Friday, April 17

SUMATRA yatangaza nauli mpya za Mabasi Ya Mikoani.......Nauli za Daladala Hazitabadilika



Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi kavu jana imetangaza nauli mpya za usafiri ambapo Mabasi ya abiria ya masafa marefu nauli zake zikipungua huku daladala nauli zikibaki vile vile.

Akitangaza Viwango hivyo vipya vitakavyoanza kutumika tarehe 30 mwezi huu Mkurugenzi Mkuu wa SUMATRA Gilliadi Ngewe alisema baada ya mchakato wa kupanga bei kukamilika, bei za mabasi ya Masafa ya mbali zimeshuka kwa asilimia 5.8 hadi 7.8 kwa kilometa kulingana na daraja la basi.
  
Ngewe amesema kuwa mabasi ya daraja ya chini yamepungua kutoka shilingi 34.8 hadi 34 kwa kilometa, Daraja la kawaida toka shillingi 46.1 hadi 42.5 kwa kilometa na daraja la kati toka shilingi 53.2 hadi 50.1 kwa kilometa huku dalalada zikishuka kwa shillingi 23 lakini kwa usumbufu wa chenji Nauli zitabaki vile vile.
  
Kwa Upande wa wamiliki wa daladala kupitia kwa mwenyekiti wao Sabri Mabrouk wao wanataka nauli iongezeke toka 400 ya sasa mpaka 600.

------

TAARIFA KWA UMMA
NAULI ZA MABASI YA MASAFA MAREFU NA MIJINI

1.0 UTANGULIZI

Kuelekea mwishoni mwa mwaka 2014 bei ya mafuta yatumikayo katika vyombo vya usafiri wa abiria nchini ilianza kushuka. Kufuatia kushuka huko kwa bei, Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) ilikuwa ikipokea wito wa kupitia upya viwango vya juu vya nauli ambavyo viliwekwa na Mamlaka mwezi Aprili, 2013. Hivyo SUMATRA ikaamua kuandaa mikutano ya wadau kwa lengo la kukusanya maoni kuhusu haja ya kurekebisha viwango vya nauli zilizopo.

Aidha, tarehe 09 Machi, 2015, Baraza la Ushauri la Watumiaji wa Huduma Zinazodhibitiwa na SUMATRA (SUMATRA Consumer Consultative Council (SCCC)) liliwasilisha kwa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) maombi ya kushusha nauli za mabasi ya masafa marefu na mijini.Katika maombi hayo Baraza liliainisha sababu za kuomba punguzo hilo kuwa ni kushuka kwa bei za mafuta na kodi ya forodha kwa mabasi mapya kutoka asilimia 25 hadi 10; punguzo hilo lilianza Julai, 2014.

1.1 MAOMBI
  1. Usafiri wa Mijini: Katika usafiri wa mijini, maombi yalikuwa ni kupunguza nauli kwa asilimia 25; hivyo kwa njia yenye umbali wa kilomita 10, nauli iliyopo sasa ya TZS 400 ilipendekezwa kushushwa hadi kufikia TZS 300.
  2. Usafiri wa Masafa Marefu: Maombi yalikuwa ni kushusha nauli iliyopo kwa kilometa moja anayosafiri abiria katika basi la kawaida kutoka TZS 36.89 hadi TZS 28.05; punguzo la asilimia 23.96. Aidha, kwa basi la hadhi ya juu (luxury bus) kushusha kutoka TZS 58.47 hadi TZS 47.19; punguzo la asilimia 19.29.

    2.0 UTARATIBU WA KUFANYA MAPITIO YA NAULI
    SUMATRA iliyafanyia kazi maombi hayo kwa mujibu wa Sheria yaUdhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), Sheria ya Bunge Na.9 ya Mwaka 2001, na Kanuni za Tozo za Mwaka 2009 ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha wadau mbalimbali wakiwemo watoa huduma, watumiaji wa huduma pamoja na wananchi kwa ujumla ili kupata maoni yao. Ushirikishwaji huo ulifanywa kupitia mikutano iliyofanyika tarehe 9 Machi, 2015 Mkoani Mwanza; tarehe 12 Machi, 2015 Mkoani Kigoma; na tarehe 18 Machi, 2015 Jijini Dar es Salaam. Maoni yaliyotolewa katika mikutano hiyo yalizingatiwa katika tathmini na Mamlaka. 

    Taarifa ya tathmini na mapendekezo ya viwango vipya vya nauli iliwasilishwa kwa Bodi ya Wakurugenzi ya SUMATRA kwa ajili ya maamuzi.

    3.0 NAULI ZA MIJINI
    Bodi ya Wakurugenzi ya SUMATRA ilikutana Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Aprili, 2015 ili kupitia taarifa ya tathmini na mapendekezo ya viwango vya nauli kwa ajili ya maamuzi.

    3.1 Masuala Yaliyobainika
    Kufuatia tathmini iliyofanywa ya usafiri wa mijini, BODI ilibaini kwamba:
  1. Bei ya mafuta ilikuwa imeshuka ikilinganishwa na bei iliyokuwepo wakati viwango vilivyopo sasa vilipoanza kutumika Mwezi Aprili, 2013; ambapo kwa wastani bei ya lita ya dizeli iliuzwa TZS 2,071.67 kufikia Machi, 2015 wastani wa bei ya Dizeli kwa lita katika vituo ulishuka mpaka TZS 1,665.38; mwezi Aprili, 2015 bei ya wastani ilipanda kufikia TZS 1,779.57.
  2. Mwenendo wa bei za mafuta kufikia Aprili, 2015 unaonyesha kuwa bei ya mafuta imekuwa ikibadilikabadilika na kwamba kulikuwa na uwezekano wa bei kupanda.
  3. Gharama za mafuta zilikuwa muhimu kuzingatiwa pamoja na gharama nyinginezo, ambazo zilifikia asilimia 70 ya gharama za uendeshaji.
  4. Kulikuwa na mabadiliko katika viashiria vya kiuchumi kama vile mfumuko wa bei na thamani ya shilingi na mabadiliko hayo yalipaswa kuzingatiwa katika kukokotoa viwango vya nauli.
  5. Punguzo la ushuru wa forodha kwa uagizaji wa mabasi mapya ulikuwa na faida katika kuchochea uingizaji wa mabasi mapya nchini ili kuboresha hali ya usafiri nchini. Hata hivyo sehemu kubwa ya mabasi yaliyopo nchini kwa sasa hayakupata punguzo hilo kwa kuwa yaliingizwa kabla ya Julai, 2014 punguzo hilo lilipoanza kutumika.
  6. Mazingira ya uendeshaji na utoaji huduma za usafiri mijini yanapaswa kuzingatiwa ili kufikia viwango vya nauli ili kuifanya huduma ya usafiri kuwa endelevu. Kwa upekee, ongezeko la msongamano wa magari mijini na athari zake katika utoaji wa huduma za usafiri mijini zinapaswa kuzingatiwa.
  7. Gharama za utoaji huduma za usafiri mijini zinapaswa kutazamwa kwa ujumla wake, ikiwa ni pamoja na punguzo la bei ya mafuta, ili kufikia viwango vya nauli vinavyostahili.
  8. Baada ya kuzingatia vigezo muhimu katika ukokotoaji wa nauli, punguzo lililojitokeza katika viwango vya nauli kikomo ni kama inavyobainishwa hapa chini: 

