Friday, August 7

Wabunge 51 waanguka kura za maoni


Wafuasi wa CCM 

Dar es Salaam. Wakati vyombo vya juu vya baadhi ya vyama vya siasa vikiwa vimeanza hatua za mwisho za kupitisha wagombea wa ubunge na udiwani tayari kwa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, hadi juzi wabunge 51 walikuwa wameanguka kwenye kura za maoni za ndani ya vyama vyao.
Idadi hiyo ni takriban asilimia 14 ya wabunge 357 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, inayojumuisha waliochaguliwa na wananchi na wa viti maalumu, ambao waliamua kwenda kupambana majimboni.
Miongoni mwa walioanguka ni mawaziri wa Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ambao walikuwa wakitetea viti vyao majimboni.
Kati ya wabunge hao walioanguka, wawili wanatoka Chadema, wanne CUF na wengine 45 waliosalia wanatoka CCM.
Matumaini pekee yaliyosalia kwa wabunge hao ambao baadhi yao wamekata rufaa kupinga matokeo ya kura za maoni, ni huruma za vikao hivyo ambavyo vinaweza kubadili matokeo ya baadhi ya majimbo, hasa ambayo taratibu zilikiukwa na ushahidi wa kuwapo matumizi ya rushwa.
Wakati wabunge walioanguka Chadema wanasubiri kwa hamu kikao cha Kamati Kuu kilichoanza juzi kupitia majina hayo, wa CCM wanasubiri mfululizo wa vikao vinavyoanza leo hadi Agosti 13, wakati mchakato kupitisha wagombea wa NCCR-Mageuzi bado.
Kwa wabunge wa CUF, hakuna matumaini kutokana na vikao vya juu vya chama hicho kukamilisha kazi yake hivi karibuni.
Mbali na walioanguka, wabunge waliopita katika kura za maoni lakini vyama vyao vinaunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), nao watalazimika kusubiri hadi vyombo hivyo vya mchujo vitakapomaliza kazi, kujua kama wamepita.
Hiyo inatokana na makubaliano ndani ya umoja huo ya kusimamisha mgombea mmoja atakayeungwa mkono na vyama vyote.
Kwa mujibu wa makubaliano ya vyama hivyo vinne; Chadema, CUF, NLD na NCCR - Mageuzi- kinachooonekana kina nguvu kwenye jimbo fulani ndicho mgombea wake ataachiwa kupeperusha bendera ya umoja huo, jambo ambalo vyama hivyo vilisema vimekamilisha kazi ya mgawanyo kwa asilimia 95.
Wakati Chadema, CUF, NCCR na NLD wakisubiri utekelezwa wa makubaliano hayo, wabunge wa CCM watakuwa njiapanda baada ya chama hicho kueleza kuwa hakitarudia makosa ya mwaka 2010 ya kupingana na maoni ya wanachama kwa kutengua matokeo ya kura za maoni.
Profesa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Jamidu Katima alisema kuanguka kwa wabunge hao kunatokana na wengi wao kutoonekana majimboni baada ya kupewa dhamana ya kuongoza wananchi.
“Kama kiongozi umepewa dhamana, lakini huonekani jimboni basi ni dhahiri wananchi watakukataa. Wakikuona unachukua fomu watakushangaa lakini ujue watakukataa kwa sababu huwatatulii kero zao kama ulivyoahidi awali.”
Profesa Katima alisema kwa sasa Watanzania wameamka, hivyo ni vigumu kudanganyika na kwamba kama kiongozi hatumii vyema dhamana aliyopewa, wananchi watamuacha apumzike kwa amani.
Maoni kama hayo yalitolewa na mhadhiri wa sayansi ya siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Alexander Makulilo ambaye alisema zipo sababu chekwa za baadhi ya mawaziri kushindwa kwenye kura za maoni, mojawapo ikiwa ni makundi na kushindwa kutimiza ahadi.
Kujaribu mtu mwingine
Dk Makulilo alisema ni rahisi kwa wananchi kuacha kumchagua kiongozi baada ya kuona hajatimiza kile alichoahidi hivyo wakaona wajaribu kiongozi mwingine pengine atawatatulia kero zao.
Kuhusu kuanguka kwa wanasiasa nguli wa CCM, mhadhiri huyo alisema sababu nyingine ni siasa za makundi ambako kundi moja tu linaweza kufanya juhudi ili mwingine ashindwe.
“Sasa hivi tunazungumzia mtu kuanguka katika chama chake, kwa hiyo siasa za makundi ndani ya chama hicho inaweza kusababisha kuanguka katika kura za maoni,” alisema.
Sababu nyingine aliyoitaja Dk Makulilo ni wimbi la vijana na kuwa inawezekana wananchi wanahamia kwa wanasiasa vijana zaidi baada ya kuona wengine amekaa madarakani kwa muda mrefu.
Pia, aliitaja rushwa kuwa miongoni mwa sababu za kuanguka kwani inawezekana kuwa mgombea mwenzake ametoa fedha au yeye ametoa, lakini mwingine ametoa nyingi zaidi.
“Nadhani umeona jinsi ambavyo Takukuru wamekamata wagombea wengi kwa tuhuma za rushwa kwa hiyo hapana shaka kuwa suala la rushwa lilikuwepo,” alisema.
Utafiti wa Twaweza
Idadi ya wagombea hao walioanguka katika hatua ya awali inaashiria kuanza kutimia kwa matokeo ya utafiti uliofanywa na taasisi ya Twaweza mwishoni mwa mwaka jana ambao ulionyesha kuwa nusu ya wabunge wataanguka kwenye kura za maoni.
Kwa mujibu wa utafiti huo uliotangazwa Novemba 12, 2014, kuanguka kwa wabunge hao kutatokana na kushindwa kutekeleza ahadi zao. Asilimia 47 ya wananchi walioulizwa iwapo watampigia tena kura mbunge wao, walisema “hapana” huku asilimia kama hiyo ikisema “ndiyo”.
Utafiti huo ulieleza kuwa ahadi nyingi zilizotolewa na wabunge kwenye mikutano ya kampeni wakati wa uchaguzi hazijatekelezwa na kwamba asilimia 78 ya wananchi bado wanazikumbuka.
CCM kutorudia makosa
Wakati utafiti wa Twaweza ukizungumzia kutotimizwa kwa ahadi, wabunge waliopita kura za maoni watakuwa wakijifariji na matamshi ya viongozi wao kuwa majina yao hayatakatwa kama ilivyokuwa mwaka 2010.
Akihutubia kwenye mkutano wa hadhara mjini Iringa Oktoba mwaka jana, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana alisema chama hicho hakitarudia makosa ya kuengua majina ya wagombea wanaopitishwa na wanachama kwenye kura za maoni baada ya Frederick Mwakalebela kuenguliwa na Halmashauri Kuu kugombea ubunge wa Jimbo la Iringa Mjini na baadaye Mchungaji Peter Msigwa wa Chadema akatwaa jimbo hilo.

