Sunday, May 26

Jeshi lafanikiwa kudhibiti vurugu Mtwara

Shughuli za mauzo na manunuzi zilirejea rasmi jana mjini Mtwara,
baada ya huduma hizo kusimama kwa siku tatu kutokana na
vurugu zilizotokea kuanzia Alhamisi baada ya kusomwa
hotuba ya Wizara ya Nishati na Madini na wana-
Mtwara kubaini kuwa suala lao la gesi halijapewa umuhimu unaostahili.
Picha na Abdallah Bakari  

Mtwara. Mkuu wa vikosi vya aridhini wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Meja Jenerali SM Kijuu amewahakikishia ulinzi wafanyabiashara hao, baada ya kukutana na uongozi wa Chama cha Wafanyabiashara Sokoni (Wabisoco) jana asubuhi, kufuatia wafanyabishara hao kudai kuendelea kusitisha biashara zao kwa kuhofia usalama.

Katibu wa Wabisoco, Saidi Namata ameliambia Mwananchi Jumapili kuwa wafanyabiashara hao wamekubaliana kufungua biashara zao, baada ya makubaliano ya kulinda eneo hilo na askari wa JWTZ.

“Sisi wafanyabiashara tulikuwa tayari kuendelea kusitisha huduma kutokana na hali ya usalama kuwa mbaya, alipokuja kiongozi wa jeshi na kutuhakikishia kuwa dhamana ya ulinzi itakuwa chini yao tulikubaliana,” alisema Namata

Alisisitiza: “Kama ulinzi ungekuwa mikononi mwa polisi, katu tusingefungua. Polisi wenyewe ndiyo hawa wanaovunja maduka na kuiba, kwa kuwa dhamana hii imebebwa na wanajeshi hatuna shaka, tunaomba wafanyabiashara wengine wafungue biashara zao.”

Tangu juzi magari ya matangazo yamekuwa yakipita mjini Mtwara na kuwatangazia wananchi kuendelea na kazi zao kama kawaida kwa kuwa ulinzi umeimarika, huku askari wa JKT na JWTZ waliosheheni silaha wakizunguka mitaani.

Pinda awasili Mtwara

Wakati tukiewnda mitamboni Waziri Mkuu Mizengo Pinda amewasili Mtwara jana jioni na kukutana na viongozi wa mkoa.

Bungeni Dodoma

Suala la mgawanyo wa rasilimali za taifa jana liliendelea kutikisa Bunge, baada ya baadhi yao kueleza kuwa ni haki kwa maeneo yanakotoka rasilimali hizo kunufaika kwanza kabla ya maeneo mengine.

Wakati wabunge hao wakieleza hayo, wengine wamesisitiza kuwa kwa kuwa nchi ni moja Tanzania, rasilimali zote ni mali ya Watanzania wote.

Wabunge wanaotaka rasilimali zinufaishe kwanza maeneo zinakotoka. Wanasema pamoja na ukweli kwamba Tanzania ni moja, watu hao wana haki ya msingi kupata huduma hizo kwanza kuliko wengine.

Mbunge wa Msalala (CCM), Ezekiel Maige alisema anashangaa kwa nini fomula ya rasilimali kuyaendeleza maeneo iliyopatikana, inatumika kwenye Idara ya Wanyamapori na haitumiki katika sekta ya nishati na madini.

“Wananchi walichosema rasilimali tugawane mrabaha. Zinufaishe wao kwanza. Kwenye wanyamapori, tunafanya hivyo kwa nini kwenye madini tunasema taifa litagawanyika? Alihoji.

Maige alisema Tume ya Bomani ilishauri kuwa asilimia 40 ya mapato itumike kuendeleza maeneo ilikopatikana rasilimali hizo na asilimia 60 zikaendeleze maeneo mengine, lakini ushauri huo haufanyiwi kazi.

Mbunge wa Mpanda (Chadema) Said Arfi alitaka hekima kutamalaki katika suala la mgororo wa gesi Mtwara ili taifa iendelee kuwa na hali ya amani na utulivu

“Naishauri Serikali wawashirikishe wananchi katika mambo yanayohusu mustakabali wa maendeleo yao. Elimu ya kutosha ingalikuwapo na ushirikishwa ulio mpana, tusingalifika hapa. Kadiri tunavyochelewa kulitatua tatizo hili, ndivyo tunavyorudi nyuma katika maendeleo,” alisema.

Kwa upande wake Mbunge Mlalo (CCM), Hassan Ngwilizi, alisema anaunga mkono msimamo wa Rais Jakaya Kikwete kuwa rasilimali za taifa ni mali ya Watanzania wote, hivyo ni mwafaka kwa watu kudhani kuwa wanastahili kunufaika na rasimali kwa sababu zimetoka kwao.

“Wale wote wanaofikiri kuleta chokochoko, wajue nchi hii inavyo vyombo vya dola. Kinachowatokea au kuweza kuwatokea, wajilaumu wenyewe,” alisema Ngwilizi na kusisitiza;

Hamad Ali Hamad (CUF) alisema gesi iliyopatikana Mtwara isiwe laana bali ionekane kama baraka. “Serikali ikazungumze na watu wa Mtwara na hili naomba serikali msione tunafanya jambo baya. hakuna lisilozungumzika,” alisema.

Christopher Ole Sendeka wa Simanjiro (CCM) alisema: “Amani ya Tanzania ni tunu isiyoweza kuchezewa na mtu yeyote yule na kwa sababu yeyote ile .

“Natambua kuna haja ya baadhi ya mambo wanayodai kuangaliwa kwa makini, lakini nawashauri Wanamtwara waendelee kuleta madai yao na Serikali iwasikilize kwa sababu wao ni watu wazima, hawawezi kupiga kelele hivi hivi tu,” alisema.

Ole Sendeka alitaka Waziri asikubali kuendelea kudanganywa na watalaamu wake kwa kuwa watamharibia.

“Usikubali kuuziwa mbuzi kwenye gunia,” alisema Sendeka na kuendelea, “ mwaka jana ulidanganywa na watalaamu wako ukalidanganya Bunge kuhusu nguzo za Tanesco na misumari.”

“Mwaka 2010 Rais Kikwete aliahidi kuwapa mgodi wa Tanzanite One wachimbaji wadogo lakini leo tunaambiwa wakifunga, mgodi huo utakabidhiwa kwa Stamico. Sasa Rais Ni Muhongo au Dk Jakaya Kikwete?”

Kamati yaundwa

Bunge limeunda kamati maalumu kwa ajili ya kuchunguza vurugu zilizotokana na mradi wa kusafirisha gesi, kutoka mkoani Mtwara kwenda jijini Dar es Salaam.

Spika wa Bunge Anne Makinda, alisema kamati hiyo itakayoongozwa na Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage, itakuwa na hadidu nne za rejea.

Wajumbe wake ni Mbunge wa Mpanda Mjini, (Chadema) Said Arfi , Mbunge wa Sikonge (CCM), Said Nkumba, Mbunge wa Wawi (CUF) Hamad Rashid Mohamed na Mbunge wa Tunduru Kaskazini (CCM) Ramo Makani na Rukia Kassim Ahmed (CCM).

Pia wamo Dk Dalaly Kafumu (CCM-Igunga), Cynthia Hilda Ngoye (Viti Maalumu-CCM), Muhamed Chombo (CCM), Agripina Buyogera NCCR- Mageuzi, Cecilia Paresso (Viti Maalumu-Chadema), Mariam Kisangi (Viti Maalumu- CCM), Seleman Jafo (Kisarawe CCM),

Hadidu za Rejea

Spika Makinda alisema kamati hiyo ambayo hata hivyo hakuipa muda maalumu, itakuwa na jukumu la kufuatilia mambo manne muhimu yanayochangia vurugu hizo.

“Kamati itakuwa na jukumu la kujua nini chanzo cha vurugu, kujua hatua zilizochukuliwa na Serikali, kukutana na wadau mbalimbali ili kupata maoni yao na kuangalia mambo yote yenye uhusiano na vurugu hizo,” alisema.

Imeandikwa na Abdallah Bakari, Elias Msuya , Mtwara na Kizitto Noya, Dodoma. - gazeti la mwananchi

Saturday, May 25

Uhasama kati ya polisi, raia Mtwara


Hali ya uhasama imeibuka kati ya polisi na raia mkoani Mtwara, kila upande ukilalamika kuhujumiwa huku hali ikiendelea kuwa tete, ambapo Jeshi la Polisi nchini limetangaza kukamatwa kwa mtu anayetuhumiwa kueneza ujumbe wa uchochezi kwa kutumia simu ya mkononi.

Barabara nyingi za mjini Mtwara ziko tupu, huku magari ya Jeshi la Wananchi na polisi yakiranda randa kuhakikisha usalama, huku maduka na biashara nyingine zikiendelea kufungwa.

Wakati uhasama huo ukiendendelea, taarifa zinaeleza kuwa vifo vimeongezeka na kufikia watu watatu, huku Mkuu wa Mkoa Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia, akisisitiza kuwa na taarifa rasmi ya kifo kimoja tu.

“Mpaka sasa tuna taarifa ya kifo kimoja tu kupitia utaratibu rasmi, kama kuna wengine wamekufa basi mtuletee taarifa kwa kufuata utaratibu,” alisema Simbakalia.

Hata hivyo, taarifa za wananchi zilisema kuwa watu wengine watatu walikufa kwa kupigwa risasi katika maeneo ya Mikindani, huku baadhi ya wanawake wakidai kubakwa na polisi.

Wakati hayo yakiendelea, Jeshi la Polisi nchini limetangaza kumshikilia mtu mmoja (jina limehifadhiwa) kwa tuhuma za kueneza ujumbe wa uchochezi na chuki kwa wananchi na viongozi wa Serikali kwa kutumia simu ya mkononi.

Taarifa ya jeshi hilo iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari imeeleza kuwa meseji hizo zinaenezwa kwa lengo la kuchochea fujo, vurugu na kutoa matusi kwa wananchi na viongozi wa Serikali.

Msemaji wa jeshi hilo, Advera Senso alisema jana kuwa mtu huyo amekuwa akifanikisha kazi hiyo kwa kutumia kadi 13 tofauti za simu za mkononi.

“Alikamatwa akiwa na kadi 13 tofauti za simu za mkononi, polisi bado inaendelea kumhoji mtu huyo na ushahidi utakapokamilika atafikishwa mahakamani,” alisema Senso na kuongeza:

“Kwa muda mrefu sasa watu wa kada mbalimbali nchini wamekuwa wakitumiwa ujumbe mfupi wa maneno katika simu zao, unaohamasisha vurugu na uchochezi wa kidini, huku baadhi ya wananchi wakizitupia lawama mamlaka husika kwa kushindwa kudhibiti hali hiyo.”

Jeshi hilo limewataka wananchi wenye taarifa mbalimbali za wahalifu kama hao kujitokeza na kutoa taarifa hizo, ili wanaotuhumiwa wasakwe na kukamatwa ikiwa ni pamoja na kuchukuliwa hatua stahiki.

Wakizungumza wakati wa ziara ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi, wananchi wengi wamelilalamikia Jeshi la Polisi kwa kutumia nguvu kubwa katika utulizaji wa ghasia na kusababisha vifo, majeruhi na uharibifu wa mali.

Wakati Waziri Nchimbi akifanya ziara hiyo Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha naye alitua mkoani humo na kusisitiza ulinzi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Akizungumza mbele ya Waziri Nchimbi, Diwani wa Kata ya Magengeni Tarafa ya Mikindani, Omar Nawatuwangu alisema, licha ya wananchi kufanya vurugu, Jeshi la Polisi lilijibu kwa kujeruhi watu na kuchoma nyumba.

“Hali hapa siyo shwari, ni kweli wananchi wamefanya vurugu lakini askari hawa tunaotegemea watatulinda, ndiyo wamechoma nyumba za watu na kujeruhi watu kwa risasi,” alidai Nawatuwangu.

Naye Issa Nambanga wa Mikindani alidai kuwa aliwaona askari waliokuwa na bunduki wakichoma nyumba ya jirani yake. “Mimi niliwaona askari wakichukua mali za jirani yangu na baadaye kuichoma moto nyumba yake. Nilishindwa la kusema kwa kuwa niliwaogopa askari hao,” alisema Nambanga.

Kwa upande wake Mariam Abdallah ambaye ni mjane mwenye watoto watatu, alilalamika kuchomewa nyumba na vyombo vyote alivyokuwa navyo.

“Juzi usiku (Mei 22), polisi walikuja na gari lao na kulisimamisha mbele ya nyumba yangu. Nilimwona polisi wa kike akinitaka nitoke nje na watoto wangu, kisha akawasha kiberiti na kuichoma nyumba yangu. Sina chochote nilichookoa na hapa sijui nitaanzia wapi, sina kazi, hata jembe ninalolimia wamelichoma,” alisema.

Waziri Nchimbi alitembelea pia askari waliochomewa nyumba zao huku akimtaka Kamanda wa Polisi mkoani humo, Linus Sinzumwa awasake wote waliohusika na uhalifu huo. Wakizungumzia tukio hilo, baadhi ya askari waliochomewa nyumba, walisema kuwa hali hiyo inaonyesha uhasama uliopo kati yao na raia.

