajibu kwani mara zote  huwa wanamuidhinisha mshindi.
Kumekuwa na lawama kuwa uchaguzi wa mwaka huu ulitawaliwa na hila ikiwamo vitendo vya udukuzi kutoka Urusi. Madai hayo yamepuuzwa na Urusi iliyosema hayana msingi wowote.
Jimbo la Texas hatimaye lilimuwezesha kufikisha idadi ya kura 270 za wajumbe alizohitaji,, licha ya wajumbe wawili wake kugeuka na kupiga kura kumpinga.
Matokeo ya kura hiyo yatatangazwa rasmi 6 Januari 6 kwenye kikao maalum cha pamoja cha Bunge la Congress.
"Nawashukuru Wamarekani kwa kunipigia kura kwa wingi kuwa rais wa Marekani," alisema Trump kupitia taarifa baada ya matokeo kutangazwa.
"Kwa hatua hii ya kihistoria tunaweza sasa kutazama mbele na kutarajia maisha ya kufana siku za usoni. Nitafanya kazi kwa bidii kuunganisha nchi yetu na kuwa rais wa Wamarekani wote," alisema.

Baba wa msaidizi wa Mbowe kukagua maiti iliyowekwa kwenye kiroba


Moshi. Wakati polisi wakisema kuwa wanaufanyia mchakato wa vipimo vya vinasaba (DNA), mwili wa mtu anayedaiwa kuuawa nje kidogo ya mji wa Moshi na kuwekwa kwenye kiroba na kuchomwa moto, familia ya Ben Saanane, msaidizi wa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ambaye hajulikani aliko imesema inaenda kuuangalia mwili huyo.
Hatua hiyo ya polisi kupima DNA ilielezwa na Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa baada ya hadi jana, mwili huo kutotambuliwa.
Mauaji hayo yaligunduliwa Ijumaa iliyopita, baada ya watu waliokuwa na gari ndogo ambao hawajafahamika, kumchoma moto mtu huyo katika Kijiji cha Ongoma na kisha kutoweka kusikojulikana.
Kamanda Mutafungwa aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa mtu huyo hajafahamika na wala hakuna mtu aliyejitokeza kuutambua mwili huo hivyo kulilazimu jeshi kufanya uchunguzi huo wa kisayansi.