Mke wa Dk Slaa afunguka


Dar es Salaam. Siku moja baada ya Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kuzungumza na gazeti hili na kusema yupo salama, mke wake, Josephine Mushumbusi amekanusha tuhuma zilizozagaa kuwa ndiye aliyemshauri kiongozi huyo wa Chadema kujiuzulu na kumzuia kushiriki vikao muhimu vya chama.
Tetesi hizo zilivuma kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari baada ya Dk Slaa kutoonekana katika vikao muhimu vya Chadema na Ukawa, kuwa Mushumbusi hakupendezwa na kitendo cha Lowassa kupitishwa kuwania urais chini ya mwavuli wa Ukawa na badala yake alitaka Dk Slaa ndiye awe mpeperusha bendera.
Kwa mujibu wa taarifa hizo ambazo Mushumbusi amezikanusha, aliamua alimfungia ndani Dk Slaa kama moja ya mbinu za kumzuia asishiriki shughuli za kichama, tuhuma ambazo amezikanusha.
“Bosi wako akija kukuomba ushauri utamsaidia, lakini akija akakuambia ameshafanya maamuzi unaweza kupingana naye?” alihoji Mushumbusi akianza kutoa maelezo yake na kuendelea:
“Wakati wa vikao nilikuwa namwona (Dk Slaa) anachelewa kurudi kila siku, siku moja akaja akaniambia uamuzi aliouchukua na mimi sikuwa na la kusema, nikachukua shuka nikajifunika.”
Katika mahojiano yake ya kwanza na Mwananchi baada ya kuzagaa kwa tetesi hizo, Mushumbusi pia alikana kumfungia Dk Slaa ndani ya nyumba, akisema wakati maneno hayo yalipokuwa yanazagaa, alikuwa nje ya nchi na wala hakujua kinachoendelea.
“Mwenyewe najiuliza nini kinaendelea, siwezi kufanya kitu kama hicho. Nyumba yangu ina milango miwili, nawezaje kumfungia mtu, tena mwanamume, hata watoto siwezi kuwafungia. Kuna mambo mengine mwanamke huwezi kuyafanya kwa mwanamume. Mwanamume ni mwanamume tu,” alisema.
Alisema viongozi wa Chadema, ndugu, jamaa na marafiki walikuwa wanafika nyumbani kwake na walikutana na Dk Slaa na kuzungumza naye... “Kama ningekuwa nimemfungia wangezungumza naye vipi?”
Mushumbusi alisema mwanamke anaweza kufanya chochote lakini kuna baadhi ya mambo ambayo mwanamume akiamua ni vigumu kumzuia.
Akifafanua tuhuma za kumshinikiza Dk Slaa kujiuzulu Chadema, Mushumbusi alisema kiongozi huyo wa Chadema ana uamuzi wake na yeye ni msaidizi tu ambaye hana uamuzi wa mwisho kwenye familia.
Hata hivyo, alisema endapo angeamua kumshawishi, uwezo wa kufanya hivyo anao lakini yeye ni mwanamke mwadilifu anayependa mafanikio ya mumewe.
“Kwani unanionaje? Mimi ni ‘strong’ (nina nguvu), ningetaka ningefanya hivyo, nisingeshindwa,” alisema.
Pamoja na hayo, Mushumbusi alilalamika kuwa tuhuma hizo dhidi yake zimesababisha asisikilizwe kama ilivyokuwa awali.
Bila kufafanua kwa undani, alisema kuna kundi linalounda propaganda hizo ili abadili mtazamo kuhusu mumewe lakini jambo hilo haliwezi kutokea.
“Nilisema nitampenda kama alivyo, sitajali chochote wala akiwa katika hali gani au chama gani. Kazi yangu ni kumtia moyo ili kile atakachofanya kifanikiwe,” alisema.
Auza mkaa
Mbali na kukanusha vikali tuhuma hizo, Mushumbusi alisema alikwishajitoa kwenye masuala ya siasa kwa miaka miwili sasa na badala yake ameamua kufanya biashara ya kuuza mkaa.
“Nimenyamaza kimya, nimekaa kando ninaendelea na biashara yangu ya kuuza mkaa, nipo mbali na siasa na sitaki kujua kinachoendelea, kwanza hata mchakato wenyewe siujui,” alisema.
Aliwashauri wanawake kuacha kushabikia masuala yanayotokea ndani ya ndoa yake na kuwataka wavae viatu anavyovivaa na wajue kuwa anapitia wakati mgumu.

Mtikisiko: Ni baada ya Profesa Lipumba kujiengua uenyekiti CUF


Aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba akiaga waandishi wa habari baada ya kuwatangazia kujivua wadhifa huo katika mkutano alioufanya Dar es Salaam jana. 


