Monday, April 15

Mbowe, Slaa: Hatukubali Chadema kuhujumiwa

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe akizungumza kwenye kongamano la chama hicho lililofanyika jana jijini Dar es Salaam. Picha na Fidelis Felix.

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa wamesema “hawatakubali wala kuvumilia” hujuma dhidi ya chama chao.
Dar es Salaam. Viongozi hao kwa nyakati tofauti jana walisema hujuma hizo zimekuwa zikifanywa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na Serikali ambayo imekuwa ikitumia vyombo vya dola na kwamba sasa wanapanga ugaidi wa kuwateka maofisa wa ngazi ya juu wa Chadema.
Suala la ugaidi liliibuka kwa nguvu katika wiki ya kwanza ya Bunge la Bajeti na sasa limehamia nje ya chombo hicho cha kutunga sheria kutokana na Chadema kuwatuhumu CCM na Serikali yake kwamba wanapanga njama za kuwateka maofisa wakuu wa chama hicho.
Jana Dk Slaa alipokuwa akimkaribisha Mbowe kufungua Mkutano wa Mafunzo na Mipango ya Vuguvugu la Mabadiliko ‘M4C’ na Kongamano la Katiba Mpya kwa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani, alisema taarifa walizonazo zinaonyesha kuwa CCM ndiyo wanaofanya vitendo vya kigaidi wakishirikiana na Serikali.
“Tuna taarifa zote zinazoonyesha kwamba CCM ndiyo magaidi wakishirikiana na Serikali yake, lakini sisi tuko makini kuliko hata Serikali ya CCM na tuko makini kuliko hata Usalama wa Taifa na umakini huu ndiyo utakaotupeleka Ikulu mwaka 2015,”alisema Dk Slaa.
Hata hivyo Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipotafutwa kujibu tuhuma hizo alisema hakuna jipya ambalo Chadema wamelisema.
“Kuna jipya katika hilo, ni yale yale ya kawaida na jana (juzi) Mwingulu alizungumza vizuri sana bungeni. Hiyo ni sawa na mchawi anapomwangia mtu na kufa anakuwa wa kwanza kwenda kulia msibani, nchi siku yoyotete haijengwi kwa ngonjera za maneno bali inajengwa kwa mipango,”alisema Nape.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Pereira Ame Silima alipotakiwa kutoa msimamo wa Serikali juu ya tuhuma hizo alisema, “Mimi siwezi kuzungumza ila mtafute Waziri (Dk Emmanuel Nchimbi),”alisema Silima.
Alipotafutwa Dk Nchimbi kupitia simu yake ya mkononi, ilikuwa ikiita bila kupokewa.
Kauli ya Mbowe
Kwa upande wake Mbowe alisema, CCM imekuwa ikitumia mbinu mbalimbali kuhakikisha inakisambaratisha chama hicho bila mafanikio.
“Watu wa Usalama wa Taifa wakishirikiana na CCM wamekuwa wakifanya mipango ya kutaka kuwateka maofisa wetu. Hawa watu ni wepesi sana na msiwaogope hata kidogo,”alisema Mbowe huku akishangiliwa na wanachama na makada waliofurika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Blue Pearl.
Mbowe alisema: “Ukiona chama chochote tawala kinatumia jeshi la polisi kutengeneza ushahidi wowote wa kihalifu hiyo ni dalili ya hatari kwa mustakabali wa usalama wa nchi.”
Mbowe alisema mbinu za sasa za CCM zinatokana na kushindwa kukivuruga chama hicho kwa propaganda kuwa ni chama cha familia, ukabila, ukanda na baadaye udini.
Katiba na Elimu
Kuhusu mchakato wa Katiba Mpya, Mbowe alisema ikiwa itafika Aprili 30 mwaka huu bila hatua zozote kuchukuliwa, watamwamuru mjumbe wa tume hiyo kutoka Chadema, Profesa Mwesiga Baregu kujiondoa.
Chadema kinataka Serikali iwasilishe bungeni, muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Katiba ili yafanywe marekebisho mbalimbali kuhusu uwakilishi katika Bunge Maalumu la Katiba.
“Serikali inaona hili kama mchezo, sasa acha wakae kimya na baada ya Aprili 30 mwaka huu watachagua kusuka au kunyoa,”alisema Mbowe.
Kuhusu elimu, Mbowe alieleza kushangazwa na kile alichosema kuwa ni Serikali kutofahamu sababu za wanafunzi kufanya vibaya katika mitihani yao.
“Serikali eti haijui na kama haijui basi Waziri Mkuu (Mizengo Pinda) hatakiwi kuwa hapo alipo, kwani haiwezekani watoto wanafeli halafu anaunda tume,”alisema Mbowe na kuongeza:
“Mwaka 2011 waliunda tume ambayo ilitoa mapendekezo 27 lakini ripoti hiyo ilifichwa hadi mimi juzi (Jumatano) nilipoisoma bungeni wabunge wa CCM wakabaki vichwa chini.”
Alisema kuundwa kwa tume nyingine ambayo itatumia fedha za walipakodi ni kuwaumiza Watanzania ilhali tatizo na chanzo kinajulikana.
Ugaidi bungeni
Juzi wakati wa mjadala wa Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, wabunge wa CCM na Chadema kwa nyakati tofauti walituhumiana kwa ugaidi kiasi cha kusababisha vurugu na kutoelewana miongoni mwao.
Alhamisi akisoma maoni ya Kambi ya Upinzani, Mbowe alisema ugaidi ni ubunifu wa polisi na Serikali kwa ajili ya kuwabambikia kesi zisizo na dhamana kwenye mahakama maofisa wa vyama vya upinzani.
Kutokana na hotuba hiyo, Mbunge wa Iramba Magharibi (CCM), Mwigulu Nchemba aliishambulia hotuba ya Mbowe akieleza kuwa wanahusika kupanga kumdhuru mwandishi wa habari.