    Viwango Vya Nauli Kutokana na Ukokotoaji

Njia
Nauli ya Sasa
Nauli iliyokokotolewa
%
0 - 10 km (+CBD)
400
376.77
5.8
11 - 15 km
450
448.62
0.3
16 - 20 km
500
485.34
2.9
21 - 25 km
600
583.34
2.8
26 - 30 km
750
742.74
1

3.2 Maamuzi ya BODI
Baada ya kutafakari viwango vilivyotokana na ukokotoaji uliozingatia masuala muhimu yaliyoainishwa, BODI imeridhia viwango vya nauli vilivyopo sasa kuendelea kutumika.

Uamuzi huu unatokana na punguzo lililokokotolewa Kuwa dogo ikilinganishwa na viwango vilivyopo sasa. Aidha, viwango vilivyokokotolewa iwapo vitapitishwa vitasababisha usumbufu katika malipo.
  1. Viwango vya Nauli Mpya kwa Watu Wazima
    Viwango vipya vya nauli kikomo vya mabasi ya mjini vilivyoridhiwa kwa watu wazima ni kama ifuatavyo: 
    Viwango Vya Nauli Mjini Vilivyoridhiwa
Njia
Nauli ya Sasa


(TZS)
Viwango Vilivyoridhiwa


(TZS)
0 - 10 km (+CBD)
400
400
11 - 15 km
450
450
16 - 20 km
500
500
21 - 25 km
600
600
26 - 30 km
750
750

  1. Viwango vya Nauli Mpya kwa Wanafunzi 
    BODI imeamua kuwa nauli ya mwanafunzi nayo ibaki kama ilivyo nauli ya sasa ambapo mwanafunzi analipa TZS 200.
     
  1. VIWANGO VYA NAULI ZA MABASI YA MASAFA MAREFU
    BODI ilipokea tathmini kuhusu nauli za usafiri wa masafa marefu.

    4.1 Masuala Yaliyobainika
    Kufuatia tathmini iliyofanywa ya nauli kikomo za usafiri wa masafa marefu, BODI ilibaini kwamba:
  1. Bei ya mafuta ilikuwa imeshuka ikilinganishwa na bei iliyokuwepo wakati viwango vya sasa vilipoanza kutumika Mwezi Aprili, 2013; ambapo kwa wastani bei ya lita ya dizeli iliuzwa TZS 2,071.67 kufikia Machi, 2015 wastani wa bei ya Dizeli kwa lita katika vituo ulishuka mpaka TZS 1,665.38; mwezi Aprili, 2015 bei ya wastani ilipanda kufikia TZS 1,779.57.
  2. Mwenendo wa bei za mafuta kufikia Aprili, 2015 unaonyesha kuwa bei ya mafuta imekuwa ikibadilikabadilika na kwamba kulikuwa na uwezekano wa bei kupanda.
  3. Gharama za ununuzi wa mafuta zilikuwa muhimu kuzingatiwa pamoja na gharama nyinginezo, ambazo zilifikia asilimia 70 ya gharama za uendeshaji.
  4. Kulikuwa na mabadiliko katika viashiria vya kiuchumi kama vile mfumuko wa bei na thamani ya shilingi na kwamba mabadiliko hayo yalipaswa kuzingatiwa katika kufikia viwango vya nauli.
  5. Punguzo la ushuru wa forodha kwa uingizaji wa mabasi mapya lilikuwa na athari chanya katika kuchochea uingizaji wa mabasi nchini. Hata hivyo sehemu kubwa ya mabasi yaliyopo nchini kwa sasa hayakupata punguzo hilo kwa kuwa yaliingizwa kabla ya punguzo hilo kuanza kutumika.
  6. Katika ukokotoaji wa nauli ni muhimu kuzingatia madaraja ya mabasi kama yalivyoelekezwa katika Kanuni za Huduma za Abiria, 2014 (The Road Transport (Passenger Service) Regulations, 2014 zinazoainisha madaraja manne ya mabasi;daraja la kawaida la chini, daraja la kawaida la juu, daraja la hadhi ya kati na daraja la Juu.
  7. Gharama za utoaji huduma za usafiri kwa ujumla wake zinapaswa kuzingatiwa kwa madaraja mbalimbali ili kufikia viwango vya nauli vinavyostahili.
  8. Udhibiti wa nauli unapaswa kujielekeza katika madaraja matatu yafuatayo: (1) daraja la kawaida la chini, (2) daraja la kawaida la juu na (3)daraja la hadhi ya Kati ili kutimiza wajibu wa kuwalinda watumiaji wenye kipato cha chini.

