Friday, October 28

Maajabu matokeo ya darasa la saba


Dar/Shinyanga. Matokeo ya darasa la saba mwaka huu yameacha kicheko kwa Shule ya Msingi Kwema Modern iliyopo Kahama mkoani Shinyanga, baada ya kuibuka mshindi wa kwanza kitaifa.
Shule hiyo imefanya maajabu kwa kutoa wanafunzi saba katika orodha ya watahiniwa 10 bora kitaifa.
Hata hivyo, wanafunzi 238 wamefutiwa matokeo kutokana na sababu mbalimbali, ikiwamo ya baadhi ya wasimamizi wa mitihani, wamiliki wa shule na walimu wakuu kuwapatia majibu na kubainika kuwa yanayofafana.
Pia, wanafunzi 21 watarudia mitihani yao kutokana na sababu mbalimbali kama maradhi.
Akitangaza matokeo hayo jana, Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), Dk Charles Msonde alisema watahiniwa 555,291 (sawa na asilimia 70.36) wamefaulu kati ya 789, 479 waliofanya mtihani huo Septemba mwaka huu.
Matokeo hayo yanaonyesha kiwango cha ufaulu mwaka huu kimepanda kwa asilimia 2.52 ikilinganishwa na ufaulu wa mwaka 2015 ambao ulikuwa asilimia 67.84.
Mbali ya Kwema kuwa shule ya kwanza kwa matokeo ya jumla, imetoa mtahiniwa bora wa kwanza kitaifa.
Mtahiniwa huyo, Japhet Elia (12) ambaye anatoka familia ya wakulima mkoani Kigoma, amefuatiwa na wenzake wawili, Jamal Ally na Enock Daud pia wa shule hiyo walioshika nafasi ya pili na tatu.
Dar, Shinyanga zachuana
Tofauti na matokeo ya mwaka 2015 ambayo shule za Kanda ya Ziwa zilitamba, mwaka huu mikoa ya Dar es Salaam na Shinyanga imechuana vikali.
Kwa mujibu wa Dk Msonde, Dar es Salaam imeibuka kinara kwa kutoa shule nyingi katika orodha ya shule 10 bora, huku Shinyanga ikiongoza kwa kutoa wanafunzi wengi bora kitaifa.
Alisema Dar es Salaam imetoa shule nne kati ya 10 bora, ikifuatiwa na Shinyanga yenye shule mbili.
Katika orodha ya wanafunzi bora kitaifa ambayo mwaka huu imetawaliwa na wahitimu tisa wa kiume na mmoja wa kike, Shinyanga imeongoza kwa kutoa wanafunzi saba kati ya 10. Dar es Salaam imefuatia kwa kutoa wahitimu wawili na Kagera mhitimu mmoja.
Mikoa hiyo pia imechuana vikali katika orodha ya wanafunzi bora kitaifa kwa jinsia. Wakati Dar es Salaam ikitoa wanafunzi watano kati ya kumi kwa upande wa wasichana, Shinyanga imeongoza kwa wavulana kwa kutoa wanafunzi wanane.
Shule 10 bora
Dk Msonde alizitaja shule 10 bora kwa kigezo cha kuwa na wanafunzi 40 na zaidi kuwa ni Kwema (Shinyanga), Rocken Hill (Shinyanga), Mugini (Mwanza), Fountain of Joy (Dar es Salaam), Tusiime (Dar es Salaam), Mudio Islamic (Kilimanjaro), Atlas (Dar es Salaam), St Achileus (Kagera), Gift Skillfull (Dar es Salaam) na Carmel (Morogoro).
Shule zilizofanya vibaya ni Mgata (Morogoro), Kitengu (Morogoro), Lumba Chini (Morogoro), Zege (Tanga), Kilole (Tanga), Magunga (Morogoro), Nchinila (Manyara), Mwabalebi (Simiyu), Ilorienito (Arusha) na Chohero (Morogoro).
Ushirikiano siri ya ushindi
Mkurugenzi wa Shule ya Kwema Modern, Pauline Mathayo alisema mafanikio waliyopata yanatokana na ushirikiano wa karibu uliopo shuleni hapo kati ya walimu, wazazi na wanafunzi.
Pia, alitaja siri nyingine kuwa ni kufuata miongozo ya elimu wanayopewa na Serikali.
Baba, mwana washangaa
Katika kile kinachoonekana ni kutoamini kilichotokea, Elia Stephano, mzazi wa mwanafunzi aliyeshika nafasi ya kwanza kitaifa, alisema hakutegemea kama mwanawe angeweza kupata mafanikio hayo makubwa, licha ya kuwa amekuwa na nidhamu kubwa tangu akiwa mdogo.
“Ukweli baada ya kuelezwa hivyo kwamba mtoto wangu amekuwa wa kwanza kitaifa, nilianza kutetemeka kwa furaha,” alisema Stephano anayejishughulisha na kilimo na ujasiriamali mkoani Kigoma.
“Hayakuwa mategemeo yangu ingawa nilikuwa namwamini mtoto wangu. Lakini si kwa kiasi cha kuwa mshindi wa kwanza kitaifa.”
Alisema mtoto wake anapenda kusoma na kufundisha wenzake huku mara nyingi akipenda kumuomba Mwenyezi Mungu.
Mtoto aliyeongoza kitaifa, Japhet alisema pamoja na kufanya vizuri kwenye mitihani alipokuwa akisoma, hakuwa na matarajio ya kushika nafasi ya kwanza.
“Namshukuru Mungu kwa matokeo hayo. Pia, nawaomba watoto wenzangu katika mambo yao yote wamtangulize Mungu kwa kila jambo hata kama wana uwezo binafsi,” alisema Japhet huku akieleza kuwa ndoto yake ni kuwa mhandisi wa ndege.
Tusiime wazungumza
Akizungumzia matokeo ya mwanafunzi wa kike aliyeshika nafasi ya kwanza kitaifa kwa wasichana Justina Gerald, mwalimu mkuu wa Shule ya Msingi ya Tusiime, Philibert Simon alisema siri ya mwanafunzi huyo kufanya vizuri ni usikivu, nidhamu na uchu wa kujifunza.
Simon alisema msichana huyo ambaye pia ameshika nafasi ya nne kitaifa, alikuwa akifanya vizuri katika mitihani yake shuleni hapo.
Alisema wakati akiwa darasa la saba aliongoza mara 19 katika mitihani 32 waliyofanya wanafunzi hao. Akishuka sana amekuwa wa pili,” alisema Simon.
Udanganyifu
Licha ya ongezeko la ufaulu kwa asilimia 2.5 katika mitihani ya darasa la saba, matokeo yametiwa dosari na udanganyifu uliojitokeza wakati wa uendeshaji wake.
Msonde alisema wakati wa mitihani hiyo, matukio machache ya udanganyifu yalifanywa na baadhi ya wasimamizi, wamiliki wa shule na walimu wakuu.
Udanganyifu uliofanyika unahusisha wamiliki na walimu wa shule kuiba mtihani na kuandaa majibu kwa ajili ya wanafunzi, walimu kuwasaidia wanafunzi kufanya mtihani, walimu kuwapa majibu wanafunzi na kufanana kwa majibu kusiko kwa kawaida.
Kwa mfano, katika shule ya Tumaini, Sengerema mkoani Mwanza, mmiliki wa shule aliandaa majibu ambayo watahiniwa waliandika kwenye sare za shule na kuyatumia ndani ya chumba cha mitihani.
Katika shule ya Mihamakumi wilayani Sikonge, mwalimu mkuu na walimu wengine waliwafanyia watahiniwa mitihani lakini baadaye maafisa wa Takukuru waliwakamata.
Msonde alisema tukio jingine la udanganyifu lilifanywa Shule ya Msingi Qash wilayani Babati, Manyara ambapo mwalimu alijificha chooni, kupokea maswali kutoka kwa watahiniwa na kuandaa majibu ili kuwapa wanafunzi.
Katika shule ya St Getrude mkoani Ruvuma, mwalimu mkuu na walimu wengine walijificha mabwenini na watahiniwa walijifanya wanaomba ruhusa ya kwenda chooni, kisha walienda mabwenini kuchukua majibu na kuyasambaza ndani ya chumba cha mtihani.
Shule nyingine zilizohusika katika udanganyifu huo ni Tumaini iliyopo Halmashauri ya Sengerema (kuiba mtihani na kuandaa majibu), Little Flower Halmashauri ya Serengeti (kuiba mitihani na kuandaa majibu).
“Necta imewafuta matokeo yote watahiniwa 238 kutoka shule sita za mikoa tofauti tofauti waliobainika kufanya udanganyifu na tumezishauri mamlaka zinazohusika kuwachukulia hatua wote waliohusika kulingana na kanuni za utumishi na sheria za nchi,” alisema Msonde.
Aliongeza kuwa Necta haitamvumilia mtumishi yeyote anayevunja kanuni na sheria za nchi kwa kuvuruga usimamizi wa mitihani ya Taifa.
Imeandikwa na Shija Felician, Suzan Mwillo na Ephrahimu Bahemu.

