Monday, July 20

HABARI Habari Wavuvi wapamba mapokezi ya Dk Magufuli Sengerema 33 MINUTES AGO Msigwa asimamisha shughuli Iringa 52 MINUTES AGO Lembeli akataa kubadili msimamo 1 HOUR AGO Vita kali ya ubunge CCM, Chadema BIASHARA Biashara MICHEZO Michezo MAKALA Makala SWAHILI HUB Swahili Hub AJIRA VIDEO MONDAY, JULY 20, 2015 Vita kali ya ubunge CCM, Chadema

Baada ya mchakato wa kuwania urais, sasa vita ya Uchaguzi Mkuu imehamia kwenye ubunge na udiwani hasa kutoka katika vyama vikubwa vya CCM kinachotawala na Chadema kinachoongoza upinzani.
Hadi jana, ambayo ilikuwa ni siku ya mwisho kwa vyama hivyo kuchukua na kurejesha fomu, jambo moja lilijidhihirisha katika baadhi ya majimbo kwa upande wa CCM; baadhi ya majina makubwa katika siasa za ubunge yanachuana hivyo kufanya mchakato wa kumpata mteule mmoja kuwa mgumu.
Mchuano huo na kuimarika kwa Chadema mikoani hasa kutokana na majeraha ya mchakato wa urais ndani ya CCM, vinaufanya upinzani wa kuwania ubunge katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu kuwa sawa na vita.
Nzega Vijijini
Makada wawili wa chama hicho, Lucas Selelii na Dk Hamisi Kigwangalla wamechukua fomu kuwania ubunge wa Nzega Vijijini.
Katika uchaguzi uliopita wa 2010, makada hao walivaana katika Jimbo la Nzega lakini wote wakaangushwa na Hussein Bashe aliyeibuka wa kwanza akifuatiwa na Selelii.
Hata hivyo, matokeo hayo yalibatilishwa na Halmashauri Kuu ya CCM na kumchukua Dk Kigwangalla aliyekuwa mshindi wa tatu.
Mgawanyo wa majimbo uliofanywa wiki iliyopita na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), umerahisisha mpambano wa makada hao, hivyo wawili hao wakamwachia Bashe Nzega Mjini. 
Akichukua fomu hiyo jana, katika ofisi za CCM za Wilaya ya Nzega, Dk Kigwangalla akiwa ameambatana na wazee wa jimbo hilo, alisema shinikizo la kugombea Nzega Vijijini limetoka kwa wananchi wanaotambua umuhimu wake.
Selelii aliyekuwa Mbunge wa Nzega kwa miaka 15 hadi 2010, alichukua fomu kimyakimya bila kuzungumza na vyombo vya habari.
Katibu wa CCM Wilaya ya Nzega,  Empimark Makuya alithibitisha kuwa kada huyo alishachukua fomu. Wawili hao watakabiliana na upinzani mkali kutoka kwa wengine wawili waliochukua fomu, John Dotto na Paul Kabelele.
Maiga aibukia Iringa
Baada ya kukwama katika harakati za kuwania urais kupitia CCM, Balozi Dk Augustine Mahiga amejitokeza kuwania ubunge katika Jimbo la Iringa Mjini.
Dk Mahiga aliyechukua fomu jana na kurudisha, atapambana na Mwenyekiti wa CCM mkoani humo, Jesca Msambatavangu, Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe, Frederick Mwakalebela na mwandishi wa habari, Frank Kibiki ambao tayari wamechukua na kurejesha fomu zao.
Mchuano katika jimbo hilo unatarajiwa kuwa mkali wakati na baada ya kura za maoni ndani ya CCM hasa ikizingatiwa kwamba Mwakalebela alikuwa amechukua namba moja katika kura za maoni za chama hicho mwaka 2010 kabla ya jina lake kukatwa na NEC.
Mshindi atakuwa na wakati mgumu kukabiliana na kishindo cha upinzani hasa kutoka Chadema ambako Mchungaji Peter Msigwa aliyeshinda katika uchaguzi uliopita, jana alipokewa na umati mkubwa wa watu alipowasili mjini hapo.
Profesa Maghembe na Thadayo tena
Mshikemshike mwingine unatarajiwa kuibuka katika Jimbo la Mwanga ambako Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe anatarajiwa kupambana tena na hasimu wake mkubwa katika kiti hicho, Joseph Thadayo.
Katika uchaguzi wa 2010, Profesa Maghembe alimshinda Wakili huyo ambaye alionekana kuungwa mkono na wanasiasa wengine wenye nguvu katika jimbo hilo. Mbali yao wengine waliojitokeza ni Aminieli Kibali na Karia Magaro.
Wasira, Bulaya wavaana
Mchuano mwingine mkali unatarajiwa kuwapo katika Jimbo la Bunda Mjini ambako Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira atavaana na Mbunge wa Viti Maalumu, Ester Bulaya.
Wabunge hao wa CCM wamekuwa wakitambiana muda mrefu na wakati mwingine waliwahi kurushiana maneno hadi bungeni, lakini mwisho wa tambo zote ni kwenye kura za maoni.
Mamia warejesha fomu
Hadi muda wa mwisho wa kurejesha fomu unakamilika saa 10 jioni jana, mamia ya makada wa Chadema na CCM walikuwa wamejitokeza na kudhihirisha kuwa mchuano utakuwa mkali katika kura za maoni na hata kwenye uchaguzi wenyewe.