“Siku zote nimeishi hapa na wananchi hata wengine nilikuwa nikiwapa kazi ya ujenzi, lakini katika vurugu za juzi, nilishangaa tu watu wanavamia nyumba yangu na kuichoma moto. Mke na watoto wangu walikimbia kujificha kwa jirani,” alisema Sajini Fakih Sajih anayeishi Kata ya Chikongola.

Wengine waliokumbwa na zahama ya kuchomewa nyumba ni pamoja na mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC), Kassim Likongolo na mkewe Koplo Fatuma na Koplo Philemon Yatitu.

Mbali na askari hao, waandamanaji pia walichoma ofisi ya CCM, Kata ya Chikongola na ofisi ndogo ya Mbunge iliyopo Mikindani.

Kauli ya Mkuu wa Mkoa

Akizungumzia malalamiko ya wananchi Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali mstaafu Joseph Simbakalia, alikiri kupokea malalamiko ya wananchi na kusema kuwa askari waliohusika na vitendo hivyo wakibainika watawajibishwa kijeshi.

“Malalamiko ya wananchi tumeanza kuyapokea, yatachunguzwa na kama yatabainika kuwa ya kweli askari watachukuliwa hatua za kijeshi,” alisema Simbakalia.

Akizungumzia mfululizo wa vurugu hizo tangu zilipoanza Desemba mwaka 2012, Simbakalia alisema hazina uhusiano na suala la gesi bali ni hujuma dhidi ya maendeleo.

“Ni kweli tulianza kuona viashiria mapema kwa kuwepo vipeperushi na ujumbe wa simu, ndiyo maana tuliweka ulinzi mkali wa polisi. Hali ilipozidi kuwa mbaya, kwa kutumia utaratibu wa kisheria, kama mkuu wa mkoa nikaomba kuongezewa nguvu za kijeshi,” alisema Simbakalia.

Hata hivyo, Simbakalia alishindwa kueleza hatua zilizochukuliwa kwa watu hao tangu vurugu hizo zilipoanza mwishoni mwa mwaka jana, licha ya kukamata zaidi ya watu 90 katika vurugu za sasa.

Vurugu Msimbati

Ghasia zimezuka katika Kijiji cha Msimbati inapochimbwa gesi asilia, ambapo watu wasiojulikana wamechoma moto Ofisi ya Hifadhi ya Bahari jana usiku.

Habari zinasema tukio hilo limetokea kati ya saa 4 na 5 usiku na kwamba polisi waliingia kijijini hapo usiku huo kutuliza ghasia. Mkuu wa Mkoa, Simbakalia amethibitisha kutokea kwa vurugu hizo.

Kauli ya Waziri Nahodha

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Mtwara, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha alitetea uamuzi wa kuleta Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) Mtwara kwa lengo la kulinda amani.

“Kwa mujibu wa Katiba, tumepewa dhamana ya kulinda wananchi dhidi ya maadui wa ndani na nje hivyo ni wajibu wetu wa msingi inapotokea haja ya kufanya hivyo,” alisema Nahodha.

Alizungumzia pia ajali ya gari la jeshi wilayani Nachingwea mkoani Lindi na kusababisha vifo vya wanajeshi wanne, alisema kuwa vimewasikitisha na majeruhi watapelekwa Dar es Salaam kutibiwa.

“Kwa hiyo wale wenzetu waliopoteza maisha damu yao haikumwagika bure, walikuwa katika kutimiza wajibu wao kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wamepotea wakiwa katika harakati za kuleta amani.”

Kiama hiki cha gesi Mtwara kisiigawe Tanzania - GAZETI MWANANCHI



Licha ya utajiri huo mkubwa unaweza kujiuliza, je, ni kwanini bara hili limeendelea kuwa maskini kwa miaka mingi huku likikabiliwa na mizozo mingi na migogoro kuhusu mgawanyiko wa rasilimali hizi.

Jiulize, leo ikiwa ni miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU), sasa Umoja wa Afrika (AU), kwanini bara hili tajiri kiasi hiki bado linatajwa kuwa maskini pengine kuliko mabara mengine duniani?

Tunaambiwa, Afrika ina asilimia kubwa ya madini, lakini, jiulize, kwa nini asilimia kubwa ya madini hayo haitumiwi vizuri au kikamilifu katika kuliinua bara hili. Kwanini hayalisaidii bara hili?

Kwa kutaja machache, Afrika ni tajiri kwa madini kama vile, almasi, dhahabu, shaba urani na mengine mengi.

Bara hilo linajivunia asilimia 40 ya umeme wa nguvu za maji unaopatikana duniani, linazalisha madini mengine kama chromium, asilimia 30 ya uranium na asilimia 50 ya dhahabu inayopatikana kote duniani.

Pia, asilimia 90 ya cobalt, asilimia 50 ya phosphates, asilimia 40 platinum, asilimia 7.5 au zaidi ya makaa ya mawe, asilimia 8 ya petroli na bidhaa zake, asilimia 12 ya gesi asilia, asilimia 3 ya madini ya chuma na mamilioni ya ekari za ardhi nzuri na inayofaa kwa kilimo cha mazao mbalimbali yakiwamo ya chakula, biashara ambayo ni mengi mno kuyataja.

Pia, bara hili linayo mito, maziwa, bahari ambako kwa kiasi kikubwa wanapatikana samaki wengi na wa aina mbalimbali wakiwamo hata wale wenye bei kubwa katika soko la dunia.

Pia, Afrika inavyo vitu vingine vingi kama mbuga za wanyama ambazo zimejaa tele, zinavutia watalii wengi, ambao huongeza fedha za kigeni, lakini mbona havijaweza kulisaidia bara hili kuondokana na lindi hili la umaskini?

Huenda ni bahati mbaya kwamba mgawanyo usiyo sahihi au sawa kwa rasilimali hizi, ulafi wa baadhi ya viongozi, hasa wale waliokabidhiwa jukumu la kusimamia idara au taasisi zinazoshughulikia uchimbaji, usambazaji wake na usiri mkubwa katika mikataba.

Kutokana na usimamizi duni wa rasilimali hizi zinaweza kuwa baadhi ya sababu za kuzuka kwa mizozo hii mikubwa ambayo inalikumba bara hili, kama ambavyo inaanza kuzuka Tanzania.

Rais Yoweri Museveni wa Uganda katika moja ya hotuba zake mwaka jana wakati akizindua mradi wa kuchimba mafuta katika Ziwa Natron nchini mwake alieleza mengi kuhusu rasilimali hizi na jinsi zinavyoweza kuigawa nchi na Afrika kwa jumla.
Dar es Salaam. Bara la Afrika kwa hakika limebarikiwa kuwa na rasilimali lukuki ambazo ni lulu katika kukuza uchumi.

“Tunafurahi kuwa tunayo mafuta hapa, hii ni rasilimali ambayo haina budi kutuunganisha zaidi sisi (Waganda) badala ya kutugawa,” alieleza Museveni mbele ya wageni, wenyeji na wawekezaji kutoka China ambao wanashiriki katika mradi huo.

Rasilimali hizi nyingi zinapatikana katika Afrika ikiwamo Tanzania ambako imegunduliwa gesi asilia kiasi cha trilioni 41 futi za ujazo kule Mtwara na Lindi.

Kwa bahati mbaya, rasilimali hii imeanza kuimega tunu ya amani, utulivu ambayo nchi yetu ilijaliwa kuwa nayo kwa muda mrefu na sasa ni dhahiri inaweza kuigawa nchi.

Upo ushahidi wa jinsi ambavyo Muungano wa Tanzania, uliotokana na kuungana kwa Tanganyika na Zanzibar kwa siku za karibuni umekuwa ukitiwa majaribuni, kisa ni hisia za kugundulika au kupatikana kwa mafuta kule Pemba au kwingineko katika bahari kuu.

Huu ni mtihani mkubwa ambao matukio haya ya Mtwara yanasababisha wananchi kuamini kuwa gesi inaweza kuwakomboa kutoka katika lindi la umaskini tena kwa haraka bila kuwashirikisha wenzao wa maeneo mengine ya nchi. Huu ni mtihani ambao nchi inatakiwa kuushinda, lakini kwanza inatakiwa kuwa makini.

Kauli za ubabe au vitisho dhidi ya wananchi hao, ziwe kutoka kwa viongozi wetu kama wa Wizara ya Nishati na Madini, chini ya Profesa Sospeter Muhongo na wasaidizi wake, George Simbachawene na Stephen Masele, hazifai.

Pia, kwa kuwa Rais Jakaya Kikwete ndiye amepewa mamlaka na katiba yetu kusimamia mgawanyo huu wa rasilimali, hana budi naye kuchukua hatua sasa, wala si kusubiri wananchi waanze kukumbatia kile kinachozalishwa kwao, kwa maslahi yao.

Ni wazi kwamba kama kuna wanasiasa, kundi la wanaharakati wanaodhani kuwa watafanikiwa kuwatumia wananchi wa Mtwara kudai gesi ibaki ili wapate maendeleo, wanapaswa kujitazama upya.

Ni wazi kwamba gesi inataka uwekezaji mkubwa, inataka masoko ya uhakika, ambayo yanaweza kuwa mbali ya eneo lao, ilimradi wao wahakikishiwe huduma zote muhimu za jamii kama shule, zahanati, barabara nzuri na kadhalika.

Hakuna shaka kwamba huu ni mradi mkubwa ambao Tanzania kama nchi haikuwahi kuwekeza, lakini pia ni mtihani ambao Serikali ya awamu ya nne, chini ya uongozi wa Rais Kikwete na wenzake wote hawana budi kujifunza kutoka yaliyotokea kwingineko.

Afrika, imeshuhudia nchi iliyokuwa kubwa kieneo, Sudan imegawanyika na mojawapo ya sababu ni mgawanyo wa rasilimali, mafuta na sasa imeparaganyika na kubakia mataifa mawili, Sudan na Sudan Kusini, ambazo zote hazijiwezi kiuchumi.

Kumbukumbu za Nigeria na mizozo kule Niger Delta ni ushahidi mwingine wa jinsi ambavyo bila umakini, nchi inaweza kuingia katika vita.

Miundombinu iliyogharimu kiasi kikubwa cha fedha imekuwa ikichezewa, kuharibiwa karibu kila mwaka kule Nigeria ambako nchi imepata hasara, wananchi wamepoteza maisha, jambo ambalo linapaswa kuepukwa kwa gharama zozote zile, kwani nafasi bado ipo ya kuweza kufanya hivyo.

Kwa mfano, mzozo baina ya Nigeria na Cameroon ambazo awali ziliingia kwenye mzozo mkubwa zikigombea rasi ya Bakassi yenye mafuta, hadi jumuiya ya kimaifa imelazimika kuingilia kati, sote tumeona. Je, tumepata fundisho gani kuhusu rasilimali na jinsi zinavyoweza kuwa sababu na chanzo cha mizozo na migogoro?

Kumbukumbu zetu kule Bungeni mjini Dodoma zinatuonyesha kuwa hivi karibuni kuwa wabunge walijadili rasimu ya sera ya gesi na wengi walionekana kuwa na wasiwasi kuhusu ugawaji wa rasilimali hiyo ndani na kwa wageni.

Wabunge wengi walitaka mikataba iwekwe wazi kwa viongozi na wananchi wote ambao kimantiki gesi hiyo ni mali yao.

Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe(Chadema ) alitaka vitalu vya gesi visiuzwe mapema kwa wawekezaji hadi pale sheria rasmi ya gesi itakapokamilika.

Hata hivyo, Profesa Muhongo alisema serikali iliamua kuanza uuzaji wa vitalu hivyo ili isiwe nyuma katika soko la dunia la nishati.

“Hatuna haja ya kubaki nyuma, tukichelewa katika hili tunaweza kukosa fursa kwani nchi nyingine zinazonunua gesi zipo katika mchakato wa kutafuta mbinu mbadala za nishati hiyo” alisema Profesa Muhongo.

Ni dhahiri kwamba hili la Mtwara linaweza kuichelewesha Tanzania, hasa wakati huu ambao jirani zetu, Msumbiji wamewekeza katika gesi kwa kiasi kikubwa.

Ushauri hapa ni kuwa busara zaidi itumike, pande zote ili zichume na kuvuna kutoka kwenye gesi asilia ya Mtwara hadi bomba litakapojengwa, viwanda kama kile cha saruji, wananchi wanufaike, serikali ikusanye kodi, ambazo hatimaye zitasaidia kukuza uchumi.

Inawezekana kuwa hiki kinachotokea kule Mtwara, bila umakini kinaweza pia kuibuka Ruvuma au hata Manyoni (Singida) ambako pia imegundulika urani, madini mengine ambayo pia yameanza kuzua mijadala na mizozo mingi ikiwamo ile ya kimazingira.

Kuna madini aina ya nickel kule Kabanga, Ngara Mkoani Kagera, ambayo pia yana thamani kubwa na ambayo pia yanaweza kuzua mzozo mwingine. Kama nchi, tujihadhari, tujaribu kuwa makini!

Sakata la gesi Mtwara: Wabunge CCM wacharuka


Dodoma. Wabunge wa CCM wamekuja juu na kumtaka Rais Jakaya Kikwete kuwafukuza kazi vigogo wa Serikali mkoani Mtwara, wakiwamo Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya kutokana na kile walichoeleza ni uzembe uliochangia vurugu zinazoendelea za wananchi kugomea gesi kutoka nje ya mkoa huo.