Wahifadhi wamwambia Majaliwa, hakuna kaburi la Faru John


Arusha. Sakata na kifo cha Faru John (38), limechukua sura mpya baada ya wahifadhi wa eneo la Sasakwa Singita Grumet kueleza kuwa hakuna kaburi lake kwa kuwa hakuzikwa.
Wamesema hayo siku moja baada ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kutangaza kuunda timu mpya kuchunguza mazingira ya kifo cha faru huyo huku akihoji mambo manne yaliyozua utata.
Mambo aliyohoji wakati akifanya majumuisho ya ziara yake mkoani Arusha ni juzi, Faru John aliumwa lini, aliumwa nini, daktari gani aliyemtibu na zilipo taarifa za matibabu yake.
Pia aliagiza mwili wa faru huyo kufukuliwa na kutazama kama vinasaba vyake vinaendana na watoto wake 26 ambao bado wapo katika Creta ya Ngorongoro.
Akizungumza na mwandishi wetu jana, mmoja wawahifadhi wa Sasakwa Grumet aliyeomba kutotajwa jina ili kutoathiri uchunguzi wa tukio hilo, alisema kitaalamu wanyama ambao wanakufa bila kuwa na magonjwa ya mlipuko katika maeneo ya hifadhi hawazikwi.
“Faru John baada ya kufa aliondolewa pembe zake na kutupwa ili kiwe chakula cha wanyama wengine wanaotegemea mizoga, lakini kuna mifupa yake,” alisema.
Alisema faru huyo aliombwa na Grumet kwenda kupanda faru waliopo katika eneo hilo, hasa baada ya dume aliyekuwapo huko kuuliwa na tembo.
“Baada ya kuonekana kuna haja ya kutafuta dume, ndipo tuliomba kupata faru dume na tukaletewa na baadaye alikufa,” alisema.
Eneo hilo la Sasakwa Singita Grumet ni mali ya mfanyabiashara mkubwa raia ya Marekani, bilionea Tudor Jones ambaye amewekeza katika maeneo kadhaa ya uhifadhi.
Akifafanua hatua zinazochukuliwa baada ya mnyama kufa katika hifadhi, mhifadhi Peter Isango alisema kwa kawaida huzikwa au kuchomwa moto pale tu wanapobainika kuwa na magonjwa kama kimeta.
“Kama mnyama ana magonjwa ambayo yanaweza kuambukiza, basi anachomwa moto au kufukiwa lakini kama anakufa kawaida na magonjwa ya kawaida huwa anatupwa ili fisi, bweha na wanyama wengine wanaokula mizoga wale na hii ndiyo ikolojia,” alisema.
Kauli hiyo iliungwa mkono na mkurugenzi mkazi wa shirika la uhifadhi la kimataifa la Frankfurt Zoological Society, Gerald Bigurube ambaye alisema kwa kawaida wanyama wanaokufa hifadhini huwa hawazikwi.
Bigurube ambaye aliwahi kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) alisema kwenye kanuni za uhifadhi kitu chochote, kinachokufa ndani ya hifadhi huachwa kwa ajili ya kulinda ikolojia na bionuwai.
“Mnyama ambaye anakufa kwa kifo cha kawaida mzoga wake unapaswa kuachwa kuoza na kutumiwa na wanyama wengine,” alisema.
Alisema hata wanyama wa kawaida kama swala na wengine wanapoumwa huwa hawatibiwi tofauti na wanyama kama tembo, faru na wengine wakubwa ambao hutibiwa.
Hata hivyo, alipoulizwa kuhusu Faru John, Bigurube alisema taasisi yake haikuwahi kushiriki katika suala hilo.
Wapata dhamana
Katika hatua nyingine, Polisi imewaachia kwa dhamana maofisa watano wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na Tanapa waliokuwa wanashikiliwa kwa tuhuma za kumhamisha Faru John kutoka Creta ya Ngorongoro na kumpeleka Sasakwa Grumet.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alisema jana kuwa licha ya dhamana hiyo, uchunguzi unaendelea.
Watuhumiwa hao ni Israel Naman ambaye alikuwa kaimu mkuu wa idara ya hifadhi wakati faru huyo akiondolewa, Cuthbert Lemanya aliyekuwa mkuu kanda ya Creta, Dk Athanas Nyaki ambaye ni daktari wa mifugo wa mamlaka hiyo.
Wengine ni aliyekuwa kaimu mkuu idara ya maendeleo ya jamii, Kuya Sayaleli na kaimu mkuu idara ya ikolojia, Patrice Mattey.
Kabla ya kukamatwa, maofisa hawa walikiri kushiriki kumhamisha Faru John kutoka Creta ya Ngorongoro hadi Sasakwa kwa maelezo kuwa ilikuwa ni kuendeleza uhifadhi wa faru na pia kutokana na ukorofi wa Faru John kuhodhi majike yote ndani ya Creta kuua madume wengine waliozaliwa.
Akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Arusha, Waziri Mkuu alitoa taarifa za kifo cha faru John huku akiwatuhumu baadhi ya watendaji wa NCAA kuhusika na njama za kumuuza kwa Sh200 milioni ambazo alisema walishapokea malipo ya awali ya Sh100 milioni.
Baada ya maelezo hayo, Waziri Mkuu alitaka kupewa taarifa kamili za tukio hilo, pamoja na pembe za faru huyo, ambazo alikabidhiwa Desemba 8 na Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe na kaimu mkurugenzi wa msaidizi kitengo cha kupambana na ujangili, Robert Mande ambaye alimweleza kuwa taratibu zilifuatwa katika kumhamisha.

Aliyebadili dini afariki baada ya kubatizwa


Moshi. Mkazi wa Mailisita wilayani Hai, Paulo (35) amekufa maji baada ya kuzama katika mto Kikafu, dakika chache baada ya kubadili dini na kubatizwa na maji ya mto huo kwa imani ya dini ya Kikristo.
Paulo ambaye jina lake la awali lilikuwa Issa Juma kabla hajabadili dini, alifariki Jumapili iliyopita katika mto huo, wakati shamrashamra za kubatizwa kwake zikiendelea pembeni ya mto.
Hata hivyo, Jeshi la Polisi lililazimika kuwakamata wachungaji wawili wa kanisa la Efatha waliombatiza lakini waliachiliwa baada ya Polisi kujiridhisha kuwa Paulo alikufa maji baada ya kubatizwa.
Habari zilizothibitishwa na Polisi, zimeeleza baada ya kubatizwa saa 8:30 mchana na wakati waumini wakiimba kwa ajili ya kurudi kanisani, ndipo Paulo na mwenzake waliamua kurudi kuogelea.