Kawe 22: Elias Nawera, Dk Walter Nnko, Jumaa Muhina, Kippi Warioba, Atulinda Barongo, Tegemeo Sambili, Kiganga George, Edmund Lyatuu, Charles Makongoro Nyerere, Mtiti Butiku, Yusuf Nassoro, John Mayanga, Dickson Muze, Dk Wilson Babyebonela, Colman Massawe, Amon Mpanji, Amelchiory Kulwizira, Gabriel Mnasa, Abdallah Majura na Jerry Murro, wote wakikabiliana na Halima Mdee aliyejitokeza pekee Chadema, hasa iwapo atasimama pekee kupitia Ukawa.
Kinondoni 12: Idd Azan, Wagota Salum, Tonny Kalijuna, Goodchange Msangi, Emmanuel Makene, Lusajo Willy, Mage Kimambi, Mussa Mwambujule, Stevew Nengere (Steve Nyerere), Joseph Muhonda, Michael Wambura na Macdonald Lunyiliga.
Ubungo 12: Vincent Mabiki, Timoth Machibya, Jordan Baringo, Emmanuel Mboma, Zangina Zangina, Kalist Ngalo, Hawa Ng’umbi, Jackson Millengo, Didas Masaburi, Joseph Massana, wote wa CCM wakitarajiwa kumkabili John Mnyika wa Chadema.
Ilala watatu: Mussa Azzan Zungu, Mrisho Gambo na Waziri Kindamba.
Ukonga 16: Jerry Silaa, Jacob Katama, Hamza Mshindo, Frederick Rwegasira, Anthony Kalokola, Ramesh Patel, Peter Majura, Amina Mkono, Edwin Moses, Robert Masegese, John Bachuta, Edward Rabson, Nickson Tugale, Elly Ballas, Asia Msangi, Lucas Otieno, Fredrick Kabati, Mwanaidi Maghohe, Mwita Waitara, Deogratius Munishi, Deogratius Kalinga, Deogratius Mramba, Salanga Kimbaga, James Nyakisagana, Lameck Kiyenze na Gaston Makweta.
Segerea 13: Zahoro Lyasuka, Apruna Humba, Bona Kalua, Nicholaus Haule, Baraka Omary, Benedict Kataluga, Dk Makongoro Mahanga na Joseph Kessy.
Kigamboni 10: Aron Othman, Kiaga Kiboko, Abdallah Mwinyi, Dk Faustine Ndugulile, Ndahaye Mafu, Flora Yongolo, David Sheba, Mohammed Ally Mchekwa, Khatib Zombe na Adili Sunday.
Mbagala 23: Lucas Malegeli, Mindi Kuchilungulo, Kazimbaya Makwega, Adadius Richard, Tambwe Hiza, Issa Mangungu, Ingawaje Kajumba, Siega Kiboko, Peter Nyalali, Mwinchumu Msomi, Dominic Haule, Aman Mulika, Banda Sonoko, John Kibasso, Ally Makwiro, Alvaro Kigongo, Maesh Bolisha, Kivuma Msangi, Deus Sere, Abdulrahim Abbas, Salum Seif Rupia, Ally Mhando, Fares Magessa, Stuwart Matola.
Moshi: Priscus Tarimo, Amani Ngowi, Patrick Boisafi, Davis Mosha, Buni Ramole, Halifa Kiwango, Michael Mwita, Daud Mrindoko, Shanel Ngunda, Innocent Siriwa, Edmund Rutaraka, Omari Mwariko, Basil Lema, Jaffar Michael na Wakili Elikunda Kipoko.
Busokelo:  Suma Mwakasitu , Dk Stephen Mwakajumilo, Ezekiel Gwatengile, Mwalimu Juma Kaponda, Ally Mwakibolwa, Issa Mwakasendo, Aden Mwakyonde na Lusubilo Mwakibibi.
Kilombero: Kanali mstaafu Harun Kondo, Vitus Lipagila, Abdullah Lyana, Oscar Mazengo,  Japhet Mswaki, Paul Mfungahema, John Guninita, Abubakari Asenga na Abdul Mteketa.
Mlimba: Dk Frederick Sagamiko, Senorina Kateule, Godwin Kunambi, Augustino Kusalika, George Swevetta, Castor Ligallama, Profesa Jumanne Mhoma, Fred Mwasakilale, Dismas Lyassa.
Namtumbo: Edwin Ngonyani, Edwin Milinga, Mwinyiheri Ndimbo, Vita Kawawa, Anselio Nchimbi, Julius Lwena, Fitan Kilowoko, Balozi Salome Sijaona, Mussa Chowo, Salum Omera, Ally Mbawala na Charles Fussi.
Tunduru Kaskazini: Mhandisi Ramo Makani, Omary Kalolo, Michael Matomola, Hassan Kungu, Issa Mpua, Rashid Mandoa, Athuman Mkinde, Shaban Mlono na Moses Kulawayo.
Tunduru Kusini: Abdallah Mtutura, Daim Mpakate na Mtamila Achukuo.
Nyasa: Christopher Chale, Bethard Haule, Adolph Kumburu, Alex Shauri, Frank Mvunjapori, Dk Steven Maluka, Stella Manyanya, Cassian Njowoka, Jarome Betty na Oddo Mwisho.
Serengeti: Dk Stephen Kebwe, Dk James Wanyancha, Juma Kobecha na Mabenga Magonera.
Sumbawanga Mjini: Aeshi Hilaly, Anyosisye Kiluswa, Fortunata Fwema, Mathias Koni, Gilbert Simya, Frank Mwalembe, Selis Ndasi, Mbona Mpaye, Sospeter Kansapa, Paschal Sanga na Victor Vitus.
Korogwe Vijijini: Stephen Ngonyani (Profesa Majimarefu), Cesilia Korassa, Allan Bendera, Ali Mussa Moza, Abdallah Nyangasa, Christopher Shekiondo, Andrew Matili, Edmund Mndolwa, Ernest Kimaya, Peter Mfumya na Stephen Shetuhi.
Kilindi: Beatrice Shellukindo, Abdallah Kidunda, Fikirini Masokola na Dk Aisha Kigoda.
Bariadi Mashariki: Masanja Kadogosa na Joram Masaga.
Mbulu: Mary Margwe amechukua fomu ya kugombea ubunge wa viti maalumu
Mbunge wa Arumeru Magharibi, Goodluck Ole Medeye na yule wa Kilosa Kati, Mustafa Mkulo hawakujitokeza kuchukua fomu.
Imeandikwa na Julius Mathias,  Bakari Kiango, Godfrey Kahango, Ngollo John, Salim Mohammed, Joseph Lyimo, Faustine Fabian, Joyce Joliga, Daniel Mjema, Burhani Yakub, Antony Mayunga, Mussa Mwangoka na Mustapha Kapalata