Wengine waliopendekezwa kuchukuliwa hatua ni kamati nzima ya ulinzi na usalama ya ngazi ya mkoa na wilaya ya Mtwara mjini, wakiwamo makamanda wa polisi.

Kutokana na hali hiyo, vigogo kadhaa mkoani humo wako hatarini kukumbwa na ghadhabu hiyo akiwamo Mkuu wa vikosi vya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Mkuu wa mgambo na Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).

Wabunge hao walikuwa wakitoa mapendekezo hayo kwenye kikao cha Kamati ya Wabunge wa CCM iliyofanya kikao cha dharura juzi usiku, mjini hapa.

Kikao hicho kiliongozwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, huku Spika wa Bunge, Anne Makinda ambaye wakati huo alikuwa kwenye kikao cha Kamati ya Uongozi wa Bunge, aliwakilishwa na Mwenyekiti wa Bunge, Jenista Mhagama.

Katika kikao hicho maalumu kilichokusudia kutoa ushauri kwa Rais Kikwete juu ya njia mwafaka ya kutatua hali ya machafuko, wabunge wengi wali kukasirishwa na jinsi hali ilivyo mkoani Mtwara. Chanzo chetu kwenye kikao hicho kilieleza kuwa wabunge hao walichukizwa na jinsi Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya walivyokuwa wakipingana kimsimamo. Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Joseph Simbakalila, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mjini, Wilman Ndile na Kamanda wa Polisi Mkoa Linus Sinzumwa wamehusishwa.

Licha ya baadaye kuonekana kuwa kitu kimoja, wabunge hao walidai kuwa walishindwa kutumia nafasi zao katika kutatua tatizo hilo, ambalo hadi juzi Serikali ilisema walikuwa wamekufa watu watano, wakiwamo wanajeshi wa JWTZ waliofariki katika ajali wakati wakienda kutuliza machafuko.

Chanzo hicho kilieleza kuwa iwapo mapendekezo ya wabunge hao yatapelekwa kwa Rais Kikwete kama michango ya wabunge hao ilivyokuwa, huenda rungu likawaangukia pia viongozi wa kisiasa wa CCM mkoani humo. Miongoni mwa wanasiasa hao, chanzo hicho kimesema ni wale waliotoa kauli za waziwazi kuunga mkono msimamo wa kutoruhusu gesi kusafirishwa nje ya mkoa huo.

“Hapa wapo wabunge, madiwani na viongozi wa ngazi mbalimbali wa CCM,” kilieleza chanzo hicho.

Hata hivyo, baadhi ya wabunge walipendekeza mkakati wa kutatua uzembe uliofanyika Mtwara, unapaswa kuchukuliwa kwa uangalifu usije ukasababisha madhara mengine kwa Chama na Serikali.

Walisema suala hilo halina budi kuchukuliwa kwa uangalifu hasa ikizingatiwa kuwa Chama cha CUF ndicho chenye nguvu mkoani humo ukilinganisha na vyama vingine vya upinzani.

Wabunge hao walikituhumu chama hicho kuwa kimekuwa kikijaribu kutumia vurugu hizo kama kigezo cha ushawishi wa kukubalika mkoani humo.

Taarifa zilizopatikana jana mjini hapa zimeeleza kuwa tayari maazimio ya wabunge hao wa CCM yamewasilishwa kwa Rais Kikwete.

Taarifa ambazo hazijathibitishwa pia zinaeleza kuwa leo Kamati ya Uongozi ya Bunge huenda ikatangaza Bungeni maazimio yao kuhusu vurugu za Mtwara.

Kamati ya Uongozi ilianza kukutana kuanzia Jumatano jioni na hadi jana wajumbe walikuwa wamejifungia wakijadili namna wanavyoweza kushiriki na kuishauri Serikali kuhusu hatua mwafaka za kuchukua.

RAMA MLA WATU AACHIWA HURU



Ramadhani Suleiman 'Rama mla kichwa' (kulia) na mama yake mzazi,
Khadija (katikati) walipofikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza.

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imemuachiwa huru Ramadhani Suleiman (Rama mla kichwa) aliyekuwa anakabiliwa na kesi ya mauaji, baada ya kubaini hana akili timamu.

Jaji Rose Temba alitoa hukumu hiyo jana kutokana na ripoti ya Dk Mdeme Erasto iliyowasilishwa mahakamani hapo kuonesha kuwa, wakati mshitakiwa huyo anatenda kosa hilo hakuwa na akili timamu.

Ramadhani, ambaye alishitakiwa pamoja na mama yake Khadija Suleiman, alidaiwa kukutwa na kichwa cha mtoto Salome Yohana (3) katika eneo la Hospitali ya Taifa Muhimbili kikiwa katika mfuko wa plastiki maarufu kama rambo.


Jaji Temba alisema mshitakiwa alitenda kosa la mauaji, lakini kwa kuzingatia ripoti ya uchunguzi wa akili, mahakama haiwezi kumtia hatiani hivyo aliamuru mshitakiwa huyo awe chini ya uangalizi wa madaktari wa Hospitali za magonjwa ya akili na watatakiwa kuripoti maendeleo ya afya yake kwa Waziri wa Katiba na Sheria.

Aidha mahakama ilimwachia huru mama mzazi wa mshitakiwa huyo, Khadija, kwa kuwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) hakuwa na haja ya kuendelea kumshitaki.

Awali Wakili wa utetezi, Yusuph Shehe alidai kuwa mahakama ilitoa amri ya mshitakiwa kwenda hospitali kuchunguzwa kama ana akili na ripoti ya daktari iliwasilishwa mahakamani hapo na kubainisha kuwa hakuwa na akili timamu, hivyo aliomba mahakama imfutie mashitaka.

Akiwasomea maelezo ya awali washitakiwa hao, Wakili wa Serikali Cecilia Mkonongo alidai kuwa Aprili 25 mwaka 2008 saa 2:25 usiku, Salome (marehemu) alikuwa anacheza na Ramadhan pamoja na mtoto Paschal Lucas lakini baadaye alipotea katika mazingira ya kutatanisha.


Alidai saa 2:30 usiku baba wa Salome, Yohana Mussa alikwenda kwa dada yake aitwaye Furaha ambapo Salome alikuwa akiishi, alipohoji mtoto wake yupo wapi ndipo wakaanza kumtafuta bila mafanikio, wakaamua kutoa taarifa kwa balozi.

Aliendelea kudai kuwa, asubuhi ya Aprili 26 mwaka 2008, wakiwa njiani kwenda kituo cha polisi walipewa taarifa kuwa kuna kiwiliwili cha mtoto kimeonekana katika choo cha nyumba ya washitakiwa, walipokwenda walikuta mwili wa Salome ukiwa chini bila kichwa.

Mkonongo alidai wakiwa katika eneo la tukio, polisi walipata taarifa kuwa kuna mtu amekamatwa na kichwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, walikwenda wakiwa na askari na ndugu wengine na kukitambua kichwa hicho.

Ilidaiwa kuwa, Ramadhani alikamatwa na mlinzi wa Hospitali hiyo akiwa na kichwa hicho na kudai anakipeleka kwa shangazi yake anayefanya kazi ya usafi katika hospitali hiyo.

Aprili 29 mwili wa marehemu ulifanyiwa uchunguzi na ripoti ya daktari ilionesha, chanzo cha kifo chake hakikujulikana lakini, ilidai Salome alikatwa na kitu chenye ncha kali na alikuwa na michubuko mwilini.

Rama alipohojiwa na askari, alikiri kukutwa na kichwa hicho na kudai mama yake ndiye aliyemuua Salome kwa kutumia shoka na alikuwa anapeleka kichwa kwa shangazi yake.

Mama wa mshitakiwa huyo (Khadija) alipohojiwa alikiri mwili wa marehemu kukutwa kwenye choo chake na ukiwa umefungwa na shati la Ramadhani.

Baada ya uamuzi huo kutolewa, ndugu wa marehemu waliangua kilio, na walipotoka Upendo Dunstan (mama wa marehemu) na shangazi yake Furaha Mussa walikuwa wakiangua kilio huku baba wa mtoto akilia huku ameshika kiuno nje ya mahakama hiyo.


Washitakiwa walirudishwa rumande kwa ajili ya kukamilisha taratibu, baada ya kusota rumande kwa zaidi ya miaka mitano.

Friday, May 24

HAKUNA JAMII ITAKAYOACHWA NYUMA KIMAENDELEO: TANZANIA

Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa,
Balozi Ramadhan Mwinyi, akizungumza wakati wa
Mkutano wa 12 wa Masuala ya Wazawa,
kuhusu mada ya utafiti uliofanywa kuhusu Ujasiri,
Maarifa ya Jadi na Kujenga uwezo Jamii ya Wafugaji katika Afrika.
Nyuma ya Balozi ni Bi. Ellen Maduhu Afisa wa Ubalozi .


Tanzania imesisitiza kwamba inajukumu kubwa la kuhakikisha kuwa mipango yake ya maendeleo endelevu inamfikia kila mwananchi na kwamba hakuna jamii itakayo achwa nyuma.

Na kwa sababu hiyo, Tanzania imeitaka Jumuiya ya Kimataifa na wadau wengine kushirikiana na Serikali katika kufanikisha azma yake hiyo, lakini pia kutambua kuwa maamuzi mbalimbali inayoyachukua yanafanyika kwa nia njema.

Hayo yameelezwa na Balozi Ramadhan Mwinyi, Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, alipokuwa akichangia majadiliano ya mada ya utafiti kuhusu Ujasiri, Maarifa ya Jadi na Kujenga Uwezo wa Jamii ya Wafugaji katika Afrika.

Mada hiyo ni sehemu ya mada kadhaa zikiwa zao afya, elimu, haki za binadamu, ujasiliamali, vijana mila na tamadu ambazo zimekuwa zikijadiliwa kwa nyakati tofauti katika Mkutano wa Kudumu wa 12 Kuhusu Masuala ya Wazawa. ( Forum on Indigenous Issues) Mkutano huu ambao ulianza mapema wiki hii unafanyika chini ya usimamizi wa Baraza la Uchumi na Maendeleo ya Jamii la Umoja wa Mataifa ( ECOSOC).

Washiriki wa mkutano huu wapatao 2000 wanatoka katika Asasi zisizo za kiserikali wakiwamo wawakilishi kutoka baadhi ya taasisi za kifedha kama Banki ya Dunia, Banki ya Maendeleo ya Afrika na Banki ya Maendeleo ya Asia.

“Tunaendelea na jitihada za kuwaletea maendeleo wananchi wetu ili kuhakikisha kwamba hakuna jamii inayoachwa nyuma kama ambavyo imeainishwa katika Malengo ya Maendeleo ya Millenia ( MDGs) na kutafsriwa katika Mpango wa Maendeleo ya Taifa na mipango migineyo” akasisitiza Balozi Mwinyi.

Hata hivyo akasema licha ya jitihada hizo za serikali , bado kuna baadhi ya jamii chache ambazo zenyewe zimeamua kudumisha mila, tamaduni na maisha yao ya jadi .

Akasema jamii hizo ni zile ambazo hazifahamiki sana katika Jumuiya ya Kimataifa kama ilivyo kwa jamii ya wamasaai.

Akizungumzia masuala ya upatikanaji na ugawaji wa ardhi kwa wananchi zikiwamo jamii ambazo mfumo wa maisha yao unategemea zaidi ardhi na mali asili nyingine. Balozi Mwinyi amewaeleza washiriki wa mkutano huo wakiwamo washiriki kutoka Tanzania, kwamba serikali imejiwekea sheria na taratibu zinazosimamia ugawaji wa ardhi.

Akafafanua kwa kueleza kwamba kwa sheria na taratibu za Tanzania, Hati ya umiliki wa Ardhi katika ngazi ya kijiji hutolewa kwa wanajamii ambao wanaishi au wamekusanyika katika muundo wa kijiji ambao unatambuliwa rasmi.

“ Kwa mujibu wa sheria zetu, ni kijiji ndicho kinatambuliwa kisheria kama chombo huru kinachosimamia masuala ya ardhi ambapo cheti cha ardhi hutolewa kwaajili ya matumizi ya jamii nzima”. Akasema

Na kuongea “ Hata hivyo kuna baadhi ya maeneo hasa yale ya wawindaji ambapo kama idadi ya jamii ile haikukidhi matakwa ya kisheria ya kuwa na hadhi ya kijiji kutokana na uchache wao, bado kwa mfano, mwaka 2011, serikali ilitoa hati ya kumiliki ardhi kwa ya Wahdzabe ingawa walikosa sifa zinazotakiwa kisheria.

Akizungumza kuhusu Loliondo ambako Serikali imetangaza kutenga eneo la kiasi cha kilomita za mraba 2,500 za ardhi kwaajili ya makazi ya jamii ya wamasaai na ambao wengi wao hawakuwa na ardhi na hivyo kuwa katika mazingira magumu. Balozi amesisitiza kwamba uamuzi huo ulikuwa ni wa manufaa kwa jamii hiyo na taifa kwa ujumla.