Dar es Salaam. Hakuna neno jingine linalofaa kuelezea hali ilivyo ndani ya Ukawa zaidi ya “mtikisiko” baada ya Profesa Ibrahim Lipumba kuamua kujivua uenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) wakati mkakati wa vyama vya upinzani kushirikiana kutaka kushika dola ukiwa umeshika kasi.
Uamuzi wa Profesa Lipumba, mmoja wa waasisi wanne wa Ukawa-Umoja wa Katiba ya Wananchi unaoundwa na vyama vinne vya Chadema, CUF, NCCR Mageuzi na NLD-,unamaanisha anapoteza wadhifa wake wa mwenyekiti mwenza wa umoja huo ambao umeamua kushirikiana kwenye Uchaguzi Mkuu kwa kusimamisha mgombea mmoja kuanzia ngazi ya urais hadi udiwani atakayeungwa mkono na vyama hivyo.
Wengine walioongoza harakati za kuasisi Ukawa ni Freeman Mbowe, ambaye ni mwenyekiti wa Chadema, James Mbatia wa NCCR-Mageuzi na Emmanuel Makaidi wa NLD.
Profesa Lipumba, mmoja wa wenyeviti wanne wa Ukawa walioeleza sababu za kumkaribisha Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kwenye umoja huo takribani siku 10 zilizopita, jana alieleza kuwa ameamua kujivua wadhifa huo kutokana na vyama hivyo kukubali kupokea watu walioshiriki kukataa Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na wananchi, kitu ambacho kilikuwa msingi wa kuundwa kwa Ukawa.
“Nimejitahidi sana ndugu zangu kuvumilia, lakini dhamira inanisuta,” alisema Profesa Lipumba mbele ya waandishi wa habari jana kwenye Hoteli ya Peacock baada ya mkutano wa juzi aliopanga kufanyia ofisi za CUF kuzuiwa na wanachama.
“Sisi tumekaa tunaipigia kelele Rasimu ya Katiba ya (Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyokuwa chini ya Jaji Joseph) Warioba lakini iliyopitishwa ni Katiba Inayopendekezwa sasa tunawachukua waliopitisha ili waje kuisimamia. Hivi inaingia akilini?”
Lipumba aliwaomba radhi wanachama na wananchi waliomuamini wakati wote wa uongozi wake.
Tamko la maneno 900
Katika taarifa yake ya maneno 900 ambayo aliisoma mbele ya waandishi wa habari jana, Profesa Lipumba, ambaye amekuwa akibashiriwa kuchukua uamuzi huo tangu katikati ya wiki hii, alisema pamoja na kujivua uongozi hatahama CUF na kwamba ameshalipia kadi yake hadi mwaka 2020.
“Leo hii nimeikabidhi ofisi ya Katibu Mkuu barua yangu ya kung’atuka nafasi ya mwenyekiti wa taifa, lakini naendelea kuwa mwanachama wa CUF na kadi yangu imelipiwa mpaka mwaka 2020,” alisema Profesa Lipumba aliyekiongoza chama hicho kwa miaka 16.
Huku akionekana kuwa mtulivu, alisema hajashinikizwa wala kushawishiwa na mtu yeyote kujiuzulu na kwamba uamuzi huo ameufanya baada ya kutafakari sana na kushauriana na familia yake ambayo alisema imeridhia.
Mtaalamu huyo wa masuala ya uchumi alisema ameshiriki katika vikao vingi vya Ukawa vilivyowafikisha hapo walipo, lakini dhamira na nafsi vinamsuta kuwa wameshindwa kuenzi na kuzingatia tunu za Taifa za utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi na uwajibikaji.
Alipoulizwa sababu za kugeuka wakati yeye alikuwa ni miongoni mwa wenyeviti wa Ukawa waliomkaribisha Lowassa Ukawa, alikiri akisema kuwa suala la rushwa na ufisadi ni mfumo ambao lazima uondolewe lakini kwa sasa “dhamira yangu na nafsi yangu vinanisuta”.
Profesa Lipumba alipotakiwa kueleza iwapo kujiuzulu kwake kunahusiana na tuhuma za kuhongwa mamilioni na CCM ili kuusambaratisha Ukawa, alijibu:
“Yametengwa wapi? mimi sina taarifa hizo. Tulielezwa sisi tumemkaribisha kwa sababu tumepatiwa mamilioni na sasa unasema mamilioni yametengwa kusambaratisha Ukawa. Ila ninalosisitiza ni kwamba linalonipa tatizo ni dhamira na nafsi yangu, si vingine.”
Profesa Lipumba aliyekuwa ameongozana na mdogo wake Shaaban Miraji na rafiki yake Abdallah Shaaban, alisema kama mwanachama wa kawaida atashiriki kampeni za chama lakini ataendelea kuiunga mkono Rasimu ya Katiba ya Warioba.
Ukawa iliundwa mapema mwaka jana na wajumbe wa Bunge la Katiba kutoka vyama hivyo vinne kupinga mwenendo wa chombo hicho cha kuandika Katiba, wakisema kilipuuza maoni yaliyokuwa kwenye Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Warioba na kuweka maoni yaliyotokana na maagizo ya CCM.
Miongoni mwa mambo yaliyozua mjadala mkubwa ni muundo wa Serikali ya Muungano baada ya Rasimu ya Katiba kupendekeza serikali tatu, na pia suala la Tunu za Taifa ambazo zilipendekezwa kuwa ni pamoja na utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi, uwajibikaji na lugha ya Taifa, lakini zikaondolewa.
Kikao cha dharura CUF Zanzibar
Baadaye jana jioni, uongozi wa CUF Zanzibar ulitoa taarifa ya kuitishwa kwa kikao cha dharura, huku ikiwahakikishia wanachama wake kuwa itavuka salama kwenye msukosuko huo kama ilivyofanikiwa dhoruba nyingine.