ADHANA YARUHUSIWA SWEDEN KWA MARA YA KWANZA

Msikiti mmoja katika kitongoji cha mji mkuu wa Sweden, Stockholm umeruhusiwa kuadhini kwa kutumia kipaza sauti kilicho kwenye mnara kwa ajili ya Sala ya Ijumaa.

Hii ni mara kwa kwanza kwa nchi hiyo ya Scandinavia kuruhusu adhana kwa sauti inayosikika nje ya msikiti.

Idara ya polisi mjini Stockholm imesema msikiti huo utaruhusiwa kuadhini kwa muda wa kati ya dakika tatu na tano katika kipindi cha baina ya saa sita na saa saba mchana kila Ijumaa.

Mkuu wa Jumuiya ya Utamaduni wa Kiislamu katika eneo la Botkyrka kusini mwa Stockholm Bw. Ismail Okur ameupongeza uamuzi huo. Ombi la kuadhini kwa sauti inayotoka nje ya msikiti liliwasilishwa miaka mitano iliyopita.

Kuna karibu Waislamu 7,000 katika eneo hilo na aghalabu wana asili ya Uturuki.

Chama chenye chuki dhidi ya Uislamu cha Sweden Democrats kimepinga uamuzi huo.

Katika miaka ya hivi karibuni, idadi ya Waislamu barani Ulaya imeongezeka kwa kasi na sambamba na hilo hitajio la misikiti pia limeongezeka. Waislamu raia wa nchi za Ulaya wamekuwa wakibaguliwa kwa muda mrefu na sasa wanapigania haki sawa na raia wengine wa Ulaya.

Saturday, April 13

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo by zittokabwe

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ametoa taarifa yake ya mwaka 2011/2012 na kuonyesha kuwa kuna skandali kubwa sana katika akaunti ya Deni la Taifa. Nanukuu

‘Uhakiki wa mchanganuo wa madeni ya Taifa kama ulivyokuwa tarehe 30 Juni, 2012 ulibaini kuwepo kwa marekebisho ya deni ya shilingi 619,803,554,183.91 ambayo uongozi haukuweza kutoa maelezo ya kuridhisha.’ (Taarifa ya CAG, Ripoti ya Serikali Kuu 2011/2012 uk 158). Mwisho wa Kunukuu

Katika Taarifa yake hiyo CAG anaendelea kuonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kukua na mwaka unaoishia mwezi Juni 2012 deni lilikuwa kwa asilimia 17 kutoka mwaka unaoishia mwezi Juni 2011.

Kukosekana kwa maelezo ya kuridhisha kuhusu zaidi ya nusu trilioni za Deni la Taifa ni jambo linalopaswa kutiliwa mashaka makubwa, kuchunguzwa na kupata majawabu stahiki. Tafiti mbalimbali duniani zinaonyesha kuwa kuna mahusiano makubwa sana kati ya Deni la Taifa la utoroshaji wa fedha kwenda kwenye mabenki ya ‘offshore’. Katika kitabu cha ‘Africa’s Odious Debts: How Foreign Loans and Capital flight bled a continent’ kilichoandikwa mabwana Leonce Ndikumana na James Boyce imeonekana kwamba Deni la Taifa huchochea utoroshwaji wa Fedha kwenda kuficha nje ya Tanzania.

Mabilioni haya kwenye akaunti ya Deni la Taifa yanashtusha sana. Kambi ya Upinzani Bungeni kwa miaka miwili mfululizo imekuwa ikitaka ukaguzi maalumu kwenye akaunti za Deni la Taifa lakini Serikali imeshindwa kufanya hivyo. Nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya PAC pia nimemtaka CAG afanye ukaguzi huu maalumu.