Kambi ya Lowassa sasa rasmi Chadema

Sasa ni rasmi kwamba kambi ya aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Edward Lowassa imeamua kuachana na chama hicho baada ya madiwani 18 kutangaza kuhamia Chadema, huku mratibu wa wanachama wanaomuunga mkono kada huyo wa CCM kuamua kujiunga na vyama vinavyounda Ukawa.
Matukio hayo yametokea ikiwa ni mwendelezo wa wimbi la wanachama wa CCM kutangaza kuhamia vyama vya upinzani, hasa Chadema baada ya madiwani tisa pamoja na wanafunzi 28 wa vyuo vikuu kutangaza kuhamia Chadema ambayo ni chama kikuu cha upinzani.
Wote wameeleza sababu ya kuhama CCM ni kutokubaliana na uamuzi wa Kamati Kuu wa kukata jina la Lowassa wakati wa mchujo wa wagombea urais kwa tiketi ya chama hicho tawala mwishoni mwa wiki iliyoishia Julai 12.
Akizungumzia kuhama kwa madiwani hao, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema hawezi kujibu lolote kwa madai kuwa hana taarifa rasmi na kutaka waulizwe viongozi wa chama wa mkoa.
“Madiwani hao siwajui na sina taarifa rasmi ninaweza kutoa maoni yangu, lakini kesho ikabainika kuwa hazikuwa taarifa rasmi juu ya kuhama kwao?” alihoji.
Nape alisisitiza kuwa hakuna kanuni zilizokiukwa wakati wa kumsaka mgombea urais kama wanachama hao wanavyodai.
Nape pia alizungumzia kitendo cha mwanasiasa mkongwe, Kingunge Ngombale-Mwiru cha kuilaumu Kamati ya Maadili na Kamati Kuu akisema kinaweza kukigawa chama hicho.
“Kama wakiendelea CCM kitaitisha mkutano na kuwajibu. Lakini kwa sasa tunawataka tu wawasilishe malalamiko yao sehemu husika maana huo utaratibu wanaujua,” alisema
Jana, mkoani Arusha, madiwani hao, walioongozwa na viongozi wa kijadi wa jamii ya Kimasai wanaofahamika kwa jina la Malaigwanan, walipokewa jana na aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema kwenye hafla fupi iliyofanyika mjini Monduli.
Mwenyekiti wa CCM wa mkoa, Onesmo ole Nangole alisema chama chake hakina uwezo wa kuzuia mtu kuondoka CCM.
“Tumepata taarifa za kuondoka madiwani na viongozi wetu na kuchomwa kadi lakini hatuwezi kuzuia uamuzi wa watu kufanya wanachotaka,” alisema.
Alisema tayari wameanza kufuatilia kinachoendelea kutokea katika maeneo mbalimbali mkoani Arusha ili kujua athari za matukio hayo kwa CCM.
Viongozi hao waliohamia Chadema ni 10 wakati Halmashauri ya Wilaya ya Monduli ina kata 20. Awali, halmashauri hiyo ilikuwa na kata 15 kabla nyingine tano kuongezwa mwaka huu.
Akisoma tamko la kujiengua CCM na kuhamia Chadema, mwenyekiti wa madiwani hao, Julius Kalanga ambaye ni diwani wa Kata ya Lepurko, alisema hatua hiyo imetokana na kuchoshwa na vitendo alivyoviita vya hila, uonevu, ubaguzi na unyanyasaji vinavyofanywa ndani ya chama hicho tawala.
“Tumetafakari usalama wetu ndani ya CCM kwa umoja wetu tumeshindwa kuuona… CCM iliyokuwa ikiongozwa kwa Katiba, kanuni na miongozo hivi sasa inaongozwa kwa matakwa ya familia chache kwa jinsi watakavyoona inawapendeza wao,” alisema Kalanga.
Alisema mchakato wa CCM wa kumpata mgombea urais uliomalizika hivi karibuni mjini Dodoma ni miongoni mwa ishara za wazi za chama hicho kukosa maadili kuanzia kwenye vikao vya Kamati ya Maadili alichodai kilikosa maadili hadi kukatwa kwa majina ya wagombea akiwemo Lowassa.
Kalanga, mmoja wa wasaidizi wa karibu wa Lowassa katika shughuli zake za kisiasa, alisema wana-CCM wamepoteza haki na uwezo wa kuchagua viongozi wanaowataka kutokana na kunyimwa uwezo wa kufikiri kwa sababu uamuzi hauzingatii utaratibu wa vikao.
“Tunakataa kuwa watumwa katika misingi hii na ndiyo maana leo tunaondoka sisi viongozi wote na kuamua kujiunga Chadema,” alisema Kalanga.
“Tunamwomba Mheshimiwa Lowassa aungane nasi katika safari yetu hii inayoendelea. Awe na moyo wa ujasiri na kufanya uamuzi mgumu maana hakuna busara nyingine inayoweza kutumika zaidi ya kuondoka CCM,” alisisitiza Kalanga.
Diwani wa Kata ya Mererani, Edward Lenana ambaye ni mmoja wa waliotimkia Chadema alisema yeye na wenzake watazunguka kwenye majimbo yote ya jamii ya Wamaasai kuhamasisha jamii hiyo kutochagua wagombea wa CCM kuanzia ngazi ya udiwani, ubunge na urais.
Akizungumza baada ya kuwakabidhi viongozi hao kadi za Chadema, Lema aliwataka kuingia kazini kukijenga chama chao kipya ili kufanikisha ushindi katika uchaguzi mkuu ujao wa Oktoba 25.
“Ndani ya Chadema hakuna mheshimiwa, kiongozi wala mwanachama mdogo. Wote ni makamanda wanaopaswa kupambana dhidi ya uovu na ukandamizaji. Kuanzia leo ninyi nyote ni makamanda. Hakuna kamanda mgeni wala mwenyeji, bali sote ni wapiganaji wenye lengo moja la ushindi mwezi Oktoba,” alisema Lema.
Mwenyekiti wa Chadema wa mkoa, Amani Golugwa aliwataka wanachama hao wapya kujifunza na kuishi katika misingi ya uadilifu, unyenyekevu na utumishi kwa umma aliosema ndiyo miongoni mwa imani kuu ya Chadema.
Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari na wa viti maalumu, Joyce Mukya waliwahakikishia viongozi hao fursa ya kuendelea kuwatumikia wananchi katika kata zao wakiwa Chadema kwa sababu wapigakura ni wale wale, bali kilichobadilika na jukwaa la kusimamia kuwatumikia.
Wengine Dar wajiengua
Jijini Dar es Salaam, wanachama waliokuwa kundi la 4U Movement linalomuunga mkono Lowassa, walitangaza kuihama CCM chama hicho na kujiunga na Ukawa, kutokana na kile walichodai kuchukizwa na mchakato wa kumpata mgombea urais.
Mratibu wa wanachama hao, Hemed Ally alisema wamefikia uamuzi wa kujiunga na Ukawa inayoundwa na vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema, NLD na CUF, kwa ajili ya “kutafuta mabadiliko nje ya CCM”, kutokana na kushindwa kuyapata wakiwa ndani ya chama hicho tawala.
Wadai njama zimewatoa
Wanachama hao wanaodai wana wafuasi wapatao milioni 10 ambao wengi ni vijana, walitangaza uamuzi huo jana jijini Dar es Salaam katika mkutano na waandishi wa habari, huku wakisisitiza kuwa kulikuwa na njama za kuhakikisha kuwa Lowassa anaenguliwa huku wakinukuu maneno yaliyosemwa na kada mkongwe wa CCM, Kingunge Ngombale-Mwiru ambaye naye alikilalamikia chama hicho kutomtendea haki Lowassa, ambaye ni mbunge wa Monduli.
Makada wa CCM waliopitishwa kuwania nafasi ya kupeperusha bendera ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 walikuwa 38, huku Dk John Magufuli akiibuka kidedea.
Waliongia tano bora walikuwa Dk Magufuli, Bernard Membe, Balozi Amina Salum Ali, Asha-Rose Migiro na January Makamba.
Wanachama hao walisema kwa pamoja wamekubaliana kutumia kura zao kuking’oa CCM madarakani katika uchaguzi wa mwaka huu.
Ally alisema kulikuwepo na ukiukwaji mkubwa wa kanuni katika uteuzi, jambo linalowafanya waamini kuwa Kamati ya Maadili ilikosa maadili.
“Tunaomba ieleweke wazi hatuna nia ya kumpinga Magufuli ila upatikanaji wake ulijaa maovu hivyo tumeamua hatutaiunga mkono CCM na kura zetu tutazipeleka upinzani.
“Lowassa hakutendewa haki na kila mmoja anatambua hilo, sisi tumeamua kutoka kwa sababu tulikuwa tunamuunga mkono yeye tukiamini atatuletea mabadiliko lakini kwa mtindo huu tunaona kiu yetu haiwezi kutimizwa ndani ya CCM,” alisema Ally.
Alivitaka vyama vya upinzani kuunganisha nguvu kwa pamoja na kushirikiana nao kuindoa CCM kwa demokrasia ya upigaji kura. Kwa mujibu wa Ally, wafuasi hao wamegawanyika katika makundi kadhaa ambayo ni 4 U Movement, Lowassa for Presidency, Team Lowassa, Umoja wa Waendesha Bodaboda na Shirikisho la Walimu.
“Upinzani ukijipanga vizuri tunaweza kuindoa CCM madarakani ikizingatiwa kura zetu zote tutazielekeza upande huo kumuunga mkono mgombea yoyote watakayemsimamisha,” alisema.
Katibu wa Shirikisho la Walimu Wafuasi wa Lowassa, Maulid Nkungu alisema kama vijana hawana sababu ya kukubaliana na utaratibu ambao hata wakongwe wa chama hicho hawajaridhishwa nao.
“Tuliipenda sana CCM, lakini imeonyesha kutopenda mabadiliko hilo ndilo linalotuondoa tumechoka kuonewa tunataka kulinda heshima na kuwakomboa wanaonyanyaswa,” alisema.