“Katika historia yake, CUF imepita katika dhoruba na misukosuko mingi lakini mara zote imeonyesha uwezo mkubwa wa kuhimili dhoruba na misukosuko hiyo na kukabiliana na athari zake. Hatuna chembe ya wasiwasi kwamba hata mtihani huu tutauvuka na tunaamini tutaibuka tukiwa chama imara zaidi,” inaeleza taarifa ya CUF Zanzibar.
“Katibu Mkuu ameagiza kuitishwa kwa vikao vya dharura vya Kamati ya Utendaji ya Taifa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa siku ya Jumapili, tarehe 9 Agosti, 2015 ili kujadili hatua hiyo na kufanya uamuzi juu ya hatua muafaka zinazopaswa kuchukuliwa katika kipindi hiki hadi hapo chama kitakapomchagua mwanachama mwingine kujaza nafasi hiyo ya mwenyekiti.”
Kuondoka kwa Lipumba kunaacha nafasi mbili za juu kuwa wazi baada ya aliyekuwa makamu mwenyekiti, Juma Duni Haji kuhamia Chadema na kupitishwa kuwa mgombea mwenza wa Ukawa kutokana na makubaliano ya kimkakati ya vyama vinavyounda umoja huo. Hali hiyo inafanya kiongozi mkuu kwa sasa kuwa Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
CUF wajibu mapigo Dar
Nusu saa baada ya kutangaza kujivua uenyekiti, uongozi wa CUF jijini Dar es Salaam uliitisha mkutano wa ghafla na wanahabari kwenye ofisi za makao makuu yake zilizoko Buguruni na kueleza kuwa kama kiongozi, Profesa Lipumba ana uhuru na haki kikatiba kujiuzulu na CUF kama taasisi bado ipo imara.
“Tunakubaliana na uamuzi wake, lakini tuwaeleze wanachama wetu na Watanzania kwa ujumla kuwa uongozi wa CUF umebaki imara na unaendelea na shughuli zake kwa kufuata taratibu zote na vikao vyetu vitaendelea kama kawaida. Bado katibu mkuu yupo na viongozi wengine wapo,” alisema mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CUF, Mustafa Wandwi.
Aliwatoa hofu makada wanaogombea ubunge na udiwani akiwataka waendelee na mikakati yao ya uchaguzi kwa sababu uamuzi wa kugombea umebarikiwa na Baraza Kuu la Uongozi na hakuna mfarakano wowote ndani ya chama.
Alipoulizwa kuhusu kauli ya Profesa Lipumba kuwa Ukawa imevunja misingi na maadili wanayoiamini, alisema:
“Yeye alikuwa kiongozi wetu mkuu na aliridhia mengi kama kiongozi wa chama na yapo maandishi yanayoonyesha tulivyoridhia ndani ya Ukawa na tunaendelea vizuri bila tatizo lolote katika umoja huo.
“Kama amegundua udhaifu huo sasa, anaujua yeye kama kiongozi na mwanachama. Sisi hajatupatia taarifa rasmi katika kikao cha aina yoyote na siwezi kuyazungumzia kwa sababu kama chama hatujajadili hayo na tukijadili tutatoa maelezo.”
CUF bila Lipumba
Wakati uongozi ukieleza hayo, makada waliokuwa makao makuu ya CUF walikuwa katika makundi wakijadili kung’atuka kwa Profesa Lipumba huku wengi wakisema “CUF bila Lipumba inawezekana”.
Ili kuondoa simanzi na taharuki, walianza kushawishiana kuimba nyimbo za hamasa zikiwamo za “tuna imani na Ukawa, hoyaa, hoyaaa…tuna imani na Lowassa hoyaa, hoyaaa” na kuchagiza pia salamu ya maarufu ya CUF ya “CCM kwisha kwisha kwisha kabisa, mlalo wa chali, kifo cha mende, kwisha kabisa”.
“Taarifa za kujiuzulu imetushtua sana, mheshimiwa hakutumia hekima na busara,” alisema katibu wa vijana Kata ya Magomeni, Salim Mzee. Jana (juzi) wazee na viongozi wa dini walimwita kujadiliana lakini inaonekana alikuwa na chuki katika nafsi yake na kama kulikuwa na tatizo ndani ya Ukawa angetuita tukajadiliana lakini kama wana-CUF hatutatoka ndani ya Ukawa na tutajenga chama kuhakisha tunaing’oa CCM,” aliongeza.
Licha ya Profesa Lipumba kueleza kuondoka kwake hakuhusiani na kupatiwa mamilioni ya fedha kuvuruga Ukawa, kada Abdallah Mohamed alisema kuondoka kwa Lipumba siyo bure kuna mkono wa CCM.
“Juzi tu alikuwa akitoa kauli za wazi mbele ya vyombo vya habari kuhusu kuunganisha nguvu ya Lowassa na Ukawa CCM chali, chali, mlalo wa mende, sasa kwa hapa nani kawa mlalo wa mende?
Chadema walonga
Mwanasheria mkuu wa Chadema, Tundu Lissu alisema hatua ya Profesa Lipumba kujiuzulu ni sawa na jenerali wa jeshi aliyeanguka katikati ya mapambano ya kuelekea Ikulu na harakati za mageuzi na mabadiliko alizoanza miaka 20 iliyopita.
Akizungumza nje ya Hoteli ya Ledger Bahari Beach kilipofanyika kikao cha Kamati Kuu ya Chadema jana, Lissu alisema katika mapambano kuna majenarali na askari wa kawaida, lakini Profesa Lipumba ni sawa na jenerali aliyeanguka katikati ya uwanja wa mapambano ya mabadiliko.
Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la chama hicho (Bawacha), Halima Mdee alisema Profesa Lipumba alikuwa kikwazo katika maamuzi ya Ukawa.
“Sishangai kwa sababu tulikuwa tunajua kuwa yeye ndiyo kikwazo cha Ukawa tangu mwanzo wa vikao vyetu. Alikuwa na sababu nyingi, akimaliza hii anaibua nyingine,” alisema Mdee.
Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa alimfananisha Profesa Lipumba na abiria wa treni anayeamua kushukia njiani kabla hajafika anakokwenda.

