Wednesday, January 11

Fundi sudi maarufu kama Mzee Kipara amefariki

Fundi sudi maarufu kama Mzee Kipara amefariki muda si mrefu huko Kigogo kwenye nyumba ambayo alikuwa amepangishiwa na kundi la sanaa ambalo alikuwa anafanyia kazi la Kaole.

Kwa taarifa ambazo tumezipata sasa hivi kutoka kwa Swebe ambaye yupo nyumbani kwa mzee Kipara, kwa sasa wanauandaa mwili wake kwenda kuupeleka Hospitali ya mwananyamala kuuhifadhi.
Mazishi yake yanatarajiwa kufanyika kesho, kwa taarifa zaidi tutawaletea hapo baadae.

Kigamboni bridge a dream which is about to happen

A Sh 214.639 billion project was signed yesterday to build a bridge across the Kigamboni Creek.
Under the deal signed by the National Social Security Fund (NSSF), the China Railways Construction Engineering Group and the China Major Bridge Engineering Company, it will take 36 months to complete the construction.

Works minister John Magufuli and his Labor and Employment counterpart Gaudencia Kabaka witnessed the signing of the contract by NSSF managing director Ramadhan Dau, China Railways Construction Engineering Group CEO Shi Yuan and Major Bridge Engineering representative Zhou Yiqiao.

NSSF will bear 60 per cent of the construction cost while the rest will come from the government.Before signing the pact, Dr Dau said the idea of constructing the bridge was mooted in 1977.
According to him, the project involves the construction of a one-kilometre tarred road of six lanes from Kurasini, a 680-metre cable stayed bridge and another 1.5km tarmac road that will also have six lanes. 

The construction will start immediately after a site for placement of equipment is found. Dr Magufuli challenged the two companies to finish the work at an agreed time to win the hearts and minds of the public.
“I visited China recently and I found a 27km super bridge that was constructed in 18 months…I wonder why it should take 36 months to construct a bridge of less than 2km in Dar es Salaam,” he said. “Do whatever you can to complete the bridge before President Kikwete’s term ends. Kikwete is the one who is supposed to inaugurate it.”

Tanzania National Roads Agency chief executive Patrick Mfugale said the bridge would have an international standard.Arab Consulting Engineers from Egypt would supervise its construction.


Lowassa aponda nguvu ya umma

Anthony Kayanda, Kigoma
WAZIRI Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, ameibuka na kukemea matumizi ya nguvu ya umma, yanayoendeshwa na baadhi ya vyama vya siasa nchini kushinikiza mambo mbalimbali, akisema hayalifikishi taifa popote.

Akizungumza katika harambee ya kuchangia ujenzi wa Sekondari ya Kanisa la FPCT Bigabiro, mkoani Kigoma, Lowassa alisema nguvu wanazotumia wanasiasa kuhamasisha nguvu ya umma, ingefaa kutumika kushiriki kazi za maendeleo ili kuliletea taifa maendeleo endelevu.

Ingawa Lowassa hakutaja chama cha siasa kwa jina, lakini Chadema ndicho ambacho kimekuwa kikitumia kauli mbiu ya Nguvu ya Umma (Peoples Power) kushinikiza mambo mbalimbali.

"Badala ya kuonekana wakihamasika kufanya maandamano ya kupambana na Serikali, jambo ambalo halitasaidia taifa kuondokana na umasikini, nguvu hiyo ingetumika kushiriki kazi za maendeleo," alisema Lowassa.

Alisema miradi mingi ya maendeleo imekuwa ikikwama kutokana na wananchi kukataa kushiriki kujitolea nguvu zao kwa kufanya kazi, badala yake, wanataka kulipwa fedha kutekeleza miradi maeneo yao.

“Nguvu ya umma tunayoshuhudia kwenye maandamano ya baadhi ya vyama vyetu, ingekuwa inatumika kwa kiwango kilekile kufanya kazi za kujitolea kwenye miradi ya maendeleo kama ujenzi wa sekondari zetu, hakika taifa lingepiga hatua kubwa ya maendeleo, lakini linapokuja suala la kufanya kazi nguvu ya umma hutoweka,” alisisitiza Lowassa.


Harambee
Katika harambee hiyo, Lowassa na rafiki zake walichangia Sh60.5milioni taslim na kufanya michango yote kufikia Sh125 zikiwamo ahadi.