Thursday, July 16

UCHAGUZI CCM: Mambo matano mazuri ya Magufuli akiwa rais

Dk John Magufuli akiwasalimia Wajumbe wa Mkutano Mkuu 
katika ukumbi mpya wa CCM mjini Dodoma kabla ya kuanza kupiga kura juzi usiku.
Chama cha Mapinduzi (CCM) kimempitisha Dk John Pombe Magufuli kuwa mgombea urais wa chama hicho kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa Tanzania utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu.
Kwanza kabisa napenda kumpongeza sana Magufuli kwa hatua aliyofikia na kumtakia kila la heri. Naomba kukiri kwa uwazi kwamba katika uchaguzi unaohusisha vyama vya siasa ni lazima mshindi atapatikana na kwa Tanzania ni lazima mshindi huyo atoke kwenye chama cha siasa.
Tanzania ina vyama 22 vilivyosajiliwa na vinavyofanya kazi sasa, tutake tusitake ni lazima rais wa nchi atatoka katika chama kimojawapo, na kwa sababu CCM imeshapitisha mgombea wake na yeye ana fursa ya kushinda uchaguzi kama ambavyo fursa hiyo ilivyo kwenye vyama vingine. Natumia nafasi hii kufanya uchambuzi wa dhati juu ya taswira ya serikali ya Magufuli ikiwa atafanikiwa kushinda uchaguzi wa mwaka huu. Taswira ya namna hii pia nitaifanya kwa wagombea wengine wa vyama ambavyo vitaamua kuweka wagombea urais.
Katika kulifanya jukumu hili nitachambua masuala 10 ambayo nafikiri kwamba yanaweza kujenga utawala wa Magufuli, ikiwa atachaguliwa na Watanzania kuwa rais wa awamu ijayo.
Mambo matano kati ya hayo nayatazama kama taswira bora na mengine matano yanaweza kuwa taswira hasi. Katika uchambuzi wa leo nitaanza na mambo matano ambayo ni taswira bora.
Usimamizi bora
Taswira ya kwanza ambayo Magufuli anaweza kuirejesha bila wasiwasi ni usimamizi thabiti wa serikali na nidhamu ya utendaji ndani ya serikali. Naamini kuwa serikali ya Magufuli itakuwa ya kiusimamizi na yeye mwenyewe anaweza kulifanya jambo hilo bila kusita. Katika nyadhifa nyingi alizopitia hadi sasa ameijenga taswira hii kila alikopita na bado inambeba hata ikitokea anachaguliwa kuwa rais wa awamu ya tano.
Tukumbuke kuwa moja ya mambo ambayo yameanguka kabisa nchini hivi ni utendaji ndani ya serikali. Tunafahamu kuwa wafanyakazi ndani ya serikali ukiachilia mbali matatizo waliyonayo kwa maana ya vipato, hata mambo madogo ambayo wangeweza kuyasimamia ndani ya dakika au saa chache huchukua wiki kadhaa na hata miezi kadhaa. Utaratibu wa utoaji huduma umekwama sana na nadhani kama akiwa na uwezo huo atafanikiwa kutatua changamoto kubwa na ya siku nyingi. Ikiwa utendaji wa serikali unaimarika na huduma zinatolewa kwa wakati, tutaweza kujenga taifa linalokwenda mbele bila kujali chama gani kiko madarakani.
Msimamo imara
Taswira bora ya pili ya serikali ya Magufuli inaweza kuwa ni misimamo katika masuala ya msingi na kutoyumba sana. Magufuli muda wote ambao amekuwa kiongozi ameonyesha jambo hilo. Kila mara amekuwa na misimamo hata kama siyo sahihi. Kwa tafsiri nyingine hii huwa ni njia bora ya uongozi wa nchi japokuwa misimamo ya serikali au kiongozi mkuu wa serikali huwa haipaswi kuwa juu ya haki na matakwa ya wananchi.
Moja ya mambo ambayo serikali iliyopita ilikosa, ni pamoja na kukosa misimamo na kuwa na “double standard”. Mfano mdogo tu ni kwenye mchakato wa katiba mpya ambapo Rais anayeondoka alisimamia uanzishwaji bora wa mchakato huo, akaunga mkono katika hatua zote na rasimu zote, lakini akaja kuwageuka wajumbe wa tume hiyo na rasimu yao ya pili alipolihutubia Bunge Maalumu la Katiba. Naamini Magufuli si mtu wa kugeuka na kuna masuala mengi anaweza kuyasimamia kwa dhati na kila mmoja wetu akakubali kuwa, naam! Hapa kuna kiongozi anasimamia masuala haya.
Uwezo wa kusimamia miradi
Taswira ya tatu ya serikali inayoweza kuundwa na Magufuli ikiwa atachaguliwa kuwa rais ni uwezo wa kusimamia miradi ya maendeleo. Magufuli ni mtu wa namna hiyo na ametuonyesha katika sekta ya ujenzi na hasa katika eneo la barabara. Moja ya masuala ambayo nayaona kama mafanikio makubwa ya serikali ya Kikwete ni ujenzi wa barabara, ukiniuliza, nitakwambia jambo hili ndilo Kikwete anapaswa kujivunia atakaporudi nyumbani kwake pale ‘Msoga’. Lakini aliyeleta mapinduzi hayo kiusimamizi ni Magufuli.
Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kuwa “ikitolewa tenda ya ujenzi wa barabara nchini Tanzania na India halafu nchi zote zikakabidhi tenda hizo kwa watoto wa marais wa nchi, kule India walau barabara ya ‘kudanganyishia’ itajengwa lakini hapa Tanzania unaweza usione hata kokoto” (tafsiri yangu). Dhana hiyo ina maana kwamba huku kwetu wizi na kujijazia manoti ndivyo vitu vinavyoshamiri na kwa tafsiri ya Mwalimu “ilipasa Magufuli awe anaongoza kwa kuchukua noti za barabara na kuzijaza tumboni kwake”,  jambo ambalo limekuwa nadra kutokea na kama liliwahi kuwepo ndiyo tutajua sasa wakati watu wataanza kutoa taarifa zake kwa sababu anataka kwenda Ikulu. Kwa uwezo huu wa kiusimamizi namuona Magufuli akisimamia miradi ya serikali kwa ustadi mkubwa hata kama siyo “waziri wa miradi” katika serikali atakayoiunda.
Mawaziri imara
Taswira ya nne nayoiona katika serikali ya Magufuli ikitokea anashinda urais wa Tanzania ni uundaji wa Baraza la Mawaziri na nyadhifa za kiutendaji zilizojaa watu wenye uwezo kuliko marafiki. Serikali zetu kadhaa zilizopita ikiwamo hii inayoondoka zimekuwa na sifa ya kubeba marafiki kufa au kupona. Siyo siri kwa JK amelalamikiwa mno na mara kadhaa serikali yake ilionekana kama “imejaa washkaji” watu wanaolindana na kuoneana haya kwa heshima za urafiki kuliko kuangalia maslahi ya nchi.
Magufuli anaweza kuwa dawa ya serikali za ushkaji kwani tangu kwenye mchakato wa kupata wagombea ndani ya CCM hakuonekana kama “kitisho” na hakuwa na makundi nyuma yake, penyeza yake ya kimya kimya hadi anakuwa mgombea urais wa CCM imemsaidia kuanza kujenga marafiki wasio na masharti ya kutaka kubebwa naye. Marais wengi huunda mitandao na mitandao hiyo huwapa fedha mapema na huwasaidia kila jambo, wanapofika madarakani huwa na deni la kuilipa mitandao hiyo, malipo yenyewe ni miradi ya serikali, tenda mbalimbali na vyeo lukuki. Naamini Magufuli hatakuwa na tatizo hilo na itamsaidia kutengeneza serikali isiyo na “washkaji kibao.”
CCM yenye nguvu
Taswira ya tano inayoweza kujitokeza ni uwezekano wa kurejesha nguvu ya CCM ambayo inasambaratika, na naamini hili linaweza kujitokeza sana hasa kwenye kipindi cha kwanza cha uongozi wake. Siamini kama ataweza kurekebisha taswira ya CCM kwa miaka mitano mingine (ikiwa atapata vipindi vyote viwili) kwa sababu hatujaona utendaji halisi wa serikali ijayo, ikiwa CCM ndiyo itashinda. Wananchi wengi hawaiamini tena CCM na jambo hilo linaweza kuipeleka ikaangushwa katika uchaguzi wa mwaka huu, lakini ikitokea CCM inavuka kizingiti na inapona kuangushwa halafu Magufuli anakuwa rais, anaweza kujizatiti na akatumia miaka mitano kufanya mambo makubwa yatakayowafanya wananchi warudishe imani kwa chama hicho. Ila akifanya vibaya sana atazidi kuididimiza. Kwa mtazamo wangu wa msisitizo ni kwamba naona akifanikiwa kwenye eneo hili, japokuwa naweka msisitizo wa pili kuwa ni lazima tusubiri kujua ikiwa atashinda kipindi chake cha kwanza kitakuwaje kiuongozi.

UCHAGUZI CCM: Mambo matano ‘mabaya’ Magufuli akiwa rais

Dk John Magufuli akiwasalimia Wajumbe wa Mkutano Mkuu 
katika ukumbi mpya wa CCM mjini Dodoma kabla ya kuanza kupiga kura juzi usiku.