    4.2 Maamuzi ya BODI
    Baada ya kutafakari tarifa iliyowasilishwa BODI iliridhia viwango vipya vya juu vya nauli kwa mabasi ya masafa marefu kuwa kama vinavyoonyeshwa hapo chini: 
    Viwango Vipya vya Nauli za Mabasi ya Masafa Marefu

Daraja la Basi
Nauli ya Sasa


(TZS/Abiria/Km)
Viwango Vipya vya Nauli Vilivyoridhiwa


(TZS/Abiria/Km)

Daraja la Kawaida la Chini

(Lower Ordinary bus -Lami
36.89
34.00

Daraja la Kawaida la Chini

Lower Ordinary Bus) - Vumbi
46.11
42.50

Daraja la Kawaida la Juu

(Upper Ordinary Bus)
-
44.96

Daraja la Kati

(Semi-Luxury Bus)
53.22
50.13


BODI pia imeamua kwamba nauli za mabasi ya hadhi ya juu ( luxury bus) hazitadhibitiwa ili kuchochea ubunifu katika utoaji huduma na ushindani kati ya huduma za barabara na njia nyinginezo za usafiri.

Mamlaka imeandaa majedwali ya nauli kwa kuzingatia viwango vipya. Majedwali hayo yanaweza kupatikana katika tovuti ya Mamlaka www.sumatra.go.tz.

HITIMISHO

Viwango hivi vipya vinapaswa kuanza kutumika siku 14 baada ya taarifa kutolewa kwa umma. Hivyo basi viwango hivi vitaanza rasmi tarehe 30 Aprili, 2015.

Wamiliki wa mabasi pamoja wafanyakazi wao wanaagizwa kutoza viwango vya nauli vilivyoridhiwa na Mamlaka.

Aidha, abiria na wananchi kwa ujumla wanahamasishwa kutoa taarifa SUMATRA kupitia namba za simu za bure ambazo ni 0800110019 na 0800110020 pale wanapotozwa nauli ya juu zaidi ya nauli kikomo iliyoridhiwa.

Imetolewa na:
Mkurugenzi Mkuu
SUMATRA
15 Aprili, 2015 

Zitto Kabwe: Sitaki kulumbana na CHADEMA

Kiongozi wa chama cha ACT- Wazalendo, Zitto Kabwe amesema hawezi kulumbana na viongozi wa chama chake cha zamani cha Chadema kwa kuwa anachofanya sasa ni kutafuta wanachama wa chama chake kipya. 
 
Zitto alisema hayo juzi mjini Morogoro wakati wa mkutano wa ziara ya uzinduzi wa chama hicho uliofanyika katika kiwanja cha ndege mjini hapa.
 
Akihutubia huku akishangiliwa na wananchi, Zitto aliwataka kumpima na kumchuja yeye kwa matendo yake na kwamba kwa sasa jitihada zake amezielekeza mikoani kupata wanachama.
 
“Nimekuwa nikisikia maneno maneno mengi kutoka kwa viongozi wangu wa zamani lakini nawaheshimu na sitoweza kuwajibu kwani siasa za chuki kwa sasa zimepitwa na wakati, ninachofanya ni kukijenga chama,”alisema Zitto.
 
Kiongozi huyo alisema Morogoro ni moja ya mkoa unayoifanya nchi kukosa maendeleo kutokana na viwanda vingi kubinafsishwa na hivyo kutokuwa na faida kwa wananchi.
 
“Morogoro ni mkoa wa sita katika kuchangia pato la Taifa na takribani Sh2.2 trilioni zimekuwa zikipatikana kwa ajili ya maendeleo ya watu wa mkoa huo,” alisema Zitto.
 
Mwenyekiti wa chama hicho, Anna Mghwira aliwataka wanawake nchini kuacha kushiriki siasa za vurugu na malumbano hasa katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu.
 
Mghwira alisema ni vyema wakaangalia namna gani nchi inakua kiuchumi na watoto na vijana wanapata elimu iliyo bora ambayo itawafanya kufanya kazi kwa uzalendo.
 
Aliwataka wananchi kuwa na taratibu za kuwakumbuka mashujaa wa Taifa hasa kwa mambo mema na mzuri waliyoyafanya wakati wa uhai wao.
 
Mpaka sasa chama hicho cha ACT kimefanya mikutano yake ya uzinduzi katika mikoa ya Ruvuma, Njombe, Iringa na Morogoro 

Mkwara wa Gwajima kwa Polisi wazaa matunda.....Mahojiano Yasitishwa Kusubiri Uamuzi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali



Hoja za kisheria alizowasilisha Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima kuhusu kutakiwa kuwasilisha nyaraka 10 za utajiri na usajili wa kanisa lake polisi zimezaa matunda. 
 
Sasa, agizo la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam la kumtaka Askofu Gwajima kuwasilisha nyaraka hizo leo limesitishwa kusubiri utatuzi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali au Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka.
 
Wakili John Mallya anayemtetea Askofu Gwajima alimweleza mwandishi jana usiku kuwa baada ya makubaliano na polisi mteja wake leo hatafika Kituo Kikuu cha Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kama ilivyokuwa imepangwa mpaka hoja hizo za kisheria zitakapotolewa uamuzi.
 
Alhamisi iliyopita, polisi ilimtaka Gwajima kuwasilisha vielelezo hivyo, lakini hatua hiyo ilipingwa na kiongozi huyo akieleza kuwa hatapeleka nyaraka yoyote iwapo jeshi hilo halitajibu barua aliyoliandikia kutaka liombe vitu hivyo kwa maandishi.
 
Nyaraka zilizotakiwa kuwasilishwa polisi ni hati ya usajili wa kanisa, namba ya usajili, majina ya Baraza la Wadhamini (Baraza la Kiroho), idadi ya makanisa (matawi) anayohudumia na nyaraka za helikopta ya kanisa.
 
Nyaraka nyingine ni; muundo wa uongozi wa kanisa, waraka wa maaskofu uliosomwa makanisa yote, nyaraka za nyumba na mali za kanisa, nyaraka kuonyesha taarifa za hesabu kutoka kwa Msajili wa Vyama vya Hiari na kuambatana na mtu anayepiga picha za video kanisani hapo.
 
“Siwezi kuwasilisha kwa mdomo kwa kuwa hizi si mali za Gwajima… ni mali ya taasisi na si vitu vyake binafsi,” alisema wakili huyo.
 
Katika barua yake kwa polisi, Wakili Mallya alisema: “Tunaiomba Polisi kumwandikia rasmi mteja wetu kimaandishi nyaraka mnazozihitaji na vifungu vya sheria vinavyotumika na polisi kutaka nyaraka hizo… tutashukuru kupata hati hiyo.”
 