Sumaye apewa notisi ya siku 90 kuendeleza mashamba


Dar es Salaam. Serikali imemtaka Frederick Sumaye kuendeleza mashamba yake mawili ndani ya siku 90, la sivyo itafuta hati ya umiliki wake, lakini waziri mkuu huyo mstaafu amesema notisi hiyo ni matokeo ya chuki ya Serikali dhidi yake baada ya kuhama CCM na kujiunga Chadema.
Sumaye, ambaye alikuwa mmoja wa wasemaji tegemeo kwenye mikutano ya kampeni za Uchaguzi Mkuu uliopita ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), anamiliki shamba lililoko mkoani Morogoro na jingine lililoko Mabwepande jijini Dar es Salaam, ambalo limevamiwa na wananchi.
Waziri wa Ardhi, William Lukuvi alisema hati ya shamba la Sumaye iko katika hatua ya kufutwa na kwamba Ofisa Ardhi Mteule wa Wilaya ya Kinondoni, Rehema Mwinuka ameshatoa barua ya notisi.

Sita wafutiwa adhabu ya kunyongwa hadi kufa



Dar es Salaam. Mahakama ya Rufani imewafutia adhabu ya kunyongwa hadi kufa na kuamuru kuachiwa huru watu sita waliohukumiwa kwa mauaji  ya askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) na mfanyakazi wa Benki ya NMB, tawi la Wami Morogoro.

Uamuzi huo ulisomwa jana na Jaji Projest Rugazia wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam baada ya kutolewa na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani lililoongozwa na Jaji Mkuu, Mohamed Chande. Wengine ni Jaji Ibrahimu Juma na Jaji Augustine Mwarija.

Jopo hilo lilikubali hoja za warufani waliowakilishwa na mawakili Richard Rweyongeza, Majura Magafu, Barnabas Luguwa, Samson Mbamba na Gabinus Galikano kuwa Mahakama Kuu ilikosea kuwatia hatiani kwa kuwa haikuwa na ushahidi wa kutosha.



NATIONAL EXAMINATIONS COUNCIL OF TANZANIA PSLE-2016 EXAMINATION RESULTS

http://necta.go.tz/matokeo/2016/psle/psle.htm

MATOKEO YA MTIHANI WA DARASA LA SABA 2016 – PSLE-2016 EXAMINATION RESULTS

Wednesday, October 26

Wachina Wawili Wadakwa kwa Kumteka Mwenzao

DAR ES SALAAM: JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata Wachina wawili, Wang Young Jing (37) Chen Chung Bao (35) kwa makosa ya utekaji nyara jijini Dar katika eneo la Palm Beach Hotel.


Kamishna wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, CP Simon Sirro, akilionyesha gari hilo lililokuwa limeibwa kwa wanahabari (hawapo pichani).
Akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam, Kamishna wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, CP Simon Sirro, amesema watu hao walimteka raia wa China mwanamke aitwaye  Liu Hong (48) ambaye alikuwa ni mfanyakazi wa  Le Grande Cassino waliyemteka Oktoba 23 mwaka huu ambapo  polisi walimkuta akiwa ndani ya chumba cha Hotel ya Palm Beach iliyoko Upanga jijini Dar es Salaam na walimkamata pia mtu aliyekuwa amekodi chumba hicho.

…Akizungumza na wanahabari (hawapo pichani).
Alifafanua kuwa Oktoba 24 majira ya saa kumi na moja jioni kikosi kazi cha wizi wa makosa ya kimtandao cha polisi kilifanikiwa kumtia nguvuni raia mmoja  wa China akiwa ndani ya chumba cha hoteli hiyo baada ya kuvunja mlango.


Madawa ya kulevya aina ya mirungi yaliyokamatwa na jeshi la polisi kwenye operesheni hiyo.
Sirro alisema baada ya kufungua chumba hicho walimkuta raia aliyetekwa akiwa hajitambui na akiwa na majereha usoni, pia palikutwa vipande vya taulo vyenye damu vilivyotumika kumfungia mikono ambapo alichukuliwa na kukimbizwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa ajili ya matibabu.
Ameeleza kuwa sababu kubwa ya utekaji nyara huo ilikuwa kumtaka majeruhi huyo atoe YEN 100,000 ambazo ni  sawa na dola za Marekani 19,000.
…Sirro akionyesha mitambo ya kutengenezea pombe aina ya gongo iliyokamatwa wakati wa operesheni.
Katika hatua nyingine Sirro amesema kuwa wamefanikiwa kukamata wezi wa magari na kupatikana kwa gari la ofisa wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Mkoa wa Morogoro, Capt. Innocent  Philipo Dallu ambaye alikuwa ameegesha gari lake maeneo ya Mbezi Juu akitokea kanisani  kwa ajili ya kuingia kwenye duka la vifaa vya ofisini na mashuleni ambapo gari hilo liliporwa.
…Akionyesha baadhi ya funguo bandia zilizokamatwa katika oparesheni hiyo.
Amesema jeshi lake  limefanikiwa kulikamata gari hilo aina ya Toyota Harrier lenye namba za usajili T 400 DEH huko Kiwangwa, Bagamoyo mkoani Pwani likiwa na watu wawili ambao ni  Ezekiel David (25) na Geofrey Nkwabi (52) na upelelezi utakapokamilika watuhumiwa watafikishwa mahakamani.