Lowassa alisema elimu ikitiliwa umuhimu ni wazi taifa litajikomboa kutoka kwenye hali duni kwa kuwa litakuwa na watu wenye uelewa wa kutosha juu ya mabadiliko na mifumo mbalimbali ya dunia, kiasi kwamba itakuwa rahisi kufundishwa na kuelekezwa mambo muhimu.

“Baada ya kubaini hakuna usawa katika taifa, tulilazimika kutembea nchi nzima kuhamasisha ujenzi wa sekondari za kata ili kila eneo watoto wasome. Watoto wa Kigoma wawe kama wenzao wa Kilimanjaro au mikoa mingine iliyopata mwanga wa elimu mapema, ndiyo maana angalau watoto wengi wanafika kidato cha nne sasa ikilinganishwa na miaka ya nyuma,” alisema Lowassa.

Ajira
Lowassa alitumia harambee hiyo kurejea kauli yake kuhusu tatizo kubwa la ukosefu wa ajira kwa vijana nchini, ambao wamehitimu masomo yao ngazi mbalimbali lakini wanaishia mitaani bila kupata kazi zinazoeleweka.

Alisema tatizo la ajira kwa vijana ni bomu linaloweza kulipuka wakati wowote na kuleta shida kwa taifa, kwa vile ndiyo nguvu kazi inayohitajika zaidi kujenga uchumi imara wa nchi, hivyo kusaidia kuondokana na umaskini, mfumko wa bei na hata kudorora kwa uchumi.

“Nimekuwa nikilisemea sana suala hili la ukosefu wa ajira kwa vijana, kiasi kwamba kuna watu walinibatiza jina la Yohana Mbatizaji, lakini bado natoa mwito kama jamii tutafakari kwa makini jambo hili,” Lowassa alirejea kauli hiyo na kuongeza:

“Kila tunapokutana kwenye semina na makongamano tulijadili kwa kina, vinginevyo tutakuja kujilaumu siku moja kwa sababu hata wanaohitimu vyuo vikuu, wanaopata ajira ni asilimia tano tu kwa mwaka.”

Alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali mstaafu Issa Machibya, kusaidiana na kanisa hilo kuwashawishi watu wanaomiliki eneo inapojengwa sekondari hiyo, wapunguze gharama za fidia ya ardhi na mazao yao ya kudumu, inayofikia Sh75milioni kwa madai kwamba ni nyingi ikilinganishwa na thamani ya mradi unaotekelezwa.

Mchungaji
Awali, katika risala yao iliyosomwa na Mchungaji Kiongozi wa Kanisa hilo la FPCT Bigabiro, David Nkone, alisema wameamua kujenga sekondari ya kidato cha kwanza hadi sita kutokana na uhaba mkubwa wa sekondari za ngazi hiyo mkoani Kigoma, hususan zenye michepuo ya sayansi.

Mchungaji Nkone aisema Chuo cha Theolojia cha FPCT Bigabiro kinachotoa mafunzo ngazi ya stashahada pia kinakusudiwa kupanuliwa na kufikia kutoa Shahada, hivyo kuongeza fursa za elimu na ajira kwa baadhi ya Watanzania.

Kanisa hilo lilimteua Lowassa kuwa mlezi wa sekondari hiyo aliyowekea jiwe la msingi ambayo kwa sasa ina madarasa matatu yaliyofikia hatua ya rinta, lengo likiwa ni kujenga madarasa ya kidato cha kwanza hadi sita.

Katika hatua nyingine, mjumbe wa Halmashauri Kuu (Nec) ya CCM Mkoa wa Kigoma, Muhsin Abdallah Sheni, aliahidi kuchangia Sh10 milioni na kompyuta mbili, huku Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba akiahidi Sh3 milioni, Mbunge wa Viti Maalumu, Josephine Ngenzabuke aliahidi kutoa Sh2 milioni na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Machibya akiahidi Sh2.5 milioni.

Tuesday, January 10

MPANGO WA SERIKALI KUPUNGUZA MATUMIZI - ZITTO KABWE MB.