Akasema kuwa eneo lililotengwa ni kubwa kuliko nchi ya Luxeburg au mara nne ya eneo la nchi ya Singapore ambayo ina kilomita za mraba 624.

Akasema eneo lililobaki la kilomita za mraba 1,500 Serikali imelitenga kwaajili ya hifadhi ya wanyama pori na mazalia yake ikiwa ni pamoja na uhifadhi wa uoto wa asili, utunzaji wa vyanzo vya maji kwa maendeleo endelevu ya uwepo wa wanyama na kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Naibu Mwakilishi wa Kudumu akafafanua Zaidi kwa kueleza kwamba, uamuzi huu wa Serikali wa kutenga ardhi kwaajili ya matumizi ya binadamu na mengine kwa hifadhi ya maliasili ni uamuzi halali na wala haukuanza sasa bali umekuwa ukitekelezwa katika maeneo mengi ya nchi tangu uhuru.

HALI BADO NI MBAYA MTWARA....WANAFUNZI WAWILI WAMETANDIKWA RISASI, MMOJA AMEFARIKI HAPOHAPO

Hivi sasa baadhi ya wananchi wa eneo la magomeni mkoani mtwara wamekimbilia katika Hospitali ya Mkoa wa Mtwara Lugula wakihofia usalama wao kutokana na vurugu za kuchomwa kwa nyumba zao pamoja na vibanda vya biashara zilizotokea leo asubuhi katika eneo hilo..

Maduka maeneo ya Magomeni yamechomwa moto ikiwamo pia mali za Askari magereza . Mwanafunzi wa CHUNO amefikishwa hospitali Ligula na majeraha ya risasi mguuni.
Mwanamke mwingine anayekadiriwa kuwa na miaka 25 mjamzito ameuawa kwa kupigwa risasi maiti ipo Ligula.

Inaelezwa kuwa katika baadhi ya mitaa hali imetulia na ni idadi ndogo ya wananchi ndiyo inayoonekana wakitembea mitaani isipokua eneo la magomeni ambako mbomu yanaendelea kusikika huku huduma za kijamii katika mji huo zikiwa zimesimama zikiwemo usafiri, huduma za kibenki na shule








MTWARA: ASKARI WATUHUMIWA KUBAKA NA KUMUUA MJAMZITO......INASEMEKANA WANAFANYA MAKUSUDI ILI KULIPIZA KISASI

Askari wakiwa lindoni/doriani, Mtwara

Hali ya usalama katika Manispaa ya Mtwara Mikindani mkoani Mtwara imezidi kuwa mbaya baada ya askari polisi kudaiwa kufanya unyama kwa kuwabaka wanawake na kumpiga risasi mjamzito

Mbali na unyama huo polisi pia wanadaiwa kuchoma moto nyumba tatu za wananchi katika mtaa wa Magomeni na vibanda vya maduka kadhaa na kupora vitu vilivyomo ndani.

Hata hivyo Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara, Linus Sinzumwa anasema hali ni shwari na kwamba wananchi watoke nje kuendelea na shughuli zao kama kawaida.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Ligula, Mohamedi Kodi amethibitisha kupokea mwili wa mjamzito ukiwa na tundu tumboni, zinazoaminika kuwa za risasi na hivyo kufanya idadi ya maiti zilizopokelewa hospitalini hapo kufikia mbili na majeruhi 18:

“Ni kweli kwa leo( jana) tumepokea maiti moja ya mwanamke ambaye ni mjamzito wa miezi saba, amepigwa risasi tumboni.pia tumepokea mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Chuno, amevunjwa miguu yote kwa risasi.”

Habari zinadai kuwa mjamzito huyo ameuawa akiwa nyumbani kwake baada ya polisi kuvamia makazi yake.

Huduma za kijamii zimesimama, hakuna maduka yaliyo wazi, hakuna usafiri wa daladala wala pikipiki, mji upo kimya, sauti za milio ya mabomu na bunduki zimetawala, wanajeshi waliovalia sare wameuzingira mji wakiwa katika magari na pikipiki.

Wakizungumza na Waandishi wa Habari kwa nyakati tofauti wakazi hao wamelalamikia kitendo cha askari wa jeshi la polisi kuingia katika makazi yao, kuwapiga, kuwabaka na kuwapora mali zao:

“Magomeni A hatuna amani askari wanaingia majumbani mwetu wanatupiga na kutunyang’anya simu, yani huku Magomeni hatuna amani kabisa, tumepoteza watoto na hatujui hata waume zetu wako wapi” alisema Paulina Idd na kuongeza:

“Majumba yetu yamechomwa moto , wanaofanya fujo ni polisi wenyewe halafu wanakuja wanatubaka na kuiba mali zetu halafu tunateseka sisi yaani tumechoka kabisa na serikali yenyewe,” alisema Paulina.

Kamanda Sinzumwa alipoulizwa kuhusiana na tuhuma hizo alisema hawezi kuzungumzia suala hilo kwa madai kuwa atapingana na Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Mchimbi aliyewasili Mtwara leo: “Kuhusiana na suala hilo siwezi kulizungumzia kwa sasa kwani nitapingana na Waziri wangu kwani leo ametoa tamko bungeni na leo atawasili,” alieleza Sinzumwa

Wananchi wazungumzia bajeti

Wakizungumzia uwasilishwaji wa hotuba ya Wizara ya Nishati na Madini wakazi wa hapa wamesema kuwa hawakubaliani na ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kwani mpango huo utawaletea dhuluma:

“Mpango wa kusafirishwa kwa gesi asilia hatuna mpango nao kwa wakazi wote wa Mtwara kwa kifupi akina mama wa mtwara hatutaki itoke,” alisema Fatuma Abdallah.

Thursday, May 23

VURUGU ZA MTWARA ZAUA WANAJESHI WANNE NA KUJERUHI 20


Katika tukio lingine askari wanne wa jeshi la wananchi kikosi cha 41 KJ wamefariki dunia na wengine 20 kujeruhiwa baada ya gari lao kupinduka eneo la Kilimani hewa Nachingwea njiani kuelekea Mtwara kuongezea nguvu jeshi la polisi kufuatia vurugu zilizotokea mkoani humo


Mtu mmoja amefariki dunia na kadhaa kujeruhiwa katika vurugu zilizoibuka mkoani Mtwara baada ya bajeti ya wizara ya nishati na madini kusomwa ambapo pia ofisi za CCM wilaya ya Mtwara vijijini imeteketezwa moto pamoja na nyumba nyingine nne ikiwemo nyumba ya mbunge na mwandishi wa habari wa TBC



Nyumba ya mwandishi wa habari wa tbc yachomwa moto huku mabomu yakirindima huko mtwara


Hali imezidi kuwa mbaya katika Mji wa Mtwara na hivi punde watu wanaendelea kufanya uharibifu katika maeneo mbalimbali ya mji huo.
Jengo moja ambalo linadaiwa kumilikuwa na CCM limechomwa moto katika eneo la Majengo na daraja linalounganisha Lindi na Mtwara limevunjwa.
Mbali na hayo pia nyumba ya mwandishi wa habari wa Shirika la Utangazaji la Tanzania (TBC)imechomwa moto.
Katika Mji wa Mtwara milio ya mabomu na risasi ndio inayosikika kila kona. Jeshi la Polisi linajaribu kuwadhibiti vijana na watu wengine ambao wanafanya vurugu hizo.

Kwa mujibu wa - freebongo.blogspot.com

Umefika wakati wa kubadili muundo wa Tanesco


ahitaji ya umeme kwa wateja wake ni Megawati 906, lakini uwezo wake ni kuzalisha 705 tu. Megawati hizo zinazalishwa kupitia mabwawa ya Kidatu (204), Kihansi (180), Mtera (80), Pangani (68), Hale (21) na Nyumba ya Mungu (8).
Jana bungeni, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo aliwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka huu wa fedha na ndani ya hotuba yake alielezea hali mbaya ya Tanesco akisema inadaiwa zaidi ya Sh900 bilioni.
Haishangazi kusikia Tanesco ina hali mbaya kifedha, kwa sababu tangu shirika hilo lianzishwe mwaka 1964, limeshindwa kutoa huduma ya umeme kwa walau nusu ya Watanzania, hata hao waliounganishiwa, hawapati umeme wa uhakika.
Wizara inayoisimamia Tanesco imeshaongozwa na mawaziri 21 na makatibu wakuu 18. Hoja za baadhi yao ni shirika hilo kuzidiwa kimajukumu, ikiwamo mzigo wa madeni.
Katibu Mkuu aliyepita, David Jairo hakutafuna maneno aliposema hali ya Tanesco ni mbaya, mapato yake ya mwezi hayazidi Sh30 bilioni, wakati kwa siku inatumia Sh566 milioni kuwalipa Songas na IPTL.
Kwa mfano, mahitaji ya umeme kwa wateja wake ni Megawati 906, lakini uwezo wake ni kuzalisha 705 tu. Megawati hizo zinazalishwa kupitia mabwawa ya Kidatu (204), Kihansi (180), Mtera (80), Pangani (68), Hale (21) na Nyumba ya Mungu (8).
Umeme mwingine ni wa nguvu za mitambo iliyopo katika Vituo vya Tanesco vya Ubungo, Megawati 100 na Tegeta 45. Wakati uzalishaji wa umeme ni megawati 705, mahitaji ya Dar es Salaam pekee, ni Megawati 455. Profesa Muhongo ambaye ni waziri wa 21 katika wizara inayoongoza Tanesco, kwenye hotuba yake ya kwanza kwenye Bunge la Bajeti la mwaka jana, alizungumzia hoja ya kuinusuru Tanesco kwa kuipa ruzuku. Hata hivyo, msaada wa ruzuku ya Serikali kwa Tanesco umeonekana kutofua dafu.
Profesa Muhongo ameshawahi kukaririwa akitaka marekebisho makubwa katika shirika hilo, hoja ambayo inaungwa mkono na wananchi wengi. Kwa mfano, wananchi wa Wilaya ya Bunda, Mara wakizungumza kwenye mkutano wa wadau wa umeme walitamka bayana kuwa shirika hilo limezidiwa. Walisema limebeba mzigo mkubwa wa kuzalisha umeme, kuuza na kusambaza.
Ufanisi wa Tanesco umegubikwa na ‘umwinyi’ unaochangia kulidhoofisha, wateja wanaoomba kuunganishiwa umeme hawapewi huduma hiyo kwa wakati, kumekuwa na ulegevu wa ufuatiliaji madeni kwa wateja na hujuma nyingine zinafanywa na wafanyakazi wenyewe.
Kumekuwa na mianya mingi ya hujuma za mapato ya Tanesco, kumekuwa na tatizo la ‘vishoka’ wa kuunganisha umeme na wanaouza Luku na wote hao wana uhusiano na baadhi ya wafanyakazi wa Tanesco.
Pamoja na kuiona Tanesco kwamba imekuwa mzigo, bado kuna waliolifikisha shirika hilo hapo, Serikali na taasisi zake ni mojawapo na kwa kiasi kikubwa hawawezi kukwepa lawama.
Siyo siri, Serikali imekuwa mdaiwa mkubwa wa Tanesco na kutolipa hayo kumechangia kulidhoofisha shirika hilo kimapato.
Tunadhani kwamba hakuna haja ya kuendelea kuibebesha Tanesco mzigo wa kuzalisha umeme, kuuza na kusambaza. Ni wakati sasa kwa Serikali kulivunja shirika hilo ili kulipunguzia mzigo wa majukumu lakini pia kuongeza ufanisi kwa kuleta ushindani katika sekta ya nishati.
Wakati mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini ukiendelea bungeni, tungependa kuwashauri wabunge kuishauri Serikali kubadili muundo wa shirika hilo ili Watanzania wengi ambao ni zaidi ya milioni 40 waweze kunufaika na huduma ya umeme.

Bajeti Nishati kupoza kiu ya Wanamtwara?