Mwijage Kuzindua Maonyesho ya Magari Dar


Mratibu wa maonyesho hayo, Ally Nchahaga (wa kwanza kulia) akizungumza na wanahabari.
WAZIRI  wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Charles Mwijage, atakuwa mgeni maalum katika kuzindua tamasha la  maonyesho magari nchini lijulikanalo kama Automotive Festival (Autofest) linalotarajiwa kuonyesha magari mapya na ya kisasa katika viwanja vya Biafra, Kinondoni,  jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 28 hadi 30 mwaka huu.
Akizungumza leo jijini Dar es Salaam Mratibu wa Maonyesho hayo, Ally Nchahaga, amesema tamasha hilo litakuwa na matoleo mapya ya kila aina ya magari kama vile magari ya abiria, ya biashara, bodi za magari, mashine zinazohusiana na magari sambamba na pikipiki za kisasa na burudani mbalimbali za kusisimua zitakazofanywa katika kuyaendesha magari na kurukisha pikipiki juu kwa mbwembwe na kadhalika.
“Tukio hili linahusisha moja ya maonyesho muhimu na yenye mvuto katika ulimwengu wa vyombo vya moto na lengo letu ni kuendelea kuleta aina mbalimbali ya bidhaa za vyombo vya moto na huduma kwenye ‘Autofest’ ili wadau wapate kujifunza na  kufurahia na kukidhi tamaa yao kwani magari yatakayokuwepo yanatumia teknolojia mpya na si ya zamani,” alisema Nchahaga.
Aidha alitaja viingilio katika tamasha hilo kuwa ni 10,000/= kwa sehemu ya kawaida, 5,000/= kwa watoto,  40,000/= ni kwa tiketi za  VIP na 100,000/= kwa tiketi za musimu.
Kaulimbiu ya tamasha hilo ni “Kuendesha tunaelekea wiki ya usalama barabarani, ni muhimu madereva kutoa fursa kwa madereva wenzao hata kama una haki”.

MFALME MOHAMMED VI WA MOROCCO AWEKA JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA MSIKITI


Mfalme Mohammed VI wa Morocco akibusu Masahaf kabla ya kumkabidhi Waziri Mkuu Kasim Majaliwa katika hafla fupi ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa msikiti kwenye eneo la BAKWATA Kinondoni jijini Dar es salaam Oktoba 25, 2016.  Kulia ni Mufti Mkuu wa Tanzania, Abukary Zubeir. Jumla ya Masahaf 10000 zilikabidhiwa na Mfalme huyo.(Picha n Ofisi ya Waziri Mkuu)


Mfalme Mhammed  VI wa Morocco na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  wakishuhudia wakati Mufti Mkuu wa Tanzania, Abubakary Zubeir (kulia)  akitia saini Makubaliano ya ujenzi wa Msikiti kwenye eneo la BAKWATA, Kinondoni jijini Dar es salaam Oktoba 25, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Mfalme   Mohammed VI wa wa Morocco,  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa , Rais Mstaafu Alhaj  Ali Hassan Mwinyi na Makamu wa Rais Mstaafu, Dkt. Mohammed Bilal wakiwa katika hafla fupi ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi wa msiki uliofnywa na Mfalme Mohammed wa Morocco kwenye  eneo la BAKWATA, Kinondoni jijini Dar es salam Oktoba 25, 2016. (icha na Ofisi ya Waziri Mkuu)




Tuesday, March 22

Salma asimulia alivyotekwa


Mwandishi wa habari wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) na DW, Salma Said amedai alitekwa na wanaume wawili baada ya kumkamata na kumuingiza kwenye gari lao kisha kuondoka naye na kumpeleka kusikojulikana.
Salma aliyetekwa Ijumaa iliyopita na watu hao katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) akitokea Zanzibar kwa ajili ya  kuchunguzwa afya yake kwenye moja ya hospitali za jijini hapa, alisimulia mkasa huo jana mbele ya  waandishi wa habari huku akimwaga machozi.
Alisema alipoteremka uwanjani hapo, alimpigia simu dereva wake amfuate na wakati akimsubiri,  ndipo wakatokea watu hao.
Salma alisema watu hao walimfunga mtandio wake mweusi usoni ili asibaini mahali walikokuwa wakimpeleka na kumfungia chumbani
Alisema ndani ya chumba hicho kulikuwa na vitambaa.  
“Waliponiingiza ndani ya chumba kile siku ya kwanza, wakanifungua tambala usoni kwa hivyo nikawaona nyuso zao, mmoja alikuwa na kovu shavuni, mrefu na mwingine mweupe kidogo, waliniweka kule ndani bila kupata chakula chochote,” alisema.
Salma alisema alitakiwa kurudi Zanzibar kwa ajili ya kuripoti marudio ya Uchaguzi Mkuu wa marudio uliofanyika juzi, lakini alishindwa baada ya watu hao kumteka na kumfungia kwenye chumba hicho.
Alidai kuwa watu hao walimwambia watamuachia baada ya uchaguzi huo kufanyika na mgombea wa CCM kutangazwa kuwa mshindi.
Katika mkutano huo na waandishi wa habari uliofanyika katika ofisi za Baraza la Habari Tanzania(MCT), Salma aliongozana na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Theophil Makunga, Katibu Mtendaji wa MCT, Kajubi Mukajanga na Mratibu wa Kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Bara (THRDC), Onesmo Ole Ngurumwa, ambao kwa pamoja walieleza kupinga ukatili huo huku wakiliomba Jeshi la Polisi kuwasaka wahalifu waliohusika.
“Walinisababishia maumivu makali, walinipiga mabuti na makofi huku wakiniambia maneno ya vitisho kama ilivyokuwa kwa Dk Ulimboka na Kibanda,” alidai Salma.
Kabla ya watekaji hao kumrudisha katika eneo walilokuwa wamemteka, Salma alidai kuwa watu hao walimpiga kila walipoingia na kutoka nje ya chumba alichowekwa na kumsababishia apumue kwa tabu.
Akijibu swali la mwandishi wa habari aliyetaka kupata ufafanuzi wa taarifa za uvumi wa kujiteka mwenyewe, Salma alijibu swali hilo  huku akidondosha machozi: “Hakuna sababu ya kusema uongo, mimi ni Mwislamu na dini yangu inakemea kufanya hivyo.” 
Pia, alisema amefanya kazi kwa miaka zaidi ya 20 na matukio ya vitisho yalianza alianza kuyapata muda mrefu kwa kupigiwa simu, kutumiwa meseji na kufuatwa nyumbani kwake.
Salma ambaye alizungumza huku akionyesha ushahidi wa meseji za makundi ya mitandao yanayojadili kufurahishwa na kutekwa kwake, alisema kujiteka ni kauli zisizokuwa na uhusiano wowote na ukweli, kwani alijitambulisha kuwa mwandishi mtetezi wa haki za binadamu na siasa ambazo zinazokinzana na maslahi ya wachache.
Wakati huohuo; Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Siro alisema ni mapema kuzungumzia tukio la kutekwa kwa Salma kwa madai kuwa bado wanaendelea kufanya uchunguzi.