Kambi ya upinzani Bungeni ilisema hivi katika Bajeti yake kivuli 2012/13:

DENI LA TAIFA

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasikitika kwa serikali kuendelea kutengeneza madeni kwa Taifa kwa kuendelea kukopa zaidi kwa matumizi ya kawaida ya serikali. Wakati Serikali inasisitiza kwamba Deni letu linastahmilika, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali anaonyesha mashaka makubwa sana kutokana na kasi ya kukua kwa Deni la Taifa. Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kuongezeka kwa asilimia 38% kutoka shilingi trillion 10.5 mwaka 2009/2010 hadi shilingi trillion 14.4 mwaka 2010/2011. Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha Deni la Taifa limefikia shilingi trillion 20.3 mpaka ilipofika mwezi Machi mwaka 2012. Ukisoma taarifa ya Mwezi wa Mei 2012 ya Benki Kuu ya Tanzania, Deni la Taifa sasa limefikia shilingi trillion 22.

Mheshimiwa Spika, Suala hapa sio ustahmilivu wa Deni kama inavyodai Serikali bali ni kwamba tunakopa kufanyia nini? Bajeti ya Mwaka 2012/13 inayopendekezwa inaonyesha kwamba Serikali itakusanya shilingi trilioni 8.7 kama makusanyo ya ndani na itatumia shilingi trilioni 10.6 kama matumizi ya kawaida. Ni dhahiri kwamba sehemu ya mikopo ambayo serikali inachukua sasa itakwenda kwenye matumizi ya kawaida. Hatutaki mikopo kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya posho, kusafiri, magari nk. Tuchukue mikopo kuwekeza kwenye miradi itakayokuza uchumi na kuzalisha kodi zaidi. Bajeti inaonyesha kwamba Serikali itakopa shilingi takribani trillion 5 mwaka 2012/13. Serikali ikubalikutekeleza mapendekezoya Kambi ya Upinzani ya kuimarisha ukusanyaji wa kodi na kupanua wigo wa kodi katika maeneo muhimu kama sekta ya madini na mawasiliano, kuzuia misamaha ya kodi, kutokomeza ukwepaji kodi, na kuepuka matumizi mabaya ili kuepuka madeni yasiyo ya lazima.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inapenda kusisitiza kwamba Bunge lifanye ukaguzi maalumu kuhusu akaunti ya Deni la Taifa ili kuweza kubaini ukweli kuhusu ustahmilivu wa Deni na mikopo ambayo Serikali inachukua kama inakwenda kwenye Maendeleo na miradi ipi na kama miradi hiyo ina tija. Vilevile tumependekeza kwamba Mikopo yote ambayo Serikali inachukua iwe inapata idhini ya Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi au Bunge litunge sharia ili kiwango cha juu cha kukopa ambacho Serikali haipaswi kuvuka. Kuiacha Serikali inaendelea kukopa bila mpango ni kuliweka Taifa rehani na kupeleka mzigo wa kulipa madeni haya kwa kizazi kijacho. Hatuwezi kukubali Wazee wetu waishi maisha yao, waishi maisha yetu na pia wakope maisha ya watoto wetu. Mwisho wa kunukuu.

Kambi ya Upinzani inarejea kutaka ukaguzi maalumu kuhusu akaunti za Deni la Taifa na maelezo ya kina ya Serikali kuhusu shilingi 620 bilioni ambazo hazina maelezo kwenye Deni la Taifa. Hatuwezi kukaa kimya kuona Watanzania wanabebeshwa madeni ambayo kimsingi ni madeni bandia yanayotajirisha watu wachache wenye uwezo na ujasiri mkubwa wa kuiba, kupora nakufisidi hazina ya Taifa letu.

Kabwe Zuberi Zitto,Mb

Waziri Kivuli Fedha na Uchumi

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo by zittokabwe

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ametoa taarifa yake ya mwaka 2011/2012 na kuonyesha kuwa kuna skandali kubwa sana katika akaunti ya Deni la Taifa. Nanukuu

‘Uhakiki wa mchanganuo wa madeni ya Taifa kama ulivyokuwa tarehe 30 Juni, 2012 ulibaini kuwepo kwa marekebisho ya deni ya shilingi 619,803,554,183.91 ambayo uongozi haukuweza kutoa maelezo ya kuridhisha.’ (Taarifa ya CAG, Ripoti ya Serikali Kuu 2011/2012 uk 158). Mwisho wa Kunukuu

Katika Taarifa yake hiyo CAG anaendelea kuonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kukua na mwaka unaoishia mwezi Juni 2012 deni lilikuwa kwa asilimia 17 kutoka mwaka unaoishia mwezi Juni 2011.