Punguza Matumizi ya Posho SIYO Matumizi ya Reli, Barabara, Elimu na Afya

Mwezi Disemba mwaka 2011 Waziri wa Fedha na Uchumi alimwandikia barua Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Fedha Duniani (IMF) kumwahidi mambo yepi Serikali ya Tanzania itafanya ili kurekebisha Bajeti yake. Utaratibu huu hufanyika kila mwaka kupitia mpango unaoitwa ‘Policy Support Instrument (PSI). Katika barua hiyo Waziri wa Fedha wa Tanzania ameahidi kwamba Serikali itafanya juhudi kupunguza matumizi ili kuweza kupunguza uwiano wa nakisi ya Bajeti na Pato la Taifa (fiscal deficit to GDP ratio) kutoka asilimia 7.2 mpaka asilimia 6.6 ya Pato la Taifa.

Waziri wa Fedha na Uchumi ameiambia IMF kwamba ifikapo mwisho wa Mwezi Disemba mwaka 2011 (wiki mbili zilizopita) Baraza la Mawaziri la Tanzania limefikia maamuzi ya kupunguza nakisi ya Bajeti kwa kiwango kilichotajwa. Maeneo yanayotajwa ni Pamoja na Miradi ya Maendeleo ambapo jumla ya miradi yenye thamani ya Tshs 157bn itakatwa. Waziri
wa Fedha ametaja miradi hiyo katika Ukarabati na Ujenzi wa Miundombinu.

Kambi ya Upinzani Bungeni inapinga kuondolewa kwa miradi ya maendeleo ili kupunguza matumizi ya Serikali. Kimsingi wakati kama huu ambapo hali ya uchumi ni mbaya na vijana wengi vijijini na mijini hawana ajira tunasisitiza umuhimu wa kutumia zaidi kwenye miradi ya maendeleo.

Punguza matumizi ya kawaida

Kambi ya Upinzani Bungeni inarejea wito wake kwa Serikali kupunguza matumizi ya kawaida ili kupata fedha za kutosha kwa ajili ya maendeleo. Haiwezekani kamwe tukawa Taifa huru iwapo miradi yetu yote ya maendeleo inafadhiliwa na wahisani. Kiwango kidogo tulichokiweka katika Bajeti ya mwaka huu ndicho hicho sasa kinakatwa na hivyo miradi yote ya maendeleo kubakia kwa wahisani ama kwa mikopo au misaada. Kiwango cha Tshs 203bn sawa na 0.5% ya Pato la Taifa ambacho Serikali imeahidi kupunguza ni kidogo mno na kinalenga kuumiza watumishi wa kada ya chini ya Serikali na sio viongozi wakubwa. Bajeti ya Mafunzo inayoenda kukatwa itaumiza Manesi na Walimu au watumishi wanaoongeza ujuzi ili kuboresha kazi zao. Serikali ikate matumizi yote yasiyo ya lazima na hasa posho (360bn), ipunguze matumizi ya magari na yale yasiyo na uhitaji yapigwe mnada na viongozi wote isipokuwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Spika na Jaji Mkuu washushwe madaraja ya kusafiria kwenye ndege. Safari zote ambazo hazina mahusiano na miradi ya maendeleo zipigwe marufuku kwa muda wote wa miezi sita ya Bajeti iliyobakia.

Serikali ihakikishe matumizi katika Sekta ya Elimu na Afya hayakatwi kabisa ili kuhakikisha tunalinda mafanikio kiduchu ya upanuzi wa sekta hizi na kuongeza uwezo wa Serikali kutoa huduma bora kwa wananchi hasa wa vijijini.

Matumizi ya Maendeleo yasiguswe, yaongezwe

Tayari imeonekana kwamba katika kipindi chote cha nusu ya Bajeti Halmashauri za Wilaya hazijapata fedha za maendeleo. Mfano Halmashauri ya Wilaya Kigoma imepata asilimia 0.3 tu ya Bajeti ya Maendeleo ilhali Halmashauri ya Mji wa Mpanda imepata asilimia 4 tu. Ni dhahiri miradi ya maendeleo kwa maeneo mengi ya vijijini itakwama kwani ni wazi kabisa kwamba Halmashauri hazipati fedha zote za Bajeti ya Maendeleo. Serikali itambue kwamba miradi ya maendeleo sio anasa bali ndio vyanzo vya baadaye vya mapato ya serikali. Miradi ya maendeleo hutoa ajira kwa wananchi na hivyo kuwapunguzia umasikini wa kipato. Jumla ya Tshs 157bn zinazotakiwa kukatwa zisikatwe bali ziongezwe ili kupata fedha za kurekebisha miundombinu kama Reli ya Kati.Kwa mfano Reli ya Kati inahitaji Tshs 200bn katika kipindi cha miaka 3 ili iweze kusafirisha mizigo tani 1.5m kwa mwaka kila siku na kuzalisha faida.