Chenge akiri kupokea Sh1.6 bilioni

Dar es Salaam. Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge amekiri mbele ya Baraza la Maadili kupokea Sh1.6 bilioni kutoka Kampuni ya VIP Enginering and Marketing Limited, zikiwa ni malipo ya kutoa ushauri.
Pia, alihoji kama kuna tatizo kutumia taaluma yake ya sheria kuzishauri kampuni binafsi na kujipatia fedha.
Chenge ambaye alitoa utetezi wake jana saa 7:30 mchana, alisema hakulipwa fedha hizo kwa sababu ni kiongozi wa umma, bali kwa kutoa ushauri.
Alisema aliingia mkataba na kampuni hiyo wa kutoa ushauri wa kisheria dhidi ya Kampuni ya Mechmer ambazo ni kampuni binafsi zilizokuwa na mgogoro.
“Nawashangaa mnalalamika Chenge kulipwa na Kampuni ya VIP au wamewafuata na kulalamika kwamba hayakuwa malipo halali,” alihoji.
Alisema hakuna kufungu cha sheria kinachomzuia kutoa ushauri wa kisheria kwa kampuni binafsi.
Kuhusu malalamiko kwamba akiwa Mwanasheria wa Serikali aliishauri kuingia mkataba wa kuuziana umeme kati ya Kampuni ya IPTL na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Chenge alisema anawashangaa wanasheria wa sekretarieti kwa malalamiko hayo.
“Sikuishauri Serikali kuingia mkataba na IPTL bali ofisi yangu ndiyo iliyotoa ushauri kisheria. Nakubaliana na walalamikaji kwamba mwaka 1995 nilikuwa mwanasheria wa Serikali, lakini sikubaliani na madai yao.”
Alisema Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali ilitoa ushauri huo kwa sababu ndiyo jukumu lake.
“Wanasheria ni lazima wafahamu kwamba ile ni taasisi na siyo mtu kama Chenge,” alisema.
Alisema ofisi yake ilitoa ushauri wa mikataba mitatu ya IPTL na Serikali kwa lengo la kuongeza umeme hasa kutokana na ukame uliolikumba Taifa.
“Naomba baraza lako liyapuuze kwa dharua zote na kuyatupilia mbali malalamiko ya sekretarieti kwa sababu hayawezi kukusaidia kutoa uamuzi ulio sahihi,” alisema.
Kuhusu kutumia taarifa alizozipata akiwa mwanasheria wa Serikali na kuzitumia kwa masilahi binafsi, Chenge alisema: “Naomba wachanganue taarifa hizo ni zipi kwa sababu huwezi kumlalamikia mtu kwa jumla lakini kwenye malalamiko husemi.
Shahidi wa mlalamikaji, Waziri Kipacha alisema Chenge akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) mwaka 1995, aliishauri Serikali kuingia mkataba wa miaka 20 na IPTL.
Alisema baada ya kustaafu mwaka 2005 aliingia mkataba wa kuwa mshauri mwelekezi wa kampuni hiyo iliyokuwa inamiliki asilimia 30 ya hisa za IPTL.
Alisema kitendo cha kuingia mkataba na VIP ni ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Tuesday, August 4

Chadema yamweka pembeni Dk Slaa



Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe
akihutubia wajumbe wa Baraza Kuu la chama hicho 
alipokuwa akifungua kikao chao Dar es Salaam jana. 


Dar es Salaam. Baraza Kuu la Chadema limeridhia Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa apumzike wakati chama hicho kikiendelea na mchakato wa Uchaguzi Mkuu baada ya kiongozi huyo kutofautiana nao katika uamuzi wa kumkaribisha Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.