Kukosekana kwa maelezo ya kuridhisha kuhusu zaidi ya nusu trilioni za Deni la Taifa ni jambo linalopaswa kutiliwa mashaka makubwa, kuchunguzwa na kupata majawabu stahiki. Tafiti mbalimbali duniani zinaonyesha kuwa kuna mahusiano makubwa sana kati ya Deni la Taifa la utoroshaji wa fedha kwenda kwenye mabenki ya ‘offshore’. Katika kitabu cha ‘Africa’s Odious Debts: How Foreign Loans and Capital flight bled a continent’ kilichoandikwa mabwana Leonce Ndikumana na James Boyce imeonekana kwamba Deni la Taifa huchochea utoroshwaji wa Fedha kwenda kuficha nje ya Tanzania.

Mabilioni haya kwenye akaunti ya Deni la Taifa yanashtusha sana. Kambi ya Upinzani Bungeni kwa miaka miwili mfululizo imekuwa ikitaka ukaguzi maalumu kwenye akaunti za Deni la Taifa lakini Serikali imeshindwa kufanya hivyo. Nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya PAC pia nimemtaka CAG afanye ukaguzi huu maalumu.

Kambi ya upinzani Bungeni ilisema hivi katika Bajeti yake kivuli 2012/13:

DENI LA TAIFA

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasikitika kwa serikali kuendelea kutengeneza madeni kwa Taifa kwa kuendelea kukopa zaidi kwa matumizi ya kawaida ya serikali. Wakati Serikali inasisitiza kwamba Deni letu linastahmilika, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali anaonyesha mashaka makubwa sana kutokana na kasi ya kukua kwa Deni la Taifa. Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kuongezeka kwa asilimia 38% kutoka shilingi trillion 10.5 mwaka 2009/2010 hadi shilingi trillion 14.4 mwaka 2010/2011. Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha Deni la Taifa limefikia shilingi trillion 20.3 mpaka ilipofika mwezi Machi mwaka 2012. Ukisoma taarifa ya Mwezi wa Mei 2012 ya Benki Kuu ya Tanzania, Deni la Taifa sasa limefikia shilingi trillion 22.

Mheshimiwa Spika, Suala hapa sio ustahmilivu wa Deni kama inavyodai Serikali bali ni kwamba tunakopa kufanyia nini? Bajeti ya Mwaka 2012/13 inayopendekezwa inaonyesha kwamba Serikali itakusanya shilingi trilioni 8.7 kama makusanyo ya ndani na itatumia shilingi trilioni 10.6 kama matumizi ya kawaida. Ni dhahiri kwamba sehemu ya mikopo ambayo serikali inachukua sasa itakwenda kwenye matumizi ya kawaida. Hatutaki mikopo kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya posho, kusafiri, magari nk. Tuchukue mikopo kuwekeza kwenye miradi itakayokuza uchumi na kuzalisha kodi zaidi. Bajeti inaonyesha kwamba Serikali itakopa shilingi takribani trillion 5 mwaka 2012/13. Serikali ikubalikutekeleza mapendekezoya Kambi ya Upinzani ya kuimarisha ukusanyaji wa kodi na kupanua wigo wa kodi katika maeneo muhimu kama sekta ya madini na mawasiliano, kuzuia misamaha ya kodi, kutokomeza ukwepaji kodi, na kuepuka matumizi mabaya ili kuepuka madeni yasiyo ya lazima.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inapenda kusisitiza kwamba Bunge lifanye ukaguzi maalumu kuhusu akaunti ya Deni la Taifa ili kuweza kubaini ukweli kuhusu ustahmilivu wa Deni na mikopo ambayo Serikali inachukua kama inakwenda kwenye Maendeleo na miradi ipi na kama miradi hiyo ina tija. Vilevile tumependekeza kwamba Mikopo yote ambayo Serikali inachukua iwe inapata idhini ya Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi au Bunge litunge sharia ili kiwango cha juu cha kukopa ambacho Serikali haipaswi kuvuka. Kuiacha Serikali inaendelea kukopa bila mpango ni kuliweka Taifa rehani na kupeleka mzigo wa kulipa madeni haya kwa kizazi kijacho. Hatuwezi kukubali Wazee wetu waishi maisha yao, waishi maisha yetu na pia wakope maisha ya watoto wetu. Mwisho wa kunukuu.

Kambi ya Upinzani inarejea kutaka ukaguzi maalumu kuhusu akaunti za Deni la Taifa na maelezo ya kina ya Serikali kuhusu shilingi 620 bilioni ambazo hazina maelezo kwenye Deni la Taifa. Hatuwezi kukaa kimya kuona Watanzania wanabebeshwa madeni ambayo kimsingi ni madeni bandia yanayotajirisha watu wachache wenye uwezo na ujasiri mkubwa wa kuiba, kupora nakufisidi hazina ya Taifa letu.

Kabwe Zuberi Zitto,Mb

Waziri Kivuli Fedha na Uchumi