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimempitisha Dk John Pombe Magufuli kuwa mgombea urais wa chama hicho kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa Tanzania utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu. Tanzania ina vyama 22 vilivyosajiliwa na vinavyofanya kazi sasa, tutake tusitake ni lazima rais wa nchi atatoka katika chama kimojawapo, na kwa sababu CCM imeshapitisha mgombea wake na yeye ana fursa ya kushinda uchaguzi kama ambavyo fursa hiyo ilivyo kwenye vyama vingine. Natumia nafasi hii kufanya uchambuzi wa dhati juu ya taswira ya serikali ya Magufuli ikiwa atafanikiwa kushinda uchaguzi wa mwaka huu. Taswira ya namna hii pia nitaifanya kwa wagombea wengine wa vyama ambavyo vitaamua kuweka wagombea urais..
Uamuzi wa haraka
Moja ya taswira mbaya zinazoweza kujitokeza na kuikumba serikali ya Dk John Magufuli (ikiwa atashinda uchaguzi) ni maamuzi ya haraka na yasiyo na tija ya uhakika. Katika utendaji mzuri wa Magufuli serikalini, madoa makubwa aliyopata ni kwa nyakati kadhaa kusimamia mambo ambayo baadaye yalilalamikiwa sana. Niliwahi kutoa mfano namna ambavyo amewahi kulalamikiwa juu ya maamuzi yake ya kubomoa nyumba za wananchi bila kuwapa muda wa kutosha kuhama. Kibinadamu hayo ni matendo ya ukatili na yanatokana na ufanyaji maamuzi wa haraka katika jambo linalohitaji muda. Sijui kama Magufuli ataachana na tabia hiyo ya “haraka haraka” ili pia kuifanya serikali yake ijiendeshe kistratejia na kimipango kuliko haraka na nguvu. Ikiwa atasonga mbele na tabia hiyo na serikali yake ikaenda kwa kasi hiyo ya “pupa” kuna uwezekano kuwa kila mambo kumi atakayoyasimamia basi mawili hadi matatu yakawa yanafanywa bila kuwa na tija kwa taifa.
Kuyumba kichumi
Mtihani wa pili ambao unaweza kujenga taswira mbovu ya utawala au serikali itakayoundwa na Magufuli (ikiwa atachaguliwa kuwa Rais wa Tanzania) ni usimamizi wa masuala ya kiuchumi. Eneo hili naliona kama muhimu sana kwa sababu kama nilivyoeleza hapo juu, Magufuli amekuwa waziri bora katika serikali inayomaliza muda wake na amekuwa akitumwa na kufanya kila jambo haraka kwa wakati na kwa maamuzi yenye misimamo. Sielewi uwanda wake katika masuala ya kiuchumi na misimamo yake kwenye eneo hilo, hapa sina maana kuwa Rais wetu lazima awe mchumi, la hasha! Benjamin Mkapa hakuwa mchumi lakini alikuwa na uwezo mpana wa kusimamia uchumi, Jakaya Kikwete ni mchumi lakini amefanya vibaya kwenye eneo hilo kuliko Mkapa. Magufuli amejionyesha mara zote kama mtendaji kuliko “mfikiriaji na mpanga mambo”. Uchumi wa nchi uliopo kama Tanzania unahitaji akili ya ziada kuweza kuufufua tena, nchi haina viwanda, inanunua kila kitu kutoka nje. JK anaiacha ikiwa hoi sana kwenye eneo hilo. Ikiwa Magufuli ataingia na mtindo wa kusimamia utendaji zaidi kuliko kufikiri na kubuni vyanzo vipya vya uchumi, serikali yake itabeba taswira ya kushindwa kusimamia uchumi.
Serikali ya mtu mmoja
Taswira nyingine ya tatu ambayo si salama na ambayo inaweza kujitokeza kwenye serikali itakayoundwa na Magufuli ni serikali ya “One Man Show” (serikali ya mtu mmoja). Watu waliozoea kuwa watendaji wa juu kama Magufuli huwa na kasumba ya kutaka kila jambo liende kama wanavyotaka kila wakati na wakiona haliendi huingilia haraka na kutaka walifanye wao wenyewe, hili ni jambo la kisaikolojia zaidi. Kilema cha serikali za namna hii huwa ni kumjenga mtu mmoja zaidi kuliko wengine si kwa makusudi, bali kwa sababu watendaji wake wanashindwa kwenda na uwezo wa rais wao. Madhara ya hali hii ni kujenga serikali inayokosa vionjo pale ambapo rais anapokuwa hayupo, kunakuwa na hofu ya dhahiri kuwa ni nani anaweza kusimamia masuala mbalimbali kama awezavyo rais na huyo mtu hayupo. Taswira hii itavunjwa tu iwapo mkuu wa nchi ataamua kuwaachia watendaji wafanye maamuzi magumu wao wenyewe, wajifunze kukosea na kukosolewa.
Haki za binadamu
Jambo la nne ambalo linaweza kuwa “taswira dhaifu ya serikali ya Magufuli” (ikiwa atashinda) ni uwezo wa kusimamia masuala ya haki za binadamu na haki za msingi za raia. Hili linaweza kuunganishwa na ile kanuni yake ya ‘kufanya maamuzi kwa mbio na haraka sana kila mara’. Maamuzi ya haraka na yasiyotoa mwanya wa kutosha wa kuzingatia masuala mengine muhimu ya haki za kiraia huwa hayana tija na huumiza dhana ya usimamizi wa haki hizo na yasipokomeshwa huwaumiza raia. Mmoja wa wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM ambaye nimeongea naye na hakumpigia kura Magufuli katika mkutano mkuu huo amenieleza kuwa hakufanya hivyo kwa sababu nyumba yake ya urithi iliwahi kubomolewa bila kupewa muda wa kutosha kwa sababu ilikuwa karibu na barabara. Dhana ya usimamizi wa sheria lazima iendane na dhana ya kusimamia haki za raia, watu wa namna hii wanaweza kuwa wengi na ni kielelezo cha wazi kwamba Magufuli atawajibika kurekebisha sana taratibu za ufanyaji maamuzi katika serikali yake ili aweze kulinda haki za raia. Serikali yake inaweza kuepukana na taswira hii mbovu kwa kuchukua muda na kutafakari kwa kina juu ya mustakabali wa wananchi kila jambo fulani linapotokea
Mwenyekiti wa CCM
Taswira ya tano mbaya inayoweza kujitokeza katika uongozi “serikali” ya Magufuli ikiwa atachaguliwa kuwa Rais wa Tanzania ni uwezo wa kukiongoza Chama Cha Mapinduzi. Mtu yeyote hawezi kuwa na shaka na uwezo wa Magufuli katika utendaji wake muda wote serikalini, lakini kunaweza kuwa na shaka kubwa katika uwezo wa kukiongoza chama chake. Mahasimu wake kisiasa tayari wameanza kuwa na hofu na uwezo wa CCM miaka ya mbele chini ya Magufuli, namna ambavyo anaweza kupambana na changamoto za kuongoza chama chenye watu wengi wenye maslahi tofauti tofauti sana.
Ukweli uliopo ni kwamba muda wote ambao Magufuli amekuwa serikalini hakuwahi kuwa kiongozi mkubwa wa moja kwa moja ndani ya CCM. Jambo hili linatafsiriwa kama linaweza kumsababishia makosa ya kiutendaji kwa sababu ya “kutaka kujinasibisha kama yuko karibu na wanachama wa CCM” kumbe akawa anaingizwa kwenye makosa.
Mfano mzuri ni wakati anashukuru wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM na kabla hajataja jina la mgombea mwenza, mara kadhaa alisikika akisema “CCM kwanza, chama chetu kwanza….” Na kisha baadaye ndiyo anasema “Tanzania kwanza”. Wafuatiliaji wa mambo wanaweza kuanza kuhoji, gia hii ya Magufuli ndiyo kutaka kuwaonyesha wanachama kuwa yeye anaifahamu CCM vizuri sana? Kwa chama kikongwe kama CCM unatarajia kiongozi akitanguliza maslahi, kwanza aseme “Tanzania kwanza” chama baadaye. Kusimama hadharani na kusema “Chama Kwanza, Chama Chetu kwanza…” inaleta mtazamo kwamba anaweza kujikuta anafanya makosa ya kiutendaji katika serikali yake kwa lengo tu la kutaka “kuwaridhisha wana CCM”.  Ni bora Magufuli akajiamini, akajiona ni mwana CCM imara na asijione kama vile “kapewa hisani” kuwa mgombea wa chama hicho. Kujiamini kutamfanya akitazame na kukihukumu chama chake bila woga kila mara na pia aitazame nchi yake kama kipaumbele cha kwanza kabla ya chama, kama Rais wa nchi.
Hitimisho
Magufuli ni mtu mahiri ndani ya chungu kibovu. Ule ule mkakati wa kuiokoa CCM mwaka 2005 kwa “kumleta Jakaya” ndiyo unatumika mwaka 2015 tena, kwamba CCM inajitahidi na inajaribu kutaka kuendelea kuishi kwa kutumia mgongo wa kukubalika kwa mgombea wake, kwamba Watanzania wakaipigie kura kwa kumuamini zaidi Magufuli kuliko kutazama makosa ya kihistoria ya chama hicho tangu miaka 50 iliyopita. Kwa Watanzania waliokata tamaa na uongozi unaomaliza muda wake, aina ya watu kama Magufuli wanaweza kuwa kimbilio kubwa sana kwa maana ya upigaji kura, lakini hatujui baada ya kura hizo nini kitatokea, maana Magufuli anakwenda kuzungukwa na wana CCM, na watendaji lukuki serikalini ambao kwao “kuiba fedha za umma na kufanya utendaji mbovu ni amri ya kila siku”. Mambo haya yanaweza kuanza kuwa kikwazo kikubwa kwake hadi pale atakapoamua kuchukua hatua thabiti sana.Mimi binafsi napenda kumtakia kila la heri kiongozi huyu, katika safari aliyoianza.