Ongeza Mapato ya Ndani

Inashangaza kwamba katika mpango wa Serikali kupunguza nakisi ya Bajeti mkazo umewekwa kwenye kuondoa miradi ya maendeleo badala ya kuongeza mapato. Nakisi hupunguzwa ama kwa kupunguza matumizi au kwa kuongeza Mapato. Serikali katika Taarifa yake kwa IMF imeibua njia moja tu ya kuongeza mapato, kodi ya mapato kutoka Kampuni ya Geita Goldmine. Huu ni uvivu wa kufikiri.

Serikali imeambiwa mara kadhaa suala la kuanza kutumika kwa sheria mpya ya madini kwa Kampuni za Madini zilizokuwapo. Makusanyo ya Mrahaba peke yake kwa sheria mpya, kiwango kipya na kanuni mpya ya kukokotoa ingeongeza mrahaba mpaka Tshs 203bn kutoka Tshs 99bn za sasa. Kwanini Serikali ianvuta miguu katika kutekeleza hili? Waziri wa Nishati na Madini aliahidi Bungeni kwamba mazungumzo na Kampuni za Madini yanaisha Mwezi Septemba. Mbona Serikali imekuwa BUBU katika hili?

Serikali iliahidi kuangalia suala la mauzo ya mali za makampuni zilizoko Tanzania na kodi ambayo tunapaswa kukusanya, Serikali imekuwa kimya kabisa katika suala hili. Marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwa kuondoa msamaha kwenye ‘deemed capital goods yangeongeza mapato ya Serikali kwa kiwango kikubwa na kupunguza mzigo wa
misamaha ya Kodi.

Uwajibikaji kwa Bunge

Inashangaza zaidi kwamba sasa imekuwa ni mtindo kwa Serikali kutoa ‘commitments’ muhimu za kibajeti kwa Shirika la IMF badala ya wananchi kupitia Bunge. Bunge limepitisha Bajeti, mapitio yeyote ya Bajeti yanapaswa kuidhinishwa na Bunge. Bila kufanya hivyo maana ya Bunge kupitisha Bajeti inakuwa haina mantiki na uhuru wa Taifa letu unakuwa haupo kwetu.

Umuhimu wa Bunge kutunga haraka Sheria ya Ofisi ya Bajeti ya Bunge (Parliamentary Budget Act) sasa unaonekana waziwazi. Muswada umewasilishwa Bungeni na Wabunge binafsi kutaka kuundwa kwa mfumo wa kuisimamia Serikali katika Bajeti. Ofisi ya Spika wa Bunge ihakikishe muswada huu unachapishwa katika Gazeti la Serikali mara moja ili usomwe kwa mara ya kwanza katika mkutano wa Sita wa Bunge na kutungwa kuwa sheria katika mkutano wa Saba.

Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali ilete mpango wa kupunguza matumizi Bungeni ili ujadiliwe na kuidhinishwa na Bunge kabla ya kuanza kutumika. Vinginevyo Mpango wa Serikali kwa IMF utakuwa ni kudharau wananchi na kuuza uhuru wetu kwa Shirika la Fedha la Kimataifa. Mwalimu Nyerere aliwahi kusema mwishoni mwa miaka ya Sabini ‘toka lini Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) limekuwa Wizara ya Fedha ya Kimataifa (International Ministry of Finance)?’

Kabwe Zuberi Zitto, Mb

Waziri Kivuli Fedha na Uchumi

Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni (NKUB)

Dar es Salaam, 10 Januari 2012.