MOTISHA KWA WALIMU NA ARI YA UFUNDISHAJI

Siri ya madini Tanzanite kutoroshwa yabainika


Dar es Salaam. Udhaifu wa sheria zinazosimamia uchimbaji wa Tanzanite umetajwa kuwa chanzo cha madini hayo kuuzwa kwa wingi na nchi za Kenya, India na Afrika Kusini badala ya Tanzania yanakopatikana.
Hayo yalibainika wiki iliyopita katika ziara ya wahariri wa vyombo vya habari kwenye mgodi wa TanzaniteOne Mine Limited (TML), uliopo Mirerani Simanjiro mkoani Manyara.
Mkuu wa Usalama wa TML, George Kisambe alisema ingawa wameimarisha ulinzi kwa asilimia 90 kwa kushirikiana na Stamico chini ya Serikali, udhaifu kwenye sheria unatoa mwanya kwa hujuma dhidi ya Tanzanite na kampuni yao.
“Usimamizi wa sheria ndiyo unaosababisha Kenya na India zionekane kuongoza katika uuzaji Tanzanite inayochimbwa Tanzania pekee,” alisema Kisambe.
Hali hiyo inatajwa pia kudhoofisha usalama na kuwasukuma wawekezaji kuweka idadi kubwa ya walinzi kwenye migodi yao kudhibiti hali ya usalama kwa kuhofia uvamizi wa maeneo yao ya uchimbaji.
“Ili kurekebisha hali hiyo ni vyema Serikali ije na mkakati mbadala wa usimamizi wa madini haya, ikiwezekana iweke ukuta kama ilivyo kwa Israel na Palestina kuzitenganisha na kutambua maeneo yote ya uchimbaji,” alisema.
Alisema kitakwimu kampuni hiyo inachimba chini ya asilimia 30 ya madini yote ya Tanzanite na mapato yake yanajulikana na Serikali kwa kuwa na udhibiti huku ikilipa kodi.
Kaimu Mkurugenzi wa TML, Modest Apolinary alisema uvamizi wa wachimbaji wadogo katika mgodi huo ni changamoto inayopoteza kiwango kikubwa cha mapato na kuiomba Serikali kumaliza tatizo hilo.
“Serikali ina mamlaka ya kufanya uamuzi dhidi ya wachimbaji wavamizi ili TML iendelee kuchimba eneo lake, iongeze ajira kwa vijana na ichangie zaidi mapato ya Serikali kwa kulipa kodi inayotakiwa,” alisema Apolinary.

Wawili wafariki Dar kwa dalili za ebola

Dar es Salaam. Watu wawili wamefariki dunia kwa maradhi ambayo dalili zake zinafanana na ugonjwa wa ebola.
Watu hao walifariki baada ya kufikishwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wakiwa wanatoka damu sehemu mbalimbali za miili yao ikiwamo kwenye ngozi, mdomoni, puani na matundu mengine ya mwili.
Mgonjwa wa kwanza alifariki dunia Machi 16 saa nane usiku na mwingine jana mchana. Wote walifariki ndani ya saa 12 baada ya kufikishwa hospitalini hapo.
Mkuu wa Kitengo cha Uchunguzi wa Magonjwa MNH, Dk Praxeda Ogweyo alisema wamewapokea wagonjwa hao wawili,  lakini vipimo havijaonyesha kama wana ebola.  “Ni kweli kuwa tumewapokea wagonjwa hao wawili na vipimo vya mgonjwa wa kwanza kinaonyesha hana ebola, lakini bado wanaendelea kufanya uchunguzi wa kina kujua ni ugonjwa gani,” alisema.
Dk Ogweyo alisema majibu ya mgonjwa wa pili aliyefariki jana bado hayajatoka.
Taarifa za awali zilizopatikana kutoka kwa ndugu wa marehemu zinaeleza kuwa wagonjwa hao wote walipita Mafinga, Iringa kabla ya kuja Dar es Salaam.
Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu alisema wizara yake imepokea taarifa hizo: “Tumepeleka sampuli kwenye maabara ya Taifa, majibu yote ni negative (hawana ebola). Hata hivyo, tumeamua kupeleka nje ya nchi kwa ajili ya kujiridhisha zaidi,” alisema.
Waziri Mwalimu alisema sampuli hizo mbili za damu zimepelekwa Taasisi ya Uchunguzi wa Magonjwa Kenya (KIMR).
Hata hivyo, alisema miili yao itazikwa na Serikali kupitia ofisi ya Mganga Mkuu wa Serikali na ndugu wa marehemu watapewa ushauri nasaha.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Dk Grace Mganga alisema kutokwa na damu kunaweza kuwa na sababu nyingi, ikiwamo homa ya dengue, ebola na upungufu wa chembe ndogo za damu zinazouia damu kutoka kwa wingi.
Shemeji wa mmoja wa marehemu hao, Juma Seromba alisema ndugu yao alianguka akiwa kazini kama mgonjwa wa kifafa, akaanza kutokwa damu sehemu mbalimbali mwilini na baadaye walimpeleka MNH.