Baraza hilo jana lilipiga kura ya wazi huku likishauri kuwa endapo atafikiria kubadili uamuzi wake, atarejea kuendeleza safari ya chama hicho kuelekea Ikulu chini ya mwavuli wa Ukawa.
Uamuzi huo ulifikiwa jana wakati wa kikao cha Baraza Kuu kilichofanyika hapa baada ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kueleza tofauti iliyojitokeza mwishoni mwa mchakato wa kumpokea Lowassa baina ya Dk Slaa na Kamati Kuu kiasi cha kumfanya Katibu Mkuu huyo kutohudhuria baadhi ya shughuli muhimu za chama.
Mbowe alisema Kamati Kuu ilifanya vikao kadhaa kutafakari ujio wa Lowassa na mashauriano ya muda mrefu ambayo hayakuwa rahisi kufikia uamuzi wa pamoja.
“Tulifanya mashauriano yaliyoambatana na hali ya kitafiti na tukaridhika pasipo shaka kwamba ujio wa Lowassa na wenzake katika chama hiki ni mpango wa Mungu ambao tunatakiwa tuunge mkono, utusadie kuwaunganisha wenzetu wa CUF, NLD na NCCR-Mageuzi na Watanzania wote kufikia malengo ya pamoja,” alisema.
“Katika hatua zote hizo tulikuwa sambamba na Dk Slaa lakini katika dakika za mwisho akatofautina kidogo na Kamati Kuu.”
Maelezo hayo ya Mbowe yanamaliza sintofahamu iliyokuwa imetanda kwa makada wa Chadema juu ya sababu za Dk Slaa kutoonekana kwenye hafla ya kumpokea Lowassa Julai 28, wakati wa kuchukua fomu za kugombea urais Julai 30, siku aliporudisha fomu Agosti Mosi na kwenye vikao vya Sekretarieti na Kamati Kuu juzi.
Mbowe ambaye pia ni Kiongoni wa Upinzani Bungeni alisema: “Kwa hiyo tumekubaliana na Katibu Mkuu apumzike kwa muda na nina hakika kwa tabia na hulka za Dk Slaa… kwa sababu anajua tunampenda na yeye anakipenda chama hiki, tunamwombea kwa Mungu ampe nguvu na ujasiri wa kuona kwamba kauli ya wengi ni kauli ya Mungu.
“Tutaendelea kuongea naye, bado nafasi yake ipo na kwa wengine wote wenye hofu ya aina hii na naomba niseme kuwa nafasi zetu za kiuongozi au kiuchaguzi ni dhamana, hakuna yeyote mwenye hatimiliki na nafasi mliyonayo ni kwa sababu ya watu, tukielewa hivyo wala hatuna ugomvi.”
Huku akizungumza kwa hisia, Mbowe alisema kauli yake ni uamuzi wa vikao vya chama na kwamba hakuna ugomvi wowote na kiongozi huyo, hivyo makada na Watanzania waachane na uzushi wa mitandaoni akisema hofu kama ya Dk Slaa ipo pia kwa makada wengine na kwamba ilikuwa na mashiko na inayozungumzika, lakini wasingezuia matakwa safari ya mamilioni kwa “sababu ya matakwa ya Mbowe au Slaa... tunasema lazima tuendelee kwa sababu uchaguzi upo kesho.”
Katika hotuba hiyo ya dakika 35, Mbowe alisema Dk Slaa ni kiongozi ambaye wanamheshimu, wanampenda na wataendelea kumpenda siku zote kwa sababu chama chao ni cha kujengana na siyo kubomoana.
Ili kupitisha uamuzi huo, Mbowe aliwahoji wajumbe wa baraza hilo iwapo wanataka waendelee na kazi au wasubiri ili kila mmoja afanye uamuzi wake binafsi na kujibiwa “tuendelee…”
Aliuliza swali hilo mara mbili na kuungwa mkono na wajumbe wote kwa sauti kubwa na alipowataka wajumbe wanaounga mkono uamuzi huo wasimame, walifanya hivyo na kuimba wimbo wa chama “Chadema, Chadema…people’s power.”
Alisema amezungumza suala hilo mbele ya wanahabari ili kama kuhukumiwa, ahukumiwe kwa sababu wajibu wake akiwa kiongozi ni kusema ukweli daima.
Aliwataka makada wa Chadema wawe na amani na kwamba chama hicho kipo salama na wanaofikiri kitameguka ni ndoto za mchana.
“Wengine wakasema Lissu (Tundu) huyoo, wakahamia Mnyika (John), Mnyika alikuwa mgonjwa, huyoo… mtasema na Slaa amesharudisha na gari mtakuta Jumatatu huyooo, lakini kwa leo amepumzika mzee wangu,” alisema Mbowe na kushangiliwa.
Mwenyekiti huyo aligusia moja ya ajenda ya mkutano wa Baraza Kuu kuwa ilikuwa ni kujadili ilani ya uchaguzi kabla ya kupitishwa leo na mkutano mkuu.
Baada ya mkutano huo, kuanzia kesho kwa siku tatu mfululizo chama hicho kitakuwa na vikao vya Kamati Kuu kuteua majina ya wabunge na wawakilishi watakaosimamishwa na chama hicho.
Hofu ya Lowassa
Akizungumzia hofu iliyotanda baada ya Lowassa kujiunga na chama hicho, Mbowe alisema kila jambo jema mara nyingi hujitokeza likiwa na changamoto.
Alisema baada ya kutambulishwa kwa Lowassa, hofu ilionekana kutanda ndani ya wajumbe wa Mkutano Mkuu na Baraza Kuu kwa kuhofia nafasi za uongozi na hatima ya chama hicho.
“Lakini inawezekana hofu hiyo wameipata zaidi CCM, kwa kipigo ambacho wamekipata hakijawahi kutokea katika historia ya siasa nchini, hali hii inataka kufanana na kuondoka kwa Augustino Mrema lakini naweza kuilinganisha nguvu ile kwa asilimia 25 tu na nafasi ya kuondoka Lowassa.”
Kuhusu madai ya kupokea mafisadi ndani ya chama, Mbowe alisema katika mazingira yoyote kwa mwanasiasa anayetafuta mbadala wa chama, lazima atakifikiria Chadema kwa sababu ni chama kilichojijengea msingi.
Alisema ilikuwa ni lazima kwa chama kuweka mkakati wa kumpokea mwanasiasa yeyote atakayekuwa tayari kuingia.
“Kwa mpango huohuo wa Mungu, leo yamejitokeza makundi yameingia ndani ya chama na miongoni mwao aliyekuwa anawika sana ni Lowassa... sasa katika siasa kuna kitu kinaitwa ‘game change’, yaani kwamba siasa zinaelekea mrengo huu halafu ghafla zinageuka na kuelekea mrengo mwingine, hiyo ndiyo ‘dynamism’ ya siasa.
“Hatuwezi kufunga milango ya chama kwa kuhofia nafasi zetu za uongozi, eti nafasi ya mwenyekiti, udiwani itachukuliwa...je, tutakuwa tunajenga chama?
“Hali hiyo ndiyo imekuwa sababu vyama vingi vilijisahau na kuendekeza masilahi binafsi wakasahau masilahi mapana ya chama. Kila mwanachama anaheshimika katika nafasi yake ndani ya chama. Kwa hivyo fursa iliyojitokeza usipoitumia utakuwa ni mwendawazimu.”
Mwalimu abeba mikoba ya Dk Slaa
Chama hicho kimemkaimisha Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalimu nafasi ya Dk Slaa na papo hapo, Mwalimu aliwaeleza wajumbe kuwa hotuba maalumu ya Katibu Mkuu itatolewa leo wakati wa mkutano mkuu.
“Lazima mjue tunakwenda kuwa chama tawala, hivyo hakuna kiongozi mdogo wala hakuna mwanachama aliye mdogo ndani ya chama hiki, kila mwanachama mmoja atakuwa na thamani, hivyo mjilinde msije kunufaisha maadui zetu,” alisema Mwalimu.
Msindai atua Chadema
Mwenyekiti wa wenyeviti wa CCM, Mgana Msindai jana alijiunga na Chadema na kutambulishwa katika mkutano wa Baraza Kuu la chama hicho.
Mgana, ambaye aliwahi kuwa mbunge wa Iramba Mashariki (2000-2010) alitambulishwa pamoja na Mbunge wa Arumeru Magharibi (CCM), Goodluck Ole Medeye na ofisa mwandamizi wa chama hicho, Matson Chizii.
Makada hao wa CCM jana usiku waliambatana katika kikao hicho na aliyewahi kuwa waziri mkuu Edward Lowassa. Habari zinasema kuna makada zaidi wa CCM wakaotambulisha katika mkutano mkuu wa Chadema leo.