Monday, January 9

Muziki wa Bongo 2011

HIVI wasanii wa kike walikuwa wapi 2011? Ndiyo swali ambalo mashabiki wengi wa muziki nchini wanajiuliza wanapofanya majumuisho ya mwaka 2011 katika siku ya leo Jumamosi tunapoufunga mwaka.
Ukiachilia wachache ambao waliibuka na kupotea, vidole wananyooshewa zaidi wakubwa wawili ambao ni Ray C na Lady Jaydee. Walikuwa kimya muda mrefu na walikuwa wakifanya mambo kimahesabu zaidi.
Ray C aliamua kujichimbia Nairobi, Kenya na kupiga dili zake huko kimya kimya na kudondosha Dar es Salaam baadhi ya singo zake ambazo hazikutamba kama enzi hizo.

Jaydee akakomaa na bendi yake ya Machozi ambayo ilipata shoo nyingi ndani na nje, lakini hakuwa mwepesi kuachia singo kwa fujo kama siku za nyuma, waliokuwa wakienda kwenye kumbi za starehe Bongo ndiyo walimfaidi, lakini upande wa pili alikuwa kibiashara zaidi alizindua miradi yake mingi na kila mara alikuwa bize kuiendesha.

Lakini kuna vichwa ambavyo viliburuza sana kwenye Bongofleva japokuwa wengi wao walikuwa wana nyimbo za kufurahisha na kujirusha zaidi, ambazo zilikuwa hazina ujumbe wowote.

Inawezekana wakati mwingine labda ulizisikia ukaamua kusogeza mbele DVD yako ili zisikuchefue. Lakini huko mitaani wenzio walizipenda na jamaa wakapata mwanya wa kutengeneza fedha ndani na nje ya nchi.

BONGOFLEVA
Wasanii wengine walikuwa wakiibuka na wimbo mmoja na kupotea baada ya wiki chache, wala shoo hawakuambulia. Ingawa baadhi walijitahidi kujitengenezea kashfa na kucheza dili na magazeti ya udaku kupandisha majina yao, lakini bado wakashindwa kuhimili vishindo kutokana na kutokuwa na kazi za maana.

Wasanii wafuatao angalao walijitahidi kuwa bize mwaka mzima wa 2011 na walitengeneza kiasi cha fedha kutokana shoo nyingi za ndani na nje ya nchi, hawakutoka masikioni mwa mashabiki.

20 Percent:
Hakuhitaji kubebwa na prodyuza, redio wala kujitengenezea kashfa ili aibuke. Muziki wake ulimbeba na kumpa tuzo tano kwa wakati mmoja, kitu ambacho hakuna msanii aliyempiku.
Alizurura sana mikoani kufanya shoo pengine kuliko msanii mwingine yeyote na nyimbo zake zilizotamba ni zile zile kama �Tamaa Mbaya�, �Ya Nini Malumbano� mpaka mwisho wa mwaka alipoachia �Pasu Kwa Pasu� ambayo ni jibu baada ya kuacha na prodyuza wake wa siku nyingi Man Walter kwa ugomvi.

Ally Kiba:
Huyu jamaa ameshanasa kwenye masikio ya mashabiki na aliishi kiujanjaujanja kwa kujitangaza zaidi nje ya nchi ambako alipiga shoo nyingi sana.
Alipiga shoo Afrika Mashariki na Ulaya na wimbo wa �Dushedede� ambao uko kwenye staili ya Bolingo ulimbeba kwa kiasi fulani kwa vile ulipendwa na wote.

AY:
Huyu jamaa ni mjanja sana, kama alivyofanya mwaka jana na mwaka huu alifanya hivyo hivyo tena alipiga hatua zaidi na kuwa msanii wa Bongo aliyefanya shoo na wasanii wengi zaidi wa nje achilia mbali Afrika Mashariki hakuna aliyeamini kama angeweza kuwanasa Lamya na Romeo wa Marekani.
Amejiimarisha pia Bongo kwa kufungua maduka mengi ya biashara za nguo na saluni na hata maisha anayoishi ni bora.

DULLY Sykes:
Alifuata nyayo za mastaa wa Uganda na Kenya kibiashara. Ndiye msanii wa Bongofleva aliyekuwa na dili ya kueleweka ya matangazo mengi ya kampuni ya simu za mikononi ya Tigo.
Kama kawaida yake hakuna na nyimbo za kuumiza kichwa, ujumbe wake ulikuwa ni mwepesi sana uliojaa masihara, lakini vijana walimpenda sana na kumsapoti kwa kucheza nyimbo zake na kuibuika kwenye shoo.