Kauli ya Kova
Mapema alipoulizwa kuhusu kitakachotokea leo, Kamanda Kova alisema: “Suala la Mchungaji Gwajima kwenda na vielelezo alivyoagizwa na Polisi siwezi kulizungumzia hadi hapo itakapotokea hakuja navyo ndipo nitakapotoa tamko langu la mwisho.
 
“Nitazungumziaje hili? Si hadi itokee hakuja na vielelezo na kama akija navyo halafu mimi nimeongea tofauti, nimeona italeta malumbano kati yangu na yeye na mimi sitaki ifikie huko.
 
“Kuna mambo mengi ya kufanya hivyo nitalitolea tamko la mwisho kwa waandishi wa habari kuhusu mchungaji Gwajima kama itatokea hivyo ili tuendelee na mambo mengine.”
  
Kwa msisitizo zaidi
Mallya alisema nchi inaongozwa kwa sheria, hivyo kila kitu kinatakiwa kiwe cha kisheria na kwamba wameiandikia polisi kuitaka waombe nyaraka hizo kimaandishi na kuonyesha vifungu vya sheria vinavyowaongoza kuziomba badala ya kusema kwa mdomo kwa sababu vitu hivyo ni vya kanisa na siyo vya Gwajima peke yake.
 
Askofu Gwajima alihojiwa na Polisi, Kanda ya Dar es Salaam kwa tuhuma za kumtolea maneno makali Polycarp Kardinali Pengo baada ya kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki kutoa tamko lililotofautiana na la viongozi wa Jukwaa la Wakristo Tanzania kuhusu suala la Katiba

Monday, April 13

HABARI KUBWA-ZITTO KABWE AENEZA UWONGO WAKE TENA,ATUMIA ZIARA YAKE KUUCHAFUA UKAWA MIKOANI,SOMA HAPA KUJUA



KIONGOZI Mkuu wa chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ameendelea kuwadanganya wananchi kuwa kufukuzwa kwake katika Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kumetokana na umakini wake wa kufuatilia “mambo yanayowakandamiza wanyonge.” Anaandika Ditha Nyoni, Songea … (endelea).

Akihutubia mkutano wa hadhara mkoani Ruvuma, Zitto amewadanganya wananchi kuwa kufukuzwa kwake Chadema, kumetokana na msimamo wake wa kutetea maslahi ya wananchi. Amesema baada ya kutambua baadhi ya viongozi wa Chadema hawataki kuwatumia wanyonge kwa kuwapigia kura na kujipatia ruzuku, yeye wenzake wengine wameamua kuanzisha chama kitakacho watetea wanyonge wakiwemo wakulima ambao nguvu zao zikiisha wanakufa maskini.

Amedai kuwa yeye ndiye aliyeibua hoja ya mkataba wa madini wa Buzwagi ambako waziri wa nishati na madini, alifutwa kazi; hoja ya kumng’oa aliyekuwa waziri mkuu Edward Lowassa, Operesheni Tokomeza, wanaoficha fedha nje ya nchi na sakata la Escrow.
Amewataka wananchi madai kuwa yeye ni msaliti na kwamba wawapime wabunge wao kwa kazi walizozifanya. Hata hivyo, katika yote aliyoeleza Zitto hakuna hata moja ambalo ni kweli.

Mathalani, hoja ya mkataba wa Buzwagwi, iliibuliwa na gazeti la kila wiki la MwanaHALISI; katkka sakata la Buzwagwi, kinyume na madai yake, hakuna waziri hata mmoja aliyefutwa kazi. Aliyekuwa waziri wa nishati na madini, Nazir Karamagi ambaye alisaini mkataba huo nchini Uingereza, alifutwa kazi 18 Februari 2008, kutokana na kashifa ya maarufu ya Richmond. Sakata la Richmond liliibuliwa bungeni na Kamati ya Nishati na Madini iliyokuwa chini ya aliyekuwa mbunge wa Bumbului (CCM), William Shelukindo. Vilevile, kinachoitwa “Operesheni Tokomeza,” kiliibuliwa bungeni na Christopher ole Sendeka, mbunge wa Simanjiro (CCM).

Kamati Kuu (CC) ya Chadema, ilimfukuza uanachama Zitto na wenzake watatu – Prof. Kitila Mkumbo aliyekuwa mjumbe wa CC na Samson Mwigamba aliyekuwa mwenyekiti wa chama hicho mkoani Arusha – kwa madai ya usaliti, kusingizia viongozi wakuu wa chama na kushirikiana na maadui wa chama.

Akisoma maamuzi ya CC, tarehe 22 Novemba 2013, mwanasheria mkuu wa Chadema, Tundu Lissu alisema, Zitto na genge lake wametuhumiwa kwa makosa 11 ya usaliti, yaliyotokana na “Waraka wa Mabadiliko.” Waraka huo ulioandaliwa na Mwigamba na Kitila, ulilenga kuteka chama na kukikabidhi kwa maadui wa chama wakiwamo watu kutoka Idara ya Usalama wa Taifa (TISS).




Zitto ndiye aliandaliwa kuwa mwenyekiti wa chama hicho; naye akakiri kutaka kufanya mapinduzi ya uongozi kinyume na katiba. “…baada ya kumsikiliza Dk. Kitila, Kamati Kuu imebaini kuwa mkakati huo haukulenga kumfanya Zitto kuwa mwenyekiti pekee, bali ulikuwa na malengo makubwa ya kukibomoa chama hicho,” ameeleza Lissu.

Amesema, Zitto alikihujumu chama hicho na kushiriki kujitoa kwa wagombea wake wa ubunge katika majimbo ya Mpanda Mashariki, Musoma Vijijini, Singida Mjini na kuwa mwaka 2006, alipewa magari mawili na Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM).

Saturday, April 11

Polisi wamshika pabaya Gwajima

Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima (kushoto) na Mchungaji Ngwandu Mwangasa wakitoka
katika Kituo Kikuu cha Polisi, jijini Dar es Salaam jana. Kulia ni Wakili wa Askofu Gwajima, John Mallya.  