Thursday, December 8

Kardinali Pengo akerwa na matanuzi


Pwani. Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewataka waumini wa madhehebu hayo kutotumia muda na mali zao kufanya sherehe kubwa, badala yake wajikite katika ujenzi wa makanisa.
Alitoa rai hiyo juzi alipokuwa mgeni rasmi kwenye harambee ya kuchangia Sh50 milioni kwa ajili ya ujenzi wa Kanisa Katoliki Tumbi, Kibaha mkoani hapa.
Kanisa hilo litakuwa na uwezo wa kuhudumia waumini 1,232 kwa wakati mmoja.
Kardinali Pengo alisema ili wanadamu waishi kwa furaha, upendo na amani wanapaswa kupewa ujumbe wa neno la Mungu wakiwa kwenye mazingira bora, hivyo ni vyema jitihada za dhati zikafanyika kujenga makanisa zaidi.
“Nakushukuru Padri Beno (Kikudo) wa kanisa hili ambaye uliona ni vyema utumie siku ya maadhimisho ya miaka yako 50 ya kuzaliwa kufanya harambee hii kukusanya fedha za kukamilisha ujenzi wa kanisa, kuliko wengine ambao wamekuwa wakitumia sherehe hizo maeneo ya fukwe za bahari,” alisema. Alisema makusudi ya Mungu siyo kufuja mali ambazo anawajalia wanadamu, bali kutumia mapato yao kwenye mambo ya maendeleo.
Padri Kikudo aliwashukuru waumini kwa kuonyesha juhudi na moyo wa michango ya hali na mali tangu ujenzi wa kanisa hilo ulipoanza.
Alisema ujenzi wa kanisa hilo umefanyika kwa njia tofauti, ikiwa ni pamoja na waumini kuuza kuku na kujitolea kwa nguvukazi kulingana na vipawa na ujuzi walionao ili kufanikisha ujenzi huo.

Serikali yaombwa kuisadia Dangote

Mtwara. Serikali imetakiwa kukaa na mmiliki wa Kiwanda cha Saruji cha Dangote, Aliko Dangote kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazokikabili kiwanda hicho kwa kuwa anaweza kuwa balozi wa wawekezaji nchini.
Katibu wa CCM Mkoa wa Mtwara, Shaibu Akwilombe  ametoa ombi hilo jana akisema Dangote ana jina kubwa, iwapo kungekuwa na mazingira mazuri ya uwekezaji angesaidia kuwavutia wengine.
 “Siku za hivi karibuni kumekuwa na taarifa kadhaa katika vyombo mbalimbali vya habari zinazohusiana na kiwanda cha Dangote, kutozalisha kwa kile kinachoelezwa ni kutokana na hitilafu za ufundi.  Kwa kuwa tatizo la ufundi limejitokeza kipindi ambacho tayari kulikuwa na malalamiko kutoka kwa wamiliki juu ya gharama za uzalishaji, inasababisha kuwapo mkanganyiko kujua kiini cha tatizo,” amesema Akwilombe.

Sunday, November 20

Urefu wazuia matibabu yake MOI

KIJANA Baraka Elias (35), mwenye urefu wa futi 7.4 ambaye ameshindwa kufanyiwa matibabu ya kubadilishwa nyonga katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (MOI), amevunja ukimya na kueleza changamoto zilizosababisha ashindwe kupatiwa matibabu kutokana na urefu wake usiokuwa wa kawaida.
Akizungumza na MTANZANIA nyumbani kwa wazazi wake Mtaa wa Bwela, Pugu Majohe, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam jana, Elias alisema madaktari wameshindwa kumtibu kwa sababu mashine za MOI hazilingani na urefu wake.
Alisema anatarajia kupewa rufaa ili akatibiwe nje ya nchi.
“Madaktari wamenieleza bado wanafanya mazungumzo na wenzao wanaoshirikiana nao kutoka nje ya nchi ili wajue ni nchi gani itakuwa tayari kunichukua kufanikisha matibabu yangu.
“Sielewi matibabu yatagharimu kiasi gani cha fedha, nitatumia muda gani na vifaa gani hadi kukamilika,” alisema.
Elias alisema alifikishwa katika taasisi hiyo, Aprili mwaka huu baada ya kupewa rufaa kutoka Hospitali ya Peramiho mkoani Ruvuma.
Akizungumzia chanzo cha tatizo lake, Elias alisema alipata hitilafu ya nyonga baada ya kuanguka kwenye ngazi za nyumbani kwake mkoani Ruvuma na tangu wakati huo hakuweza kuendelea kufanya shughuli zake za kiuchumi.
Alisema baada ya muda kidogo alipelekwa Hospitali ya Peramiho ambako alifanyiwa kipimo cha X-ray na kuonekana nyonga yake ilikuwa imevunjika.