BANANA
Kwenye redio hakusikika sana lakini akiwa na B-Band yake alikuwa bize sana kwenye kumbi za Dar es Salaam karibu wiki nzima alikuwa bize kuliko msanii yoyote yule wa muziki wa kizazi kipya. Kilichombeba ni ubunifu wake na bendi yake ambayo imekuwa na vijana wanaovutia wengi.

LINAH na BARNABA
Ukiachilia mbali nyimbo walizofanya kwa kushirikiana hata kila mmoja kivyake walibamba sana mashabiki ndani na nje ya Bongo, ni kizazi kipya kilicholeta mageuzi masikio mwa wengi na hawakutaka makuu.

Shoo za Ulaya wamepiga sana, Linah aliosha jina zaidi baada ya kunasa tuzo mbili za Muziki za Kili, ile ya Mwimbaji Bora wa Kike na Msanii Bora anayeibukia. Usisahau 2011 ndiyo mwaka ambao Linah alinunua gari aina ya Vitz.

DIAMOND
Awali wapinzani wake walidai kwamba alikuwa akichonga dili na magazeti ya udaku ili kujipandisha chati pamoja na kupanua njia yake kibiashara, ingawa hakuna aliyeweza kuthibitisha hilo.

Msanii huyo kama alivyo Ally Kiba walitunisha sana akaunti zao 2011 na walicheza karata zao vizuri na kufunika hata wakongwe.

Skendo zake na wasanii mbalimbali wa kike zimechangia kumweka bize machoni na masikioni mwa mashabiki, lakini hata kazi alifanya nzuri na yenye ubunifu.

BOB JUNIOR
Aliibuka kama masihara, lakini mwisho wa siku akaingia kwenye chati ya wasanii wanaovuma Bongo, singo zake kama Oyoyo zimembeba na kumpa shoo nyingi ingawa zote ni ndani ya mipaka ya Tanzania ya Rais anayependa michezo na Burudani, Jakaya Mrisho Kikwette.

PROF JAY
Kama ipo ndiyo wimbo wake uliotamba miezi ya hivi karibuni, lakini huwezi kuamini ndiyo msanii wa Bongo aliyefanya shoo nyingi zaidi Afrika Mashariki na Ulaya.
Heshima yake kimuziki imeendelea kuwa palepale licha ya kwamba ni mwajiriwa kwenye kampuni moja kubwa ya jijini Dar es Salaam.

Ni msanii msomi na anayefanya kazi kwa hesabu sana na anayefaa kuigwa na chipukizi ambao wamekuwa wakikimbia shule na kung�ang�ania muziki.
Alipokanyaga Uganda, Kenya, Rwanda au Burundi mashabiki walichanganyikiwa.

ROMA MKATOLIKI
Aliibuka kimasihara, lakini amefanya shoo nyingi pengine kuliko alivyotarajia, katika kila shoo kubwa 2011 lazima ungemkuta. Pengine hata yeye hakutarajia kama mashabiki wangeikubali staili yake kiasi hicho.

MWANA FA
Ni Msanii msomi ambaye ukikutana naye ana kwa ana mtaani ukilinganisha na makali yake kwenye kipaza sauti ni vitu tofauti kabisa.
Yuko simpo sana. Alikanyaga Afrika Kusini mara kadhaa na humu ndani ya Bongo aliendelea kujitunzia heshima yake hususani kwa vijana.

BELLE 9
Singo yake ya Sumu ya Penzi imembeba sana na ni mbishi kwelikweli kwenye fani, hachuji. Ameshirikishwa kwenye singo za mastaa kadhaa Bongo na wimbo wake wa Nilipe Nisepe hauna maneno halisi ya kuelezea kwa jinsi ulivyopokelewa mitaani.

JOH MAKINI
Kwa wanaoijua Hip Hop ya Tanzania, wanamjua na hata ambao hawafuatilii aina hiyo ya muziki wanamkubali. Ameonyesha ukomavu sana bila kutetereka au kupotea kama walivyofanya wasanii wengine wa aina hiyo ya muziki.

Wapinzani wake kama Chid Benz, Fid Q, Afande Sele walikuwa wakiibuka na kupotea kipindi kirefu zaidi na walionekana kujishughulisha na dili zingine binafsi zaidi.