Dar es Salaam. Sasa ni dhahiri kwamba polisi wamemshika pabaya Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima baada ya kumhoji na kisha kumtaka arejee katika Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam Aprili 16, mwaka huu akiwa na vitu 10 vinavyohusu usajili, umiliki, uongozi na mali za kanisa analoliongoza.
Hatua hiyo imekuja kinyume na matarajio yake na ya wengi kuwa kiongozi huyo angekuwa anahojiwa tu kuhusu matamshi yake ya kashfa dhidi ya Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo.
Kutokana na matamshi hayo yaliyosambaa kwa kasi kwenye mitandao ya kijamii kwa njia ya video na sauti, Gwajima alitakiwa kuripoti polisi kuhojiwa Machi 27, mwaka huu lakini kabla ya mahojiano yao kukamilika aliishiwa nguvu na kupelekwa hospitalini alikolazwa kwa siku nne, huku taarifa zikieleza kuwa alishtushwa na kuhojiwa taarifa binafsi badala ya tuhuma alizoitiwa polisi.
Hata baada ya kutoka hospitalini, Gwajima aliendelea kutembea akiwa kwenye kiti chenye magurudumu, alichotumia hadi Aprili 6 alipohubiri katika Ibada ya Pasaka.
Siku iliyofuata askofu huyo alitupa kiti hicho akidai kuwa amepona baada ya maombi ya wachungaji wageni waliofika kanisani hapo kutoka Japan.
Baada ya mahojiano ya jana, wakili wake, John Mallya alilalamikia hatua ya polisi akisema mahojiano kuchukua mkondo wa mambo binafsi badala ya kile alichoitiwa na kusema watakwenda kulalamikia hatua hiyo mahakamani.
Mambo 10
Wakili huyo alitaja mambo yanayotakiwa kuwasilishwa polisi kuwa ni hati ya usajili wa kanisa, namba ya usajili, majina ya Baraza la Wadhamini (Baraza la Kiroho), idadi ya makanisa (matawi) anayohudumia, nyaraka za helikopta ya kanisa, muundo wa uongozi wa kanisa, waraka wa maaskofu uliosomwa makanisa yote, nyaraka za nyumba na mali za kanisa, nyaraka kuonyesha taarifa za hesabu kutoka kwa Msajili wa Vyama vya Hiari na kuambatana na mtu anayepiga picha za video kanisani hapo.
Mallya alisema watalalamika suala hilo litakapofika mahakamani kutokana na mteja wake kuhojiwa masuala tofauti na kile kinachodaiwa kutoa lugha ya matusi.
Alisema mteja wake amehojiwa muda mrefu kwa sababu alikuwa akihojiwa masuala binafsi yakiwamo ya familia yake, watoto wake, ndugu zake hadi waliokufa.
“Mahojiano yamekuwa ya muda mrefu, cha kushangaza kaulizwa maswali binafsi badala ya kile anachodaiwa kukifanya, mahakamani tutahoji hilo,” alisema Mallya.
Alisema licha ya kuambiwa walete vitu hivyo ambavyo kimsingi vipo, hawajaambiwa watafanywa nini kama wasipoviwasilisha.
Ilivyokuwa
Saa 1.15 asubuhi akiwa ameongozana na watu wawili akiwamo msaidizi wake ambaye alikuwa amemshikilia kutokana na kutembea kwa kupepesuka na wakili wake Malya, Gwajima alionekana akikunja uso kila alipopandisha ngazi moja kwenda nyingine kuelekea ndani ya Kituo Kikuu cha Polisi.
Baada ya kukaa ndani hadi saa 6.45 mchana, Gwajima alitoka akiwa ameshikiliwa kama alivyoingia na kuzungumza na waandishi wa habari na kusema mahojiano yalikwenda vizuri kuliko walivyotarajia, huku akimtaka wakili wake kufafanua zaidi, ndipo wakili huyo alipotaja mambo hayo.
Katika eneo la polisi, wafuasi wa Gwajima walikuwa katika makundi na ilipofika saa 1.40 asubuhi, Kamishna Msaidizi wa Polisi, Simon Sirro aliwaita wapatao 20 miongoni mwao na kuwaliza wanachotaka, nao wakamjibu bila hofu kuwa wamemfuata baba yao.
Sirro aliwataka waumini hao waondoke akiwaeleza kuwa baba yao yupo katika mikono salama na wao waende wakafanye kazi za kutafuta mkate wa siku.
Hata hivyo, waumini hao walimjibu kuwa hawaondoki hadi baba yao atakapotoka na wao ndipo watakapoondoka.” Majibu yaliyomuacha hoi na kumfanya kucheza na kisha kuondoka kurejea ofisini kwake huku akisema... “Makubwa.”
Waumini hao walikuwa wakiongezeka kadri muda ulivyokwenda na hadi saa tano walikuwa wengi katika makundi wakiwamo walinzi shirikishi ambao walipata mafunzo kwa ufadhili wa Gwajima, ambao walikuwa wamejipanga langoni mwa kituo hicho wakiwa watulivu.
Waumini wazungumza
Wakizungumza kituoni hapo, waumini hao walisema wamepita mapito mengi na kiongozi huyo hivyo ni vigumu kumuacha peke yake katika eneo ambalo alipata matatizo mara ya kwanza.
Mmoja wao, Eugen Mkwasa alisema hajakwenda katika biashara zake kwa sababu ya kulinda usalama wa baba yao, kwa kuwa hana imani na eneo alilokuwapo kwani ndilo lililokuwa chanzo cha mateso yake ya sasa.
“Askofu wetu mpendwa anaumwa, hali hiyo ilimuanza akiwa hapa kituoni, nitakuwa na raha gani kubaki nyumbani au kwenda kibaruani bila kufahamu kama baba ametoka salama?” alisema Mkwasa.
Muumini mwingine, Elizabeth Peter alisema hajali jua na hata ikinyesha mvua kwa sababu analipa kile anachotendewa na Askofu Gwajima... “Askofu tumepita naye katika mapito mengi, siwezi kukaa mbali na suala lake kwa sababu ana mchango mkubwa maishani mwangu, siwezi kumtupa wakati huu mgumu wa kusumbuliwa na Jeshi la Polisi.”