Profesa Sospeter Muhongo 

Dodoma/Mtwara. Wakati mjadala mkali ukitarajiwa kuibuka bungeni leo wakati Serikali itakapokuwa ikiwasilisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini, joto limezidi kupanda mkoani Mtwara ikielezwa kuwa wananchi wamehamasishana kwa mara nyingine kuacha shughuli zote ili kusikiliza kama hotuba hiyo italinda masilahi yao.
Hotuba hiyo ambayo itasomwa leo mara baada ya kipindi cha maswali na majibu bungeni na Waziri wa wizara hiyo, Profesa Sospeter Muhongo, inatarajiwa kuibua mengi yakiwamo yanayohusu suala la gesi ya Mtwara.
Mjini Mtwara vipeperushi vinavyopingana vilisambazwa kuhamasishana ‘kuacha shughuli zao zote na kubaki nyumbani ili kufuatilia matangazo ya televisheni wakati Profesa Muhongo atakapotangaza bajeti hiyo, huku vingine vikipinga.
Ahadi za matumaini
Licha ya kampeni hizo za watu wa Mtwara, Serikali nayo imeweka matangazo katika vyombo vya habari likiwemo gazeti hili ikieleza namna mikoa ya Mtwara na Lindi itakavyonufaika na utafutaji na uendelezaji wa Gesi Asilia.
Tangazo lililotolewa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania limeainisha faida za gesi hiyo kwa Mkoa wa Mtwara ukiwamo umeme utakaotokana na gesi asilia. Pia imeelezwa jinsi mafunzo kwa vijana juu ya matatizo ya gesi asilia yaliyodhaminiwa na Wizara ya Nishati na Madini na kampuni mbalimbali kuanzia mwaka 2010.
Vilevile imeelezwa jinsi uboreshaji wa huduma za jamii kama ujenzi wa shule, hospitali na ujenzi wa viwanda kama kile cha saruji cha Dangote na mitambo ya kusafishia gesi utakavyowanufaisha wakazi wa mkoa huo.
Gesi hiyo ambayo pia inachimbwa katika Kisiwa cha Songosongo inatajwa kwamba itawanufaisha wakazi wa Mkoa wa Lindi kwa kupata umeme, kunufaika na kodi ya wawekezaji wa gesi na udhamini wa mafunzo kutoka kampuni mbalimbali na wizara.
Wiki iliyopita Profesa Muhongo alijigamba kuwa bajeti ya wizara yake atakayosoma leo itakuwa ya karne ya 22 itakayomaliza tatizo la umeme nchini kwa kuwa imetoa vipaumbele kwa sekta binafsi kusaidia upatikanaji wa umeme wa uhakika.
Wabunge wapania
Dalili za kuibuka mjadala mkali katika bajeti ya leo zilianza kujitokeza mwishoni mwa wiki wakati wa semina ya wabunge kuhusu masuala ya gesi ambapo wizara hiyo ilibanwa juu ya mambo ya mikataba.
Hata hivyo, semina hiyo ilitafsiriwa kuwa ililenga kuwapoza wabunge na kupunguza hasira zao huku wizara ikijipanga namna ya kuwashawishi waikubali bajeti baada ya kuona mwelekeo wao.
Wasiwasi Mtwara
Hali ya wasiwasi imeanza tena kutanda mkoani hapa hasa kutokana na vipeperushi vinavyokinzana na ujumbe tofauti kwa njia ya simu unaosambazwa.
Hali hiyo imejirudia tena huku ikionekana dhahiri kuwa na kauli kutoka makundi tofauti zinapishana katika vipeperushi hivyo huku wengine wakitaka mwendelezo wa kusitisha huduma ufanyike na wengine wakipinga.
Mojawapo ya kipeperushi kilisisitiza huduma zote zisitishwe kuanzia bajaji, bodaboda, masoko na magari yote yaendayo mikoani na wilayani yasiingie wala kutoka.
Huku vipeperushi vingine vikipinga: “Tunafahamu gesi ni mali yetu wote Wanakusini na tunafahamu kunyanyasika kwetu na Serikali ya nchi yetu na Mei 17 tuliunga mkono kufunga maduka na biashara zote, lakini hatukunufaika na chochote.
“Sasa Jumatano tena tusifanye biashara. Tuache ujinga Wanakusini wenzetu wengine hawana kazi wala gesi. Kampeni zitafanya tuwe maskini zaidi. Tarehe 22.05.2013 hatufungui duka wala hoteli, hata soko,” kilisomeka kimoja kati ya vipeperushi hivyo.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Linus Sinzumwa aliwataka wananchi waendelee na shughuli zao za kila siku bila kujali vitisho hivyo kwa kile alichokidai kuwa ulinzi umeimarishwa.
ya za Tandahimba, Masasi, Newala na Nanyumbu waliendelea na shughuli za uzalishaji bila bughudha


Wednesday, May 22

BUNGE lisitishwa jioni hii kutokana na hali tete ya mtwara



Spika ameahirishwa bunge hadi kesho kutokana na hali ya Mtwara. Spika kasema amepokea hali ya vurugu mtwara, hivyo bunge limeahirishwa ili kutoa fursa kwa kamati ya bunge kujadili suala hilo na serikali imetakiwa kutoa majibu katika kikao cha kesho.
Spika kasema kuwa wabunge wangependa kujadili hali ya Mtwara leo  lakini watajadili nini wakati hata wao wabunge wamepata taarifa hizo  kwenye vyombo vya habari? Hivyo, akaiagiza serikali kuleta majibu sahihi kesho bungeni na kuwaomba wabunge kuwa na subira hadi kesho na kisha akaahirisha bunge.
Akahitimisha kwa kusema kamati ya bunge inakwenda kujadili suala hilo sasa hivi.

Breaking News: Vurugu za Mtwara


Askari wanne na Wananchi Kadhaa Wameuawa. Hadi kufikia saa hii (3:00 pm) kuna taarifa kwamba ofisiza CCM (maeneo ya Mdenganamadi na Majengo) zimechomwa moto; askari wanne wameuawa pamoja na wananchi kadhaa. Wananchi wanatumia baruti za kulipulia samaki kuwalipua majengo na askari.Hatari iliyopo ni kuchomwa kwa jengo la ofisi za mkuu wa mkoa. Yote haya ni kupinga bomba la gesi kujengwa kuelekea DSM.
Habari zilizofika muda huu zinaripoti kwamba hali sio nzuri huko Mtwara, kwa ufupi hali ni tete na hakuna amani, mabomu ya machozi yanarindima muda huu na huduma zote za kijamii zimefunngwa hakuna usafiri, masoko, maduka na bar zote zimefungwa, daladala, Taxi na Bodaboda hazifanyi kazi. Kwa ujumla kinachoendelea ni mapambano makali kati ya Jeshi la polisi na wananchi wenye hasira wanaopinga vikali kuendelea kwa mchakato wa gesi ilihali nchi ikiwa haina sera inayosimamia nishati hiyo.
Kufuatia Kambi ya Upinzani kuukataa mpango wa serikali wa ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara Mpaka Dar es salaam ilihali Waziri wa Nishati akisoma hotuba yake kwa hisia kali na mbwembwe na kusema bomba la gesi linajengwa kutoka Mtwara kwenda Dar es salaam Wananchi wa Mtwara wacharuka!
Daraja la Mikindani limevunjwa hakuna mawasiliano Mtwara na Dar es salaam.
Baadhi ya Wananchi wamepora Silaha na wanazitumia kujibu mashambulizi ya Jeshi la Polisi (habari haijathibitishwa rasmi)
Jengo la Ofisi ya CCM saba saba limechomwa moto.
Nyumba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, (Tamisemi), Hawa Ghasia yachomwa moto.
Lodge/Hotel (Shengena) inayoaminika kwamba ndiyo waliyofikia Askari wa Jeshi la Polisi (FFU) kutoka mikoa ya jirani kwaajili ya operation inayoendelea imechomwa moto.
Milio ya risasi na mabomu ndicho kinachosikika.
Nyumba kadhaa za watumishi wa Serikali zimechomwa maeneo ya Shangani. (habari haijathibitishwa rasmi)
Ni magari ya FFU ndio yaliyopo barabarani nayo yanapata wakati mgumu kupita kwasababu ya mawe na magogo makubwa yaliyowekwa na Wananchi.
Askari kadhaa wamekufa (habari hii haijathibitishwa rasmi)
Baadhi ya watu kadhaa wamechukuliwa na askari kwakuwa wamepita jirani na gari yao.
Yadaiwa askari wengi waliokuja si wa Mtwara, wengi wametoka Masasi na Lindi.
Ving'ora vinalia hovyo. Watoto wamefungiwa mashuleni walimu wamekimbia.
Vituo vya Redio vya Mtwara havizungumzii hali hii ya hatari bali vinapiga Muziki pengine vinakusanya matukio na habari ya majanga haya ili Wananchi wayapate.
Mabomu yanapigwa mfululizo maeneo ya Magomeni-Mtwara, mpaka sasa takriban mabomu 20 na ushee yameshapigwa.
Wakati waziri wa Nishati akisoma hotuba yake kwa hisia kali na mbwembwe na kusema bomba la gesi linajengwa kutoka Mtwara kwenda Dar Kauli mbiu ya Wananchi wa Mtwara ni "Gesi haitoki hata kwa bomba la peni"
Wananchi walalamikia kituo cha Television na Radio TBC kuzuia na kukata mawimbi yake kutoonekana wala kusikika katika Mkoa wa Mtwara kwa muda. Hatimaye hivi Punde matangazo yarejea.
Hili linaendelea wakati bajeti ya nishati na madini ikiendelea kujadiliwa muda huu Bungeni.

Bandari D’Salaam yapoteza Sh3 trilioni kwa mwaka


Dar es Salaam. Bandari ya Dar es Salaam imekuwa ikilikosesha taifa Dola 1.8 bilioni za Marekani (Sh2.8 trilioni) kwa mwaka, kutokana na kukosa ubora wa biashara.
Kutokana na hali hiyo, wataalamu wameeleza kuwa bandari hiyo inahitaji kufanyiwa maboresho muhimu ya hali ya juu, ili fedha hizo zisaidie nchi kuacha kutegemea misaada ya maendeleo.
Kwa mujibu wa ripoti iliyopo kwenye kitabu cha Opening the Gates: How the port of Dar es Salaam can transform Tanzania, licha ya Bandari ya Dar es Salaam kuwa sehemu nzuri, imekosa uwezo hivyo usimamiaji sera bora za kuiboresha zinatekelezwa taratibu. Ripoti hiyo inaeleza kuwa, mwaka 2012 pekee bandari hiyo ilikosesha taifa kiasi hicho cha fedha, huku ikizikosesha nchi jirani Sh1.3 trilioni.


“Fedha hizo ni sawa na asilimia saba ya pato la taifa, kitu ambacho kinawaathiri wanunuzi, wafanyabiashara na wakala mbalimbali wa Serikali,” inaeleza.
Mchumi Mkuu wa Benki ya Dunia (WB), Jacques Morisset ameihimiza Tanzania kuifanya bandari hiyo kuwa moja ya vipaumbele vyake vya juu kwa ajili ya kukua kwa uchumi.
“Watumiaji Bandari ya Dar es Salaam wanalipa fedha nyingi kwa wasimamizi wa bandari na wakala mbalimbali, kwa ajili ya huduma zao kuliko Mombasa,” alisema Morisset.
Akizungumzia ripoti hiyo, Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe alisema Serikali imekuwa ikijitahidi kuboresha bandari hiyo, lakini kazi ya ziada inahitajika kuifanya iweze kushindana na nyingine.


“Tunahitaji nchi jirani ziendelee kuitumia bandari yetu, bado tuna kazi kubwa ya kufanya ndiyo maana niko hapa, tunahitaji kuimarisha Kitengo cha Operesheni na maeneo mengine,” alisema Dk Mwakyembe.

Maalim Seif: Nitaomba kuwania tena urais mwaka 2015

Dar es Salaam. Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharrif Hamad amesema ataomba tena kugombea urais kupitia Chama cha Wananchi (CUF) katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Akizungumza katika kipindi cha Dakika 45 kinachorushwa na kituo cha runinga cha ITV, Maalim Seif alisema kuwa anachoomba tu Mwenyezi Mungu ampe afya njema.
“Ni uamuzi wa wananchi na wanachama wenyewe wa CUF lakini kama Mwenyezi Mungu akinipa afya na uzima bado nia ipo,” alisema Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.
Alisema hivi sasa chama hicho kimekuwa kikijiimarisha visiwani huko kwa kufanya mikutano Pemba na Unguja ili kuhakikisha kinaendelea kukubalika kwa wananchi.
Kauli hiyo ya Maalim Seif ambaye amekuwa akiwania nafasi hiyo tangu kuingia kwa mfumo wa vyama vingi, ilipokewa kwa hisia tofauti ambapo Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Bashiru Ali alisema vyama vya siasa ni lazima viwe vinatayarisha viongozi wa baadaye ambao watafahamu kwamba uongozi ni dhamana wanayopewa na wananchi.
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro alisema Maalim Seif kama mwanachama wa chama hicho anaruhusiwa kwa mujibu wa Katiba kugombea nafasi yoyote ya uongozi wa dola.

UJIO WA RAIS OBAMA NCHINI TANZANIA

Rais wa Marekani Bw. Baraka Obama na Mkewe wanatarajia kufanya ziara ya nchi tatu barani Afrika itakayojumuisha nchi za Senegal, Afrika ya Kusini na Tanzania, Kuanzia tarehe 26 Juni hadi tarehe 3 Julai.

Katika ziara yake hiyo, Rais atawekea mkazo umuhimu ambao Marekani inauweka katika ushirikiano wetu wa kina na unaoendelea kuimarika na nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara kupitia mipango mbalimbali ikiwemo ile ya kuimarisha ukuaji wa uchumi, uwekezaji na biashara, uimarishaji wa taasisi za kidemokrasia na uwekezaji katika kizazi kipya cha viongozi wa Kiafrika.

Rais atakutana na viongozi mbalimbali wa kiserikali, sekta binafsi na jumuiya huru ya kiraia ikiwemo vijana ili kujadili ubia wetu wa kimkakati katika ushirikano wetu rasmi na masuala mengine ya kimataifa.