DOGO JANJA
Ni msanii mdogo aliyetamba sana mwaka huu wa 2011 ingawa hakua na muda mwingi wa kufanya shoo kutokana na kubanwa na shule, lakini ameonyesha kwamba Bongofleva si jina bali kipaji na ubunifu binafsi.

CPWAA
Yupo kama hayupo, lakini ametengeneza sana na kwenye orodha ya wasanii wa Tanzania waliopiga hela kwa shoo za ndani na nje yumo, hakuna shoo ya maana itapigwa sehemu umkose. Wimbo wake wa Action umembeba.

CHEGE NA TEMBA
Hawa jamaa nuksi na pengine bila wao sasa TMK Wanaume Family itapotea kwenye ramani ya muziki, wao wako juu kuliko kundi na hakuna anayezungumzia tena kundi.

Ukiacha wimbo wao wa Mikono Juu, wametoa nyimbo ambazo zimekubalika ndani na nje na wameshirikishwa na wasanii tofauti na hata ndege wamekwea sana kwenda kufanya shoo zisizo na idadi Ulaya. Je nini hatma ya wengine waliobaki kundini?

TIPTOP CONNECTIONS
Madee na Tundaman waliwaongoza wenzao wa Tip Top kufanya shoo nyingi za ndani tofauti na makundi mengine ambayo ambayo yalionekana kupooza na hayakuwa na jipya 2011 labda tusubirie 2012.


BENDI ZA DANSI
Upepo wa bendi za dansi bado ulibaki kwa Twanga Pepeta, FM Academia, Akudo Impact na Extra Bongo ambazo zilikuwa zikipokonyana mashabiki na kuacha bendi nyingine zikitumbuiza viti katika shoo zao nyingi za Dar es Salaam.


Lakini 2012 huenda ukawa mwaka wa Twanga na Extra endapo FM na Akudo wasipojipanga kwani katika siku za hivi karibuni wameonekana kuyumba na kutokuwa na jipya jukwaani.

MUZIKI WA TAARAB
Taarab ilizoa mashabiki kadhaa wa dansi mwaka 2011, jambo ambalo liliwalazimu watu wa bendi kuwa wanafanya shoo za pamoja na bendi za Taarab ili kujaza mashabiki.

Bendi za Taarab zilizotamba sana ni Jahazi, Five Stars na Mashauzi Classic.

Filamu Bongo 2011

WASANII wa filamu Bongo mwaka 2011 walifanya mambo makubwa na kupiga hatua katika tasnia ya filamu, huku wasanii wengine wakiibuka na kuwa gumzo.

RAY
Ray yeye kama ilivyo kawaida ndiye kioo cha tasnia ya filamu kwa mwaka huo. Aliweza kufanya mambo makubwa ikiwa ni pamoja na kusafiri kwenda kununua vifaa vyake vya kazi Ulaya.
Pia kwa kutumia kampuni yake aliibua wasanii wapya kama Otilia Joseph.

MONALISA
Yvonne Cherryl �Monalisa� alishiriki tuzo za Pan African zilizofanyika nchini Marekani kupitia filamu yake ya Binti Nusa iliyotengenezwa na kampuni yake.

Mwaka jana pia alipata nafasi ya kwenda kushiriki filamu nchini Ghana ikiwa ni sehemu mojawapo ya kutafuta soko la kimataifa. Jambo jingine kubwa kwa mwanadada huyo ni kuwa alisambaza filamu ya Binti Nusa yeye mwenyewe.

KANUMBA
Kanumba naye hakuwa nyuma kwani alitoa filamu nyingi zilizofanya vizuri, si hayo tu bali pia alitumia uwezo wake katika kumleta msanii nyota wa kimataifa kutoka nchini Nigeria, Ramsey Nouah, kushiriki katika filamu yake ya Devil Kingdom.

Filamu ilitikisa katika tasnia ya filamu Bongo. Pia ndiye msanii ambaye amekuwa balozi wa makampuni mbalimbali kwa mwaka jana. Alisafiri kwenda nchini Marekani katika shughuli za sanaa, pia alikwenda Ghana kwa ajili ya kurekodi filamu akishirikiana na nyota wa filamu Afrika kutoka nchi kama Nigeria, Ghana na Afrika Kusini.