Thursday, July 2

Lukuvi: Marufuku kuchukua ardhi bila fidia.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi.



Serikali imepiga marufuku halmashauri za wilaya na manispaa nchini, kuchukua ardhi ya wananchi bila kuwalipa fidia.
Amri hiyo imetolewa mjini hapa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi (pichani),   wakati akijibu malalako ya wananchi kuhusu upatikanaji na umiliki wa ardhi.
 
Lukuvi, alisema halmashauri na manispaa nchini, zimekuwa zikichukua ardhi ya wananchi bila makubaliano na kuwalipa fidia kwa kisingizo cha upimaji viwanja au kutoa maeneo hayo kwa ajili ya uwekezaji.
 
Alisema kitendo hicho ni dhuluma kwa wananchi na kwamba kamwe hakikubaliki.
 
Awali baadhi ya wakazi hao, walimlalamikia Waziri Lukuvi wakidai kuwa wamekuwa wakiporwa ardhi na maofisa wa halmashauri na manispaa bila maelezo.
 
Walidai wanapofuatilia kwenye ofisi zao, wamekuwa wakijibiwa vibaya na wakati mwingine kulipwa fidia kidogo ambayo haitoshi kununua kiwanja na kuwa  kero kubwa kwao na kukatisha tamaa.
 
Akizungumza huku akibubujikwa na machozi mbele ya Lukuvi ambaye pia ni Mbunge wa Ismani,  Zuhura Chavala, Mkazi wa Kijiji cha Migori, alidai maofisa ardhi wamekuwa wakiwadhulumu baada ya kuwaponya ardhi yao.
 
Zuhura alidai wanapofuatilia kwa lengo la kulipwa fidia, wamekuwa wakizungushwa hivyo kushindwa kujua hatma yao.
 
Wakati huo huo: Waziri huyo amewataka wakuu wa wilaya nchini kushiriki mikutano ya vijiji na  kutoa ardhi kwa wawekezaji ili kuondoa malalamiko ya wananchi.
 
Alisema wakuu hao wanatakiwa kuwadhibiti baadhi ya viongozi wa vijiji ambao wamekuwa wakighushi mikutano hiyo na kuuza ardhi ya vijiji kwa wageni bila kupita kwenye mkutano mkuu wa kijiji.
 

Kilio bei mpya ya petroli kila kona.


Zikiwa ni siku mbili zimepita tangu Mamlaka ya Usimamizi wa Nishati na Maji (Ewura), itangaze kuongezeka kwa bei elekezi ya mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa, wananachi wengi wameingiwa hofu kwa kuamini kuwa uamuzi huo utawaongezea makali ya maisha maradufu.
 
Juzi mamlaka hiyo ilitangaza ongezeko la bei elekezi ya mafuta na kuonyesha kuwa bei ya petroli imeongezeka kwa Sh. 232 kwa lita, dizeli Sh. 261 na mafuta ya taa Sh. 369. Katika soko la dunia, bei ya mafuta imekuwa ikishuka. Hata hivyo, taarifa ya Ewura ilitaja sababu za kupanda kwa bei ya nishati hiyo nchini kaunzia jana kuwa ni kuporomoka kwa thamani ya Shilingi na pia kuanza kutumika kwa tozo mpya za mafuta zilizopitishwa na bunge la bajeti kwa mwaka wa fedha 2015/2016.
 
Kufuatia mabadiliko hayo, bei ya petroli kwa sasa jijini Dar es Salaam ni Sh. 2,198, dizeli Sh. 2,043 na mafuta ya taa ni Sh.1, 993; Arusha petroli Sh. 2, 282, dizeli Sh. 2, 127, mafuta ya taa Sh. 2, 077 huku maeneo mengine kama Bukoba bei ikiwa juu zaidi kwa petroli kuuzwa Sh. 2,413, dizeli Sh. 2, 258 na mafuta ya taa Sh. 2, 208.
 
TUCTA: BEI HII INAUMIZA WAFANYAKAZI 
Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana,  Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), Gratian Mukoba, alisema, wafanyakazi wataumia zaidi kutokana na ongezeko hilo la bei ya mafuta kwani wanahitaji kutumia usafiri kwenda kazini huku wakiwa hawana marupurupu ya usafiri.
 
Mukoba aliongeza kuwa, ongezeko hilo pia litamuathiri mkulima kwa bei ya mazao kupanda kutokana na gharama za usafiri.
 
“Maoni yetu ni kwamba ukiongeza bei ya mafuta, unaongeza matumizi kwa mafanyakazi katika usafiri na chakula. Ni mzigo kwa mfanyakazi ukizingatia hawana ‘allowance ya commuter’ bajeti  ya usafiri,” alisema rais huyo. 
Alisema, serikali ilitakiwa kuangalia kitu kingine ambacho wangeongeza bei kisingeweza kuathiri  moja kwa moja.
 
CHAMATA: ONGEZEKO LIMETUATHIRI MNO
Kwa upande wake, Chama cha Madereva Tanzania, kimesema kuwa ongezeko hilo la bei ni kubwa na hivyo litaahiri madereva na kuwaneemesha wamiliki wa magari yao.
 
Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana, Katibu Mkuu wa chama hicho, Rashid Salehe, alisema, bei hiyo ni kubwa kwani inawaumiza Watanzania wote kwani ndiyo wanaotumia usafiri wa pamoja.
 
“Athari ni kubwa… juzi tu ilikuwa Sh. 1, 900, sasa Sh. 2, 200. Tunaoathirika ni sisi tunaotumia usafiri wa pamoja,” alisema Salehe na kuongeza.
 
Hamad Mohamed, dereva wa daladala inayofanya safari zake kati ya Makumbusho na Posta, jijini Dar es Salaam, alisema, kupanda kwa bei ya mafuta ya petroli kumewaathiri katika biashara hiyo ya usafiri kwani mabosi wao hawaguswi na hilo.
 
DARCOBOA: TUPENI MWEZI MMOJA
Umoja wa Wamiliki wa Mabasi ya Daladala Dar es Salaam (Darcoboa), umesema kwa sasa unasubiri hali itakuwaje baada ya mwezi mmoja kabla ya kutoa maoni yao rasmi kuhusiana na  ongezeko hilo la bei ya mafuta.
 
Mwenyekiti wa umoja huo, Sabri Mabrouk, alisema, athari ni kubwa kwani bei imepanda kwa kishindo tofauti na kipindi cha nyuma ambacho ilikuwa ikipanda kati ya Sh. 50 na Sh. 60.
 
“Tumeshauriana na viongozi wenzangu, tuvumilie mwezi mmoja maana Ewura wana utaratibu wa kutangaza bei elekezi kila mwezi ili baada ya hapo tutoe madai yetu,” alisema mwenyekiti huyo.
 
TRAWU: HALI YA MFANYAKAZI KUWA MBAYA ZAIDI
Kaimu  Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Reli (Trawu) Kanda ya Dar es Salaam, Yasin Mleke, alisema kupanda kwa bei ya mafuta nchini kutaendelea kusababisha maisha ya wafanyakazi na wananchi kwa ujumla kuwa magumu kwa kuwa gharama ya usafiri itaongezeka na  bei ya bidhaa kuwa juu.
 
Aliishauri serikali kudhibiti mfumuko wa bei ili kuboresha maisha ya wafanyakazi na wananchi kwa ujumla.

Lowassa: Nimechoka kuitwa fisadi

Wafuasi wa mbunge wa Monduli, Edward Lowassa 
wakimsindikiza nje ya ofisi za CCM Makao Dodoma jana
wakati wa kurejesha  fomu za kugombea urais.