Ziara hii itadhihirisha dhamira ya dhati ya Rais ya kupanua na kuimarisha ushirikiano kati ya Marekani na watu wa nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara katika kuimarisha amani na ustawi katika kanda hii na duniani kote kwa ujumla

Lissu abadili mbinu uzinduzi kampeni

Mbunge wa Same Mashariki (CCM), Anna Kilango akizozana na mnadhumu wa kambi ya upinzani, Tundu Lissu nje ya ukumbi wa Bunge jana baada ya Spika kuahirisha Bunge akiagiza hotuba ya kambi ya upinzani kuhusu Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kufanyiwa marekebisho.Picha na Emmanuel Herman 

Ikungi. Mgeni rasmi katika uzinduzi wa kampeni ya uzinduzi wa nafasi ya udiwani Kata ya Iseke Tarafa ya Ihanja, Wilaya ya Ikungi, Tundu Lissu, juzi alishindwa kuuza sera za Chadema, na badala yake alitumia muda mwingi kuhimiza ‘sera ya kuwakataza’ wananchi kuchangia maendeleo yao .
Tundu ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki kupitia chama hicho, alipanda jukwaani huku akiwa amebeba makabrasha ya michanganuo ya Bajeti ya Serikali ya kuanzia mwaka wa fedha wa 2010/11 hadi 2013/14.

“Mimi leo sitaki kabisa kuzungumzia habari za Amosi Mghenyi ambaye ametusaliti kwa kuhama Chadema na kurejea CCM. Amosi kisiasa ni mfu, kwa hiyo siwezi kupoteza muda wangu kuzungumiza mambo ya mfu”,alisema na kushangiliwa kwa nguvu na wananchi waliohudhuria uzinduzi huo uliofanyika katika kijiji cha iseke.
Alisema ufunguzi wake utajikita zaidi katika kuwaelimisha wananchi wa Kata ya Iseke kwamba Serikali inazo fedha nyingi na za kutosha kugharamia maendeleo ya wananchi.
Akijenga hoja yake hiyo, alisema kwa mfano katika mwaka wa fedha wa mwaka 2010/11, Mkoa wa Singida, ulipewa zaidi ya Sh903 milioni za undeshaji wa shule, lakini zilizotumika ni Sh464 milioni na kubaki Sh438.2.
Alisema fedha hizo zaidi ya Sh438.2 milioni zilizobaki, hazijaainishwa zilipelekwa wapi. “Kwa vyo vyote zitakuwa zimeishia kwenye matumbo ya mgambo na watendaji wa Serikali ya CCM”.
Lissu ambaye pia ni mwanasheria kitaaluma, aliwataka wakazi wa Kata ya Iseke, kumchagua Emmnuel Jackson Jingu awe diwani wao.
ili waondokane na manyanyaso ya michango kama walivyojikomboa wakazi wa Jimbo la Singida Mashariki.
Wagombea wengine wa nafasi ya udiwani Kata ya Iseke, ni Amosi Munghenyi wa CCM na Abdallah Kinyenje maarufu kwa jina la Petro wa CUF.

JK: Lowasa jembe


Dodoma/Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete amemwagia sifa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa hatua ambayo inaweza kutafsiri mengi katika medani ya siasa nchini.
Akizungumza na wabunge wa CCM kwenye Ukumbi wa White House Dodoma juzi, Rais Kikwete ambaye pia mwenyekiti wa chama hicho, alisema nguvu za Lowassa pekee zinatosha kushinda uchaguzi mdogo wa kiti cha udiwani Kata ya Makuyuni kilichoko wilayani Monduli.
Kata ya Makuyuni iko wilayani Monduli, ambako Lowassa amekuwa mbunge wake tangu mwaka 1995.
Habari za kutoka ndani ya kikao hicho zinaeleza kuwa Rais Kikwete alitoa kauli hiyo kuhusu kampeni za uchaguzi huo wa Makuyuni, baada ya kuwa ametoa ruksa kwa makada wa chama hicho wanaotaka urais kuanza kujipitisha pitisha miongoni mwa wanachama wa chama hicho. Lowassa anatajwa kuwa miongoni mwa wanaCCM wanaotaka kumrithi Rais Kikwete kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.
“Sina tatizo na pale Makuyuni, najua muscles (misuli) za Mzee Lowassa zinatosha kutupa ushindi; au vipi mzee?” alidokeza mmoja wa wabunge wa CCM akimnukuu Rais Kikwete.
Uchaguzi wa Udiwani Kata ya Makuyuni unaotarajiwa kufanyika Juni 16, mwaka huu, utakuwa wa ushindani mkali kati ya CCM na Chadema ambao historia yao kisiasa mkoani Arusha ni ya uhasama.
Katika uchaguzi huo, unaofanyika baada ya kifo cha Abdillah Warsama (CCM), chama hicho kitatetea nafasi yake kwa kumsimamisha Godluck Lerunya na Chadema ni Japhet Sironga.
Mbali na Kata ya Makuyuni, uchaguzi wa udiwani mkoani Arusha utafanyika pia katika Kata za Kaloleni, Themi, Kimandolu na Elerai, kutokana na waliokuwa madiwani wa kata hizo (Chadema), kufukuzwa na chama chao.
“Mnaweza kuchafuana leo, kesho mkapata mgombea mwenye nundu nyingi na mabandeji kila mahala, halafu mkapata shida kumnadi,” alisema.
Siyo mara ya kwanza kwa Kikwete kumsifia Lowassa kwani aliwahi kufanya hivyo mwaka jana huko Longido wakati akikabidhi ng’ombe.
Pia aliwahi kumsifia wakati wa kampeni za uchaguzi za mwaka 2010 wakati Kikwete alipomwelezea Lowassa kama Mbunge makini na kuwaomba watu wa Monduli kumchagua tena.
Hata hivyo, alipoulizwa kama baada ya kuruhusiwa kuanza kujipitisha kwa wanaCCM kama anataka kuwania urais, Lowassa alijibu kupitia watu wake wa karibuni kuwa asingependa kuzungumzia suala hilo hasa baada ya Rais kutoa kauli hiyo.
Kutangaza nia ruksa
Rais Kikwete aliwaeleza wabunge hao kuwa si kosa kwa watu kutangaza nia ya kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ikiwamo urais mwaka 2015.
“Wabunge na mawaziri wenye nia ya kutangaza nia ya kugombea urais wawe huru, kwani hiyo ni haki yao, isipokuwa wafanye kwa wema bila kukivuruga chama na kuwagawa wanaCCM katika makundi. Sioni tatizo watu kujipitisha. Sisi sote hapa tulijipitisha. Lakini tufanye hivyo kistaarabu bila kuvurugana.”
Aliwaagiza wabunge wa chama hicho kwenda majimboni mwao kusikiliza kero za wananchi badala ya kusubiri wakati wa uchaguzi.
Membe
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ambaye naye anatajwa kuwa miongoni mwa wagombea amewataka waandishi waache kuandika kila siku habari za urais na badala yake waandike mambo ya maendeleo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana baada ya kukutana na mabalozi wa nchi zinazoendelea kuhusu Mkutano wa Smart Partnership, unaotarajiwa kufanyika nchini, Membe alisema ni vizuri yakaandikwa mambo ya maendeleo na si kila wakati kuandika mambo ya urais.
“Mkutano kama huu nchi kama Kenya watauripoti vizuri na kwa undani hivyo mfanye hivyo si kila kitu urais 2015,” alisema Membe. Mkutano huo utaanza Mei 28, hadi Juni Mosi na utajadili jinsi gani sayansi na teknolojia vinaweza kutumika kuzikwamua kiuchumi.
Imeandikwa na Kizitto Noya, Habel Chidawali na Boniface Meena.

Tuesday, May 21

hotuba ya SUGU bungeni


Hotuba ya upinzani yaahirisha Bunge


Dodoma. Mjadala wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo jana uliingia dosari na kulazimika kusitishwa kwa muda baada ya Bunge kukubaliana na hoja ya Mbunge wa Mbozi Magharibi (CCM), Godfrey Zambi kuwa Hotuba ya Kambi ya Upinzani, imejaa uchochezi.
Zambi alitoa hoja hiyo wakati Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi alipokuwa akiwasilisha hotuba ya Kambi ya Upinzani kuhusu makadirio hayo, baada ya kuomba mwongozo wa Spika.
“Kuhusu utaratibu,” alisema Zambi. Baada ya kurudia kauli hiyo mara kadhaa, Spika wa Bunge, Anne Makinda alimsitisha Mbilinyi kuendelea na hotuba yake na kumpa Zambi nafasi.
“Mheshimiwa Spika, hotuba hii ya upinzani ni ya uchochezi. Sisi kama Bunge hatuwezi kuruhusu ikaendelea kusomwa hapa na Watanzania wakasikiliza uongo. Kuanzia ukurasa wa kwanza hadi wa 14, imejaa uongo tu,” alisema Zambi na kuongeza:
“Kusema kwamba Tanzania inawatesa waandishi wa habari kwa kuwang’oa meno na kucha, siyo kweli. Huu ni uchochezi na ningependa kutoa hoja hotuba hiyo iondolewe bungeni, ni ya kichochezi.”
Baada ya kutoa hoja hiyo, karibu wabunge wote wa CCM walisimama kumuunga mkono na baadaye, Spika wa Bunge Anne Makinda alisimama na kusema: “Naomba wote mkae chini... kwanza kaeni,” kisha aliendelea: “Humu humu bungeni, sisi wenyewe, tulipitisha kanuni kwamba tusiingize neno uchochezi kwenye mijadala yetu. Haya, sasa naahirisha kikao mpaka jioni na naagiza Kamati ya Kanuni iende ikapitie hotuba hiyo kwanza kabla haijaletwa tena bungeni.”
Nje ya Bunge
Wakiwa wanatoka bungeni, mvutano ulioanzia ndani ya ukumbi, uliibuka nje ya lango kuu la Bunge ambako wabunge kadhaa wa CCM na Chadema waliendeleza mjadala huo na kuzozana hadharani.
Wabunge waliozozana kuhusu hotuba hiyo nje ya ukumbi ni Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani bungeni, Tundu Lissu, Mbunge wa Same Mashariki (CCM), Anna Kilango, Mbunge wa Tabora Mjini (CCM), Ismail Aden Rage na Lucy Kihwelu (Viti Maalumu Chadema).
“Hamuwezi mkaharibu kanuni za Bunge letu kwa hotuba zenu za uchochezi,” alisema Kilango akimwambia Lissu.
“Hiyo kanuni ni ipi ambayo tumeiharibu? Huo ni ukorofi wenu tu, tunafahamu siku nyingi,” alijibu Lissu.
Baadaye akadakia Rage; “Hawa dawa yao ni .....” Kauli hiyo ya Rage ilijibiwa na Kihwelu aliyemwambia “Makofi yako ni Yanga tu. Umesahau umepigwa mabao 2-0.”
Mbilinyi atetea hotuba yake
Akizungumza na waandishi wa habari nje ya Ukumbi wa Bunge, Mbilinyi alitetea hotuba yake akisema kuwa haina tatizo lolote na imefuata kanuni zote za kusomwa bungeni.
“Hili kwetu (Chadema) ni changamoto, ila niseme tu kwamba hotuba yangu haikuwa na tatizo lolote na ilipitia hatua zote halali kabla ya kusomwa bungeni,” alisema.
Utaratibu uliowekwa na Bunge unataka hotuba za hoja za bajeti kuwasilishwa kwa Spika siku mbili kabla ya kusomwa.
Alisema hotuba hiyo haina chembe ya uongo, akisema ni ukweli kwamba waandishi nchini hawana uhuru wa kufanya kazi na baadhi wanateswa na kunyanyaswa.
Baadaye jioni
Katika kikao cha jioni, Spika Makinda alitoa mwongozo wake na kueleza sababu za kuahirisha hotuba ya Mbilinyi na kusema anakubaliana na hoja iliyokuwa imetolewa asubuhi na Zambi kwamba maneno yaliyopo katika hotuba ya Mbilinyi kuanzia ukurasa wa kwanza hadi wa 14 yaondolewe kwa kuwa yanaingilia Mahakama.
“Kwa kutumia Kanuni ya 72 ni mamlaka ya Spika kusimamia Bunge hivyo kwa kutumia Kanuni ya 64, naagiza maneno yote yanayozungumzia mauaji ya Daudi Mwangosi yaondolewe,” alisema Spika Makinda.
Alisema amefikia uamuzi huo baada ya Kamati ya Kanuni kupitia hotuba hiyo na kuona kwamba maneno yaliyopo katika kurasa hizo yanaingilia mhimili wa mahakama.
Baada ya Spika kueleza hayo, Mbilinyi aliruhusiwa kuendelea na hotuba yake na kuomba kuanzia jana jina la Sugu lisitumike tena bungeni.

SPIKA WA BUNGE AAMURU KUFUTWA KWA HOTUBA YA SUGU ILIYOSABABISHA BUNGE LISITISHWE ASUBUHI




Spika wa Bunge la Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mh Anne Makinda, ameamuru kambi ya upinzani kuyaondoa maneno yote yaliyomo kuanzia ukurasa wa kwanza mpaka wa 14 katika hotuba rasmi ya Kambi ya upinzani iliyosmwa na mbunge wa Mbeya Mjini, Mh. Joseph Mbilinyi ‘Sugu,’ ambaye ni Waziri Kivuli wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo.

Mh. Makinda ametoa amri hiyo baada ya Kamati ya Kanuni ya Bunge kujadili hotuba hiyo na kubaini kuwa ina kauli za uchochezi; na kusema kuwa kuwa Bunge sio sehemu kugombanisha wananchi, hivyo maneno yote ya uchochezi hayaruhusiwi.