ALIVYOPOKEA RIPOTI YA MOI
Elias ambaye muda wote anaonekana kuwa mchangamfu, alisema taarifa aliyopatiwa na madaktari wa MOI kwamba anapaswa kupewa rufaa kwenda kutibiwa nje ya nchi aliipokea kwa mtazamo chanya.
“Niliona ni hali ya kawaida kwa sababu kupewa rufaa ni mfumo wa kawaida wa kimatibabu, madaktari wana utendaji wao… wanapoona wameshindwa wanakupeleka kwingine ambako unaweza kupata msaada zaidi na ndiyo maana nilitolewa Peramiho kuja MOI.

HAWEZI KUPANDA DALADALA
Alisema kwa sasa hawezi kupanda daladala kutokana na urefu wake kwani kukaa kwenye kiti huwa ni changamoto kubwa kwake kwa sababu siti zake zimetengenezwa kwa kujibana.
“Zamani nilipokuwa mzima nilikuwa napanda daladala, nilikuwa napata shida kukaa, jinsi zilivyotengenezwa hazina nafasi ya kutosha tofauti na gari za wenzetu (wazungu) zimetengenezwa kwa kuachanishwa nafasi mtu yeyote anaweza kukaa bila usumbufu,” alisema.

UREFU KWENYE DNA
Elias alisema wazazi wake wamemweleza kuwa urefu alionao ni wa kurithi kutoka kwenye kizazi chao, kwani hata mababu zake wapo ambao walikuwa warefu.
“Wazee hao wanatoka katika pande zote mbili, yaani kwa baba na kwa mama, sijui watu wananichukuliaje jinsi nilivyo, binafsi najiona kawaida na wengine kwa sababu hata hapa nyumbani hakuna aliye mrefu zaidi yangu,” alisema.

CHANGAMOTO
Alisema changamoto kubwa anayokabiliana nayo hivi sasa ni usafiri wa kumtoa nyumbani hadi Muhimbili kupata matibabu.
“Huwa tunalazimika ama kukodi gari kutoka nyumbani hadi hospitalini au tunaazima la mtu tunaweka mafuta,” alisema.

KUPANDA NDEGE
Elias alisema iwapo rufaa itapatikana hahofii kama atashindwa kuingia ndani ya ndege kwa safari ya matibabu nje ya nchi.
“Kama nilivyoeleza awali, wazungu huwa wanafikiri mbali, wanafanya vitu vikubwa. Huko kwenye nchi zao wapo warefu zaidi yangu na wanapanda ndege kama watu wengine.
“Hata gari zao wanazotengeneza siku hizi ni za tofauti, hivi karibuni tu Japan ilitoa hizi gari ndogo ambazo zina uwezo wa kusogeza kiti nyuma na ukakaa vizuri, najua nitaweza kuingia ndani ya ndege,” alisema.

AOMBA MSAADA
Elias alisema ingawa kanisa analoabudu linashirikiana naye bega kwa bega, msaada mkubwa kwake umebaki kwa familia yake.
Kutokana na hali hiyo, anaomba msaada kutoka kwa mtu, mashirika au taasisi yoyote itakayoguswa na mkasa wake.
“Siwezi kufanya kazi, kila siku nahitaji fedha za matumizi, nahitaji msaada, naamini wapo watakaoguswa, nipo tayari kwa msaada wowote kwa sababu nina changamoto nyingi, naumwa sijui lini nitapata matibabu, nategemea majibu ya madaktari,” alisema.