WOLPER
Jacqueline Wolper ni moja kati ya wasanii ambao kwa mwaka uliopita alifanya vizuri katika mauzo hata kuweza kuwafunika baadhi ya wasanii wa kike katika tasnia ya filamu.
Wolper pia alitengeneza filamu zake akiwa kama mtayarishaji, amefanya vema katika tasnia hii ya filamu Bongo anastahili Pongezi.

JB
Jacob Stephen �JB� ndiye msanii anayeshikilia nafasi ya kwanza kwa mauzo Bongo kupitia filamu anazoshiriki na kutengeneza mwenyewe.
Filamu yake ya Senior Bachelor ilionyesha uwezo wake wa hali ya juu na kumfanya ashikilie nambari moja.
Filamu zake nyingine ni pamoja na Nipende Monalisa, DJ Ben na Regina.

PATCHO
Patcho Mwamba ni mwanamuziki, lakini tangu alipoingia katika tasnia ya filamu akiwa sambamba na swahiba yake Kanumba. Moja ya sifa ya Patcho pamoja na kuigiza vizuri ni bingwa wa viwalo Bongo, kwa hiyo kama unampatia nafasi ya kuigiza suala la pamba unasahau.

DOTNATA
Dotnata alifungua kampuni ya Tanganyika Entertainment kwa ajili ya kusambaza kazi zake. Alitengeneza filamu iliyojulikana kwa jina la Chupa Nyeusi akiwashirikisha wasanii kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na Burundi.

MR. MTUNIS
Amefanya vizuri sokoni baada ya filamu yake ya Mrembo Kikojozi kuwa gumzo. Hata filamu zake nyingine za Clinic Love na Kisasi zilitamba.

NDAUKA
Rose Ndauka ni moja kati ya akina dada waliofanya vizuri katika tasnia ya filamu Bongo, ikiwa ni pamoja na kufungua kampuni yake ya Rose Ndauka Entertainment kwa ajili ya kazi zake na kufanikiwa kutengeneza filamu kama Bad Girl, The Diary, Reuben na Angel.
Alienda Rwanda kwa ajili ya kurekodi filamu ya Maisha Baada ya Vita Rwanda.
Alitangaza ndoa na meneja wake Mariki iikiwa sambamba na kubadili dini, sasa anaitwa Aisha.


RICHIE
Single Mtambalike �Richie� ni moja kati ya wasanii waliofanya vizuri katika mauzo ya filamu Bongo na aliwaingiza wanaye katika uigizaji kwenye filamu ya Uswahilini Kwetu.

TINO
Hisani Muya �Tino� msanii huyu anarudi kwa nguvu zote, baada ya filamu yake ya Cut Off kufanya vizuri na kufuatiwa na Zowa, sasa ameingiza sokoni filamu ya Loreen inayofanya vizuri sokoni.

Kumbuka kuwa filamu yake ya Shoga ilikuwa gumzo baada ya Bodi ya filamu kuizuia na hatimaye kuibadili jina na kuwa ni Shoga Yangu badala ya Shoga.


DR CHENI
Naye alifanya vema kupitia filamu yake ya One By One na kuwa gumzo akiendelea kuuza sokoni.

Funga mwaka kubwa kuliko zote ni lile wazo la magwiji wa tasnia hiyo, Vincent Kigosi �Ray The Greatest� na Steven Kanumba �Kanumba The Great� walipoamua kutengeneza filamu kwa pamoja na kuipa jina la Off Side,

Walipoenda kuizindua nchini Kongo, ilisababisha baadhi ya watu kupoteza maisha wakipigania kuwaona nyota hao ambao waliandamana na Irene Uwoya, Jenifer na Johari.

Ukija katika fani ya uchekeshaji kwa vichekesho vya filamu, waliofanya vizuri ni King Majuto, Kingwendu, Sharo Milinea, Pembe bin Kichwa na Erick.
Katika upande wa wachekeshaji wa televisheni, kijana Lucas Mhuvile �Joti�' hakuwa na mpinzani. Kila siku amekuwa akibuni na kuibuka na kitu kipya ambacho ni burudani kwa mtazamaji.

Joti ameufunga mwaka kwa kuwa na pointi nyingi pengine kuliko msanii mwingine yeyote.