Dodoma. Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa jana aliwataka wanaomhusisha na ufisadi kuacha mara moja kwa sababu hakuna hata chembe ya ukweli katika tuhuma hizo.
Lowassa, aliyeonekana kuzungumza kwa hisia, alisema hayo jana mara baada ya kurejesha fomu ya kuwania kuteuliwa na CCM kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25.
Mbunge huyo wa Monduli alikuwa mmoja kati ya makada tisa waliorudisha fomu jana, ikiwa ni siku moja kabla ya kuisha kwa muda uliowekwa na chama hicho. Wengine waliorejesha fomu jana ni Elidephonce Bilohe, Mwigulu Nchemba, Luhaga Mpina, Dk Hamisi Kigwangalla, Hassy Kitine, Mariki Marupu, Dk Asha Rose Migiro na Lazaro Nyalandu.
Hadi sasa, tayari wanachama 32 kati ya 42 wa CCM walioomba kuteuliwa na chama hicho kugombea urais wamerudisha fomu na kazi hiyo itahitimishwa leo.
Hakuna mtu ambaye amejitokeza hadharani kumtuhumu Lowassa kwa ufisadi, lakini tuhuma hizo zimekuwa zikisambaa kwenye mitandao ya kijamii, hasa kutokana na mbunge huyo wa Monduli kujiuzulu nafasi ya Waziri Mkuu mwaka 2008 baada ya kuibuka sakata la mkataba wa ufuaji umeme wa dharura baina ya Serikali na Kampuni ya Richmond RDC ya Marekani ambayo ilionekana haina uwezo.
Wakati huo, Lowassa alisema kwenye hotuba yake ya kujiuzulu kuwa amefanya uamuzi huo “ili kuonyesha dhana ya uwajibikaji, lakini kutokubaliana na utaratibu uliotumika wa kusema uongo ndani ya Bunge kwa kumsingizia mtu.”
Akizungumza jana kwenye ofisi za makao makuu ya CCM, Lowassa alirudia wito wake wa kutaka wenye ushahidi wa tuhuma hizo wajitokeze hadharani.
“Nataka nitumie fursa hii kuwataka wale wote ambao wamekuwa wakinituhumu kwa miaka kadhaa sasa na kunihusisha na suala zima la rushwa, nawaambia waache mara moja, kwani hakuna chembe hata ya ukweli wa maneno hayo,” alisema.
“Natoa changamoto kwa yeyote mwenye ushahidi wa tuhuma hizo za kipuuzi, autoe na aeleze kwa ushahidi rushwa yoyote inayonihusu, aseme nimechukua lini, kwa nani, kwa lipi na kiasi gani?”
Alisema yeye ni mwadilifu na anaposema atasimamia vita dhidi ya rushwa atafanya hivyo kwa vitendo bila kumuonea mtu na bila kumuonea haya yeyote.
“Ndugu wanachama wenzangu na wananchi kwa jumla, ni lazima sasa tufike mahali tuseme imetosha. Majungu yametosha, upotoshwaji umetosha, rushwa imetosha na kwa pamoja tunaweza kukomesha haya. Tutayakomesha kwa kusimamia ukweli, uadilifu, uaminifu na kutenda kwa haki,” alisema.
Ukumbi wa Whitehouse, jana ulijaa wana-CCM ambao walifika kushuhudia Lowassa akirudisha fomu tofauti na idadi iliyowahi kutokea kwa wagombea wengine kadhaa waliomtangulia. Hali hiyo ilisababisha foleni kwenye Barabara ya Mtaa wa Kuu unaopita mbele ya ofisi za CCM, na kusababisha usumbufu kwa wapita njia.
Lowassa alifika akiwa ameongozana na mwanasiasa mkongwe nchini, Kingunge Ngombale Mwiru na wenyeviti wa chama hicho wa mikoa kadhaa pamoja na wabunge.
Wabunge hao ni Andrew Chenge (Bariadi Magharibi), Peter Serukamba (Kigoma Mjini), Diana Chilolo (Viti Maalumu), Profesa Juma Kapuya (Urambo Magharibi), Mary Chitanda (Viti Maalumu), Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, Dk Makongoro Mahanga na Mary Mwanjelwa (Viti Maalumu).
Baadhi ya wenyeviti wa CCM wa mikoa waliomsindikiza ni Jesca Sambatavangu kutoka Iringa, Ramadhan Madabida (Dar es Salaam), Khamis Mgeja (Shinyanga), Mgana Msindai (Singida) na Joseph Msukuma (Geita).
Wa darasa la saba atia fora
Jana, Bilohe ambaye ni mgombea pekee mwenye elimu ya darasa saba, alitia fora kwa kushangiliwa na kupigiwa vigelegele na wananchi alipofika ofisi za CCM.
Bilohe, ambaye ni mkulima kutoka mkoani Kigoma, alipokewa kwa shangwe alipofika makao makuu ya chama hicho saa nane mchana, lakini hakuwamo kwenye orodha ya makada waliokuwa wanarudisha fomu, hivyo kulazimika kusubiri wanachama wengine wawili waliokuwa kwenye orodha.
Tofauti na makada wengine ambao si maarufu katika chama hicho, Bilohe alikumbatiwa na kupepewa na watu waliokuwa eneo hilo. Akitumia staili ya kupungia mkono watu, Bilohe aliyekuwa pekee yake, alishangiliwa hata baada ya kurejesha fomu yake ya kuomba kuwania kuteuliwa na CCM kuwania urais.
Akizungumzia safari yake ya kusaka wadhamini, alisema alipokewa vizuri na wana-CCM wenzake mikoani na hakuna aliyeonekana kujali kama yeye ni mkulima.
“Hatua hii inaonyesha ukomavu wa demokrasia ndani ya CCM. Watanzania mnapaswa kujivunia kwa kuwa Mungu kawaleta duniani na kuwachagulia Taifa mtakalozaliwa na kuishi,” alisema.
Alipoulizwa changamoto alizokutana nazo wakati wa kazi hiyo ya kusaka wadhamini, Bilohe alisema kuna baadhi ya sehemu alizokwenda ambako watu walitaka wapewe fedha ili wamdhamini.
“Umejiandaaje ilikuwa ni swali gumu sana? Wengine waliomba wapewe chochote na maji ya kunywa. Nikawaambia kwenye mkoba huu sijabeba fedha. Mimi ni mkulima wa kawaida. Nyie mna jukumu la kunidhamini kama chama. Napenda kuwahakikishia kuwa hakuna pesa niliyowazawadia watu na nilipata udhamini kama chama kilivyoniagiza. Sina cha kuwalipa wote ambao waliacha kazi zao na kuja kunidhamini.”
Mwigulu aonya vurugu
Awali, Nchemba ambaye ni Naibu Waziri wa Fedha, aliwataka wanaoipinga Katiba Inayopendekezwa kufuata utaratibu wa kisheria badala ya kufanya fujo kwa sababu hata kile wanachokitaka watashindwa kukitumia.
“Tufuate utaratibu tusije tukagawanyika na kupigana, tusije kudhani kuwa nchi zilizopigana vita hazikuwa na Katiba nzuri, la hasha. Tufuate utaratibu wa kisheria ili kubadilisha kwa sababu hii si Biblia wala Quran Tukufu,” alisema.
Mwigulu alisema, katika safari yake ya kukusanya wadhamini, alikutana na utayari mkubwa na kuungwa mkono na wanachama wenzake, ambao alisema wengine walijitokeza wakati mwingine kuanzia saa mbili usiku hadi hata saa sita usiku ili mradi wamdhamini.
Mpina ataka mdahalo
Mbunge wa Kisesa, Mpina alikiomba chama chake kuandaa mdahalo kwa watu 42 waliomba nafasi hiyo ili waweze kuelewa vizuri watalifanyia nini Taifa.
“Nilikuwa nakiomba chama changu kiruhusu mdahalo kwa wagombea ili kila mmoja aweze kueleza atalifanyia nini Taifa kabla ya vikao vya uamuzi (kuchuja wagombea),” alisema.
Alisema katika safari yake ya kusaka wadhamini alikwenda na watu watatu kwa kutumia gari aina ya Toyota Noah na kuwashangaa wagombea wenzake ambao walitumia mabasi na mafuso kusomba wanachama kutoka maeneo mbalimbali.
“Hakuna mgombea hata mmoja anayenitia presha na  namuomba Mungu nipite na kuingia tatu bora,” alisema Mpina, ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Uchumi, Biashara na Masoko.
Kigwangalla alia na ufisadi
kwa upande wake, Dk Kigwangalla ambaye ni Mbunge wa Nzega alisema Tanzania inahitaji mabadiliko na imechoshwa na ufisadi na kwamba akifanikiwa kuwa rais ataiongezea nguvu Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), ili iweze kufanya kazi.
Alisema yuko tayari kushirikiana na mgombea yeyote atakayepitishwa na chama katika vikao vyote iwapo yeye hatateuliwa.
Kitine akomalia rushwa
Akizungumza jana, Dk Kitine ambaye ni mkurugenzi wa zamani wa Usalama wa Taifa alisema endapo atapitishwa, atakomesha rushwa ndani ya kipindi cha miaka miwili ya uongozi wake.
“Ninajua namna ya kushughulikia rushwa ambayo ni chanzo kikuu cha maovu nchini. Nitatumia miaka miwili kukomesha rushwa nchini,” alisema Kitine na kuongeza kuwa sheria ya kupambana na rushwa haitaacha mwanya kwa hakimu kutoa hukumu anayoiona yeye badala yake sheria itaainisha adhabu anayotakiwa kupata mtu atakayepatikana na hatia ya rushwa.
Marupu aonya wapambe
Baada ya kurejesha fomu, Marupu (34) ambaye ni mwanafunzi huyo wa Chuo Kikuu cha Mzumbe aliwataka wagombea wenzake kuwa makini na wapambe wanaowaunga mkono wasije wakakipasua chama.
“Tunapata shida sisi wagombea, tunashindwa hata kusalimiana tukionana kwa kuogopa kupigwa na wapambe. Wagombea wenyewe hawana shida, shida ipo kwa wapambe. Mtatuua jamani,” alisema.
“Kama kuna mtu anamuabudu mgombea atuachie chama chetu. CCM haitapasuka nyie ndiyo mtapasuka nyote. Kama majina yatapita kama ilivyo nitawachakaza vizuri sana.”
Alisema amechukua wadhamini pia kutoka mkoa maalumu wa vyuo vikuu wa CCM.
Nyalandu ataka umoja
Waziri huyo wa Maliasili na Utalii, aliwataka wafuasi wa CCM kuimarisha kwa vitendo umoja ndani ya chama hicho.
Alisema katika ziara yake ya kutafuta wadhamini, aligundua kuwa vitu vinavyowaunganisha kama Taifa ni vingi kuliko vinavyowatenganisha.
Aliwataka pia wagombea wenzake na Watanzania kushiriki katika kupiga vita ubaguzi wa aina zote.