Katika hotuba hiyo, Mh. Mbilinyi aliishutumu serikali kuhusika na kuteka nyara waandishi wa habari, kauli iliyopelekea Spika Makinda kuahirisha Bunge.

Monday, April 15

Mbowe, Slaa: Hatukubali Chadema kuhujumiwa

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe akizungumza kwenye kongamano la chama hicho lililofanyika jana jijini Dar es Salaam. Picha na Fidelis Felix.

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa wamesema “hawatakubali wala kuvumilia” hujuma dhidi ya chama chao.
Dar es Salaam. Viongozi hao kwa nyakati tofauti jana walisema hujuma hizo zimekuwa zikifanywa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na Serikali ambayo imekuwa ikitumia vyombo vya dola na kwamba sasa wanapanga ugaidi wa kuwateka maofisa wa ngazi ya juu wa Chadema.
Suala la ugaidi liliibuka kwa nguvu katika wiki ya kwanza ya Bunge la Bajeti na sasa limehamia nje ya chombo hicho cha kutunga sheria kutokana na Chadema kuwatuhumu CCM na Serikali yake kwamba wanapanga njama za kuwateka maofisa wakuu wa chama hicho.
Jana Dk Slaa alipokuwa akimkaribisha Mbowe kufungua Mkutano wa Mafunzo na Mipango ya Vuguvugu la Mabadiliko ‘M4C’ na Kongamano la Katiba Mpya kwa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani, alisema taarifa walizonazo zinaonyesha kuwa CCM ndiyo wanaofanya vitendo vya kigaidi wakishirikiana na Serikali.
“Tuna taarifa zote zinazoonyesha kwamba CCM ndiyo magaidi wakishirikiana na Serikali yake, lakini sisi tuko makini kuliko hata Serikali ya CCM na tuko makini kuliko hata Usalama wa Taifa na umakini huu ndiyo utakaotupeleka Ikulu mwaka 2015,”alisema Dk Slaa.
Hata hivyo Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipotafutwa kujibu tuhuma hizo alisema hakuna jipya ambalo Chadema wamelisema.
“Kuna jipya katika hilo, ni yale yale ya kawaida na jana (juzi) Mwingulu alizungumza vizuri sana bungeni. Hiyo ni sawa na mchawi anapomwangia mtu na kufa anakuwa wa kwanza kwenda kulia msibani, nchi siku yoyotete haijengwi kwa ngonjera za maneno bali inajengwa kwa mipango,”alisema Nape.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Pereira Ame Silima alipotakiwa kutoa msimamo wa Serikali juu ya tuhuma hizo alisema, “Mimi siwezi kuzungumza ila mtafute Waziri (Dk Emmanuel Nchimbi),”alisema Silima.
Alipotafutwa Dk Nchimbi kupitia simu yake ya mkononi, ilikuwa ikiita bila kupokewa.
Kauli ya Mbowe
Kwa upande wake Mbowe alisema, CCM imekuwa ikitumia mbinu mbalimbali kuhakikisha inakisambaratisha chama hicho bila mafanikio.
“Watu wa Usalama wa Taifa wakishirikiana na CCM wamekuwa wakifanya mipango ya kutaka kuwateka maofisa wetu. Hawa watu ni wepesi sana na msiwaogope hata kidogo,”alisema Mbowe huku akishangiliwa na wanachama na makada waliofurika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Blue Pearl.
Mbowe alisema: “Ukiona chama chochote tawala kinatumia jeshi la polisi kutengeneza ushahidi wowote wa kihalifu hiyo ni dalili ya hatari kwa mustakabali wa usalama wa nchi.”
Mbowe alisema mbinu za sasa za CCM zinatokana na kushindwa kukivuruga chama hicho kwa propaganda kuwa ni chama cha familia, ukabila, ukanda na baadaye udini.
Katiba na Elimu
Kuhusu mchakato wa Katiba Mpya, Mbowe alisema ikiwa itafika Aprili 30 mwaka huu bila hatua zozote kuchukuliwa, watamwamuru mjumbe wa tume hiyo kutoka Chadema, Profesa Mwesiga Baregu kujiondoa.
Chadema kinataka Serikali iwasilishe bungeni, muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Katiba ili yafanywe marekebisho mbalimbali kuhusu uwakilishi katika Bunge Maalumu la Katiba.
“Serikali inaona hili kama mchezo, sasa acha wakae kimya na baada ya Aprili 30 mwaka huu watachagua kusuka au kunyoa,”alisema Mbowe.
Kuhusu elimu, Mbowe alieleza kushangazwa na kile alichosema kuwa ni Serikali kutofahamu sababu za wanafunzi kufanya vibaya katika mitihani yao.
“Serikali eti haijui na kama haijui basi Waziri Mkuu (Mizengo Pinda) hatakiwi kuwa hapo alipo, kwani haiwezekani watoto wanafeli halafu anaunda tume,”alisema Mbowe na kuongeza:
“Mwaka 2011 waliunda tume ambayo ilitoa mapendekezo 27 lakini ripoti hiyo ilifichwa hadi mimi juzi (Jumatano) nilipoisoma bungeni wabunge wa CCM wakabaki vichwa chini.”
Alisema kuundwa kwa tume nyingine ambayo itatumia fedha za walipakodi ni kuwaumiza Watanzania ilhali tatizo na chanzo kinajulikana.
Ugaidi bungeni
Juzi wakati wa mjadala wa Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, wabunge wa CCM na Chadema kwa nyakati tofauti walituhumiana kwa ugaidi kiasi cha kusababisha vurugu na kutoelewana miongoni mwao.
Alhamisi akisoma maoni ya Kambi ya Upinzani, Mbowe alisema ugaidi ni ubunifu wa polisi na Serikali kwa ajili ya kuwabambikia kesi zisizo na dhamana kwenye mahakama maofisa wa vyama vya upinzani.
Kutokana na hotuba hiyo, Mbunge wa Iramba Magharibi (CCM), Mwigulu Nchemba aliishambulia hotuba ya Mbowe akieleza kuwa wanahusika kupanga kumdhuru mwandishi wa habari.

ADHANA YARUHUSIWA SWEDEN KWA MARA YA KWANZA

Msikiti mmoja katika kitongoji cha mji mkuu wa Sweden, Stockholm umeruhusiwa kuadhini kwa kutumia kipaza sauti kilicho kwenye mnara kwa ajili ya Sala ya Ijumaa.

Hii ni mara kwa kwanza kwa nchi hiyo ya Scandinavia kuruhusu adhana kwa sauti inayosikika nje ya msikiti.

Idara ya polisi mjini Stockholm imesema msikiti huo utaruhusiwa kuadhini kwa muda wa kati ya dakika tatu na tano katika kipindi cha baina ya saa sita na saa saba mchana kila Ijumaa.

Mkuu wa Jumuiya ya Utamaduni wa Kiislamu katika eneo la Botkyrka kusini mwa Stockholm Bw. Ismail Okur ameupongeza uamuzi huo. Ombi la kuadhini kwa sauti inayotoka nje ya msikiti liliwasilishwa miaka mitano iliyopita.

Kuna karibu Waislamu 7,000 katika eneo hilo na aghalabu wana asili ya Uturuki.

Chama chenye chuki dhidi ya Uislamu cha Sweden Democrats kimepinga uamuzi huo.

Katika miaka ya hivi karibuni, idadi ya Waislamu barani Ulaya imeongezeka kwa kasi na sambamba na hilo hitajio la misikiti pia limeongezeka. Waislamu raia wa nchi za Ulaya wamekuwa wakibaguliwa kwa muda mrefu na sasa wanapigania haki sawa na raia wengine wa Ulaya.

Saturday, April 13

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo by zittokabwe

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ametoa taarifa yake ya mwaka 2011/2012 na kuonyesha kuwa kuna skandali kubwa sana katika akaunti ya Deni la Taifa. Nanukuu

‘Uhakiki wa mchanganuo wa madeni ya Taifa kama ulivyokuwa tarehe 30 Juni, 2012 ulibaini kuwepo kwa marekebisho ya deni ya shilingi 619,803,554,183.91 ambayo uongozi haukuweza kutoa maelezo ya kuridhisha.’ (Taarifa ya CAG, Ripoti ya Serikali Kuu 2011/2012 uk 158). Mwisho wa Kunukuu

Katika Taarifa yake hiyo CAG anaendelea kuonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kukua na mwaka unaoishia mwezi Juni 2012 deni lilikuwa kwa asilimia 17 kutoka mwaka unaoishia mwezi Juni 2011.

Kukosekana kwa maelezo ya kuridhisha kuhusu zaidi ya nusu trilioni za Deni la Taifa ni jambo linalopaswa kutiliwa mashaka makubwa, kuchunguzwa na kupata majawabu stahiki. Tafiti mbalimbali duniani zinaonyesha kuwa kuna mahusiano makubwa sana kati ya Deni la Taifa la utoroshaji wa fedha kwenda kwenye mabenki ya ‘offshore’. Katika kitabu cha ‘Africa’s Odious Debts: How Foreign Loans and Capital flight bled a continent’ kilichoandikwa mabwana Leonce Ndikumana na James Boyce imeonekana kwamba Deni la Taifa huchochea utoroshwaji wa Fedha kwenda kuficha nje ya Tanzania.

Mabilioni haya kwenye akaunti ya Deni la Taifa yanashtusha sana. Kambi ya Upinzani Bungeni kwa miaka miwili mfululizo imekuwa ikitaka ukaguzi maalumu kwenye akaunti za Deni la Taifa lakini Serikali imeshindwa kufanya hivyo. Nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya PAC pia nimemtaka CAG afanye ukaguzi huu maalumu.

Kambi ya upinzani Bungeni ilisema hivi katika Bajeti yake kivuli 2012/13:

DENI LA TAIFA

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasikitika kwa serikali kuendelea kutengeneza madeni kwa Taifa kwa kuendelea kukopa zaidi kwa matumizi ya kawaida ya serikali. Wakati Serikali inasisitiza kwamba Deni letu linastahmilika, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali anaonyesha mashaka makubwa sana kutokana na kasi ya kukua kwa Deni la Taifa. Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kuongezeka kwa asilimia 38% kutoka shilingi trillion 10.5 mwaka 2009/2010 hadi shilingi trillion 14.4 mwaka 2010/2011. Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha Deni la Taifa limefikia shilingi trillion 20.3 mpaka ilipofika mwezi Machi mwaka 2012. Ukisoma taarifa ya Mwezi wa Mei 2012 ya Benki Kuu ya Tanzania, Deni la Taifa sasa limefikia shilingi trillion 22.

Mheshimiwa Spika, Suala hapa sio ustahmilivu wa Deni kama inavyodai Serikali bali ni kwamba tunakopa kufanyia nini? Bajeti ya Mwaka 2012/13 inayopendekezwa inaonyesha kwamba Serikali itakusanya shilingi trilioni 8.7 kama makusanyo ya ndani na itatumia shilingi trilioni 10.6 kama matumizi ya kawaida. Ni dhahiri kwamba sehemu ya mikopo ambayo serikali inachukua sasa itakwenda kwenye matumizi ya kawaida. Hatutaki mikopo kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya posho, kusafiri, magari nk. Tuchukue mikopo kuwekeza kwenye miradi itakayokuza uchumi na kuzalisha kodi zaidi. Bajeti inaonyesha kwamba Serikali itakopa shilingi takribani trillion 5 mwaka 2012/13. Serikali ikubalikutekeleza mapendekezoya Kambi ya Upinzani ya kuimarisha ukusanyaji wa kodi na kupanua wigo wa kodi katika maeneo muhimu kama sekta ya madini na mawasiliano, kuzuia misamaha ya kodi, kutokomeza ukwepaji kodi, na kuepuka matumizi mabaya ili kuepuka madeni yasiyo ya lazima.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inapenda kusisitiza kwamba Bunge lifanye ukaguzi maalumu kuhusu akaunti ya Deni la Taifa ili kuweza kubaini ukweli kuhusu ustahmilivu wa Deni na mikopo ambayo Serikali inachukua kama inakwenda kwenye Maendeleo na miradi ipi na kama miradi hiyo ina tija. Vilevile tumependekeza kwamba Mikopo yote ambayo Serikali inachukua iwe inapata idhini ya Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi au Bunge litunge sharia ili kiwango cha juu cha kukopa ambacho Serikali haipaswi kuvuka. Kuiacha Serikali inaendelea kukopa bila mpango ni kuliweka Taifa rehani na kupeleka mzigo wa kulipa madeni haya kwa kizazi kijacho. Hatuwezi kukubali Wazee wetu waishi maisha yao, waishi maisha yetu na pia wakope maisha ya watoto wetu. Mwisho wa kunukuu.

Kambi ya Upinzani inarejea kutaka ukaguzi maalumu kuhusu akaunti za Deni la Taifa na maelezo ya kina ya Serikali kuhusu shilingi 620 bilioni ambazo hazina maelezo kwenye Deni la Taifa. Hatuwezi kukaa kimya kuona Watanzania wanabebeshwa madeni ambayo kimsingi ni madeni bandia yanayotajirisha watu wachache wenye uwezo na ujasiri mkubwa wa kuiba, kupora nakufisidi hazina ya Taifa letu.