Pengo la CUF lajitokeza wazi Pemba

https://youtu.be/LCY1dmtFE1E
Pemba. Kitendo cha CUF kususia uchaguzi kimeelezwa kuwa kwa kiwango kikubwa kimesababisha watu wachache kujitokeza katika uchaguzi wa marudio uliofanyika jana.
Wasimamizi wa vituo vya uchaguzi, wapigakura, ambao hawakupiga kura na baadhi ya viongozi waliozungumza na gazeti hili kisiwani Pemba walisema pamoja na mambo mengine, kitendo cha CUF kutoshiriki uchaguzi huo kimechangia hali hiyo.
Uchaguzi huo wa marudio umefanyika baada ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) Jecha Salim Jecha kufuta matokeo ya udiwani, uwakilishi na urais Oktoba 28 mwaka jana kwa maelezo kuwa ulikuwa na kasoro nyingi.
Mwandishi wetu alitembelea vituo zaidi ya 10 katika mikoa ya Kusini Pemba na Kaskazini Pemba na kukuta idadi ndogo ya wapigakura, jambo ambalo liliwafanya wasimamizi wa vituo hivyo kutumia muda mwingi kupiga stori.
Mbali na wasimamizi hao, hata mawakala wa vyama waliokuwapo katika vituo hivyo wengi walikuwa wa CCM na wachache wa ADC na Tadea, tofauti na idadi ya vyama vilivyotangazwa kushiriki uchaguzi huo.
Pemba kuna vituo vya uchaguzi 463 na kila kimoja kilipaswa kuwa na wapigakura takribani 1,000 hadi 3,500, lakini mpaka kufikia jana saa sita mchana vingi vilikuwa tupu huku wasimamizi wakikiri kuwa idadi ya waliojitokeza ni ndogo.
Msimamizi wa uchaguzi katika kituo cha Wawi A, Kusini Pemba, Ismail Issa Juma alisema jambo pekee lililojitokeza katika kituo hicho ni idadi ndogo ya wapigakura.
Alisema kituo hicho kina wapigakura 1,400 na waliokuwa wamejitokeza mpaka kufikia saa nne asubuhi walikuwa hawajafika robo ya idadi hiyo.
Mgombea urais kwa tiketi ya ADC, Hamad Rashid Mohamed ambaye alipiga kura katika kituo hicho alisema kutoshiriki kwa CUF ni sababu ya wananchi kutojitokeza.
“Hapa Pemba CUF wana nguvu. Hii ni ngome yao, hivyo usitegemee kuona watu wengi hapa ila binafsi ninaamini asilimia 40 ya watu wote waliojiandikisha kupiga kura watajitokeza leo (jana) kuchagua viongozi wanaowataka,” alisema Hamad ambaye alivuliwa uanachama wa CUF na kuanzisha ADC.
Alisema anaamini atashinda urais katika uchaguzi huo kutokana na CUF kujitoa, huku akisisitiza kuwa kasoro zilizopo ZEC na Serikali ya Mapinduzi  Zanzibar (SMZ), zitamalizwa likipatikana baraza la wawakilishi na rais na si kususia uchaguzi.
Msimamizi wa uchaguzi katika kituo cha Wawi B ambacho mgombea urais wa AFP, Said Sudi Said alipiga kura, Mussa Abdallah Kilindo alisema si rahisi wapigakura 950 katika kituo hicho wote wakapiga kura.
Mkazi wa Wawi, Omar Mohammed Hassan alisema idadi ya watu waliojitokeza ina tofauti kubwa na ya uchaguzi wa Oktoba 25 kauli ambayo iliungwa mkono na mkazi mwingine wa eneo hilo, Mafunda Abdalla.
Hali ilikuwa tofauti zaidi katika vituo vya kupigia kura vilivyopo Wilaya ya Wet, Kaskazini Pemba ambako pia kunatajwa kuwa ngome ya CUF kutokana na kujitokeza kwa watu wachache zaidi.
Mwandishi wetu alishuhudia baadhi ya wasimamizi wa vituo hivyo wakiwa wamelala katika madawati wakisubiri wapigakura ambao walikuwa wakifika mmojammoja.
“Kama unavyoona shughuli ya kupigakura inaendelea vyema kabisa na kuna usalama wa kutosha. Watu wanakuja ila si wengi kama ilivyokuwa Oktoba 25. Kituo hiki kina wapigakura 1,950,” alisema Maalim Haji, msimamizi wa uchaguzi Kituo cha Shule ya Msingi Kizimbani.
Mkazi wa Kizimbani, Sada Hamad Shamata aliyekutwa akipiga kura katika kituo hicho alisema: “Uchaguzi umekwenda vyema na hakuna usumbufu wala kusukumana maana watu ni wachache tofauti na uchaguzi uliopita.”
Mkazi mwingine wa Kizimbani, Ali Juma Fakih alisema: “Hilo siyo swali sheikh ni jibu. CUF kususia uchaguzi huu ndiyo sababu ya wapigakura kuwa wachache.”
Mkuu wa wilaya ya Wete, Rashid Hadid Rashid aliyekuwa akizunguka vituo vyote vya uchaguzi vilivyopo katika wilaya hiyo alisema ni kawaida uchaguzi wa marudio kujitokeza watu wachache.
“Pemba CUF wapo wengi hilo lipo wazi ila binafsi kama mkuu wa wilaya nina jukumu la kuhakikisha hali ya usalama inakuwa shwari,” alisema Rashid.
Katika Kituo cha Ukunjwi, Jimbo la Gando, Kaskazini Pemba mwandishi wetu alishuhudia wapigakura watatu waliojitokeza baada ya kukaa hapo kwa nusu saa.
Katika kituo hicho baadhi ya majina ya wapigakura yaliyobandikwa ukutani yalikuwa yamechanwa hivyo kuwapa wakati mgumu waliofika kupigakura.