Chadema yaibwaga CCM mahakamani

Kiteto. Chama cha Mapinduzi (CCM), Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara imezidi kupata pigo baada ya Mahakama kutengua matokeo ya uchaguzi wa wenyeviti wa vitongoji 16 vya mji mdogo wa Mirerani, kwa maelezo kuwa ulikiuka sheria na utaratibu wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
Hii ni mara ya pili katika kipindi cha mwezi mmoja kwa Mahakama kutengua matokeo ya uchaguzi huo ambao uliwaweka madarakani makada wa CCM.
Awali, Mei 30 Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Kiteto ilitengua matokeo ya uchaguzi wa mwenyekiti wa Kijiji cha Lobosireti kwa kukiuka sheria na utaratibu.
Chadema ilifungua kesi kadhaa mahakamani hapo kupinga kitendo cha wagombea wa CCM kupewa ushindi bila kufanya uchaguzi Desemba 14, mwaka jana.
Hukumu hiyo ya jana, inatokana na kesi zilizofunguliwa na Chadema wilayani Simanjiro kwenye kata za Endiamtu na Mirerani, wakipinga wagombea wa CCM kupewa ushindi bila kupigiwa kura kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika Desemba 14 mwaka jana.
Hakimu Mkazi Mfawidhi mahakama hiyo, Elimo Massawe aliagiza kurudiwa kwa uchaguzi wa viongozi wa vitongoji vya Zaire, Kisimani, Tenki la Maji, Endiamtu, Kairo na Kazamoyo vilivyoko Kata ya Ediamtu.
Hakimu Massawe alitaja vitongoji vingine kuwa ni Sekondari, Kilimahewa, Tanesco, Kazamoyo Juu, Mji mpya, Tupendane na vitongoji vya Kata ya Mirerani ambavyo ni Kangaroo, Songambele A, Getini na Songambele B.
Katika kesi hiyo, Chadema iliwakilishwa na mawakili James Millya, Shadrack Kimomogoro na Daudi Haraka na Mahakama iliamuru walipwe Sh160 milioni za gharama za kesi hiyo ambayo ilichukua takribani miezi sita hadi kutolewa hukumu.
Katibu Mwenezi wa Chadema mkoani Manyara, Ambrose Ndege alisema Mahakama imetenda haki kwa kutoa hukumu sahihi na wanajipanga ipasavyo kuhakikisha watashinda vitongoji vyote pindi uchaguzi huo utakaporudiwa.
“Tuliwaeleza tangu awali kuwa uchaguzi ukifanyika tutawashinda saa nne asubuhi hivyo tunawasubiri uwanjani na tutaongoza Mamlaka ya Mji wa Mirerani kwani wananchi wanatukubali,” alisema Ndege.
Hata hivyo, Katibu Mwenezi wa CCM wa Kata ya Endiamtu, Mashaka Jeroro alisema wanatarajia kukata rufaa kupinga hukumu hiyo akisema wagombea wa Chadema walikosea kujaza fomu ndiyo sababu wakawekewa pingamizi.

Maranda apangua kesi ya fedha za Epa

Dar es Salaam. Baada ya kupatikana na hatia katika kesi tatu za wizi wa Fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje (Epa) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na hivyo kutumikia adhabu ya kifungo jela, hatimaye jana Kada wa CCM, Rajabu Maranda alipangua kesi mojawapo iliyokuwa ikimkabili.
Maranda alikuwa anakabiliwa na jumla ya kesi tano za Epa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, pamoja na wenzake akiwamo binamu yake na baadhi ya maofisa wa BoT.
Jana, Mahakama ya Kisutu ilitoa hukumu ya kesi ya nne kati ya tano zinazomuhusisha Maranda na kwa mara ya kwanza alishinda kesi hiyo na hivyo kuachiwa huru.
Maranda, ambaye hata hivyo alikuwa nje baada ya kumaliza vifungo katika kesi tatu alizokuwa ametiwa hatiani, aliachiwa huru jana baada ya Mahakama ya Kisutu kumuona hana hatia katika kesi hiyo.
Hukumu hiyo ilisomwa jana mchana na Hakimu John Utamwa kwa niaba ya jopo la mahakimu waliokuwa wakisikiliza kesi hiyo. Mbali na Utamwa ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama Kuu, mahakimu wengine katika jopo hilo ni Ignas Kitusi (sasa Msajili Mkuu wa Mahakama Kuu) na Eva Nkya.
 Katika kesi iliyotolewa hukumu jana, mbali na  Maranda washtakiwa wengine ambao pia waliachiwa huru ni pamoja na binamu yake Farijala Hussein, mfanyabiashara Ajay Somani na maofisa watatu wa BoT,  Iman Mwakosya, Ester Komu na Bosco Kimela.
Washtakiwa hao walikuwa wakidaiwa kuiba Sh207.3 milioni kutoka katika akaunti hiyo kwa kutumia nyaraka za kughushi, kuonyesha kuwa kampuni yao ya  Rashaz imepewa jukumu la kukusanya madeni kwa niaba ya Kampuni ya General Marketing ya India.
Walikuwa wakidaiwa kutenda makosa hayo kati ya Septemba 8, 2003 na Agosti 18, 2008.
Hata hivyo, katika hukumu yake jana, Mahakama ya Kisutu iliwaachia huru washtakiwa wote baada ya kujiridhisha kuwa hawana hatia kwa mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili.  Akisoma hukumu hiyo, Utamwa alisema, upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili bila kuacha mashaka yoyote.