Kabwe Zuberi Zitto,Mb

Waziri Kivuli Fedha na Uchumi

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo by zittokabwe

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ametoa taarifa yake ya mwaka 2011/2012 na kuonyesha kuwa kuna skandali kubwa sana katika akaunti ya Deni la Taifa. Nanukuu

‘Uhakiki wa mchanganuo wa madeni ya Taifa kama ulivyokuwa tarehe 30 Juni, 2012 ulibaini kuwepo kwa marekebisho ya deni ya shilingi 619,803,554,183.91 ambayo uongozi haukuweza kutoa maelezo ya kuridhisha.’ (Taarifa ya CAG, Ripoti ya Serikali Kuu 2011/2012 uk 158). Mwisho wa Kunukuu

Katika Taarifa yake hiyo CAG anaendelea kuonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kukua na mwaka unaoishia mwezi Juni 2012 deni lilikuwa kwa asilimia 17 kutoka mwaka unaoishia mwezi Juni 2011.

Kukosekana kwa maelezo ya kuridhisha kuhusu zaidi ya nusu trilioni za Deni la Taifa ni jambo linalopaswa kutiliwa mashaka makubwa, kuchunguzwa na kupata majawabu stahiki. Tafiti mbalimbali duniani zinaonyesha kuwa kuna mahusiano makubwa sana kati ya Deni la Taifa la utoroshaji wa fedha kwenda kwenye mabenki ya ‘offshore’. Katika kitabu cha ‘Africa’s Odious Debts: How Foreign Loans and Capital flight bled a continent’ kilichoandikwa mabwana Leonce Ndikumana na James Boyce imeonekana kwamba Deni la Taifa huchochea utoroshwaji wa Fedha kwenda kuficha nje ya Tanzania.

Mabilioni haya kwenye akaunti ya Deni la Taifa yanashtusha sana. Kambi ya Upinzani Bungeni kwa miaka miwili mfululizo imekuwa ikitaka ukaguzi maalumu kwenye akaunti za Deni la Taifa lakini Serikali imeshindwa kufanya hivyo. Nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya PAC pia nimemtaka CAG afanye ukaguzi huu maalumu.

Kambi ya upinzani Bungeni ilisema hivi katika Bajeti yake kivuli 2012/13:

DENI LA TAIFA

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasikitika kwa serikali kuendelea kutengeneza madeni kwa Taifa kwa kuendelea kukopa zaidi kwa matumizi ya kawaida ya serikali. Wakati Serikali inasisitiza kwamba Deni letu linastahmilika, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali anaonyesha mashaka makubwa sana kutokana na kasi ya kukua kwa Deni la Taifa. Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kuongezeka kwa asilimia 38% kutoka shilingi trillion 10.5 mwaka 2009/2010 hadi shilingi trillion 14.4 mwaka 2010/2011. Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha Deni la Taifa limefikia shilingi trillion 20.3 mpaka ilipofika mwezi Machi mwaka 2012. Ukisoma taarifa ya Mwezi wa Mei 2012 ya Benki Kuu ya Tanzania, Deni la Taifa sasa limefikia shilingi trillion 22.

Mheshimiwa Spika, Suala hapa sio ustahmilivu wa Deni kama inavyodai Serikali bali ni kwamba tunakopa kufanyia nini? Bajeti ya Mwaka 2012/13 inayopendekezwa inaonyesha kwamba Serikali itakusanya shilingi trilioni 8.7 kama makusanyo ya ndani na itatumia shilingi trilioni 10.6 kama matumizi ya kawaida. Ni dhahiri kwamba sehemu ya mikopo ambayo serikali inachukua sasa itakwenda kwenye matumizi ya kawaida. Hatutaki mikopo kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya posho, kusafiri, magari nk. Tuchukue mikopo kuwekeza kwenye miradi itakayokuza uchumi na kuzalisha kodi zaidi. Bajeti inaonyesha kwamba Serikali itakopa shilingi takribani trillion 5 mwaka 2012/13. Serikali ikubalikutekeleza mapendekezoya Kambi ya Upinzani ya kuimarisha ukusanyaji wa kodi na kupanua wigo wa kodi katika maeneo muhimu kama sekta ya madini na mawasiliano, kuzuia misamaha ya kodi, kutokomeza ukwepaji kodi, na kuepuka matumizi mabaya ili kuepuka madeni yasiyo ya lazima.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inapenda kusisitiza kwamba Bunge lifanye ukaguzi maalumu kuhusu akaunti ya Deni la Taifa ili kuweza kubaini ukweli kuhusu ustahmilivu wa Deni na mikopo ambayo Serikali inachukua kama inakwenda kwenye Maendeleo na miradi ipi na kama miradi hiyo ina tija. Vilevile tumependekeza kwamba Mikopo yote ambayo Serikali inachukua iwe inapata idhini ya Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi au Bunge litunge sharia ili kiwango cha juu cha kukopa ambacho Serikali haipaswi kuvuka. Kuiacha Serikali inaendelea kukopa bila mpango ni kuliweka Taifa rehani na kupeleka mzigo wa kulipa madeni haya kwa kizazi kijacho. Hatuwezi kukubali Wazee wetu waishi maisha yao, waishi maisha yetu na pia wakope maisha ya watoto wetu. Mwisho wa kunukuu.

Kambi ya Upinzani inarejea kutaka ukaguzi maalumu kuhusu akaunti za Deni la Taifa na maelezo ya kina ya Serikali kuhusu shilingi 620 bilioni ambazo hazina maelezo kwenye Deni la Taifa. Hatuwezi kukaa kimya kuona Watanzania wanabebeshwa madeni ambayo kimsingi ni madeni bandia yanayotajirisha watu wachache wenye uwezo na ujasiri mkubwa wa kuiba, kupora nakufisidi hazina ya Taifa letu.

Kabwe Zuberi Zitto,Mb

Waziri Kivuli Fedha na Uchumi

Thursday, March 21

‘Tunahitaji dunia inayolinda maisha’

Vatican City. Mkuu wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis amesimikwa rasmi, huku akiitaka dunia kuungana kwa ajili ya kuwatetea wanyonge na kulinda mazingira.
Akizungumza wakati wa misa maalumu ya kumsimika katika wadhifa huo mpya iliyofanyika kwenye Kanisa Kuu la Mtakatifu Peter mjini Vatican, Papa Francis alisema hiyo ndiyo njia pekee ya kuijenga dunia iliyo njema na salama, isiyo na vifo visivyo vya lazima na maangamizi.
Francis akitoa hotuba yake alikuwa akishangiliwa na kufunikwa kila mara kwa sauti ya hadhira iliyokuwa ikimsikiliza, hasa alipozungumzia umuhimu wa kulinda mazingira, kusaidiana, kupendana na kutoruhusu namna yoyote ya maangamizi, chuki, wivu na majivuno yanayoweza ‘kuharibu maisha yetu’.
Alisema kwamba wajibu wake mkuu ni kunyoosha mikono yake na kulinda utu, hasa ‘wa maskini, wasiojiweza, wale wanaodharauliwa hasa ambao Mtakatifu Mathayo aliwataja alipokuwa akihitimisha falsafa ya upendo: wenye njaa, wenye kiu, wageni, wasio na mavazi, wagonjwa na wale waliofungwa magerezani’.
“Leo tunahitaji kuona mwanga wa matumaini katika giza lililopo mbele yetu na kuwa wanaume na wanawake wanaotoa tumaini jipya kwa wengine. Kulinda uumbaji, kulinda wanaume na wanawake, kuwaangalia kwa upendo na kujali, hii ikiwa njia pekee ya kutoa tumaini jipya, ili kutoa mwanga mpya na kuangaza kuliko na wingu nene,” alisema.
Kauli hiyo ilianza kutolewa na kiongozi huyo mkuu wa Kanisa lenye zaidi ya waumini 1.2 bilioni duniani tangu alipotangazwa rasmi kuchaguliwa na jopo la makadinali Jumatano wiki iliyopita, ambapo alianza kutangaza ujumbe wake wa amani wa kuwajali na kuwapenda maskini.
Katika misa hiyo maalumu iliyohudhuriwa na wageni maalumu 132 wakiwamo viongozi wa kidini na wa mataifa mbalimbali akiwamo Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe, ujumbe wake kwa wafuasi wa Kanisa hilo na watu wote duniani ulichukua muda mfupi usiofikia saa moja, hivyo kumfanya aonekane mtu mwenye staha na kujali muda.
“Ninawaomba wote wenye wajibu katika kusimamia uchumi, siasa, maisha ya watu kuwajibika.” pamoja na wanaume na wanawake wote wenye nia njema, tuwe walinzi wa uumbaji wa Mungu, tulinde mpango wa Mungu ulio wa asili, tulindane na kupendana na kuyalinda mazingira.”
Papa Francis alijumuika na waumini waliokusanyika katika uwanja huo ambapo alizunguka katika eneo hilo kwa kutumia gari maalumu, akisalimiana na waumini kuwabariki wasiojiweza na kuwabusu watoto wenye matatizo.

Lowassa afufua kashfa ya kigogo Ikulu

Dar es Salaam. Sakata la Mkuu wa Itifaki wa Ikulu, Anthony Itatiro, ambaye anahusishwa na njama za kutaka kuchota kiasi cha Sh3 bilioni kwa ajili ya safari hewa ya Rais, limechukua sura mpya baada ya Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje kutaka kujua hatima ya kigogo huyo jana.
Itatiro na maofisa wanne wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa walituhumiwa mwaka jana kuidhinisha kuchota kiasi hicho cha fedha bila ya kuwapo kwa ziara ya Rais kwenda nchi yoyote ya kigeni.
Mpango huo unadaiwa kusukwa Juni mwaka jana kwa maofisa haokuitaka Wizara ya Fedha kutoa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya safari hewa ya Rais.
Naibu Waziri wa wizara hiyo, Juma Mahadhi alitoa maelezo hayo baada ya kuulizwa swali na Mwenyekiti wa Kamati ya Mambo ya Nje ya Bunge, Edward Lowassa.
Lowassa, ambaye pia ni Mbunge wa Monduli aliuliza swali hilo ghafla kwa Mahadhi wakati akitoka nje, baada ya kumalizika kwa kikao cha kamati yake kilichofanyika kwenye ofisi za Bunge jijini Dar es Salaam.
Mahadhi, ambaye alilazimika kutoa ufafanuzi wa swali hilo baada ya kubanwa zaidi na waandishi wa habari, alisema Rais Kikwete ndiyo mwenye mamlaka ya kuchukua hatua dhidi ya Itatiro kutokana na ripoti ya uchunguzi ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na Mkaguzi wa Ndani wa Wizara hiyo.
Alisema pia kuwa walishauriwa kuwa maofisa walioshirikiana na Itatiro nao wachukuliwe hatua za kinidhamu kufuatia njama hizo.
Alipotafutwa kuzungumzia suala hilo, Katibu Mkuu Ombeni Sefue hakupokea simu. Pia hakujibu pindi alipotumiwa ujumbe mfupi kwa njia ya simu. Naye Katibu Mkuu katika Ofisi ya Rais anayeshughulikia Utumishi, George Yambesi alisema hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo kwani alikuwa likizo.
Mahadhi alisema wakati tukio hilo linatokea viongozi wakuu wa wizara hiyo walikuwa kwenye majukumu mengine ya Serikali, jambo ambalo lilisababisha nafasi zao kukaimiwa na watendaji hao.
“Wale maofisa walitumia mwanya wao wa kukaimu nafasi ile ndiyo wakasuka mpango huo,” aliongeza Mahadhi.
Alisema kutokana na hali hiyo baadhi ya maofisa hao wamechukuliwa hatua za kinidhamu ikiwamo ya kuwashusha vyeo na kuwabadilisha vitengo.
Mahadhi alisema kwamba huwa ni utaratibu wa kawaida kwa Rais anaposafiri maofisa wa Itifaki na wale wa Wizara ya Mambo ya Nje kupewa fedha na hazina kwa ajili ya kufanikisha ziara zake.
“Ila maofisa hawa walitumia mwanya huo kuihadaa Wizara ya Fedha kwa kuandaa hoja ya safari feki ili kupata fedha hizo,” aliongeza Mahadhi.
Maofisa wengine ni pamoja na ofisa katika Idara ya Itifaki, Shamim Khalfa, Kaimu Mhasibu Mkuu, Kasim Laizer, Mhasibu, Deltha Mafie na karani wa fedha) aitwaye, Shabani Kesi.

OBAMA AFANANISHWA NA SHETANI...


Rais wa Marekani Barack Obama amefananishwa na shetani baada ya muigizaji Mohamen Mehdi Quazann kucheza sinema inayofanana na muonekano wa shetani huku akionekana kufafana na Obama

Kwa mujibu wa repoti ya CNN filamu hiyo ambayo imeonekana kuteka mashabiki wengi teyari imeshaanza kurushwa vipande vichache vinavyoonyesha jinsi Obama alivyofanana na Mohamen huku akionekana kama shetani kupitia channel ya 'The History'

Mpaka sasa inaonekana filamu hiyo kupata mashabiki wengi na kuteka vichwa vya habari vingi huku mashabiki wengi wakiwa wamemiminika katika mtandao wa twitter na kupata tweets zaidi ya 200 kwa muda mfupi

PRO-24