Saturday, March 19

Wakuu 21 wa wilaya kwenye chekeche

Baada ya kufanya uteuzi wa wakuu wa mikoa uliowaondoa makada 12, homa ya chekeche la Rais John Magufuli sasa linahamia kwa wakuu wa wilaya, ambao baadhi wameshaanza kuaga wakisema hawana uhakika wa kuendelea kushika nafasi zao.
Hali hiyo inatokana na Rais kuweka bayana vigezo atakavyotumia kufanya uteuzi wa wakuu hao wa wilaya ambavyo ni pamoja na suala la migogoro ya ardhi, tatizo la elimu hasa upungufu wa madawati, njaa na mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu.
“Nikisikia wilaya inaomba chakula wakati mvua zinanyesha wakati huu, nitakuwa na shaka na viongozi waliopo. Wanashindwaje kuhamasisha kilimo?” alihoji Rais.
Vigezo hivyo alivitangaza wakati akizungumza na wazee wa Jiji la Dar es Salaam, lakini katika uteuzi wa wakuu wa mikoa alizungumzia pia suala la wafanyakazi hewa ambao wamekuwa wakilipwa mishahara bila ya wahusika kuchukua hatua kudhibiti.
Kwa maana hiyo, vigezo vya Dk Magufuli vinaweza kuwa vingi zaidi kulingana na matatizo ya eneo la wilaya, hasa baada ya mkuu huyo wa nchi kuamua kutumia vijana wake kwenda kuchunguza matatizo kwenye maeneo ambayo anataka kusimika uongozi.
Suala la udhibiti wa fedha za umma, hasa mishahara ya wafanyakazi hewa, linaweza kuwa kigezo kikubwa cha Dk Magufuli hasa kutokana na tatizo hilo kuzungumzwa kwa muda mrefu bila ya kutafutiwa ufumbuzi na udhibiti wa mapato kuwa moja ya ajenda kubwa za Serikali ya Awamu ya Tano.
Kwa mujibu wa uchunguzi ambao Mwananchi imeufanya kwenye baadhi ya mikoa, chekeche hilo la Rais linawaweka kwenye hali ngumu wakuu wa wilaya 21 iwapo watabainika hawajachukua hatua madhubuti za kukabiliana na matatizo hayo manne.
Suala la njaa litakuwa limewagusa viongozi wa Wilaya ya Isimani mkoani Iringa, Chamwino (Dodoma) na Rorya (Mara) pamoja na Kilindi mkoani wa Tanga ambako kuliripotiwa baa la njaa.
Akizungumza katika mkutano ulioandaliwa na wazee mkoani Dar es Salaam Februari 15, Rais Magufuli aliitoa mfano wa Wilaya ya Bariadi iliyopo Mkoa wa Simiyu, akisema imejenga kilomita 4.5 za barabara ya lami kwa Sh9.2 bilioni, fedha ambazo zingetosha kujenga kilomita 22 mpaka 23 za lami.
“Viongozi wao wapo, mkuu wa mkoa yupo, mkuu wa wilaya yupo, mkurugenzi wa manispaa yupo, injinia yupo! Kwa hiyo, ninapozungumza kutumbua majipu, mniunge mkono nitumbue kwelikweli,” alisema.
Mkuu wa wilaya hiyo, Ponsiano Nyami, ambaye aliwahi kumuomba Rais wa Serikali ya Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete atengue uteuzi wake kwa kushindwa kushughulikia kikamilifu ujenzi wa maabara, atakuwa akiangalia mlango wa kutokea.
Siku chache zilizopita alitoa kauli iliyoonekana kama anaaga baada ya kusema kwenye mkutano kuwa hakuna mwenye uhakika wa kubaki kwenye nafasi hizo.
Migogoro ya ardhi isiyokwisha mkoani Morogoro, hasa Wilaya ya Mvomero ambayo ilisababisha Dk Rajab Rutengwe avuliwe ukuu wa mkoa, itamuweka kwenye hali mbaya mkuu wa wilaya hiyo, Betty Mkwasa baada ya mapigano kutokea mara mbili tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani Novemba mwaka jana.
Hivi karibuni, zaidi ya mbuzi na kondoo 38 waliuawa kutokana na migogoro ya wakulima na wafugaji. Hii ilitokea wiki chache baada ya mtu mmoja kuuawa sawia na ng’ombe zaidi ya 71.
Wakati mapigano yalipotokea Desemba, Mkwasa alisema mapigano hayo yamekuja wakati Serikali ya wilaya ikijipanga kufanya operesheni ya kuwaondoa wafugaji wavamizi kwa kuwa asilimia kubwa kijiji hicho ni wakulima.
Mkwasa alisema mifugo inayoingia ni ile inayoondolewa katika Hifadhi ya Wami Mbiki na mingine inayotokea wilaya za Handeni na Kilindi za mkoani Tanga na Manyara, hivyo imekuwa ikiingia katika vijiji vya wakulima na kusababisha migogoro.
Migogoro ya ardhi pia iko wilayani Nyamagana ambako Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi aliunda kamati ya ushauri kuhusu kuhusika kwa maofisa ardhi kwenye migogoro hiyo.
Kutokana na wafanyakazi wa halmashauri kuwa chanzo cha migogoro ya ardhi Nyamagana, tayari Waziri Lukuvi amesimamisha kazi wafanyakazi mara mbili baada ya kupelekewa malalamiko na wananchi.
Mkuu wa wilaya aaga watumishi
Suala la elimu ambalo lilimfanya Paul Makonda kupanda cheo kutoka mkuu wa wilaya hadi mkoa, litakuwa mwiba mchungu kwa mkuu wa Wilaya ya Nyamagana ambayo ina upungufu wa madawati 16,558 katika shule zake 153 za msingi na sekondari.
Mkuu wa wilaya hiyo, Baraka Konisaga jana alitumia mkutano wa kujitambulisha kwa mkuu mpya wa Mkoa wa Mwanza, kuaga watumishi wa Serikali akisema anaweza asiwemo kwenye uteuzi mpya.
“Naweza kuongea nanyi hapa muda huu nikiwa mkuu wa wilaya, lakini jioni mkasikia uteuzi wa wakuu wapya wa wilaya. Naweza kuwamo na nikabakishwa hapahapa Nyamagana, nikahamishiwa wilaya nyingine au nisiwemo kabisa kutokana na vigezo kadhaa ikiwamo utendaji na umri.”
Hata hivyo, alijimwagia sifa kuwa kwa kipindi chote alichokuwa mkuu wa wilaya hiyo kwa vipindi vitatu tofauti vya uteuzi, alifanya kazi kubwa kusimamia maendeleo, ulinzi na usalama wa wananchi, huku akikaimu nafasi ya mkuu wa mkoa.
Alipoulizwa mara baada ya kikao hicho kumalizika kwa nini aliamua kuaga, Konisaga alisema: “Ni jambo la kawaidia kuwaandaa kisaikolojia watumishi wenzako iwapo kutatokea mabadiliko yoyote. Hakuna ajabu na wala hii haimaanishi kwamba sijiamini katika utendaji wangu. Najiamini sana na nimetekeleza wajibu wangu kikamilifu.”
Mkoani Tanga, aliyekuwa mkuu wa mkoa huo, Mwantumu Mahiza alisema wakati akimkabidhi rasmi ofisi mbadala wake, Martin Shigela kuwa kwa migogoro ya ardhi kwenye maeneo sugu kama Jiji la Tanga na wilaya za Kilindi na Handeni, kamati iliyoundwa kushughulikia tatizo hilo imeshamaliza kazi na dawa imeshapatikana.
Pamoja na maelezo hayo ya Mwantumu, migogoro ya ardhi ni tatizo kubwa mkoani Tanga na kumekuwa na malalamiko mara kwa mara ya kutokuwa na imani hata na kamati ilivyofanya kazi hiyo ya kutafuta dawa ya migogoro isiyokwisha baina ya wafugaji na wakulima, pia ugomvi wa mipaka ya vijiji mkoa wa Tanga na Manyara.
Ikiwa kitafuatwa kigezo cha  migogoro ya ardhi basi wakuu wa Wilaya za mkoa huo, Abdullah Lutavi (Tanga) Selemani Liwowa (Kilindi ) na Husna Rajab (Handeni) wanaweza kuwa katika hatihati ingawa maeneo yao kwa kipindi hiki yametulia ikilinganishwa na miaka ya nyuma.
Kipindupindu jipu Kyela
Mkoa wa Mbeya, Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Thea Ntara yuko kwenye hali ngumu kutokana na tatizo la ugonjwa wa kipindupindu.
Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Clemence Kasongo alisema ugonjwa huo unamnyima usingizi kutokana na kuibuka kwenye mwambao wa Ziwa  Nyasa ambako kuna wagonjwa wengi ambao alisema hutokea Wilaya ya Ludewa.
Kutokana na tatizo hilo kuwa kubwa wilayani Kyela, mwezi uliopita wazee wawili wa kitongoji cha Bulinda waliuawa na wananchi kwa madai kuwa ndiyo wanaosababisha watu waugue kipindupindu kwa njia za kishirikina.
Ugonjwa huo pia uko kwenye wilaya za Musoma Vijijini, Ilala na Mpanda.
Wakuu wa wilaya mbili za mkoani Kilimanjaro wamekalia kuti kavu katika vigezo hivyo.
Wilaya ya Same inakabiliwa na migogoro ya ardhi baina ya wananchi wa jamii ya wafugaji wa Kimasai katika Kijiji cha Ruvu Mferejini na mwekezaji wa kampuni ya IBIS International Ltd.
Tangu mwaka 1988, mmiliki wa IBIS International Ltd ambaye ni raia wa Sweden aliingia mkataba na wananchi wa Kijiji cha Ruvu kabla ya kijiji hicho kugawanyika na kuunda kijiji kingine cha Ruvu Mferejini kwenye shamba lenye ukubwa wa ekari 642.
Pia, Wilaya ya Mwanga inakabiliwa  na mgogoro wa ardhi baina ya wanakijiji cha Jipe na mwekezaji wa kampuni ya kitalii ya Asante Tours kuhusu eneo la ekari 3,000. Migogoro yote hiyo bado haijatatuliwa.
Mkoani Dodoma ukiacha Wilaya ya Chamwino ambayo imekuwa ikabiliwa na njaa, Kongwa kumekuwa na mgogoro wa ardhi wa muda mrefu kati ya wakulima na wafugaji ambao pia umekuwa ukihusisha Wilaya ya Wilaya ya Kiteto na kusababisha mgongano kwa wanasiasa.
Mgogoro wa wakulima na wafugaji katika wilaya hizo mbili umekuwa wa muda mrefu na uliingia kwenye Bunge la Kumi.
Mauaji mengi yamekuwa yakitokea upande wa Kiteto lakini yakihusisha wakazi wa Kongwa, kiasi cha kusababisha mbunge wao, Job Ndugai, ambaye sasa ni Spika wa Bunge, kulalamika bungeni dhidi ya ungozi wa Wilaya ya Kiteto.
Arusha na migogoro ya ardhi
Wilaya tatu za Mkoa wa Arusha; Ngorongoro, Monduli na Arumeru, bado zinakabiliwa na tatizo la migogoro ya ardhi lakini kuna jitihada zinaendelea kuitatua.
Wilaya ya Ngorongoro ambayo mkuu wake ni Hashim Mgandilwa bado ina migogoro ya mipaka ambayo imekuwa ikisababisha mapigano ya jamii ya Wasonjo na Wamasai. Monduli, ambayo mkuu wake ni Francis Miti kulikuwa na migogoro ya ardhi ya mashamba kutokana na maofisa ardhi kugawa ovyo viwanja kwa masilahi yao.
Wilayani Arumeru, hasa eneo la Meru, ambako Mkuu wa Wilaya ni Wilson Nkumbaku kuna migogoro ya ardhi baina ya wamiliki wakubwa na vijiji. Wakuu wa wilaya hizo wameeleza changamoto zote zinaendelea kupatiwa ufumbuzi. Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Mngandilwa alisema wilaya yake ni salama baada ya migogoro kupungua, wakati Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Fadhili Nkurlu alisema Arusha sasa ni shwari na wananchi wanashiriki mambo ya maendeleo.
Imeandaliwa na Burhani Yakub, Lauden Mwambona, Happiness Tesha, Sharon Sauwa, Ngollo John na Mussa Juma.     