Rushwa barabarani yamtia kichefuchefu JK


Rais Jakaya Kikwete akihutubia 
wakati wa hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani 
iliyofanyika kwenye Viwanja vya Tangamano 
mjini Tanga jana. 

Tanga. Rais Jakaya Kikwete amekiagiza Kikosi cha Usalama Barabarani kufanya mabadiliko ya teknolojia katika utendaji wake ili kuondoa mianya ya rushwa.
Alitoa agizo hilo jana wakati akizindua Wiki ya Nenda kwa Usalama inayofanyika kitaifa jijiji hapa kwenye Uwanja wa Tangamano.
Alisema miongoni mwa mambo yanayochangia ajali ni kukosekana kwa tekonolojia ya kisasa kudhibiti mwendo kasi wa vyombo vya moto, hivyo kutoa mianya kwa baadhi ya trafiki wasio waaminifu kudai rushwa kutoka kwa madereva wanaowakamata kwa makosa mbalimbali.
“Vikiwekwa vidhibiti mwendo kwenye barabara zote kuu, dereva atakayeendesha gari lake kwa kasi namba zinaonekana kwenye kompyuta, hapo tena hakutakuwa na mazungumzo baina ya dereva na askari,” alisema Kikwete.
Pia, Rais Kikwete aliliagiza
Baraza la Usalama Barabarani kurekebisha baadhi ya sheria zilizopitwa na wakati ili kuongeza ufanisi.
“Baraza liende na wakati, sheria pia ziende na wakati, kadhalika askari. Tukifanya hivyo, tutapunguza ajali za barabarani,” alisema.
Agizo jingine alilotoa kwa baraza hilo ni kudhibiti vyanzo vya ajali kwa kuweka alama kwenye leseni za madereva wanaosababisha ajali, kukomesha rushwa na kutoa elimu ya usalama barabarani.
Rais Kikwete alisema asilimia 99 ya vifo vinatokana na uzembe na madereva kutofuata sheria za barabarani.
“Madereza wanaendesha kwa kasi bila sababu, wanayapita magari mengine bila kuchukua tahadhari, madereva wa pikipiki wanabeba abiria kwa staili ya mshkaki na magari mabovu yako mengi barabarani,” alisema.
Mwenyekiti wa baraza hilo, Pereira Ame Silima, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani alisema takwimu zinaonyesha kati ya mwaka 2010/14, watu 19,264 wamepoteza maisha kutokana na ajali za barabarani.
Alisema kuanzia Januari hadi Juni mwaka mwaka huu, watu 1,747 wamepoteza maisha, ambapo kati ya vifo hivyo, 1,352 vilitokana na ajali za pikipiki pekee yake.

Peter Kisumo afariki dunia


Moshi. Muasisi wa Tanu na baadaye CCM, Mzee Peter Kisumo (pichani) amefariki dunia.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini ambaye aliwahi kushika nyadhifa kadhaa katika Serikali ya Awamu ya Kwanza, alifariki Dunia jana saa moja usiku katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Mtoto wa marehemu, Michael Kisumo alilithibitishia gazeti hili jana juu ya kifo cha baba yake akisema kilitokana na maradhi ya figo ambayo yamekuwa yakimsumbua kwa muda mrefu.
“Tulikuja hapa Muhimbili kwa ajili ya mzee kufanyiwa dialysis (usafishaji damu katika figo) sasa ikajitokeza complication (utata) akaanza kuharisha damu,” alisema.
Michael alisema baba yake alilazwa wodi ya kawaida juzi ili jana apatiwe tiba hiyo kabla ya hali yake kubadilika ghafla.
“Daktari wake alipokuja leo (jana) na kumwangalia aliagiza atolewe wodi ya kawaida ahamishiwe ICU lakini ilipofika saa moja usiku akatutoka” alisema Michael.
Kifo cha mwanasiasa huyo kimekuja takribani mwezi mmoja tangu arejee kutoka India ambako amekuwa akienda mara kwa mara kuchunguzwa afya yake.
Hali ya ugonjwa wake huo ilifikia katika kiwango cha juu na kulazimika kufanyiwa uchujaji wa figo mara tatu kwa wiki kila Jumatatu, Jumatano na Ijumaa.
Kisumo aliwahi kuwa mmoja wa mameneja wa kampeni wa Rais Jakaya Kikwete mwaka 2005 akisimamia kanda ya kaskazini iliyojumuisha mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Tanga.
Mbali ya kuwa waziri, aliwahi pia kuwa mkuu wa mkoa na mdhamini wa CCM.