Taarifa ya Jeshi la Polisi Nchini Kufuatia Upotoshwaji Unaoenezwa Kwa Njia ya Mtandao ili Kuwatia Watu Hofu

Katika siku za hivi karibuni kumeibuka tabia ya baadhi ya watu wachache wasiofahamika kutunga na kusambaza ujumbe kupitia simu za mikononi na mitandao mbalimbali ya kijamii wenye lengo la kuwatia hofu wananchi, jambo ambalo ni kinyume cha sheria. 
  
Aidha, watu hao wanaosambaza taarifa hizo wanajifanya kwamba taarifa hizo zimetoka kwenye taasisi za kimataifa na taasisi zingine zinazoaminika jambo ambalo siyo kweli.

Jeshi la Polisi nchini linawataka wote wenye tabia hiyo kuacha mara moja na badala yake, endapo mtu yeyote anayo taarifa ya uhalifu wa aina yoyote ama kikundi chochote cha uhalifu atoe taarifa hiyo katika kituo chochote cha Polisi au kupitia simu za makamanda wa polisi wa mikoa ama vyombo vingine vya ulinzi na usalama ili taarifa hizo ziweze kufanyiwa kazi haraka.

Aidha, Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa taarifa zote zinazopokelewa ili kuhakikisha kwamba usalama wa raia na mali zao unaendelea kuimarika.
  
 Hata hivyo, Jeshi la Polisi halitasita kumchukulia hatua mtu yeyote atakayebainika kusambaza ujumbe wenye mlengo wa upotoshaji, uchochezi ama kuwatia hofu wananchi.

Imetolewa na:-
Advera Bulimba -SSP
Msemaji wa Jeshi la Polisi.

Polisi Ajiua Kwa Kujipiga Risasi.


Askari wa Kituo cha Polisi Wilaya ya Sikonge mkoani Tabora, H 3416 PC Charles, amejiua kwa kujipiga risasi.

Baadhi ya wananchi wanaoishi jirani na kituo hicho cha polisi, Paulo Lazaro na Furahisha Felix, walisema tukio hilo lilitokea Aprili 4, mwaka huu, saa 1:00 usiku kituoni hapo.

“Suala hili limetushangaza, kwani sisi tulikuwa nyumbani. Ghafla tulisikia mlio wa bunduki katika kituo cha polisi. Tulipofika, tulimkuta askari huyo akiwa amekufa kwa kujipiga risasi,” alisema Lazaro.

Wananchi hao walisema kutokana na hali hiyo, walilazimika kuwauliza baadhi ya askari waliokuwa zamu, ambao walidai hata wao hawajui ni kwanini mwenzao amechukua uamuzi wa kujiua.

Waliomba ufanyike uchunguzi wa kina ili kubaini chanzo cha kujiua kwa askari huyo kwani inawezekana kuna kitu ambacho alikuwa amechukizwa nacho.
  
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Suzana Kaganda, alithibitisha kujiua kwa askari huyo. “Ni kweli askari huyo amejiua kwa kujipiga risasi wakati akiwa kituoni majira ya saa 1:00 usiku,” alisema Kamanda Kaganda.

Hata hivyo, Kamanda Kaganda alisema hakuna ujumbe wowote ulioachwa na askari huyo kuelezea sababu za kujiua. Kutokana na hali hiyo, Kamanda Kaganda aliwataka askari wote kutatua matatizo yao kupitia kwa viongozi wao badala ya kujichukulia sheria mkononi.

Alisema uchunguzi unaendelea ili kubaini chanzo cha askari huyo kujiua.

Monday, April 6

ACT: Tunajipanga kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Agosti


Dar es Salaam. Chama cha ACT- Tanzania, kimesema hakina muda wa kufanya siasa za chuki na malumbamo dhidi ya vyama vingine vya siasa, badala yake kinajipanga vizuri na kuandaa mazingira ya kushiriki katika uchaguzi mkuu ujao.
Mwenyekiti wa chama hicho Anna Mghwira, aliliambia gazeti hili mwishoni mwa juma kuwa, baada ya chama hicho kuzinduliwa rasmi Machi 29 mwaka huu,  nguvu yake sasa imeelekezwa katika kujijenga na kujiimarisha.
Alisema katika kujiimarisha, chama hicho kinatafuta wanachama, kwa kuwa kinatambua kuwa ni mtaji wa kujihakikishia ushindi katika uchaguzi mkuu, pamoja na kuandaa wagombea  kwa kuangalia uwezo wao kadri watakavyojitokeza.
“Mimi mwenyewe ni miongoni mwa wagombea ubunge, nitagombea Jimbo la Singida mjini na naamini kwamba nitaweza kupata nafasi hiyo kwa sababu ninafahamika kule ni nyumbani nilikozaliwa . Nimesoma huko, nimekulia huko na najua changamoto zinazotukabili wakazi wa kwetu na jinsi nitakavyoshiriki kukabiliana nazo nikiwa mbunge,”
Mghwira alieleza kuwa chama hicho kinajiimarisha, huku kikitambua kuwa kina wajibu wa kuendeleza ushirikiano na vyama vingine vya siasa, badala ya kujitenga na kuendesha shughuli zake kama kisiwa.
Mwenyekiti huyo, alitolea mfano siku ya uzunduzi wa chama hicho akisema kuwa kulikuwa na watu wengi kutoka vyama mbalimbali ambao walitaka kurudisha kadi za vyama hivyo hadharani na kuchukua kadi za ACT, lakini walisitisha shughuli hiyo kuepuka uhasama.
“Kuwa vyama tofauti haina maana kwamba tuwe maadui, kulikuwa na wanachama wapya siku ya uzinduzi (wa ACT) walitaka kuonyesha hadharani wanavyorudisha kadi za vyama vyao vya awali hatukuwapa nafasi hiyo, kwa sababu hatuoni kuwa hilo ni jambo la kuvutia kwetu,” alisema.
Kwa mujibu wa Mghwira siku hiyo walipokea wanachma wapya 2,000 na bado wanaendelea kupokea wanachama wengine kutoka vyama mbalimbali vya siasa lakini kwa siri.
Ingawa  Mghwira hakutaja watu, asilimia kubwa ya viongozi wa kitaifa wa chama hicho, akiwamo Zitto Kabwe ambaye sasa ni Kiongozi Mkuu wa chama hicho na Katibu Mkuu  Samson Mwigamba  na Profesa Kitila Mkumbo, wamejiunga na chama hicho baada ya kufukuzwa na vyama vyao.
“Pia katika kuonyesha nia yetu ya kuhitaji ushirikiano mwema wa kisiasa tuliwaalika viongozi mbalimbali wa vyama vya upinzani, ikiwemo Chadema na CUF,” alisema.  Alisisitiza kuwa Profesa Ibrahimu Lipumba ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) ni miongoni mwa wasomi  na viongozi wa vyama vingine vya siasa walioalikwa kutoa mada katika uzinduzi wa chama hicho, lakini alipata udhuru hivyo hakufika.
“Hata hivyo tulifarijika kuona shughuli yetu ya uzinduzi wa chama ikifanyika vizuri na kwa amani,” alisema.