‘Namuunga mkono Mpungwe kuhusu Z’bar’


Dar es Salaam. Ikiwa imebaki siku moja kabla ya Uchaguzi wa Marudio kufanyika Zanzibar, mfanyabiashara maarufu nchini, Hashim Ismail amesema Taifa haliwezi kujidanganya kwamba kila kitu ni shwari visiwani humo.
Alisema hayo jana akiunga mkono kauli ya Balozi Ami Mpungwe aliyoitoa katika mahojiano na gazeti hili wiki hii akisema, Taifa halipaswi kujidanganya kwamba Zanzibar hakuna tatizo. Alisema: “Mtanzania yeyote aliyesoma yale aliyozungumza Ami (Mpungwe) hana budi kumuunga mkono. Pia, mimi nakubaliana naye; kuna shida, hatari kubwa na ufisadi mkubwa wa kisiasa. Na kama alivyosema hatuwezi “ku-pretend everything in the garden is rosy (hatuwezi kujidanganya kwamba kila kitu kilichopo katika bustani ni waridi).
“Lakini kama ilivyo kawaida yetu ya uchwara, woga na kujikomba, yale aliyozungumzia Ami yalienda na gazeti la jana (juzi) na kubaki karatasi tu ya kufungia vitumbua.
“Jambo hili si la ZEC (Tume ya Uchaguzi Zanzibar), CCM na CUF tu, ni suala la haki za binadamu. Linatuhusu sote.”
Mzee Ismail alisema Balozi Mpungwe alipendekeza kurudi kwenye meza ya mazungumzo akisisitiza kwamba ni jambo sahihi kabisa lakini akahoji:
“Uchaguzi unaorudiwa Machi 20 (kesho) chini ya ulinzi mkali wa vyombo vya dola... Unaosusiwa na vyama vingine vya siasa, utakuwa umeshamalizika. Sasa itakuwaje?
Hoja ni kuufuta kwanza kisha turudi katika meza.” Katika mahojiano maalumu na Mwananchi, Mpungwe ambaye ni balozi wa zamani wa Afrika Kusini alihadharisha kuhusu hali ya kisiasa Zanzibar akisema “tusijidanganye kuwa hakuna matatizo” kwenye visiwa hivyo na kutaka ufumbuzi utafutwe kabla haujasababisha madhara.    