Panga la urais CCM kuhamia kwa wabunge


Dar es Salaam. Chama cha Mapinduzi (CCM), kimesema kitatumia ‘panga’ lilelile lililotumika kumpata mgombea wake wa urais katika kuchuja wagombea ubunge na udiwani kupitia vikao vyake halali ili kupata wagombea safi.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnaye alisema hayo jana Dar es Salaam katika mkutano na waandishi wa habari, kuzungumzia mchakato wa vikao vya kamati za chama hicho ili kupata wagombea wa ubunge, uwakilishi na udiwani baada ya mchakato wa kura za maoni kukamilika.
Alisema mchakato huo utaanza kwa kikao cha Kamati Maalumu ya CCM Agosti 6 na 7 kuchuja na kupitisha wagombea ubunge na uwakilishi. Agosti 8 na 9, Sekretarieti itakutana ikifuatiwa na Kamati Kuu pia kwa siku mbili kabla ya Halmashauri Kuu kukutana Agosti 12 na 13 kuteua wagombea ubunge na uwakilishi.
“Kura za maoni siyo mwisho wa safari, ni hatua ya kwanza ya kuona ni nani anayekubalika… siyo kibali cha kupeperusha bendera ya CCM, kama kuna upungufu vikao vitachukua hatua. Kura ya maoni si kigezo… kama wamecheza rafu au kutumia rushwa, hata kama wameshinda kwa kura nyingi, ikithibitika wanaweza kuondolewa,” alisema Nape na kuongeza:
“Tutafanya kama ilivyokuwa kwa wagombea urais, kama maadili hayakufuatwa wanaweza kuondolewa siyo tu wa kwanza, hata wanne, hata kufuta matokeo. Tutachukua hatua kwenye ubunge, tutachukua hatua kwenye udiwani kwa wale watakaojihusisha na rushwa. Hawatapata nafasi ya uteuzi kwenye chama chetu. Hatuna muda wa kuanza kuosha watu na madodoki.”
Alikumbusha jinsi chama hicho kilivyomteua Dk Khamis Kigwangallah kuwania ubunge wa Nzega alikoteuliwa licha ya kushika nafasi ya tatu katika kura ya maoni.
 Changamoto kura za maoni
Kuhusu changamoto kwenye upigaji kura za maoni ikiwamo vitendo vya rushwa, Nape alisema kwa takwimu walizonazo, changamoto zilizojitokeza ni kidogo ikilinganishwa na miaka ya nyuma... “Hii ni kwa sababu tumeboresha utaratibu tofauti na huko nyuma. Maeneo mengi yamemaliza na hata yale ambayo yamekuwa na kasoro za hapa na pale tumezitatua.
“…Kura za maoni katika chama chetu zimetoa demokrasia na bila shaka tumefundisha vyama vingine. Vyama vingi vinatoa wagombea mfukoni, lakini sisi tunawapeleka kwa wanachama wanapigiwa kura,” alisema Nape.
 Vigogo kuanguka
Alisema kuwa kutokana na kukua kwa demokrasia katika chama hicho na kujenga mfumo mzuri zaidi wa upigaji kura za maoni, hata vigogo wasiofanya vizuri wameanguka katika kura za maoni.
Kauli hiyo ya Nape imekuja huku kukiwa na ripoti ya baadhi ya mawaziri na wabunge wanaomaliza muda wao kuanguka katika kura za maoni.
Vigogo kuhama CCM
Alipoulizwa kuhusu kuhama chama hicho kwa waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa na Mbunge wa Segerea, Dk Makongoro Mahanga na wanaCCM wengine, Nape alisema siyo jambo la ajabu na kwamba si wa kwanza na wala hawatakuwa wa mwisho. “Wapo wanaotoka CCM kwenda vyama vingine na wapo wanaotoka vyama vingine na kuja CCM. Lakini niseme tu kwamba wapo ambao wanataka uongozi na wapo ambao wanataka kwenda kuongoza watu:
“Anayetaka kuongoza watu ni mvumilivu, mtulivu na hufuata taratibu. Lakini wapo ambao lengo siyo kwenda kuongoza watu, lengo ni masilahi binafsi. Wakikosa uongozi huonyesha tabia zao waziwazi.”

Mtikila aandaa makabrasha ya kumburuza Lowasa, Magufuli kortini


MWENYEKITI wa Chama cha Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, amesema chama chake kinaandaa taratibu za kwenda

mahakamani ili kumshtaki mgombea urais mteule wa CCM, Dkt. John Magufuli na mgombea urais wa CHADEMA, Bw. Edward Lowassa.

Alisema wagombea hao kwa nyakati tofauti, wameshiriki kuiingizia Serikali hasara ya mabilioni ya fedha ambapo wanasheria wa chama hicho wapo katika hatua za mwisho ili wafunguliwe mashtaka mahakamani.

Mchungaji Mtikila aliyasema hayo Dar es Salaam jana, alipozungumza na waandishi wa habari akisisitiza kuwa, wagombea hao wamepoteza sifa za kuwania nafasi hiyo akidai hawana vigezo kwa mujibu wa sheria.

Aliongeza kuwa, Bw. Lowassa, anahusishwa na sakata la kampuni ya kufua umeme ya Richmond na kuishangaa CHADEMA akidai chama hicho kilipata umaarufu wa kupinga vitendo vya ufisadi lakini wamempokea Bw. Lowassa na ana tuhuma kama hiyo.

"Kipindi cha nyuma, CHADEMA walianzisha operesheni nyingi ikiwemo ya Sangara na Movement for Change zikiwa na lengo la kupinga ufisadi, kwanini wamempokea Lowassa waliyemuita fisadi.
"Hii ina maana kuwa, ndani ya CHADEMA hakuna siasa, nawapongeza baadhi ya viongozi wa chama hicho na wanachama wao ambao kimsingi hawakubaliani na matakwa ya viongozi wa juu," 
Akimzungumzia Dkt. Magufuli, alimhusisha na tuhuma ya uuzwaji wa nyumba za Serikali akidai kitendo hicho kimeisababishia hasara Serikali lakini hakupelekwa mahakamani kwa kutumia madaraka yake vibaya kama ilivyokuwa kwa Basil Mramba, Daniel Yona ambao hivi sasa wanatumikia kifungo gerezani.

Alisema nyumba hizo zilikuwa makazi ya viongozi kama Majaji, Makatibu Wakuu na Watendaji waandamizi serikalini ambao wengi wao walilazimika kuishi hotelini kwa gharama za Serikali.