Ukawa yadai mambo manne kabla ya Uchaguzi


Dar es Salaam. Uamuzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuahirisha Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa umewafungulia viongozi wa Ukawa kuishinikiza Serikali kuiboresha Katiba ya sasa katika maeneo manne ili kuondoa mvutano katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba.
Mambo manne yanayodaiwa na Ukawa ambayo ni ushindi wa urais kuamuliwa kwa asilimia zaidi ya 50, mgombea binafsi katika nafasi za udiwani, ubunge na urais, tume huru ya uchaguzi na urais kupingwa mahakamani ni yale yaliyoafikiwa baina ya Rais Jakaya Kikwete na vyama vya siasa Septemba 8, mwaka jana.
Mwenyekiti mwenza wa umoja huo, James Mbatia amesema maboresho yaliyofanyika chini ya Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) ni ya lazima ili kufanikisha uchaguzi huo kabla ya kupitishwa kwa Katiba Mpya na kuondoa uwezekano wa vurugu.
Katika kikao hicho, Mbatia alisema walitiliana saini kuwa iwapo uchaguzi wa mwaka huu utafanyika kwa kutumia Katiba ya 1977, Bunge lingekutana Novemba mwaka jana kufanya marekebisho hayo ya 15 ya Katiba na endapo hilo lingeshindikana, basi lingekutana Februari, jambo ambalo pia halikufanyika.
Utekelezaji wa masuala hayo utawezekana iwapo Serikali itawasilisha marekebisho hayo bungeni ili yajadiliwe kwa dharura katika mkutano ujao wa Bajeti wa mwisho wa Bunge la Kumi, kwa kuwa uwezekano wa kupata Katiba Mpya kabla ya uchaguzi ni kama haupo.
Alipoulizwa iwapo jambo hilo linawezekana katika Mkutano wa Bajeti, Mkurugenzi wa Shughuli za Bunge, John Joel alisema: “Ndiyo inawezekana. Serikali inaweza kuwasilisha jambo hili kwa dharura na litajadiliwa na Kamati ya Uongozi, kama ikiona linafaa litapelekwa bungeni kujadiliwa.”
Katika hilo Mbatia alisema: “Bado kuna nafasi ya Bunge kufanya marekebisho. Hili linatakiwa kufanyika kama ambavyo tulikubaliana na Rais kupitia TCD.”
Alisema ushauri wa TCD kwamba mchakato wa Kura ya Maoni uahirishwe hadi mwakani umepuuzwa na matokeo yake yameonekana wazi na kwa msingi huo, suala la kurekebisha maeneo hayo manne, si la kupuuza hata kidogo.
“Hili lisipofanyika utaibuka mgogoro mkubwa. Tatizo la Serikali yetu ni kutotaka kutekeleza mambo yanayoonekana wazi kuwa na mkanganyiko, ndiyo sababu ya kukithiri kwa migogoro ya wakulima, wafugaji, wafanyakazi na mingine mingi,” alisema Mbatia.
Dk Slaa akata tamaa
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema endapo Serikali itashindwa kutekeleza makubaliano hayo, vyama vya upinzani havina budi kuingia katika mapambano kwa katiba hiyohiyo.
“Kama hatumwelewi Rais Kikwete katika suala hili, basi hatuwezi kumwelewa tena. Sioni juhudi zozote za Serikali kubadili maeneo haya. Tulikubaliana naye mambo mengi lakini yote ameshindwa kuyatekeleza, hata hili pia hawezi kulitekeleza,” alisema Dk Slaa.
Katibu mkuu huyo wa Chadema alisema umefika wakati wa vyama vya upinzani kupambana hivyohivyo licha ya kuwapo tume ya uchaguzi isiyo huru.
“Nimeshinda ubunge Karatu vipindi vitatu na tume ikiwa ni hiihii. Wapinzani tuna wabunge zaidi ya 100, nadhani tupambane tu,” alisema.
Alisema umefikia wakati wa kuing’oa CCM kwa kutumia Katiba mbovu (iliyopo sasa) na kinachotakiwa kufanywa na vyama vya upinzani ni kujipanga kuanzia vijijini hadi mijini ili kuzoa kura zote.
“Tumeshinda Kawe, Ubungo, Mbeya Mjini na hata Nyamagana. Tuache kulialia sasa, twende katika mapambano. Kwanza Bunge lijalo ni la Bajeti na kwa vyovyote vile mabadiliko tunayoyataka hayawezi kufanyika,” alisema.
Kiongozi Mkuu wa chama cha ACT-Tanzania, Zitto Kabwe alisema kinachotakiwa kufanywa sasa ni Baraza la Vyama vya Siasa kuitisha mkutano wa vyama vyote ili kukubaliana mambo ya kuboresha katika Katiba ya sasa.
“Jambo la pili ni Rais kuitisha Bunge kabla ya kuanza kwa Bunge la Bajeti kujadili mabadiliko hayo na kuyapitisha ili kuufanya uchaguzi mkuu uwe wa haki na huru,” alisema Zitto.
Juhudi za kumpata Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju na Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Asha-Rose Migiro kuzungumzia hatua ambazo Serikali inachukua hazikuzaa matunda baada ya simu zao kuita mara kadhaa bila kupokewa.