Mji Mkongwe; hazina hatarini kupoteza hadhi


Zanzibar ina visiwa viwili vya Unguja na Pemba, ikitambulika duniani kutokana na historia na utamaduni wake wa asili ulioambatana na vivutio mbalimbali. Miongoni mwa mambo hayo ni Mji Mkongwe. Ni mji wa kale ambao mwaka 2000, Shirika la Kimataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (Unesco) liliamua kuupa hadhi kuwa Eneo la Urithi wa Dunia.
Kama ilivyo kwa miji mengine mikongwe duniani, Mji Mkongwe una utajiri wa historia na vivutio tofauti ukijengeka kwa ramani kwa umbo la sambusa. Ni eneo dogo lenye wastani wa majengo 1,700 ya kila aina. Kuna chochoro (Narrow Street)23, makanisa mawili, misikiti 52, maghorofa 50, varandaa na baraza zenye milango zaidi ya 200 iliyonakishiwa kwa ufundi wa hali ya juu.
Katika Mji Mkongwe kuna jumla ya majengo 1,100 yaliyotambuliwa kuwa yenye thamani kubwa katika utaalamu wa ujenzi, hivyo ni kivutio kikubwa kwa watalii. Kwa mujibu wa takwimu za Kamisheni ya Utalii Zanzibar, zaidi ya asilimia 80 ya wageni wanaotembelea Zanzibar hutembelea maeneo ya Mji Mkongwe. Majengo hayo ni Jumba la Ajabu maarufu Baitil Ajaib (House ofWonder), Old Dispensary, Bandari Kuu,
Mahakama, Hospitali ya Rufani, Ikulu, Hamamu ya Hamamni, Ngome Kongwe Jengo la Tiptip, Kanisa Kuu Katoliki la Minara Miwili na Mkunazini (Soko la Watumwa), Mahekalu ya Wahindu, Jumba la Maparisi na Jamati sita za Mashia.
Mwaka 1830, nyumba za Mji Mkongwe zilijengwa chini ya utawala wa Sultani Sayyid Said, alipohamishia makao makuu yake Zanzibar kutoka Oman.
Licha ya vivutio hivyo vya asili, kuna utamaduni unaombatana na matamasha mbalimbali ambayo hufanyika kila mwaka likiwamo la Nchi za Majahazi na Sauti za Busara, yote ni vivutio kwa watalii na hufanyika Mji Mkongwe.
Hata hivyo, mji huo umeingizwa katika maeneo ya urithi wa dunia ulio hatarini kutoweka kutokana na Serikali kushindwa kufuata vigezo na masharti yaliyowekwa na Unesco lililoupa hadhi hiyo miaka 15 iliyopita.
Mkutano wa Kamati ya Urithi wa Kimataifa uliofanyika Juni 2015 mjini Bonn nchini Ujerumani, umetoa mwaka mmoja kwa State Party kutekeleza baadhi ya mambo yaliyoonekana kuwa na athari kwa Mji Mkongwe wa Zanzibar, iwapo hayatatekelezwa yatauweka Mji Mkongwe katika orodha ya urithi uliopo hatarini (World Heritage in Danger List).
Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Utalii, Saleh Ramadhan Feruz anaona tishio hilo la Unesco siyo tu litaathiri sekta ya utalii Zanzibar, bali Taifa nzima.
“Mji Mkongwe ukitolewa kwenye urithi wa dunia utatuathiri kiuchumi, kwani uchumi wetu unategemea utalii kwa sababu kati ya watalii wote wanaokuja kutembelea Zanzibar, asilimia 85 wanatembelea mji huo,” anasema Feruzi.
Inaelezwa kwamba tangu miaka ya 1970, baadhi ya majengo yamekuwa yakiporomoka ndiyo sababu ya Zanzibar kuiomba dunia iyahifadhi majengo hayo, ikiwamo jengo maarufu la Bait El-ajaib au Jumba la Maajabu.
Kuna changamoto kadhaa zinazoweza kuuweka Mji Mkongwe kwenye orodha ya urithi wa dunia unaotoweka, tayari hatua mbalimbali zimeanza kuchukuliwa ili kuuhifadhi usiondolewe kwenye orodha hiyo.
Tatizo linalouweka Mji Mkongwe hatarini ni kutofuata taratibu zilizowekwa na Unesco na kuacha magari makubwa yenye uzito usiostahiki kupita eneo hilo, kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Mamlaka ya Mji Mkongwe, huingia magari 17,000 kwa siku yenye uzito tofauti wakati inatakiwa magari yasiyozidi uzito wa tani mbili.
Dosari nyingine ni ujenzi holela wa hoteli za kitalii ulioongezeka bila ya kuzingatia masharti ya Mji Mkongwe, jambo ambalo hutia doa urithi huo wa dunia.
Sheha wa Mji Mkongwe, Mohammed Juma Mugheiry anasema suala la kujengwa hoteli kubwa ndani ya mji huo ni jambo lisilokubalika.
“Ujenzi wa hoteli kubwa za kitalii ni hatari kwa mji wetu, ndiyo sababu ya Zanzibar kupewa onyo la kuwekwa kwenye miji hatari, kwani huwezi kuwa na hoteli kubwa kama hizi na usihitaji huduma ambazo zitachangia kuongeza magari yenye uzito wa tani kubwa kuingia Mji Mkongwe,” anasema Mugheiry.
Tatizo jingine ni watendaji wa Serikali kushindwa kuchukuwa hatua kwa makosa mbalimbali ya utendaji yanayofanywa.
“Sijui tunaogopa nini kuwachukulia hatua wale watendaji wenye kukaidi masharti hayo?” anahoji.Katika mkutano wake wa Julai mwaka jana nchini Ujerumani, Unesco ilitoa mwaka mmoja kwa Zanzibar kurekebisha kasoro zinazoonekana, ikiwamo ujenzi holela na uingizwaji magari mazito ili kuhifadhi mji huo.
Mwanahistoria na mkazi wa Mji Mkongwe, Profesa Abdul Shareef anasema hofu yake ni kutolewa kwa mji huo katika orodha ya urithi wa dunia hali itakayoiathiri Zanzibar.
“Ni hatari kubwa Zanzibar tukija kutolewa kwenye urithi wa dunia kwa sababu tutashindwa tena kuwapata watalii wengi, kwani wengi wanapokuja hufika Mji Mkongwe,” anasema Profesa Shareef.
Zanzibar imekuwa ikionywa juu ya usalama na utunzaji Mji Mkongwe katika mikutano ya wadau wanaokutana duniani, ambayo huandaliwa na Unesco.
Kuoneana tatizo la rushwa, kuogopana na ukosefu wa fedha ni miongoni mwa changamoto zinazotajwa kukwamisha maendeleo ya Mji Mkongwe hata kusababisha Zanzibar kutishiwa kuondolewa miongoni mwa vivutio hivyo.
Hata hivyo, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Mji Mkongwe Zanzibar, Issa Sariboko Makarani amesema kuna hatua ambazo lazima zichukuliwe ili kuuhami na kuuweka salama mji huo.
Makarani anasema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kupitia Mamlaka ya Mji Mkongwe iliamua kutekeleza mpango mkuu wa matumizi ya vyombo vya moto na watembea kwa miguu mwaka 2006.
Amesema mpango huo ulitayarishwa kwa kushirikishwa taasisi mbalimbali kama wadau wa mpango huo, hivyo kutakiwa kutangazwa mara moja kwa utekelezaji.
Licha ya hilo, Unesco kupitia Kamati ya Urithi wa Dunia iliitaka Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania SMZ, kutayarisha mpango mkuu wa matumizi ya vyombo vya moto na watembea kwa miguu na kuuwasilishwa mara moja kwa ajili ya utekelezaji.
“Matumizi ya vyombo vya moto ndani ya Mji Mkongwe umezidi kupitia kiwango, kutokana na uongezekaji huo utasababisha athari kubwa kwa mji ambao ni urithi wa dunia,” anasema Makarani.
Anasema Mji Mkongwe unapokea wageni wengi wa kitalii na kusababisha kuleta usumbufu mkubwa wakati wa matembezi yao, wakati wakifanya shughuli zao za kitalii maeneo mbalimbali huku magari makubwa na mazito yakihatarisha majengo hayo ya kale.
Tayari, Serikali imezishirikisha taasisi zote na wadau kwa kuupitia vizuri mpango huo kwa ajili ya utekelezaji wake mara moja, kufuatia vikao mbalimbali kutoka ngazi za juu hadi utekelezaji.
Hatua zilizochukuliwa hadi sasa zimeanza Februari 2016, ni kufunga baadhi ya njia ili kupunguza msongamano wa magari yanayoingia maeneo ya Mji Mkongwe.
Haiba ya Mji Mkongwe hupungua kila kukicha kutokana na kutoweka kidogokidogo vitu vya asili, hivyo kuingia vitu vipya ambavyo havina asili ya Zanzibar.
Kwa mfano; malalamiko makubwa ya wakazi wa Mji Mkongwe ni kukithiri kwa vinyago kama tingatinga na kuongezeka watumiaji wa dawa za kulevya.
“Wazanzibari hatuna asili ya tingatinga na vinyago, hivyo ni vitu vyenye asili ya Tanzania Bara, lakini leo Mji Mkongwe kila kona unayopita kumezagaa vinyago vya kuchongwa na vile vya Kimasai, kwa hiyo ile hadhi ya mji sasa imepotea” anasema mkazi wa Shangani, Maryam Hamid.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Issa Mringoti anasema tatizo kubwa katika Mji Mkongwe ni watembeza watalii wanaoleta usumbufu kwa wageni hao wanaotembelea maeneo ya kihistoria.
Mringoti anasema Serikali imeanzisha kikosi cha ulinzi kwa watalii na vitega uchumi vya utalii eneo lote la Mji Mkongwe, lengo likiwa ni kuondoa tatizo la watu ambao wanapotembelea.
“Mji Mkongwe wenyewe umeshaona kama una tatizo na hilo ni kubwa la kuwasumbua watalii na wakazi wake wamebaini kwamba, kuna tatizo ndiyo sababu wakabuni mambo yatakayosaidia kupata ufumbuzi,” anasema Mlingoti.
Serikali inatakiwa kuchukua hatua za makusudi kuhakikisha mji huo unabaki kwenye orodha ya Urithi wa Dunia, kwa sababu unasaidia kuingiza fedha za kigeni, lakini kuendelea kuwapo kwa manthari yanayoakisi utamaduni, silka na mila za Wazanzibari.
Kama wataalamu wanavyobainisha ukiondolewa kwenye orodha, itakuwa vigumu kuurudisha na nchi itakosa mapato hasa fedha za kigeni.