Askofu Gwajima: Siwezi kuwatupa Dk Slaa, Lowassa

KWA UFUPI
  • Asema huu si wakati wa kuchaguliwa marafiki
  • Awahimiza wafuasi wake kumsindikiza polisi Alhamisi, Kova atoa onyo

Dar es Salaam. Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima jana alihubiri akiwa katika kiti cha magurudumu na kusema hawezi kuwatupa Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowassa na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kwa kuwa ni marafiki zake wa siku nyingi.
Pia askofu huyo, amewataka waumini wote wa kanisa hilo kufika katika Kituo Kikuu cha Polisi, Alhamisi ijayo siku ambayo atakwenda kukamilisha mahojiano dhidi ya tuhuma za kumtukana Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Polycarp Kardinali Pengo.
Akihubiri mamia ya waumini waliofika kanisani hapo kwa ajili ya ibada ya Pasaka jana, Gwajima alisema kumekuwa uvumi kwamba kuhojiwa kwake na polisi kulitokana na kuwakaribisha wanasiasa hao kanisani kwake kwa nyakati tofauti na kuzungumza na waumini wake.
Alisema alifahamiana na Lowassa tangu mwaka 1996 wakati huo mbunge huyo akiwa Waziri wa Ardhi na tangu kipindi hicho amekuwa mtu wake wa karibu.
Alisema alifahamiana na Dk Slaa tangu mwaka 1994 kabla hajagombea nafasi ya urais kupitia Chadema na kwamba tangu wakati huo amekuwa rafiki wa familia.
“Hawawezi kunichagulia marafiki, hawa ni watu wangu wa karibu hata kabla hawajawa na ndoto za kugombea urais, nitaendelea kuwa nao karibu,” alisema.
Asimulia mahojiano
Akizungumzia mahojiano yake na polisi, Gwajima aliwaeleza waumini wake kwamba mambo mengi aliyohojiwa hayakuhusiana na suala la kumkashifu Kardinali Pengo.
“Polisi walinihoji mambo mengi binafsi yanayonihusu mimi na hayakuhusiana kabisa na Pengo, maswali ya Pengo yalikuwa machache sana,” alisema.
Hata hivyo, Gwajima alisema hana ugomvi na polisi wala Serikali kwa kuwa amekuwa akitoa ushirikiano kwa vyombo hivyo. Akitoa mfano, alisema Februari mwaka huu alipeleka barua polisi kueleza anataka kudhamini kampeni kwa ajili ya kupinga mauaji ya albino kwa kushirikiana na jeshi hilo.
“Niliwaeleza kwamba tungezunguka na polisi mikoa yote Tanzania na wamenijibu kwamba nipeleke ratiba ya shughuli hiyo ili tuanze,” alisema.
Alisema pia alidhamini mafunzo ya ulinzi shirikishi kwa vijana 400 kwa kushirikiana na polisi... “Shughuli hizi zinaonyesha kwamba sina ugomvi na polisi, bali nimekuwa rafiki kwa kushiriki katika shughuli zenye masilahi kwa Taifa.”
Viongozi wamiminika
Alisema pia hana ugomvi na Serikali na kwamba viongozi wake wamekuwa wakimiminika katika kanisa lake.
Aliwataja viongozi hao kuwa ni Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi na Waziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk Harrison Mwakyembe.
Viongozi wengine, alisema ni Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nauye, Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee na wabunge wa Viti Maalumu, Dk Mary Mwanjelwa na Vicky Kamata wote wa CCM “Kama ningekuwa na ugomvi na Serikali viongozi hawa wasingekuja katika kanisa langu kwa nyakati tofauti. Hii inaonyesha nilivyo na uhusiano mzuri na Serikali,” alisema.
Alhamisi ijayo
Askofu Gwajima amewataka waumini wake kumsindikiza katika Kituo cha Polisi siku ambayo atahojiwa kwa mara nyingine. “Nitakwenda Central Police Alhamisi saa moja asubuhi, nawaomba waumini wote mfike katika eneo hilo lakini msilete fujo wala kumtukana mtu, kuweni watulivu wakati wote nitakapokuwa nahojiwa,” alisema.
Askofu huyo alitakiwa kuhojiwa Alhamisi iliyopita lakini polisi waliahirisha kutokana na hali yake kutokuwa ya kuridhisha.
Hata hivyo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema Jeshi la Polisi halitaruhusu mkusanyiko wa watu katika eneo hilo wakati Askofu Gwajima atakapohojiwa.
“Atatakiwa kufika na wakili wake na mtu mmoja ambaye ataona anafaa kuingia naye kwenye mahojiano. Kama kuna waumini wanajiandaa kukusanyika katika ofisi zetu hapa Central Polisi, wafahamu kwamba haturuhusu na wakikaidi tutachukua hatua.”
Ilivyokuwa kanisani
Gwajima alifika katika kanisa hilo lililopo kwenye viwanja vya Tanganyika Packers Kawe saa 5.00 asubuhi na kupokewa kwa shangwe na waumini walioanza kufika tangu saa 2.00 asubuhi.
Msafara wa magari matatu; Toyota Land Cruiser mbili na Hammer, yaliwasili kwenye viwanja vya kanisa hilo na kulakiwa na waumini walioyazingira kwa shangwe na vigelegele wakitaka kumwona Askofu Gwajima.
Waumini hao walikuwa na shauku ya kumwona Gwajima na walionekana wakisukumana ovyo kila mmoja akitaka kumwona.
Akiwa amevaa suti ya rangi ya kijivu na shati jekundu, Gwajima aliteremka katika Hammer akishikiliwa na wasaidizi wake na kukalishwa katika kiti cha magurudumu mawili kilichokuwa kikisukumwa na wasaidizi hao kuelekea kwenye jukwaa la kanisa hilo.
Baada ya kufika, vikundi vya kwaya viliendelea kuimba na kucheza nyimbo mbalimbali za kumtukuza Mungu.
Gwajima alizungumza na waumini wake kuanzia saa 5.30 hadi saa 6.45, akiwaeleza kilichotokea kuanzia siku alipofika polisi kwa mara kwanza, mahojiano hadi alipotoka hospitali.
Katika mahubiri yake, Gwajima alisema ataendelea kuwaonya viongozi wa Serikali na wa dini watakaokosea masuala mbalimbali. “Sitajali ni kiongozi wa aina gani amekosea nitawakemea. Rais akikosea nitamkemea. Waziri akikosea nitamkemea na viongozi wa dini wakikosea nitaendelea kuwakemea,” alisema.